Ushirikina—Mbona Umedumu Sana?
HUENDA unafahamu kwamba bado kuna watu wengi wanaoona kuvuka kwa paka mweusi mbele yao kuwa bahati mbaya au wanaohofu kupita chini ya ngazi. Watu wengi huamini pia kwamba tarehe 13 Ijumaa ni siku ya bahati mbaya na kwamba ni hatari sana kuwa katika orofa ya 13 ya jengo lolote. Ushirikina wa aina hiyo unazidi kudumu hata ingawa si wa kiakili.
Ebu fikiria. Kwa nini watu fulani hubeba mguu wa sungura au kugonga mbao wanaposema juu ya matazamio yao? Je, si ni kwa sababu wanaamini pasipo uthibitisho wowote kwamba kufanya hivyo kutaleta bahati njema? Kitabu A Dictionary of Superstitions chasema: “Mshirikina anaamini kwamba vitu fulani, mahali, wanyama, au matendo fulani huleta bahati njema (ndege nzuri au hirizi) na kwamba vitu vingine huleta bahati mbaya (ndege mbaya au ishara za msiba).”—Ona Wagalatia 5:19, 20.
Jitihada za Kuukomesha Katika China
Kwa wazi, ushirikina umeokoka jitihada za kisasa za kuukomesha. Kwa mfano, mnamo 1995 bunge la People’s Congress la Shanghai lilitangaza agizo rasmi la serikali lililopiga marufuku ushirikina likiutaja kuwa zoea la kale katika historia ya taifa hilo. Lengo lilikuwa “kukomesha kabisa ushirikina wa kikabaila, kubadili desturi za maziko na kuendeleza ujenzi wa mji mkuu uliostaarabika zaidi.” Lakini tokeo limekuwa nini?
Kwa mujibu wa ripoti moja, wakazi wa Shanghai waliendelea kuwa waaminifu-washikamanifu kwa ushirikina wao. Katika kukiuka amri rasmi iliyopiga marufuku sherehe ya Wachina ya kuteketeza noti bandia kwenye makaburi ya wazazi wa kale waliokufa, mgeni mmoja alisema: “Tumeteketeza yuan bilioni 19 [takriban dola za Marekani bilioni tatu].” Aliongezea hivi: “Ni desturi kufanya hivyo. Jambo hilo huifurahisha miungu.”
Gazeti linalopendwa sana la Guangming Daily lilikazia kushindwa kwa marufuku hayo, kwa kusema kuwa “China yaweza kuwa na wapiga-ramli wa kitaaluma wapatao milioni tano, ilhali jumla ya idadi ya wanasayansi na wanatekinolojia wa kitaaluma ni milioni 10 tu.” Gazeti hilo lilisema: “Yaonekana kwamba wabashiri wanapendwa zaidi.”
Chapa ya Kimataifa ya kichapo The Encyclopedia Americana, yasema hivi kuhusu kudumu kwa ushirikina: “Desturi fulani za kale hazidumishwi tu katika tamaduni zote, bali zinafasiriwa upya na kupata maana mpya.” Chapa ya karibuni ya The New Encyclopædia Britannica ilikiri hivi: “Hata katika zile zinazoitwa nyakati za kisasa, wakati ambapo uthibitisho halisi unathaminiwa sana, kuna watu wachache ambao hata wakisihiwa sana hawawezi kukiri kwamba wanafuata kisirisiri itikadi fulani au ushirikina usio wa kiakili.”
Viwango Maradufu
Kwa wazi watu wengi wana viwango maradufu, kwa kuwa hawawezi kukiri hadharani matendo yao ya faraghani. Mtungaji mmoja asema kwamba kusitasita huko hutokana na hofu ya kuonwa na wengine kuwa wapumbavu. Hivyo, huenda watu hawa wakapendelea kuziita desturi zao za kishirikina kuwa kawaida au mazoea. Kwa mfano, huenda wanariadha wakayaona mazoea yao kuwa desturi za kabla ya michezo.
Hivi majuzi mwandishi mmoja wa habari alieleza kwa utani kuhusu barua-mkufu, barua ambayo wapokeaji huombwa kutoa nakala na kuzipeleka kwa watu wengine wengi wanaofanya vivyo hivyo. Mara nyingi, yule anayepeleka barua hiyo huahidiwa kupata bahati njema, ilhali yule anayevunja mkufu huo inaaminiwa kwamba atapatwa na matokeo mabaya. Kwa hiyo mwandishi huyo wa habari alijiunga katika uandikaji wa barua-mkufu kisha akasema: “Nataka mjue kuwa mimi sifanyi hivyo kwa sababu nafuata ushirikina. Nataka tu kuepuka bahati mbaya.”
Wanaanthropolojia na wataalamu wa elimu ya mila na desturi wanaonelea kwamba hata neno “ushirikina” linategemea sana maoni ya kibinafsi; na hawapendi kuyaita hivyo mazoea fulani ya kawaida. Wanapendelea maneno ya “ujumla” lakini yasiyoudhi kama vile “desturi za mila na itikadi,” “elimu ya mila na desturi,” au “mifumo ya itikadi.” Dick Hyman, aeleza hivi waziwazi katika kitabu chake Lest Ill Luck Befall Thee—Superstitions of the Great and Small: “Ushirikina kama dhambi na mafua, hutetewa na watu wachache sana japo wengi huuzoea.”
Hata hivyo, ushirikina upo bila kujali jinsi unavyoitwa. Kwa nini iko hivyo katika enzi ya sasa ya kisayansi iliyoendelea kitekinolojia?
Sababu Inayofanya Udumu
Kwa kweli, watu fulani husisitiza kwamba kuitikadi ushirikina ni jambo la kawaida kwa wanadamu. Hata kuna wale wanaodai kwamba mwelekeo wa kufuata ushirikina uko katika chembe zetu za urithi. Hata hivyo, kuna uchunguzi unaothibitisha jambo lililo kinyume na hilo. Uthibitisho ni kwamba watu huwa washirikina kwa sababu ya mambo wanayofundishwa.
Profesa Stuart A. Vyse aeleza: “Mtu hujifunza zoea la ushirikina maishani, sawa na mazoea mengineyo mengi. Hatuzaliwi na zoea la kugonga mbao; sisi hujifunza kufanya hivyo.” Yasemekana kwamba watu hujifunza kuitikadi mizungu utotoni na kisha huwa katika hatari ya kuitikadi ushirikina muda mrefu baada ya wao “kukomaa kiakili.” Wao hujifunza wapi itikadi nyingi za kishirikina?
Itikadi nyingi za kishirikina huhusiana sana na itikadi za kidini zinazopendwa. Kwa mfano, ushirikina ulikuwa sehemu ya dini ya wakazi wa Kanaani kabla ya Waisraeli kuja. Biblia yasema kwamba ilikuwa desturi ya Wakanaani kubashiri, kuwa wasihiri, kuloga kwa kupiga mafundo, kuwasiliana na roho-waovu, kufanya uchawi, na kuomba wafu.—Kumbukumbu la Torati 18:9-12.
Wagiriki wa kale walikuwa mashuhuri pia kwa sababu ya ushirikina uliohusiana na dini yao. Waliitikadi mizimu, uaguzi, na mizungu, sawa na Wakanaani. Wababiloni walitazama maini ya mnyama, huku wakiamini kwamba yangewaonyesha hatua waliyopaswa kuchukua. (Ezekieli 21:21) Walijulikana pia kwa sababu ya uchezaji wao wa kamari na walitafuta msaada kutoka kwa yule anayerejezewa katika Biblia kuwa “mungu wa Bahati Njema.” (Isaya 65:11, NW) Hadi leo wacheza-kamari wanajulikana kuwa washirikina.
Jambo la kushangaza ni kuwa, makanisa kadhaa yamewatia watu moyo wajitoe kucheza kamari. Mfano mmoja ni Kanisa Katoliki, ambalo limedhamini utendaji kama vile aina fulani ya mchezo wa kamari. Vivyo hivyo, mcheza-kamari mmoja alisema: “Nina hakika kwamba Kanisa Katoliki linang’amua kwamba [wacheza-kamari ni washirikina sana,] kwa kuwa sikuzote watawa wa kike walisimama karibu na barabara ya mbio wakiwa na visanduku vyao vya michango. Tukiwa Wakatoliki wengi tungekosaje kumpa mchango ‘mtawa wa kike’ na bado tutarajie kushinda mashindano ya farasi? Kwa hiyo tulichanga. Na endapo tungeshinda siku hiyo basi tungechanga sana, tukitumaini kwamba kufanya hivyo kungeleta mafanikio zaidi.”
Mifano yenye kutokeza ya uhusiano wa karibu uliopo kati ya dini na ushirikina ni ushirikina unaohusiana na Krismasi, sherehe inayoendelezwa na makanisa ya Jumuiya ya Wakristo. Huo watia ndani tumaini la kuwa kubusiana chini ya mlimbo kutaongoza kwenye ndoa na itikadi nyingi za kishirikina kumhusu Baba Krismasi.
Kitabu Lest Ill Luck Befall Thee chasema kwamba ushirikina ulianzishwa katika jitihada ya “kuchunguza mambo ya wakati ujao.” Kwa hiyo leo, kama katika historia yote, watu wa kawaida pamoja na viongozi wa ulimwengu huwasiliana na wapiga-ramli na watu wengineo wanaodai wana uwezo wa kimizungu. Kitabu Don’t Sing Before Breakfast, Don’t Sleep in the Moonlight chaeleza: “Watu walihitaji kuamini kuwapo kwa hirizi na ulozi ambao ungewalinda kutokana na hofu ya mambo yajulikanayo na yasiyojulikana.”
Hivyo utendaji wa kishirikina umejaribu kuwafanya wanadamu wajihisi wakiwa na uwezo wa kudhibiti hofu yao. Kitabu Cross Your Fingers, Spit in Your Hat chasema: “[Wanadamu] hutegemea ushirikina kwa sababu zilezile za kawaida. [Wanapokabili] hali [wasizoweza] kudhibiti—zinazotegemea ‘bahati’ au ‘nasibu’—ushirikina huwafanya [wao] wajihisi wakiwa salama zaidi.”
Ijapokuwa sayansi imeboresha kwa njia nyingi hali ya wanadamu, bado wanajihisi wakiwa bila usalama. Kwa kweli, ukosefu wa usalama umeongezeka kwa sababu ya matatizo ambayo yameletwa na sayansi. Profesa Vyse asema: “Ushirikina na kuitikadi mambo ya kifumbo ni sehemu muhimu ya utamaduni wetu . . . kwa sababu ulimwengu wetu wa kisasa umezidisha hali yetu ya kukosa uhakika.” Kitabu The World Book Encyclopedia kilimalizia hivi: “Huenda ushirikina ukaendelea kuwapo maadamu watu . . . wanakosa kuwa na uhakika juu ya wakati ujao.”
Kwa muhtasari basi, ushirikina unadumu kwa sababu unatokana na hofu ya kawaida ya wanadamu na unaungwa mkono na itikadi nyingi za kidini zinazopendwa sana. Ingawa hivyo, je, tunaweza kufikia mkataa wa kwamba ushirikina una kusudi lenye manufaa, kwa kuwa unawasaidia watu wakabiliane na ukosefu wa uhakika? Je, hauwezi kudhuru? Au ni jambo hatari linalopasa kuepukwa?
[Picha katika ukurasa wa 5]
China peke yake yaweza kuwa na wapiga-ramli wa kitaaluma wapatao milioni tano
[Picha katika ukurasa wa 6]
Makanisa mengi yamesitawisha ushirikina kwa kuendeleza aina fulani ya mchezo wa kamari
[Picha katika ukurasa wa 7]
Mapokeo ya Krismasi kama vile kubusiana chini ya mlimbo ni ya kishirikina