Dini ya Kweli Inafukuzia Mbali Woga Jinsi Gani?
EDWIN na Mona Radford watungaji vitabu Waingereza walikuwa wametatanika. Baada ya kukusanya maushirikina zaidi ya elfu mbili, wao walipata kuona woga wa kiushirikina ule ule katika Uskochi, India, na Uganda, na katika Amerika ya Kati pia. Wao walijiuliza, ‘Ni jambo gani lingeweza kusababisha hili?’ Mwandikaji Robertson Davies kwa usahihi alieleza hivi: “Ushirikina unaonekana kuwa na kiunganishi fulani pamoja na fungu la itikadi fulani ambalo hutangulia kwa mbali zile dini tunazojua sisi.” Basi, ni “fungu la itikadi” gani la kabla ya Ukristo ambalo ndilo mzizi wa ushirikina?
Mzizi na Matawi ya Ushirikina
Biblia huelekeza kwenye nchi ya Shinari (lile eneo lililo katikati ya Mito Tigiri na Eufrate, baadaye likaitwa Babulonia) kuwa mahali pa uzaliwa wa mawazo ya dini yasiyo ya kweli, kutia na ushirikina. Huko, “mwindaji mwenye nguvu” aliyeitwa Nimrodi alianza ujenzi wa ule Mnara wa Babeli wenye sifa mbaya. Ulikuwa utumiwe kwa ajili ya ibada isiyo ya kweli. Yehova Mungu, ingawa hivyo, alitatiza mipango hiyo ya wajenzi kwa kuvuruga lugha yao. Polepole ile kazi ya ujenzi ilisimamishwa, na wao wakatawanywa. (Mwanzo 10:8-10, NW; 11:2-9) Lakini po pote pale walipolowea, wao walienda pamoja na itikadi, mawazo, na hadithi za uwongo zile zile. Babeli, hata hivyo, ulibaki ukiwa kitovu cha dini isiyo ya kweli, na baada ya wakati pia ukapanua fungu lao ukiwa mama na mlezi kwa uganga, uchawi, na itikadi za kiushirikina kama vile unajimu. (Linganisha Isaya 47:12, 13; Danieli 2:27; 4:7.) Hivyo, kitabu Great Cities of the Ancient World kinatoa elezo hili: “Unajimu ulikuwa na msingi wao juu ya mawazo mawili ya Kibabuloni: ile zodiaki, na ule uungu wa ile miili ya kimbingu. . . . Wababuloni walizihesabia sayari sifa ya kuwa na nguvu ambazo mtu angetazamia miungu yao mmoja mmoja iwe nazo.”
Matukio hayo ya kale yametuathirije sisi? Kile kitabu cha Biblia cha Ufunuo kinaonyesha kwamba mfumo wa ulimwenguni pote, wa dini isiyo ya kweli umesitawi kutokana na mawazo hayo ya Babuloni ya kale. Umekuwapo mpaka siku yetu na unaitwa ‘Babuloni Mkuu.’ (Ufunuo 17:5, HNWW) Bila shaka, kupita kwa wakati na maendeleo ya mahali mahali yamekuwa na uvutano juu ya mawazo hayo ya kwanza kabisa ya Kibabuloni. Ile tofauti kubwa ya dini inayoonwa leo ndiyo tokeo. Lakini kama vile miti yenye utofautiano mara nyingi hukua katika udongo ule ule, ndivyo dini zenye utofautiano na ushirikina kuzunguka ulimwengu zilivyo na mizizi yayo katika ardhi moja—Babuloni. Kutoa kielezi, acheni sisi tuone jinsi mojapo itikadi za kiushirikina za Babuloni imepenya polepole ndani ya karibu dini zote za ulimwengu leo.
Woga wa Wafu—Msingi Ni Nini?
Wababuloni waliitikadi kwamba sehemu ya kiroho ya mtu huokoka kifo cha mwili wa nyama na ingeweza kurudi kuathiri walio hai kwa mema au kwa mabaya. Hivyo wao walibuni sherehe za kidini zilizokusudiwa kuwatuliza wafu na kuepuka kisasi chao. Itikadi hii ingali hai katika nchi nyingi leo. Katika Afrika, kwa mfano, hiyo “inatenda fungu la muhimu katika maisha ya kila siku ya karibu kila . . . jamii.”—African Religions—Symbol, Ritual, and Community.
Hata wale wanaodai kuwa Wakristo katika nchi hizo wanaathiriwa. Mathalani, Henriette, mwanamke wa umri wa miaka 63 wa asili ya Kiafrika, anakubali hivi: “Ijapokuwa mimi nilikuwa mshiriki mtendaji wa kanisa la Protestanti la kwetu, mimi niliogopa zile ‘roho’ za wafu. Sisi tuliishi karibu na maziara, na wakati wo wote mwandamano wa mazishi ulipokaribia nyumba yetu, mimi niliamsha mtoto wangu na kumkumbatia mpaka ule mwandamano ulipokuwa umepita. La sivyo, ile ‘roho’ ya mfu ingeingia ndani ya nyumba yangu na kumpagaa mtoto anayelala.”
Ushirikina kama huo unaendelea kuwako, kwa sababu lile fundisho la nafsi isiyokufa limeenea sana katika Jumuiya ya Wakristo. Historia inaonyesha kwamba wanafalsafa Wagiriki—hasa Plato—walikuza wazo la Kibabuloni la kutokufa. Chini ya uvutano wao, anaandika John Dunnett, mhadhiri wa theolojia wa cheo cha juu Uingereza, “lile wazo la kutokufa kwa nafsi likaja kuenea sana ndani ya Kanisa la Kikristo.” Fundisho hili la Kibabuloni limeweka mamilioni katika utumwa wa woga wa kiushirikina.
Dini ya kweli, hata hivyo, inafukuzia mbali woga kama huo. Kwa sababu gani? Kwa sababu dini ya kweli msingi wayo si itikadi ambazo mzizi wayo umo katika Babuloni bali katika mafundisho yanayopatikana katika Biblia.
Nafsi Kulingana na Biblia
Kile kitabu cha kwanza cha Biblia kinatuambia kwamba mtu akawa nafsi, mtu anayeishi. (Mwanzo 2:7) Kwa hiyo, wakati mtu anapokufa, nafsi inakufa. Anathibitisha hivyo yule nabii Ezekieli: “Ile nafsi inayofanya dhambi—hiyo yenyewe ndiyo itakayokufa.” (Ezekieli 18:4, NW; Warumi 3:23) Nafsi ni yenye kufa na haiendelei kuishi baada ya kifo. Badala ya hivyo, kama Zaburi 146:4 inavyosema: “Pumzi [roho, NW] yake hutoka, huurudia udongo wake, siku hiyo mawazo yake yapotea.” Kwa sababu hiyo, mhadhiri John Dunnett anakata maneno hivi, kutokufa kwa nafsi “kunabaki kuwa itikadi isiyo ya Kibiblia.”
Ikiwa hakuna. nafsi isiyokufa, hakuwezi kuwa na “roho” za wafu za kuogofya watu duniani. Hivyo ule msingi wa woga wa wafu wa kiushirikina unabomoka.
Woga Ambao Msingi Wao Ni Udanganyifu
Woga wa wafu wa kiushirikina ni vigumu kuuondoa. Kwa sababu gani? Kwa sababu mambo yenye kuogopesha yanatukia—kama usiku ule, wakati mwanamke wa makamu katika Suriname aliposikia mtu fulani akiita jina lake. Yeye alipuuza jambo hilo, lakini ndipo “mikono” isiyoonekana ikaanza kumgusa-gusa na wakati alipopinga jambo hilo, yeye alikaribia kunyongwa na kani isiyoonekana. Pengine wewe unajiuliza, ‘Ikiwa “roho” za wafu haziko hai, basi ni nani aliyehusika?’ Tena, maarifa ya Biblia yanamaliza woga wa kiushirikina.
Hiyo inaeleza kwamba kuna kani mbovu za kiroho, zinazoitwa mashetani. Mashetani hao, hata hivyo, si nafsi zilizoondoka. Wao ni malaika za Mungu ambao waliasi na kujiweka upande wa Shetani, ambaye ‘anapoteza dunia nzima inayokaliwa na watu.’ (Ufunuo 12:9, NW; Yakobo 2:19; Waefeso 6:12; 2 Petro 2:4) Biblia inaonyesha kwamba hao mashetani wanapata furaha katika kupoteza, kuogopesha, na kusumbua wanadamu. Lile simulizi kwenye Luka 9:37-43 hueleza jinsi shetani mmoja alivyoangusha chini mvulana mmoja na ‘kumtia kifafa, huku akitokwa na povu,’ na kumtaabisha kwa kumchubua-chubua. Hata wakati mvulana huyo alipoletwa kwa Yesu, yule “pepo akambwaga chini, akamtia kifafa.” Hata hivyo, lile simulizi linaendelea, “Yesu akamkemea pepo mchafu, akamponya mtoto, akamrudishia babaye.”
Kwa kupendeza, Cyclopedia of Biblical, Theological, and Ecclesiastical Literature hufasiri ushirikina kuwa “ile ibada ya miungu isiyo ya kweli.” Hivyo, ikiwa wewe unafanya vitendo kama hivyo vya kiushirikina, wewe pengine hata bila kujua, unatuliza “miungu isiyo ya kweli,” au wale mashetani! Ibada kama hiyo isiyo ya kweli ni kosa kubwa dhidi ya Yehova Mungu.—Linganisha 1 Wakorintho 10:20 na Kumbukumbu 18:10-12.a
‘Jitiisheni Wenyewe kwa Mungu’—Je! Wewe Unafanya Hivyo?
Je! wewe ungeweza kuwa na ushujaa wa kuwapa kisogo hao mashetani kwa kukataa ushirikina? Ni kweli, mashetani ni wenye nguvu nyingi. Lakini baada ya kuonyesha kwamba sisi sharti tuchague kati ya kumtumikia Yehova Mungu au mashetani, mtume Paulo aliuliza hivi: “Je! [sisi] tuna nguvu zaidi ya [Yehova]?” (1 Wakorintho 10:21, 22) Hapana, sisi hatuna nguvu zaidi yake—lakini kumbuka, wala Shetani na mashetani wake hawana nguvu zaidi yake! Badala ya hivyo, hao mashetani ‘hutetemeka’ kwa kumwogopa sana Yehova. (Yakobo 2:19) Bali yule Mungu Mwenye Nguvu Zote hukutolea wewe himaya yake ikiwa wewe unaiomba. Mwandikaji wa Biblia Yakobo anasema zaidi hivi: “Jitiisheni wenyewe, basi, kwa Mungu; bali pingeni yule Ibilisi, na yeye atakimbia kutoka kwenu ninyi.” (Yakobo 4:7, NW) Woga wako wa kiushirikina hali kadhalika utakimbia.
Maelfu kuzunguka tufe ambao wakati mmoja waliishi katika woga na utumwa kwa desturi za kiushirikina wanaweza sasa kushuhudia jambo hilo. Ibilisi alikimbia kutoka kwao! Katika njia gani? Kumbuka, adui ya woga wa kiushirikina ni maarifa. Asema Profesa Rudolph Brasch, mtaalamu wa mwanzo wa maushirikina: “Ni jambo linalohusu elimu—kwamba kadiri watu wanavyopata kuelimika zaidi, ndivyo wanavyokuwa wenye ushirikina kwa kadiri ndogo zaidi.”
Hivyo, wakati Henriette, aliyetajwa mbeleni, alipokubali mwaliko wa Mashahidi wa Yehova aanze funzo la Biblia la bure, upesi yeye akaacha kudanganywa na hila ya kishetani. Yale makucha ya ushirikina yakapoteza mbano wayo. Mwanamke huyo, na maelfu wengi kama yeye, wameuona ukweli wa yale maneno kwenye Waebrania 2:15. Ambapo mtume Paulo anasema kwamba Yesu ‘ataweka huru wale ambao maisha yao yote walishikwa katika utumwa kwa woga wao wa kifo.’ (New International Version) Kama vile jua la asubuhi la kitropiki hutowesha umande mzito wa msitu wenye mvua, nuru ya ukweli wa Biblia hufukuzia mbali woga wote wa kiushirikina.
Leo, wengi waliokuwa hapo kwanza ‘watumwa wenye woga’ wameondoa hirizi kutoka shingo zao na kamba zenye kutoa himaya kutoka kwa watoto wao. Sasa wao wanahisi kama alivyohisi Isaka mwenye umri wa miaka 68 wa Afrika Kusini ambaye hapo kwanza alikuwa mchawi. Baada ya kujifunza Biblia pamoja na Mashahidi wa Yehova, yeye alipaaza sauti hivi: “Mimi nahisi nikiwa mwenye furaha na huru sana kwa sababu mimi silemewi tena na mzigo wa woga wa maroho.” Maneno ya Yesu yamethibitika kuwa kweli kama nini: “Mtaifahamu kweli, nayo hiyo kweli itawaweka huru.”—Yohana 8:32.
Ndiyo, dini ya kweli inafukuzia mbali woga!
[Maelezo ya Chini]
a Tafsiri fulani za Biblia (Mathalani, King James Version, Douay, The Comprehensive Bible) hutumia neno “ushirikina” kwenye Matendo 25:19 kufasiri neno la Kigiriki dei·si·dai·mo·niʹas, kumaanisha “hofu ya mashetani.” Ona pia New World Translation Reference Bible maelezo ya chini.
[Picha katika ukurasa wa 5]
Maushirikina yalisambaa ulimwenguni pote kutoka chemchemi zao katika Babuloni