Kuthibitisha Masimulizi Hayo
WATU huitikia masimulizi ya kisasa ya kukutana na malaika kwa njia kadhaa. Kwanza, kuna wale wanaoamini. Wao husababu kwamba kwa kuwa masimulizi hayo ni mengi sana na yameenea kote, lazima yawe ya kweli. Pili, kuna wale wenye shuku. Wanasema kwamba hakuna ushuhuda thabiti wa kuunga mkono madai hayo. Wanabisha kwamba kuenea kote kwa itikadi fulani hakuifanyi iwe ya kweli. Kwa vyovyote, wakati fulani watu waliitikadi nguva jike. Tatu, kuna wale wasiounga mkono upande wowote. Kitabu Angels—Opposing Viewpoints kinapozungumza juu ya kutounga mkono huku, chataarifu: “Watu wengi hudai kuwa wameona malaika. Madai hayo hayawezi kuthibitishwa; hufuatwa kwa imani. Hata hivyo, watu wenye shuku hawawezi kuyapinga, na wachache hujaribu.”
Watu wengi hukubali kwamba Biblia ni chanzo kinachotegemeka cha habari juu ya makao ya roho.a Yaweza kutusaidia kuchanganua masimulizi ya kisasa juu ya malaika. Kama ambavyo huenda ukajua, Biblia hutuhakikishia kwamba malaika ni viumbe wa kiroho walio halisi, wenye nguvu nyingi, na wenye utukufu. Biblia ina masimulizi ya malaika wakipeleka ujumbe na kuwaokoa watumishi wa Mungu kutokana na madhara.—Zaburi 104:1, 4; Luka 1:26-33; Matendo 12:6-11.
Biblia huonyesha pia kwamba kuna malaika waovu. Viumbe hawa wa kiroho hudanganya na kuwaongoza vibaya wanadamu, wakiwatenganisha na Mungu. (2 Wakorintho 11:14) Ni kwa sababu nzuri kwamba Biblia hutahadharisha hivi: “Msiamini kila usemi uliopuliziwa, lakini jaribuni semi zilizopuliziwa ili kuona kama hizo zatokana na Mungu.” (1 Yohana 4:1) Kwa mfano, kabla hatujaamini utabiri wa mtu anayejiita nabii, kwa hekima tungelinganisha yale anayosema na Neno la Mungu, ambalo huenda anadai kuwakilisha. Kwa kweli, twapaswa kutarajia masimulizi ya kisasa ya kuonekana kwa malaika yathibitishwe kwa uchunguzi uohuo. Hivyo basi, masimulizi ya kisasa ya kukutana na malaika yanalinganaje na rekodi ya Maandiko?
Malaika Hawapatani na Itikadi ya Wengi
Acheni tuanze kwa kusahihisha maoni mawili yenye kosa yaliyoenea kote juu ya malaika. Kinyume cha itikadi ya watu wengi, malaika hawakuwa wanadamu mwanzoni. Waliishi mbinguni muda mrefu kabla Mungu hajaumba uhai duniani. Biblia husema kwamba Mungu ‘alipoiweka misingi ya nchi . . . , wana wote [wa kimalaika] wa Mungu walipiga kelele kwa furaha.’—Ayubu 38:4-7.
Maoni mengine ya kisasa yenye kosa ni kwamba malaika ni waendekevu na wenye kuvumilia matendo yenye kosa. Badala yake, malaika waaminifu hutegemeza viwango vya Mungu vya uadilifu na hutenda kupatana na mwelekezo wake. Wao humtumikia Mungu, si wanadamu.—Zaburi 103:20.
Malaika Wanapendezwa na Hali Yetu Njema ya Kiroho
Miongoni mwa masimulizi ya kisasa juu ya malaika, kuna masimulizi mengi kuhusu kuokoa. Katika kitabu kimoja kinachouzwa sana, twasoma juu ya msichana mdogo anayetolewa kutoka kwa nyumba inayoteketea na mkono usioonekana. Kitabu kingine kinaeleza juu ya wanafunzi wawili wa chuo wanaokwama wakati wa dhoruba kali ya theluji. Kwa ghafula, lori linatokea na kuvuta gari lao kwa usalama, na bado haliachi alama za magurudumu! Penginepo, pana simulizi jingine juu ya Ann, anayeugua kansa. Siku tatu kabla ya kulazwa hospitalini kwa ajili ya upasuaji, mtu mrefu asiyejulikana anafika mlangoni pake. Asema anaitwa Thomas na kwamba ametumwa na Mungu. Thomas aunyoosha mkono wake, na Ann anahisi mwanga mweupe wenye joto ukipita mwilini mwake. Afikapo hospitalini kwa upasuaji, madaktari wanapigwa na butaa. Kansa aliyokuwa nayo imepona!
Masimulizi haya huzusha swali la wazi, Ikiwa kila mtu ana malaika mlinzi, kwa nini watu fulani huokolewa, ilhali wengi hawaokolewi? Mamilioni yasiyohesabika wamekufa kutokana na maradhi, vita, njaa kuu, na misiba ya kiasili. Kwa hakika, wengi wao walisali kwa bidii ili kupata msaada. Mbona malaika mlinzi hakuwaokoa?
Biblia hujibu swali hilo. Huonyesha kwamba Mungu hana ubaguzi. (Matendo 10:34) Zaidi ya hayo, ingawa malaika waaminifu wa Mungu wanapendezwa na hali yetu njema ya kimwili, wanapendezwa zaidi na hali yetu njema ya kiroho. Mtume Paulo alidokeza hivi kwa njia ya swali: “Je, wao [malaika] wote si roho kwa ajili ya utumishi wa watu wote, waliotumwa kuwahudumia wale watakaorithi wokovu?” (Waebrania 1:14) Msaada wa kimwili huleta manufaa ya muda, lakini msaada wa kiroho waweza kuleta manufaa ya milele.
Masimulizi mengi juu ya malaika huonekana kuwa yasiyo ya maana. Yasemekana kwamba malaika humsaidia mama aliyechoka kubadili shuka kitandani, humkumbusha mnunuzi anunue viberiti, na huwasaidia madereva kupata mahali pa maegesho. Mwanamke mmoja kijana huko Scotland asema hivi kwa kicheko: “Kwa majuma matatu yaliyopita nimekuwa nikiegesha gari langu kwenye mstari wa manjano katika St. Mary’s Street na kumwomba malaika wangu alizingire kwa upendo na huruma. Endapo askari yeyote wa barabarani atalikaribia atashikwa kabisa na hisia za upendo hivi kwamba hatalitoza ada ya kuegesha. Sijawahi kamwe kutozwa ada ya kuegesha.” Si ajabu kwamba watu wengi hulinganisha malaika mlinzi wa kisasa na rafiki mkarimu au na Baba Krismasi wa watu wazima.
Malaika Waaminifu Hawapingi Neno la Mungu
Vitabu juu ya malaika vimejaa semi na mashauri yanayoonwa kuwa yametoka kwa makao ya roho. Mathalani, kitabu kimoja kinadai kwamba kina mafundisho yaliyowasilishwa na malaika mkuu Mikaeli kwa mwanamke fulani huko Colorado, Marekani. Mojawapo ya “semi” zitokazo kwa Mikaeli ni hii: “Barabara zote zinaongoza kwa Mungu. Itikadi zote, kweli zote zenye nuru huongoza kwa Mungu.” Tofauti na semi hiyo, Yesu alisema kwamba kuna barabara mbili tu za kidini na kwamba ni moja pekee inayoongoza katika kupata kibali cha Mungu na uhai udumuo milele. Ile nyingine huongoza katika kupoteza kibali na katika uharibifu wa milele. (Mathayo 7:13, 14) Kwa wazi, semi hizi mbili haziwezi kuwa za kweli zote.
“Malaika” wa “hali mpya ya kiroho” husema nini juu ya ndoa na adili? Katika kitabu kimoja msomaji husoma juu ya Roseann, aliyeambiwa hivi na “malaika” wake: “Ungali una watu wengi wa kuwasiliana nao, na maisha yako hayategemei tena kuwa na [mume wako]. Wampenda naye akupenda, lakini ni wakati wa kuachana.” Alipata talaka. Lakini, Biblia huonyesha kwamba Mungu anachukia kutaliki pasipo msingi unaofaa. (Malaki 2:16) Simulizi jingine hueleza kuhusu wenzi wanaofanya uzinzi, wakiamini kwamba malaika hushangilia jambo hilo na kwamba huwazingira kwa njia ya pekee. Lakini Biblia husema: “Usizini.”—Kutoka 20:14.
Je, yaweza kuwa kwamba jumbe hizi za kisasa zinaifanya Biblia iwe ya kisasa? La, Neno la Mungu halibadiliki. Mtume Paulo aliwaandikia hivi watu fulani katika karne ya kwanza: “Mimi nastaajabu kwamba mnakuwa mkiondolewa upesi hivyo kutoka kwa Yule aliyewaita nyinyi kwa fadhili isiyostahiliwa ya Kristo hadi kwenye namna nyingine ya habari njema. Lakini si nyingine; ila tu kuna watu fulani wanaowasababishia nyinyi taabu na kutaka kupotosha habari njema juu ya Kristo. Lakini, hata ikiwa sisi au malaika kutoka mbinguni tungewatangazia nyinyi kuwa habari njema jambo fulani kupita lile tulilowatangazia nyinyi kuwa habari njema, acheni alaaniwe.”—Wagalatia 1:6-8.
“Kuwaomba Malaika Wote!”
Je, twapaswa kuwaomba malaika watupe msaada wa kushughulikia matatizo na hatari maishani? Hicho ndicho kichwa kikuu cha vitabu vingi. Hapa pana mifano miwili. Kitabu Ask Your Angels husemekana kuwa kinawaonyesha wasomaji ‘jinsi wawezavyo kutumia nguvu kutoka kwa malaika ili kuweza kuelewa tena hisia zao za kiasili zisizoeleweka na kufikia miradi yao.’ Kitabu kinachofanana na hicho chaitwa Calling All Angels!: 57 Ways to Invite an Angel Into Your Life.
Hata hivyo, Biblia haitutii moyo kamwe tuwaombe malaika. Yesu alidhihirisha jambo hilo katika sala ya kigezo. Alisema: “Basi, nyinyi lazima msali kwa njia hii: “‘Baba yetu uliye katika mbingu . . . ’” (Mathayo 6:9) Vivyo hivyo, mtume Paulo aliandika: “Katika kila jambo kwa sala na dua pamoja na utoaji-shukrani acheni maombi yenu ya bidii yajulishwe kwa Mungu.”—Wafilipi 4:6.
Katika Jina la Malaika
“Hali mpya ya kiroho” hukazia umuhimu wa kujifunza majina ya malaika. Vitabu vinavyopendwa sana hutoa majina yanayokisiwa ya maelfu ya malaika. Kwa nini? Si kwa sababu tu ya kutuliza tamaa ya udadisi; kusudi waweze kuitwa. Hilo huhusiana sana na mzungu. Kitabu Encyclopedia of Angels chataarifu kwamba pamoja na desturi, vifaa vya kimizungu, na maombi, “kutumia ‘majina yenye nguvu,’ au majina ya roho mahususi, hutokeza nguvu za ajabu zinazoruhusu utendaji kati ya makao ya kimwili na makao ya roho, na humwezesha mfanya-mizungu . . . awasiliane na roho.” Lakini, Biblia hutaarifu waziwazi: ‘Msitumie uaguzi.’—Mambo ya Walawi 19:26, Zaire Swahili Bible.
Biblia yenyewe hufunua majina ya malaika wawili tu waaminifu, Mikaeli na Gabrieli. (Danieli 12:1; Luka 1:26) Kwa kutaja majina haya, Biblia huonyesha kwamba malaika ni watu wa kiroho wa pekee. Kwa nini majina zaidi hayakutajwa? Yaelekea kwamba ni kwa sababu ya kuzuia watu kukweza malaika kwa wadhifa wa heshima wasiyostahili—heshima ambayo hata malaika wenyewe hawatamani kupokea. Hivyo, Yakobo alipomwomba malaika amwambie jina lake, malaika huyo alikataa. (Mwanzo 32:29) Baadaye, malaika aliyemtokea Yoshua alijitambulisha si kwa jina bali kuwa “amiri wa jeshi la BWANA.” (Yoshua 5:14) Vivyo hivyo, babaye Samsoni alipomuuliza jina malaika mmoja, alimwambia: “Kwani wewe kuniuliza jina langu, kwa kuwa jina hilo ni la ajabu?” (Waamuzi 13:17, 18) Malaika waaminifu wa Mungu wanataka tumheshimu Mungu na kumwomba yeye, si wao.
[Maelezo ya Chini]
a Kwa habari inayoonyesha kwa nini Biblia ni chanzo kinachotegemeka, ona broshua Kitabu kwa Ajili ya Watu Wote, kilichochapishwa na Watchtower Bible and Tract Society of New York
[Blabu katika ukurasa wa 6]
“Kwa wale wanaohisi kwamba wanazuiwa sana na Mungu na sheria zake, . . . malaika wa [Enzi Mpya] ndio wanaoridhiana . . . ni wenye fadhili, si wenye kuhukumu. Nao waweza kufikiwa kwa urahisi
[Sanduku katika ukurasa wa 5]
Visa vya Kisasa vya “Kukutana” na Malaika na Viumbe Wasiotambuliwa wa Angani
Watu wengi leo hudai kwamba wameshaona malaika na kuzungumza nao. Wengine husema kwamba wamepata kukutana na viumbe wasiotambuliwa kutoka ulimwengu mwingine. Kitabu Angels—An Endangered Species huorodhesha ufanani kati ya masimulizi haya, kikidai kwamba yote yaweza kuwa na fasili moja.b Ufuatao ni muhtasari wa baadhi ya ufanani ulioorodheshwa katika kitabu hicho.
1. Malaika na viumbe wasiotambuliwa hutoka katika ulimwengu mwingine.
2. Wote ni viumbe bora, ama kiroho ama kitekinolojia.
3. Jamii yenye urafiki kati yao huonekana ikiwa na ujana na yenye umbo maridadi, na ni yenye fadhili na huruma nyingi.
4. Hawana tatizo la lugha, wao husema kwa ufasaha lugha ya msikilizaji.
5. Wote ni stadi wa kuruka hewani.
6. Malaika na viumbe wasiotambuliwa huonekana wakiwa na nuru nyangavu.
7. Wote huonekana wakiwa na mavazi kamili, kwa kawaida wanavaa kanzu au makoti marefu yenye kubana. Wanapenda mavazi ya rangi nyeupe au ya buluu.
8. Kwa kawaida wote huwa na kimo sawa na wanadamu.
9. Wote huhangaikia hali mbaya ya wanadamu na sayari yao.
10. Uthibitisho wa kukutana na malaika au na viumbe wasiotambuliwa ni ushuhuda wa mtu aliyewaona.
[Maelezo ya Chini]
b Maelezo ya kawaida kuhusu masimulizi yote mawili ni kwamba roho waovu, au mashetani, kwa wazi ndio wanaohusika katika visa hivyo vya “kukutana.” Ni kama Biblia inavyosema, “Shetani mwenyewe hufuliza kujigeuza umbo mwenyewe kuwa malaika wa nuru.” (2 Wakorintho 11:14)—Ona Amkeni!, Julai 8, 1996, ukurasa wa 26.
[Picha katika ukurasa wa 7]
Biblia ina masimulizi ya kweli ya malaika wakiwatokea watu