Ukweli Kuhusu Malaika
KAMA tulivyokwisha kuona, hoja zinazopendwa na masimulizi juu ya malaika hayapatani na mafundisho ya Biblia sikuzote. Je, tofauti iliyopo yahitaji kuchunguzwa? Je, kuna tatizo lolote kufuata itikadi zinazopendwa juu ya malaika? Bila shaka.
Kwa mfano, fikiria mitazamo inayotokezwa na ile “hali mpya ya kiroho.” Vitabu vya kisasa juu ya malaika hutia moyo kukubali tu kila jambo kama mtoto, wala si kutumia uwezo wa kufikiri. Ni nadra sana kwa wasomaji kutiwa moyo watatue matatizo yao au wapate kuelewa Biblia na ujuzi juu ya Mungu. Vitabu juu ya malaika hutuhakikishia kwamba tuna malaika mwanana na mwenye upendo anayetusaidia maishani na kwamba hatuna sababu ya kuhofu, kwa kuwa twaishi katika ulimwengu wenye furaha ambamo kila jambo ni sawa. Tatizo linapozuka, twapaswa kusubiri tu ili malaika walitatue. Hata hivyo, ikiwa ndivyo ilivyo, kwa nini Biblia hutuambia ‘tufanye pigano kali kwa ajili ya imani’?—Yuda 3.
Vitabu vingi juu ya malaika hukuza kiburi cha wanadamu na ubatili. Vinakazia masilahi ya mtu mwenyewe. Kulingana na vitabu hivyo, malaika wa siku ya kisasa hutaka tufahamu jinsi tulivyo wazuri na wenye furaha. Ijapokuwa ni vizuri kuwa na maoni yanayofaa juu yetu wenyewe, habari kuu ya “hali mpya ya kiroho” ni kujipenda wenyewe pasipo masharti. Mtungaji mmoja asema kwamba amri ya kwanza iliyo kubwa zaidi sana ni “kujipenda Mwenyewe ukiwa Bwana.” Jinsi ambavyo maneno hayo hupingana na maneno ya Yesu! Alisema: “Lazima umpende Yehova Mungu wako kwa moyo wako wote na kwa nafsi yako yote na kwa akili yako yote. Hii ndiyo amri kubwa zaidi sana na ya kwanza.” (Mathayo 22:36-39) Tutakuwa wenye furaha zaidi maishani ikiwa tutatafuta masilahi ya Mungu mbele ya masilahi yetu.
Kukazia malaika uangalifu ni kinyume cha Ukristo wa kweli. Mtume Paulo alishutumu ibada ya malaika. (Wakolosai 2:18) Kuabudu humaanisha “kuheshimu au kustahi kama mtu wa kimungu au nguvu zinazozidi zile za kibinadamu.” Na bado, vitabu vingi juu ya malaika vinavyopendwa sana kwa kweli huwatia moyo wasomaji waheshimu na kustahi malaika. Ingawa hivyo, kumbuka lililotukia Shetani alipomwomba Yesu amfanyie tendo moja la ibada. Yesu alijibu: “Ni Yehova Mungu wako ambaye lazima uabudu, na ni kwake peke yake lazima utoe utumishi mtakatifu.” (Luka 4:8) Baadaye, mtume Yohana alipoanguka chini mbele ya malaika, malaika huyo alimwambia hivi: “Uwe mwangalifu! Usifanye hivyo! Mimi ni mtumwa tu mwenzako na wa ndugu zako walio na kazi ya kutoa ushahidi kuhusu Yesu. Abudu Mungu.”—Ufunuo 19:10.
Jinsi Malaika Wanavyoweza Kukusaidia
Wapaswa kumfikia Mungu ili upate mwongozo na msaada, si malaika. Yeye yu tayari na anafurahi kuwaonyesha upendo wale wote wanaojipatanisha na matakwa yake ya uadilifu. Mtume Yohana aliwaandikia hivi Wakristo wenzake: “Na huu ndio uhakika ambao tunao kumwelekea yeye, kwamba, hata iwe ni nini ambacho twaomba kulingana na mapenzi yake, yeye hutusikia. Zaidi, ikiwa twajua yeye hutusikia kwa habari ya chochote kile tunachoomba, twajua tutakuwa na mambo yaliyoombwa kwa kuwa tumeyaomba kwake.”—1 Yohana 5:14, 15.
Kuna mambo mengi tusiyoyajua juu ya malaika waaminifu wa Mungu. Hata hivyo, twajua kwamba wanamtumikia Mungu, wakitenda kwa kupatana na kusudi lake na mwelekezo wake. Wana hamu ya kueneza ukweli kuhusu Mungu. (Ufunuo 14:6, 7) Hawatamani tuwaabudu. Kwa kuwa hatuwezi kuwaona, hatujui ni kadiri gani Mungu huwatumia ili kuwasaidia watu wake katika shughuli za kila siku. Lakini twajua kwamba Yehova Mungu huwalinda na kuwaelekeza watu wake wakiwa kikundi.
Malaika wanatuwekea kielelezo bora kama nini cha uaminifu! Wanamtukuza na kumsifu Mungu. (Zaburi 148:2) Ijapokuwa wana uwezo mkubwa sana wa kiakili na kiroho, wao hustahi sana enzi kuu ya Yehova. (Yuda 9) Wanapendezwa kwa umakini na kutimizwa kwa kusudi la Mungu. (1 Petro 1:11, 12) Tunajifunza mambo haya katika Neno la Mungu, Biblia. Naam, Biblia ndicho kitabu kinachotueleza ukweli kuhusu malaika.
[Blabu katika ukurasa wa 10]
Malaika wana hamu ya kueneza ukweli kuhusu Mungu
[Picha katika ukurasa wa 8, 9]
Mtume Yohana alipojaribu kumwabudu malaika, malaika huyo alisema: “Usifanye hivyo!”