Je, Inapatana na Akili Kuamini Kwamba Kuna Mungu?
JE, UMEWAHI kujiuliza kwa nini kila kitu, kuanzia chembe ndogo za atomi kufikia makundi makubwa sana ya nyota yanaongozwa na sheria hususa za hisabati? Je, umefikiria kuhusu uhai wenyewe—unamna-namna uliopo, utata wake, na ubuni wake wenye kustaajabisha? Watu wengi husema kwamba ulimwengu wote pamoja na uhai ulio ndani yake ulitokea kupitia aksidenti kubwa angani au kupitia mageuzi. Wengine husema ulitokezwa na Muumba mwenye akili. Kwa maoni yako, ni wazo gani linalopatana na akili?
Kwa kweli, yote mawili yanategemea imani. Kumwamini Mungu kunategemea imani. Kama Biblia inavyosema, “hakuna mwanadamu ambaye amemwona Mungu wakati wowote.” (Yohana 1:18) Vivyo hivyo, hakuna mwanadamu aliyeona ulimwengu ulipokuwa ukifanyizwa au hata uhai ulipokuwa ukianza. Wala hakuna mtu ambaye amewahi kuona uhai wa aina moja ukigeuka na kuwa mwingine bora zaidi, au hata kuwa uhai wa aina tofauti. Rekodi ya vitu vya kale vilivyochimbuliwa inaonyesha kwamba jamii kubwa za wanyama zilitokea wakati mmoja na hazijabadilika.a Kwa hiyo, swali la maana hapa ni: Ni imani gani yenye msingi imara—imani katika mageuzi au imani katika Muumba?
Je, Imani Yako Inategemea Uthibitisho Wenye Nguvu?
Biblia inasema kwamba “imani” ya kweli ni “uthibitisho ulio wazi wa mambo halisi ingawa hayaonekani.” (Waebrania 11:1) Mstari huo katika Biblia Habari Njema unasema hivi: “Imani ni . . . kusadiki kabisa mambo tusiyoyaona.” Bila shaka, kuna mambo fulani halisi yasiyoonekana ambayo unaamini kabisa kwamba yako.
Kwa mfano: Wanahistoria wengi wenye kuheshimika wanaamini kwamba Aleksanda Mkuu, Kaisari Yulio, na Yesu Kristo waliishi wakati fulani. Je, imani ya wanahistoria inapatana na akili? Bila shaka, kwa kuwa wanaweza kuonyesha uthibitisho hakika wa kihistoria.
Wanasayansi pia wanaamini mambo halisi yasiyoonekana kwa sababu kuna “uthibitisho ulio wazi” kwamba mambo hayo yako. Kwa mfano, Dmitry Mendeleyev, mwanakemia Mrusi aliyeishi karne ya 19 alipendezwa na uhusiano uliopo kati ya elementi, yaani vitu vinavyofanyiza ulimwengu. Alitambua kuwa elementi hizo zilikuwa na vitu fulani vinavyofanana na vinavyoweza kupangwa kulingana na uzito wa atomi na kemikali zinazoifanyiza. Kwa sababu aliamini mpangilio wa vikundi hivyo, alitokeza jedwali ya elementi na kutabiri kwa usahihi kuwepo kwa elementi kadhaa ambazo hazikujulikana wakati huo.
Wataalamu wa vitu vya kale huamua mambo kuhusu watu wa nyakati za kale, mara nyingi kwa kutegemea vitu vilivyokuwa vimezikwa kwa maelfu ya miaka. Kwa mfano, hebu wazia kwamba mtaalamu fulani amechimbua mawe mengi yaliyokatwa kwa uangalifu sana yenye ukubwa uleule yakiwa yamepangwa kwa uangalifu sana moja juu ya nyingine. Pia, yamepangwa kwa umbo fulani ambalo haliwezi kujitokeza lenyewe. Mtaalamu huyo atafikia mkataa gani? Je, atasema kwamba mawe hayo yalijipanga yenyewe tu? Huenda asiseme hivyo. Badala yake, atafikia mkataa kwamba yalipangwa na wanadamu wa nyakati za kale, na huo ndio mkataa unaopatana na akili.
Je, hatupaswi kufikiri kwa njia hiyohiyo tunapoona ubuni uliopo katika vitu vya asili? Watu wengi wamefikiria kwa njia hiyo kutia ndani wanasayansi wenye kuheshimika.
Ulijitokeza Wenyewe au Ulibuniwa kwa Kusudi?
Miaka kadhaa iliyopita, Sir James Jeans, mwanahisabati, mwanafizikia, na mtaalamu wa nyota nchini Uingereza, aliandika kwamba kwa sababu ya maendeleo katika ujuzi wa kisayansi, “inaonekana kwamba ulimwengu ulitokezwa na akili yenye nguvu badala ya kuonekana kama mashini kubwa.” Pia alisema kwamba “ulimwengu unaonekana kuwa ulibuniwa na mwanahisabati stadi” na hilo linatoa “uthibitisho wa kwamba kuna nguvu fulani yenye uwezo wa kubuni au yenye nguvu za kudhibiti mambo ina kitu fulani kinachofanana na akili zetu.”
Wanasayansi wengine wamefikia mkataa kama huo tangu Jeans aandike maneno hayo. “Mpangilio ulio katika ulimwengu wote umewafanya wataalamu wengi wa nyota wafikiri kwamba ubuni ulihusika katika kutokea kwa ulimwengu,” akaandika mwanafizikia Paul Davies. Albert Einstein, mmoja kati ya wanafizikia na wanahisabati maarufu zaidi, aliandika hivi: “Ni muujiza kwamba tunaweza kuuelewa [ulimwengu wa asili].” Kwa maoni ya wengi, muujiza huo unatia ndani uhai wenyewe, kuanzia chembe zake ndogo zaidi kufikia ubongo wa ajabu wa mwanadamu.
DNA na Ubongo wa Mwanadamu
DNA ni chembe za urithi za viumbe wote wenye chembe na ndizo huwapitishia watoto molekuli za wazazi wao.b Asidi hiyo tata imelinganishwa na ramani ya ujenzi au maagizo ya upishi, kwa kuwa DNA ina habari nyingi sana ambayo imefichwa kama kemikali na kuhifadhiwa ndani ya molekuli zenye uwezo wa kufichua habari hiyo na kutenda kupatana nayo. DNA ina habari nyingi kadiri gani? Ikiwa habari za msingi, zinazoitwa nukliotidi, zingebadilishwa kuwa herufi za alfabeti, “zingejaza zaidi ya kurasa milioni moja za kitabu,” kinasema kitabu fulani.
Katika viumbe vingi, DNA imetiwa ndani ya nyuzinyuzi fulani zinazoitwa kromosomu, ambazo zimehifadhiwa kwa uangalifu ndani ya kiini cha kila chembe. Viini vya chembe vina kipenyo cha milimita 0.00508 hivi. Hebu fikiria hilo—habari yote ambayo ilifanyiza mwili wako wa pekee inapatikana katika vitu vidogo sana ambavyo vinaweza kutazamwa tu kwa kutumia darubini! Mwanasayansi mmoja alisema kwa usahihi kwamba viumbe vina “mfumo tata zaidi ulimwenguni wa kuhifadhi na kufichua habari.” Hilo ni jambo la ajabu unapofikiria uwezo wa kuhifadhi habari wa kompyuta, DVD, na vifaa vingine kama hivyo! Isitoshe, hatujui habari zote kuhusu DNA. Gazeti New Scientist linasema: “Kila ugunduzi tunaofanya unatufunulia jambo lingine linalotutatanisha.”c
Je, inapatana na akili kusema kwamba ubuni na mpangilio huo wa ajabu ulijitokeza wenyewe? Ikiwa ungepata kitabu cha maagizo kilicho na kurasa milioni moja na habari zake zimefichwa kwa ustadi wa ajabu, je, ungesema kwamba kitabu hicho kilijiandika? Vipi ikiwa kitabu hicho kilikuwa kidogo sana hivi kwamba ungehitaji darubini kukisoma? Na vipi ikiwa kilikuwa na habari hususa za kutengeneza mashini yenye akili inayoweza kujirekebisha na kujifanya upya iliyo na sehemu zaidi ya bilioni moja, ambazo zilihitaji kuunganishwa wakati unaofaa na kwa njia hususa? Kwa kweli, hakuna mtu ambaye angefikiri kwamba kitabu hicho kilijiandika chenyewe.
Baada ya kuchunguza utafiti wa karibuni kuhusu utendaji wa ndani ya chembe, Antony Flew mwanafalsafa wa Uingereza, ambaye wakati mmoja alikuwa mtetezi mkuu wa fundisho la kwamba hakuna Mungu, alisema hivi: “Utata wa utaratibu unaohitajika ili kutokeza (uhai), [unaonyesha] kwamba akili ilihusika.” Flew anaamini kwamba mtu “anapaswa kufuata hoja zenye akili hata zikimwongoza mahali ambapo hataki kwenda.” Katika kisa chake, hoja zilimwongoza abadili kabisa kufikiri kwake hivi kwamba sasa anamwamini Mungu.
Wanasayansi wengi sana hushangazwa na ubongo wa mwanadamu. Ukiwa umetokezwa na DNA, ubongo umesemwa kuwa ndicho “kitu tata zaidi ulimwenguni.” Hata kompyuta ya hali ya juu sana ulimwenguni huonekana duni sana inapolinganishwa na ubongo wenye uzito wa kilogramu moja tu. Kulingana na maoni ya mwanasayansi mmoja wa mfumo wa neva, kadiri wanasayansi wanavyojifunza mengi zaidi kuhusu akili na ubongo, “ndivyo unavyostaajabisha na kutatanisha zaidi.”
Fikiria: Ubongo unatuwezesha kufanya mambo kama vile kupumua, kucheka, kulia, kufumbua mafumbo, kujenga kompyuta, kuendesha baiskeli, kuandika mashairi, na kustaajabia anga wakati wa usiku. Je, inapatana na akili kusema kwamba uwezo huo wote ulijitokeza wenyewe kwa njia ya mageuzi?
Imani Inayotegemea Uthibitisho
Ili tujielewe, je, tuwachunguze viumbe wa hali ya chini kuliko wanadamu kama vile sokwe na wanyama wengine, kama wanamageuzi wanavyofanya? Au tunapaswa kuchunguza chanzo cha hali ya juu zaidi, yaani, Mungu, ili tupate majibu? Ni kweli kwamba tunafanana na wanyama kwa njia fulani. Kwa mfano, lazima tule, tunywe, na tulale, na vilevile tuna uwezo wa kuzaa. Hata hivyo, sisi ni wa pekee katika njia nyingi. Inapatana na akili kusema kwamba tabia zetu za pekee za kibinadamu zinatokana na Mtu wa hali ya juu kuliko sisi, yaani, Mungu. Biblia inaeleza wazo hilo kwa njia hususa, inaposema kwamba Mungu alimuumba mwanadamu “kwa mfano wake” kiadili na kiroho. (Mwanzo 1:27) Mbona usitafakari kuhusu sifa za Mungu, ambazo baadhi yake zimerekodiwa kwenye Kumbukumbu la Torati 32:4; Yakobo 3:17, 18; na 1 Yohana 4:7, 8.
Muumba wetu ametupa “uwezo wa akili” unaotusaidia kuchunguza ulimwengu unaotuzunguka na kupata majibu yanayoridhisha kwa maswali yetu. (1 Yohana 5:20) Mwanafizikia na mshindi wa Tuzo la Nobeli William D. Phillips, aliandika hivi kuhusu jambo hilo: “Ninapochunguza utaratibu, umaridadi, na jinsi ulimwengu unavyoeleweka, ninalazimika kufikia mkataa kwamba mtu mwenye akili nyingi zaidi alibuni vitu ninavyoona. Ujuzi wangu wa kisayansi unaponisaidia kuona upatano na utaratibu wa kifizikia, imani yangu katika Mungu inaimarishwa.”
Miaka elfu mbili iliyopita, mtu fulani aliyeuchunguza ulimwengu wa asili aliandika hivi baada ya kutafakari: “Sifa [za Mungu] ambazo hazionekani, zinaonekana waziwazi tangu kuumbwa kwa ulimwengu na kuendelea, kwa sababu zinaeleweka kwa vitu vilivyofanywa, yaani, nguvu zake za milele na Uungu.” (Waroma 1:20) Mwandikaji wa maneno hayo—mtume Mkristo Paulo—alikuwa mtu mwenye akili na aliye na elimu ya juu katika Sheria ya Musa. Imani yake inayotegemea hoja zenye akili ilimsaidia amwone Mungu kuwa halisi, na utambuzi wake bora wa haki ulimchochea ampe Mungu sifa kwa kazi zake za uumbaji.
Tunatumaini kwamba wewe pia utafikia mkataa wa kwamba ni jambo linalopatana na akili kuamini kwamba kuna Mungu. Kwa kweli, kama Paulo, huenda ukafanya mengi zaidi ya kuamini tu kwamba Yeye yuko. Tunatumaini kwamba kama vile mamilioni ya watu tayari wamejionea wewe pia utatambua kuwa Yehova Mungu ni mtu wa roho mwenye sifa zenye kuvutia ambazo pia zinapatikana katika moyo wa mwanadamu, na zinazotuvuta kwake tumkaribie.—Zaburi 83:18; Yohana 6:44; Yakobo 4:8.
[Maelezo ya Chini]
a Ona makala yenye kichwa “Je, Mageuzi Ni Jambo Hakika?” katika toleo la Amkeni! la Septemba (Mwezi wa 9) 2006.
b Herufi DNA zinamaanisha deoksiribonyukilia asidi au chembe za urithi.
c Charles Darwin alipobuni nadharia ya mageuzi, hakujua kuhusu utata wa chembe.
[Sanduku katika ukurasa wa 24]
JE, MAOVU YANAYOFANYWA NA DINI YAKUZUIE KUAMINI KWAMBA KUNA MUNGU?
Watu wengi hawaamini kwamba kuna Muumba kwa sababu ya mambo mabaya na ufisadi ambao umefanywa na dini nyingi katika historia. Je, hiyo ni sababu nzuri ya kutomwamini Mungu? Hapana. “Mazoea mabaya na maovu ambayo yamefanywa na dini,” anasema Roy Abraham Varghese katika utangulizi wa kitabu There Is a God cha Antony Flew, “hayana uhusiano wowote na imani kwamba Mungu yuko, kama tu tisho la vita vya kinyuklia halina uhusiano wowote na ukweli kwamba E=mc2.”d
[Maelezo ya Chini]
d Herufi E=mc2 zinamaanisha nishati inalingana na uzito ukizidishwa kwa mwendo wa nuru maradufu.
[Picha katika ukurasa wa 23]
Ikiwa inasemekana kwamba wanadamu ndio waliojenga vitu vya kale, ubuni unaoonekana katika vitu vya asili ulitokezwa na nani?
[Picha katika ukurasa wa 23]
Albert Einstein
[Picha katika ukurasa wa 24, 25]
DNA ni kama kitabu kidogo sana kilicho na maagizo hususa kwa ajili ya viumbe wenye akili
[Picha katika ukurasa wa 25]
Ubongo wa mwanadamu umesemwa kuwa ndicho “kitu tata zaidi ulimwenguni”
[Hisani ya Picha katika ukurasa wa 22]
© The Print Collector/age fotostock