Jinsi ya Kupangia Matumizi ya Pesa Zako
KUNA njia tatu za kupangia matumizi ya pesa: (1) Kuzitumia, (2) kuziweka akiba, au (3) kuwapa watu. Acheni kwanza tuzungumzie jinsi unavyoweza kutumia pesa kwa hekima.
Poromoko Kubwa la Uchumi limeonyesha wazi kwamba ni jambo la hekima kuwa na bajeti iliyopangwa vizuri. Bajeti ni nini? Kwa ufupi, ni makadirio ya jinsi mapato yatakavyotumiwa na mtu binafsi, familia, biashara, au serikali.
Ushirikiano wa Familia
Unaweza kupanga bajeti jinsi gani? Kitabu Budgeting, cha Denise Chambers kinasema kwamba “watu wote katika familia wanapaswa kuhusishwa katika kupanga bajeti ili wote waweze kuifuata.” Mara kwa mara, wote wanapaswa kukutana ili kuona jinsi bajeti yao inavyoendelea. Wote wanaweza kunufaika wanaposhirikiana kupanga bajeti nzuri na kila mmoja anapojitahidi kuishi kulingana na mapato ya familia.
Watu fulani hutumia programu ya kompyuta kupanga bajeti. Wengine hutumia tu penseli na karatasi iliyochorwa safu mbili. Safu moja inaonyesha mapato, ile nyingine inaonyesha matumizi. Pia ni muhimu kutia katika bajeti kiasi fulani kila mwezi cha kushughulikia gharama zinazolipiwa mara moja kwa mwaka, kama vile kodi ya mapato au hata likizo.
Njia ambayo watu wametumia kwa muda mrefu ni ile ya kutia pesa katika bahasha au vikasha vilivyoandikwa “Chakula,” “Kodi ya Nyumba,” “Usafiri,” “Umeme,” “Gharama za Matibabu,” na kadhalika. Zamani, watu walitia pesa za matumizi hayo ndani ya bahasha kila mwezi. Leo wengi huona kuwa ni salama na rahisi zaidi kuweka pesa katika akaunti ya benki na kuzitoa wanapozihitaji.
Mara nyingi, Jonathan na Anne, wanaoishi nchini Afrika Kusini pamoja na binti zao wawili, hutumia mbinu ya kupanga bajeti kwa kutumia bahasha. Jonathan anasema hivi: “Ikiwa mshahara wako unatumwa katika akaunti ya benki, ni muhimu sana uwe mwangalifu kuhusu unavyogawa pesa hizo. Kwa mfano, ikiwa pesa ulizotenga kwa ajili ya kununua nyama kila mwezi zimeisha, hupaswi kununua nyama kwa kutumia pesa zilizotengwa kwa ajili ya kuwekwa akiba.”
Jonathan alikuwa na biashara, lakini sasa yeye na familia yake wameamua kutumikia wakiwa wafanyakazi wa kujitolea kujenga majengo ya ibada. Kwa kuwa wangependa kuendelea katika utumishi huo wa kujitolea, wanahitaji kufuata kwa makini bajeti nzuri. Familia yao hujadiliana kwa ukawaida kuhusu bajeti yao ili waone mabadiliko wanayopaswa kufanya.
Furaha Kubwa Zaidi
Uchunguzi unaonyesha kwamba kuwapa watu wengine mali, kutia ndani wakati na nguvu na vilevile kiasi fulani cha pesa, kunaleta furaha kubwa sana. Kwa kadiri ambavyo uwezo wako utaruhusu, huenda hiyo ikawa ndiyo njia bora zaidi ya kutumia pesa zako kati ya zile zilizotajwa katika utangulizi.
Katika kitabu chake The New Frugality, Chris Farrell anasema kwamba “unapoweka pesa akiba, unapata nafasi ya kufurahia kuzitumia.” Naye anapendekeza: “Jambo lenye faida zaidi na la hekima zaidi unaloweza kufanya na pesa zako ni kuwapa watu wengine.”a Farrell anaongezea hivi: “Unapofikiria jambo lililo muhimu zaidi maishani, mara nyingi utapata ni kuwa na uhusiano mzuri na watu, kujionea mambo, na kuhisi kwamba umesaidia kwa njia fulani, bali si kuwa na pesa au mali.”
Michael Wagner, ambaye ni mtaalamu wa uchumi, anakubaliana na maneno hayo. Katika kitabu chake, Your Money, Day One, ambacho kimekusudiwa kuwatia moyo vijana waweke pesa akiba, anasema hivi: “Unapochukua hatua ya kwanza kuwasaidia watu wenye uhitaji, utapata faida kwa njia mbalimbali kwa sababu ya kuonyesha fadhili na ukarimu, lakini faida kubwa zaidi itakuwa hisia ambayo utapata moyoni kwa kumsaidia mwanadamu mwenzako.”
Biblia inaonyesha kwamba kutoa huleta furaha. Kama ilivyozungumziwa hapo awali, Biblia ina semi zinazoweza kukusaidia kutumia pesa kwa hekima. Sasa, acheni tuchunguze semi nyingine saba.
[Maelezo ya Chini]
a Pesa zinaweza kutolewa kama zawadi au zitumiwe kuwaonyesha watu ukarimu kwa kutayarisha chakula kwa ajili ya marafiki na watu wa familia.