Ni Maoni Gani Yanayopatana Zaidi na Akili?
HAKUNA mwanadamu aliyeona uhai ukianza duniani. Wala hakuna mtu ambaye ameona uhai ukigeuka na kuwa aina nyingine ya uhai, yaani, mnyama anayetambaa akigeuka na kuwa mamalia.a Kwa hiyo, ni lazima tutegemee uthibitisho uliopo ili kufikia mkataa kuhusu chanzo cha uhai. Na inafaa tuamini yale ambayo uthibitisho huo unaonyesha badala ya kuulazimisha ukubaliane na maoni yetu.
Hata hivyo, watu wengi wanaoamini hakuna Mungu wanaamini kwamba uhai ulijitokeza wenyewe bila msaada wowote wa nguvu zisizo za kawaida. “Tulifanya uamuzi mapema . . . kwamba ulimwengu ulijitokeza,” akaandika mwanamageuzi Richard C. Lewontin. “Kwa kuwa wazo la kwamba ulimwengu ulijitokeza ndilo wazo pekee linalopatana na akili, hatupaswi hata kufikiri kuna Muumba.” Hivyo, watu wanaoamini kwamba ulimwengu ulijitokeza wenyewe hawana jambo lingine ila kuamini mageuzi.
Watu wa kidini pia wanaweza kuwa na maoni yasiyofaa ambayo hupotosha mtazamo wao kuelekea sayansi. Kwa mfano, kama ilivyotajwa awali, wanauumbaji fulani wanashikilia maoni yenye makosa kwamba maelfu ya miaka iliyopita Mungu aliuumba ulimwengu mzima kwa siku sita zenye saa 24. Kwa kuwa tayari waliamua hivyo mapema, wanajaribu kulazimisha uthibitisho uliopo uunge mkono ufafanuzi wao wa Biblia. (Ona sanduku “‘Siku’ Moja Ina Urefu Gani?” kwenye ukurasa wa 9.) Watu walio na maoni ya kishupavu kuielekea Biblia na sayansi hawana majibu yenye kuridhisha wanapotafuta uthibitisho wa imani yao.
Ni Maoni Gani Yanayohusisha Mambo Yote Hakika?
Wanamageuzi fulani huamini mambo yafuatayo kuhusu chanzo cha molekuli tata ambazo hufanyiza viumbe hai:
1. Vitu vya msingi viliungana kwa njia fulani na kufanyiza molekuli za msingi.
2. Kisha molekuli hizo ziliungana pamoja kwa mfuatano uleule unaohitajiwa kufanyiza DNA, RNA, au protini zenye uwezo wa kuhifadhi habari inayohitajika ili kutekeleza utendaji muhimu kwa ajili ya uhai.
3. Kwa njia fulani, molekuli hizo zilifanyiza mfuatano hususa unaohitajiwa ili ziweze kujigawanya. Hakuwezi kuwa na mageuzi wala uhai ikiwa molekuli hazitajigawanya.
Molekuli zinazohitajiwa kwa ajili ya uhai zilifanyizwa namna gani na zilipata wapi uwezo wao wa ajabu pasipo mbuni mwenye akili kuingilia kati? Utafiti wa wanamageuzi haujaeleza vizuri au kutoa majibu yenye kuridhisha kwa maswali kuhusu chanzo cha uhai. Kwa kweli wale wanaopinga kwamba Muumba alihusika kwa njia fulani, wanadai eti nguvu za asili na molekuli zisizo na akili zilikuwa na nguvu kama za Mungu za kutokeza uhai.
Hata hivyo, mambo hakika yanaonyesha nini? Uthibitisho uliopo unaonyesha kwamba badala ya molekuli kukua na kuwa viumbe hai vilivyo tata, mambo hutendeka kinyume: Sheria za fizikia zinasema kwamba vitu tata—mashini, nyumba, na hata chembe iliyo hai—huharibika baada ya muda.b Hata hivyo, wanamageuzi husema kwamba mambo hutendeka kinyume. Kwa mfano, kitabu Evolution for Dummies kinasema kwamba mageuzi hutukia kwa sababu dunia “inapata nishati nyingi sana kutoka kwa jua, na nishati hiyo ndiyo hufanya vitu viwe tata.”
Ni kweli kwamba nishati inahitajika ili kutokeza kitu tata—kwa mfano, nishati inahitajika ili kuunganisha matofali, mbao, na misumari ili ziwe nyumba. Hata hivyo, nishati hiyo inapaswa kudhibitiwa kwa uangalifu na kuelekezwa kwa njia sahihi kwa sababu huenda nishati isiyodhibitiwa ikafanya vitu vidhoofike haraka, kama vile tu nishati kutoka kwenye jua na hali ya hewa zinaweza kufanya jengo liharibike haraka.c Watu wanaoamini mageuzi hawawezi kueleza kwa njia inayoridhisha jinsi ambavyo nishati hudhibitiwa ili kufanyiza vitu tata.
Kwa upande mwingine, tukiwa na maoni ya kwamba uhai na ulimwengu ni kazi ya Muumba mwenye hekima ambaye ana “wingi wa nguvu zenye msukumo,” tunaweza kueleza chanzo cha mfumo tata wa habari na pia kani zilizopimwa kwa usahihi kabisa ambazo huongoza vitu vidogo zaidi kama atomu na vikundi vikubwa vya nyota.d—Isaya 40:26.
Kuamini kwamba kuna Muumba pia kunapatana na maoni yanayofuatwa na wengi kwamba ulimwengu ulikuwa na mwanzo. Mwanzo 1:1 inasema: “Hapo mwanzo Mungu aliumba mbingu na dunia.”
Kila mara kunapokuwa na uvumbuzi mpya, inakuwa vigumu kutetea falsafa ya kwamba ulimwengu na uhai ulijitokeza wenyewe, na jambo hilo limefanya baadhi ya watu wanaoamini kwamba hakuna Mungu wabadili maoni yao.e Watu ambao hapo awali waliamini hakuna Mungu wamefikia mkataa wa kwamba maajabu ya ulimwengu ni uthibitisho ulio wazi wa “sifa zake ambazo hazionekani” na ‘nguvu za milele’ za Muumba wetu, Yehova Mungu. (Waroma 1:20) Je, ungependa kuchunguza jambo hilo kwa undani zaidi? Kufanya hivyo kungekuwa jambo muhimu zaidi maishani mwako.f
[Maelezo ya Chini]
a Ingawa aliamini kabisa katika mageuzi, mwanabiolojia Ernst Mayr alikubali kwamba “mabaki ya wanyama yanaonyesha pengo fulani,” yaani, viumbe vipya vilitokea ghafula.
b Wanasayansi huuita mwelekeo huo wa vitu kuharibika, “athari ya joto.” Kwa ufupi, sheria hiyo husema kwamba utaratibu hudhoofika hatua kwa hatua na kutokeza mvurugo.
c DNA inaweza kubadilika kwa sababu ya mabadiliko katika chembe za urithi yanayotokezwa na mnururisho na kemikali fulani. Lakini mabadiliko hayo hayatokezi viumbe vipya.—Ona habari yenye kichwa “Je, Mageuzi Ni Jambo Hakika?” katika gazeti Amkeni! la Septemba (Mwezi wa 9) 2006.
d Ona kitabu Je, Kuna Muumba Anayekujali? kilichochapishwa na Mashahidi wa Yehova.
e Ona habari yenye kichwa “Nililelewa na Wazazi Walioamini Hakuna Mungu,” katika toleo la Amkeni! la Novemba 2010.
f Kwa habari zaidi kuhusu suala la uumbaji na mageuzi, ona broshua Uhai—Ulitokana na Muumba? na Maswali Matano Muhimu Kuhusu Chanzo cha Uhai, zilizochapishwa na Mashahidi wa Yehova.
[Sanduku katika ukurasa wa 8]
JE, WANADAMU WANAGEUKA NA KUWA VIUMBE BORA AU WANAZOROTA?
Wanasayansi fulani wana wasiwasi kwamba DNA ya wanadamu inadhoofika kwa sababu ya mabadiliko katika chembe za urithi, au kutokamilika. Ikiwa hilo ni kweli, jambo hilo lingepinga wazo la kwamba tunageuka, au hali yetu inazidi kuwa bora. Lakini ikiwa Mungu ndiye aliyeumba DNA ya mwanadamu, kwa nini ina kasoro? Biblia inatueleza mambo ambayo sayansi haiwezi kutueleza—kwamba kutokamilika kwa mwanadamu kulitokana na dhambi, au kutokumtii Mungu. Waroma 5:12 inasema: “Kupitia mtu mmoja [Adamu] dhambi iliingia katika ulimwengu na kifo kupitia dhambi.” Kwa hiyo basi, DNA inayozorota inapinga mageuzi na kuunga mkono Biblia. Je, hilo linamaanisha kwamba DNA itaendelea kuzorota mpaka wakati usiojulikana? La! Mungu ameahidi kuingilia mambo ya wanadamu na kuondoa madhara yote yaliyosababishwa na wazazi wetu wa kwanza. Naam, Muumba wetu, na si mageuzi, ndiye atakayefanya DNA yetu iwe kamilifu.—Ufunuo 21:3, 4.
[Sanduku katika ukurasa wa 9]
“SIKU” MOJA INA UREFU GANI?
Katika Biblia, neno “siku” linaweza kurejelea vipindi mbalimbali vya wakati. Kwa mfano, kwenye Mwanzo 2:4, kipindi chote cha uumbaji cha “siku” sita kinatajwa kuwa “siku ambayo Yehova Mungu aliifanya dunia na mbingu.” Ni wazi kwamba kila siku ilihusisha kipindi kirefu cha wakati. Jambo la kuzingatiwa ni kwamba ingawa Biblia inataja kihususa mwisho wa “siku” sita za kwanza, haitaji mwisho wa siku ya saba. Kwa nini? Kwa sababu bado siku hiyo inaendelea.—Mwanzo 2:3; Waebrania 4:4-6, 11.
[Picha katika ukurasa wa 8]
Vitu huharibika visipotunzwa
[Picha katika ukurasa wa 8, 9]
Nguvu na sifa nyingine za Mungu zinaonekana katika ulimwengu