Vijana Huuliza
Kwa Nini Wazazi Wangu Hawanielewi?
FIKIRIA HALI KAMA HII.
Ni saa 12 jioni siku ya Ijumaa, na Jim mwenye umri wa miaka 17 anatembea haraka kuelekea mlangoni. “Tuonane baadaye!” anawaambia wazazi wake, akitumaini kwamba hawatamwuliza atarudi saa ngapi.
Lakini amekosea.
“Jimmy, utarudi saa ngapi?” mama yake anamwuliza.
Jim anasimama. “Umh . . . eeh . . . ,” anasitasita, “nitachelewa, lakini msiwe na wasiwasi, sawa?” Jim anafungua mlango na karibu afaulu kuondoka. Lakini baba yake anamwita, “James, subiri kidogo!”
Jim anasimama tuli, na anasikia sauti imara ya baba yake: “Unajua sheria ya nyumba hii. Saa nne kamili unapaswa kuwa hapa—usichelewe!”
“Ah, baba,” Jim anaguna kisha anageuka kumtazama baba yake, “unajua jinsi inavyoaibisha kuwaambia rafiki zangu kwamba ninapaswa kurudi nyumbani mapema hivyo?”
Baba anakuwa mkali. “Nimesema saa nne kamili,” anarudia, “na usichelewe!”
PENGINE umepitia hali kama hiyo. Iwe tatizo lilikuwa saa ulizowekewa za kurudi nyumbani, muziki unaosikiliza, marafiki wako, au jinsi unavyovalia, wazazi wako walikuwekea sheria kali, na hawakuzilegeza hata kidogo. Kwa mfano:
“Baada ya kumwoa mama, baba yangu wa kambo alichambua vikali kila aina ya muziki nilioupenda. Ilinilazimu kutupa CD zangu zote!”—Brandon.a
“Mama yangu hunishutumu kwa sababu sina marafiki. Lakini nikimwuliza kama ninaweza kuwa rafiki ya mtu fulani, anakataa kwa sababu anasema hamfahamu mtu huyo. Inaudhi sana!”—Carol.
“Baba yangu na mama yangu wa kambo hawawezi kuniruhusu kuvaa t-shati ambayo inanibana vizuri, wanapenda iwe pana. Na baba yangu husisitiza kwamba kaptura ni fupi mno kama haijafunika magoti!”—Serena.
Unaweza kufanya nini ikiwa wewe na wazazi wako hamkubaliani? Je, unaweza kuzungumzia jambo hilo pamoja nao? “Kwa kawaida, wazazi wangu hawataki kunisikiliza,” anasema Joanne mwenye umri wa miaka 17. Amy, mwenye umri wa miaka 15 anasema, “Ninapohisi kwamba wazazi wangu hawanielewi, mimi hunyamaza kimya.”
Lakini usikate tamaa upesi! Huenda wazazi wako wakawa tayari kukusikiliza kuliko unavyodhania.
Fikiria hili: Hata Mungu huwasikiliza wanadamu wanapomjulisha mahangaiko yao. Kwa mfano, Yehova alimsikiliza Musa alipoongea kwa niaba ya Waisraeli wasiotii.—Kutoka 32:7-14; Kumbukumbu la Torati 9:14, 19.
Huenda ukahisi kwamba wazazi wako si kama Mungu ambaye hukubali sababu. Ni kweli kwamba mazungumzo ya Musa pamoja na Yehova kuhusu hatima ya taifa zima yalikuwa mazito ukilinganisha na mazungumzo kati yako na wazazi wako kuhusu kurudi nyumbani ukiwa umechelewa. Lakini bado tunaweza kupata kanuni inayoweza kutumika:
Ikiwa una sababu halali ya kulalamika, watu wenye mamlaka—katika kisa hiki, wazazi wako—wanaweza kuwa tayari kukusikiliza.
Kitakachoamua ikiwa utafaulu ni jinsi utakavyoeleza malalamishi yako! Hatua zinazofuata zitakusaidia kufanya hivyo kwa njia yenye matokeo zaidi:
1. Tambua tatizo. Hapa chini, andika jambo ambalo inaonekana kwamba wewe na wazazi wako hamkubaliani.
․․․․․
2. Tambua hisia zako. Hapa chini, andika jinsi maoni ya wazazi wako kuhusu jambo hilo yanavyokufanya uhisi—kama unahisi uchungu, huzuni, aibu, hawakuamini, au jambo lingine. (Kwa mfano: Katika kisa kilichosimuliwa mwanzoni mwa makala hii, Jim anasema kuwa sheria ambayo wazazi wake wameweka kwamba anapaswa kurudi nyumbani mapema inamwaibisha mbele ya rafiki zake.)
․․․․․
3. Jaribu kufikiri kama mzazi. Wazia kwamba una kijana aliye na tatizo kama lile ulilotaja kwenye Hatua ya 1. Ikiwa wewe ungekuwa mzazi, hangaiko lako kuu lingekuwa nini, na kwa nini? (Kwa mfano: Katika kisa kilichotajwa mwanzoni, huenda wazazi wa Jim wakahofia usalama wake.)
․․․․․
4. Fikiria tena kuhusu tatizo lenyewe. Jibu maswali yafuatayo:
Unaona maoni ya wazazi wako yana faida gani?
․․․․․
Unaweza kufanya nini ili upunguze wasiwasi wao?
․․․․․
5. Zungumza na wazazi wako na mjaribu kusuluhisha tatizo pamoja. Kwa kutumia hatua zilizoonyeshwa hapo juu—na kufikiria madokezo yaliyo kwenye kisanduku “Madokezo ya Kuwasiliana”—huenda ukagundua kwamba unaweza kuwasiliana na wazazi wako kwa ukomavu zaidi. Kellie sasa anafurahia uhusiano kama huo pamoja na baba na mama yake. “Kubishana nao hakutakusaidia, na huwezi kushinda,” anasema. “Siri yangu ni kuzungumza waziwazi na wazazi wangu. Kwa kawaida tunafikia makubaliano ambayo yanaturidhisha sisi sote.”
Unaweza kupata makala zaidi za “Vijana Huuliza” katika Tovuti ya www.watchtower.org/ype
[Maelezo ya Chini]
a Baadhi ya majina katika makala hii yamebadilishwa.
[Sanduku katika ukurasa wa 20]
MADOKEZO YA KUWASILIANA
“Unapata faida zaidi kwa kusikiliza kuliko kufoka. Ukiwasikiliza wazazi wako na kujaribu kuelewa maoni yao, huenda wao pia watafanya vivyo hivyo.”—Rianne.
Soma Wafilipi 2:3, 4.
“Usiwajibu kwa dharau! Nilifanya hivyo mara nyingi hadi nilipotambua kwamba ningeweza kuepuka ugomvi (na kuadhibiwa) kama tu ningedhibiti ulimi wangu!”—Danielle.
Soma Methali 17:27; 21:23.
“Subiri hadi kila mtu awe ametulia na kustarehe, wakati ambapo unajua wazazi wako watakuwa tayari kukusikiliza.”—Collette.
Soma Methali 25:11.
“Wazazi wako wanahitaji kujua kwamba unawaheshimu na kwa kweli unawasikiliza wanapozungumza. Kwa hiyo, kabla ya kuwaeleza hisia zako, wahakikishie kwamba umesikia na unaelewa wanachokuambia.”—Emily.
Soma Methali 23:22; Yakobo 1:19.
[Sanduku katika ukurasa wa 20]
UKWELI WA MAMBO
Si lazima tofauti zote zizungumziwe. Katika visa fulani, unaweza ‘kusema moyoni mwako, na kunyamaza.’ (Zaburi 4:4) Msichana anayeitwa Beatrice anasema: “Wakati mwingine nikifikiria jinsi kesho yake tatizo hilo litakavyokuwa jambo dogo, mimi huona kuwa si jambo la maana tena. Ninaweza kuachana nalo tu.”
[Sanduku katika ukurasa wa 21]
MBONA USIWAULIZE WAZAZI WAKO?
Mlisuluhishaje mabishano kati yenu na wazazi wenu? Kama mngekuwa na umri kama wangu, mngetenda kwa njia tofauti? Mngetendaje?
[Sanduku/Picha katika ukurasa wa 21]
VIJANA WENZAKO WANASEMA NINI?
Wyndia—Mimi hujaribu kufikiri kabla ya kusema. Ninatafakari maoni ya wazazi wangu, na kutoa sala kabla ya kusema jambo lolote. Nikijua kwamba jambo ninalotaka kusema litazua ugomvi, ninanyamaza mpaka nitakapoweza kujieleza bila kubishana.
Ross—Ninapoanza kupandwa na hasira, ninajaribu kujiambia kwamba huenda nikajiharibia siku nzima kwa sababu ya ugomvi usio wa lazima. Matokeo ni kwamba sasa sikasiriki upesi kama nilivyofanya nilipokuwa mchanga.
Ramona—Mimi huona kwamba sikuzote ni jambo la hekima kusikiliza maoni ya wazazi wangu. Pengine hata maoni yao hayatofautiani sana na yangu, na huenda tukahitilafiana kwa mambo madogo sana kuliko nilivyotarajia.