Watchtower MAKTABA KWENYE MTANDAO
Watchtower
MAKTABA KWENYE MTANDAO
Kiswahili
  • BIBLIA
  • MACHAPISHO
  • MIKUTANO
  • g 2/10 kur. 26-29
  • Kwa Nini Sisi Hubishana Kila Wakati?

Hakuna video yoyote kwa sasa.

Samahani, haikuwezekana kupakia video.

  • Kwa Nini Sisi Hubishana Kila Wakati?
  • Amkeni!—2010
  • Habari Zinazolingana
  • Kwa Nini Sikuzote Tunabishana?
    Maswali Ambayo Vijana Huuliza—Majibu Yafanyayo Kazi, Buku la 1
  • Kwa Nini Wazazi Wangu Hawanielewi?
    Amkeni!—2012
  • Nifanye Nini Wazazi Wangu Wanapogombana?
    Maswali Ambayo Vijana Huuliza—Majibu Yafanyayo Kazi, Buku la 2
  • Kwa Nini Baba na Mama Waliachana?
    Maswali Ambayo Vijana Huuliza—Majibu Yafanyayo Kazi, Buku la 1
Pata Habari Zaidi
Amkeni!—2010
g 2/10 kur. 26-29

Vijana Huuliza

Kwa Nini Sisi Hubishana Kila Wakati?

Katika kisa kilichoonyeshwa hapa chini, Rachel anachangia mabishano kwa njia tatu. Je, unaweza kuzitambua? Andika majibu yako chini ya kila kisa, kisha uyalinganishe na sanduku lenye kichwa “Majibu,” mwishoni mwa makala hii.

Ni Jumatano (Siku ya 3) usiku. Rachel, mwenye umri wa miaka 17, yuko tayari kupumzika baada ya kumaliza kazi zote alizopaswa kufanya! Anawasha TV na kuketi kwenye kiti anachokipenda sana.

Wakati huohuo, Mama anaingia naye haonekani akiwa na furaha. “Rachel! Kwa nini unapoteza wakati ukitazama TV na huku unapaswa kuwa ukimsaidia dada yako kufanya kazi za shule? Hakuna wakati unafanya unachoambiwa!”

“Sasa umeanza kelele tena,” Rachel anasema kwa sauti ya chini lakini inayoweza kusikika.

Mama yake anakaribia. “Eti umesema nini?”

“Mama, mimi sijasema lolote,” Rachel anasema huku akizungusha macho yake kwa dhihaka.

Sasa Mama amekasirika kabisa. “Unazungumza na nani hivyo?” Mama anauliza.

“Si hata wewe unazungumza hivyo!” Rachel anajibu.

Mapumziko yamekwisha . . . Mabishano mengine yameanza.

1. ․․․․․

2. ․․․․․

3. ․․․․․

JE, UMEWAHI kujionea kisa kama hicho kilichotajwa hapo juu? Je, wewe na wazazi wako hubishana kila wakati? Ikiwa ndivyo, hebu chunguza jinsi hali ilivyo. Ni mambo gani ambayo ninyi hubishania zaidi? Tia alama kando ya jibu lako—au unaweza kuandika jibu tofauti kando ya maneno “Sababu nyingine.”

◯ Mtazamo

◯ Kazi za nyumbani

◯ Mavazi

◯ Saa za kurudi

◯ Vitumbuizo

◯ Marafiki

◯ Watu wa jinsia tofauti

◯ Sababu nyingine ․․․․․

Hata sababu iwe nini, kubishana kutakufadhaisha wewe—na wazazi wako. Bila shaka, unaweza tu kufunga mdomo na kujifanya eti unakubali kila jambo ambalo wazazi wako wanakuambia. Lakini je, Mungu anataka ufanye hivyo? Hapana. Ni kweli kwamba Biblia inasema ‘umheshimu baba yako na mama yako.’ (Waefeso 6:2, 3) Lakini pia inakutia moyo usitawishe “uwezo wa kufikiri” na utumie ‘nguvu zako za kufikiri.’ (Methali 1:1-4; Waroma 12:1) Unapofanya hivyo, bila shaka utakuwa na maoni yako mwenyewe yenye nguvu, na huenda mengine yatatofautiana na yale ya wazazi wako. Hata hivyo, katika familia zinazofuata kanuni za Biblia, wazazi na vijana wanaweza kuwasiliana kwa amani—hata ikiwa hawakubaliani katika kila jambo.—Wakolosai 3:13.

Unaweza kujielezaje bila kubadili mazungumzo ya kawaida kuwa mashambuliano ya maneno? Ni rahisi kusema: “Ni shida ya wazazi wangu. Isitoshe, wao ndio hunisumbua kila wakati!” Lakini hebu fikiria: Wewe unaweza kuwadhibiti wengine kwa kadiri gani, kutia ndani wazazi wako? Kwa kweli, huwezi kumbadili mtu mwingine, lakini unaweza kujibadili wewe mwenyewe. Na jambo zuri ni kwamba ukifanya sehemu yako na kutuliza hali, wazazi wako watatulia na kukusikiliza unapotaka kusema jambo fulani.

Kwa hiyo, acha tuone kile ambacho wewe unaweza kufanya ili kumaliza mabishano. Tumia mapendekezo yafuatayo na huenda ukawashangaza wazazi wako—au hata ukajishangaza—na uwezo wako wa kuwasiliana.

(Dokezo: Tia alama kando ya pendekezo unalohitaji kufanyia kazi.)

◯ Fikiri kabla ya kujibu. Biblia inasema: “Moyo wa mwadilifu hutafakari ili kujibu.” (Methali 15:28) Usiropoke tu jambo la kwanza linalokuja akilini unapohisi unaonewa. Kwa mfano, tuseme mama yako anakuambia: “Kwa nini hukuosha vyombo? Hakuna siku ambayo wewe hufanya kile unachoambiwa!” Huenda ukataka kusema, “Mbona unanisumbua?” Lakini tumia uwezo wako wa kufikiri. Jaribu kuelewa sababu iliyomfanya mama yako aseme maneno hayo. Kwa kawaida, maneno “sikuzote” au “hakuna siku” hayapaswi kuchukuliwa kihalisi. Lakini yanaonyesha hisia fulani iliyofichika. Hisia gani?

Huenda mama yako ameudhika, anahisi kwamba anafanya kazi nyingi kupita kiasi ndani ya nyumba. Huenda akawa anataka tu kuhakikishiwa kwamba utamsaidia. Au, kusema kweli, huenda kwa muda mrefu hujafanya kazi unazotazamiwa kufanya nyumbani. Vyovyote vile, kusema “Mbona unanisumbua?” hakutakufaidi—huenda kukatokeza mabishano tu! Kwa hiyo, mbona usimtulize mama yako? Kwa mfano, unaweza kusema: “Naona umekasirika, Mama. Acha nioshe vyombo hivyo mara moja.” Lakini tahadhari: Usiseme maneno hayo kwa kejeli. Huenda kuzungumza kwa huruma kukapunguza hasira kati yenu.

Hapa chini, andika maneno ambayo baba au mama yako anaweza kusema na kukukasirisha.

․․․․․

Sasa hebu fikiria jibu lenye huruma ambalo unaweza kutumia ili kushughulikia hisia zake.

․․․․․

◯ Zungumza kwa heshima. Michelle amejifunza umuhimu wa kuzungumza na mama yake kwa njia nzuri. Anasema, “Hata iwe tunazungumzia jambo gani, kila mara Mama husema hapendi jinsi ninavyozungumza naye.” Ikiwa mara nyingi jambo hilo linakupata, jifunze kuzungumza kwa sauti ya chini na polepole, na uepuke kuzungusha-zungusha macho yako kwa dhihaka au kuonyesha kwa njia nyingine kwamba umeudhika. (Methali 30:17) Ukihisi kwamba uko karibu kushindwa kujidhibiti, toa sala fupi, ya kimyakimya kwa Mungu. (Nehemia 2:4) Bila shaka, kusudi lako si kupata msaada wa Mungu ili kuwafanya wazazi wako waache kukusumbua bali ni ili ufaulu kujizuia na usifanye hali iwe mbaya zaidi.—Yakobo 1:26.

Kwenye nafasi iliyo hapa chini, andika maneno na matendo fulani ambayo unapaswa kuepuka.

Maneno (mambo unayosema):

․․․․․

Ishara bila maneno (ishara za uso na za mwili):

․․․․․

◯ Sikiliza. Biblia inasema: “Katika wingi wa maneno hapakosi kuwa na kosa.” (Methali 10:19) Kwa hiyo, hakikisha kwamba unampa baba au mama yako nafasi ya kuzungumza, na uwasikilize wazazi wako kwa makini sana. Zima muziki, weka kitabu au gazeti chini, na uwatazame. Usiwakatize ili kujitetea. Sikiliza tu. Baadaye, wanapomaliza kuzungumza, utakuwa na nafasi ya kutosha kuuliza maswali au kueleza maoni yako. Kwa upande mwingine, ukiwa mgumu na kuendelea wakati huohuo kueleza maoni yako, utafanya mambo yawe mabaya zaidi. Hata ikiwa ungependa kusema mengi, huenda wakati huo ukawa “wakati wa kukaa kimya.”—Mhubiri 3:7.

◯ Uwe tayari kuomba msamaha. Inafaa sikuzote uombe msamaha kwa jambo lolote ulilofanya kuchangia mabishano. (Waroma 14:19) Unaweza hata kuomba msamaha kwa sababu tu mabishano yalitokea. Ukiona ni vigumu kusema hilo moja kwa moja, jaribu kuandika hisia zako. Kisha, ‘nenda kilomita mbili,’ yaani, jitahidi sana kubadili tabia iliyofanya kuwe na bishano. (Mathayo 5:41) Kwa mfano, ikiwa bishano linatokea kwa sababu hukufanya kazi fulani, mbona usifanye kazi hiyo? Hata ikiwa hupendi kufanya kazi hiyo, ni afadhali kuifanya kuliko kuwakasirisha wazazi wako wanapogundua kwamba hujaifanya.—Mathayo 21:28-31.

Mwishowe, kujaribu kutatua mzozo au kuuzuia kutakusaidia. Kwa kweli, Biblia inasema kwamba mtu “mwenye fadhili zenye upendo anaitendea kwa kuipa thawabu nafsi yake mwenyewe.” (Methali 11:17) Kwa hiyo, fikiria faida utakazopata kwa kutimiza sehemu yako kwa kupunguza hali ya kutoelewana kati yako na wazazi wako.

Familia zenye mafanikio huwa na matatizo, lakini wanajua jinsi ya kuyashughulikia kwa amani. Jaribu kufanya mambo yaliyotajwa katika makala hii, na huenda ukaona kwamba mtaweza kuzungumzia hata mambo magumu pamoja na wazazi wako—bila kubishana!

MAMBO YA KUFIKIRIA

● Kwa nini mara nyingi vijana wengine hujigamba kwamba wanajua kubishana?

● Kwa nini Yehova humwona mtu anayependa kubishana kuwa mjinga?—Methali 20:3.

[Sanduku/Picha katika ukurasa wa 27]

VIJANA WENZAKO WANASEMA NINI?

“Nililazimika kutambua kwamba ingawa ninafanya kazi na kujitegemeza kifedha, bado ninaishi katika nyumba ya mama yangu na lazima nimsikilize. Amenitunza kwa miaka mingi, kwa hiyo, anaponiuliza maswali—labda kuhusu wakati ninapopaswa kurudi nyumbani—ninamwelewa kabisa.”

“Nisipokubaliana na wazazi wangu juu ya jambo fulani, tunasali pamoja, tunafanya utafiti kulihusu, na kulizungumzia. Sikuzote sisi hukubaliana kupitia njia hiyo. Tunapomhusisha Yehova, mwishowe sisi hukubaliana.”

[Picha]

Daniel

Cameron

[Sanduku katika ukurasa wa 29]

MAJIBU

1. Maneno ya kejeli (“Sasa umeanza kelele tena”) yaliongeza makaa kwenye moto kwa kuwa Mama alikuwa tayari ameudhika.

2. Ishara za uso za Rachel (kuzungusha-zungusha macho kwa dhihaka) zilikuwa za kujitafutia shida.

3. Kuzungumza kwa kukosa heshima (“Si hata wewe unazungumza hivyo!”) nyakati zote huleta shida.

[Sanduku katika ukurasa wa 29]

TAARIFA KWA WAZAZI

Hebu tazama kisa kilicho mwanzoni mwa makala hii. Je, unaweza kutambua mambo kadhaa ambayo mama ya Rachel alifanya yaliyochangia mabishano? Unaweza kuepukaje kubishana na kijana wako? Yafuatayo ni baadhi ya mambo unayoweza kutilia maanani:

Epuka kusema mambo kama “Sikuzote wewe . . . ” au “Hakuna siku . . . ” Maneno kama hayo yanaweza tu kumfanya kijana aanze kujitetea. Isitoshe, kwa kawaida maneno hayo huwa yametiliwa chumvi, na mtoto wako anajua jambo hilo. Huenda pia anajua kwamba maneno kama hayo yanasababishwa na hasira badala ya jambo alilofanya.

Badala ya kutumia maneno yenye kuchoma, mbona usijaribu kueleza jinsi tabia ya mtoto wako inavyokuathiri. Kwa mfano, unaweza kusema, “Unapo . . . , mimi huhisi . . . . ” Amini usiamini, hisia zako ni muhimu kwa kijana wako. Unapomjulisha kijana wako jinsi unavyoathiriwa, itakuwa rahisi zaidi kwake kushirikiana nawe.

Hata iwe vigumu kadiri gani, jaribu kuzuia hasira yako. (Methali 10:19) Ikiwa mabishano yanasababishwa na kazi za nyumbani, zungumza kuhusu jambo hilo na kijana wako. Andika ni nini hasa anachohitaji kufanya, na ikiwezekana, mweleze wazi kitakachotukia asipofanya kile anachopaswa kufanya. Sikiliza kwa subira maoni ya kijana wako, hata ikiwa unahisi kwamba maoni yake si sahihi. Vijana wengi hufanya mambo vizuri wanaposikilizwa badala ya kuzomewa.

Kabla ya kukata kauli kwamba kijana wako ameanza kutekwa na roho ya uasi ya ulimwengu, tambua kwamba mambo mengi unayojionea ni sehemu ya ukuzi wa kawaida wa mtoto wako. Anaweza kubishana ili tu akuonyeshe kwamba yeye ni mtu mzima. Jizuie unapohisi kwamba unataka kubishana. Kumbuka kwamba kijana wako anajifunza kutokana na jinsi unavyotenda unapokasirika. Tenda kwa subira na ustahimilivu, nawe utamwekea kijana wako mfano mzuri wa kufuata.—Wagalatia 5:22, 23.

[Picha katika ukurasa wa 28]

Kubishana na wazazi wako ni kama kukimbia mahali pamoja—unatumia nguvu nyingi, lakini huendi popote

    Maktaba Kwenye Mtandao (1980-2025)
    Toka
    Ingia
    • Kiswahili
    • Shiriki
    • Mapendezi
    • Copyright © 2025 Watch Tower Bible and Tract Society of Pennsylvania
    • Masharti ya Utumiaji
    • Sera ya Faragha
    • Mpangilio wa Faragha
    • JW.ORG
    • Ingia
    Shiriki