Watchtower MAKTABA KWENYE MTANDAO
Watchtower
MAKTABA KWENYE MTANDAO
Kiswahili
  • BIBLIA
  • MACHAPISHO
  • MIKUTANO
  • g 8/14 kur. 8-9
  • Jinsi ya Kusema Hapana

Hakuna video yoyote kwa sasa.

Samahani, haikuwezekana kupakia video.

  • Jinsi ya Kusema Hapana
  • Amkeni!—2014
  • Vichwa vidogo
  • Habari Zinazolingana
  • KIKWAZO
  • Kulea Watoto tangu Uchanga
    Kufanya Maisha ya Jamaa Yako Yawe Yenye Furaha
  • Jinsi ya Kuwalinda Watoto Wako
    Amkeni!—2007
  • Zoeza Mtoto Wako Asitawishe Utawa
    Mnara wa Mlinzi Unaotangaza Ufalme wa Yehova—1985
  • Kuwafundisha Watoto Kutii
    Amkeni!—2015
Pata Habari Zaidi
Amkeni!—2014
g 8/14 kur. 8-9
Mtoto anataka kuchukua kitu cha kuchezea dukani, baba yake anamwambia hapana

MSAADA KWA AJILI YA FAMILIA | KULEA WATOTO

Jinsi ya Kusema Hapana

KIKWAZO

Mtoto wako anasisitiza umpe kitu anachotaka. Unapokataa, anaendelea kusisitiza na kufanya ushindwe kuvumilia. Hata useme nini hatulii, na mwishowe unakubali shingo upande. Kwa mara nyingine tena umeshindwa kukataa na kulazimika kumpa anachotaka.

Unaweza kujifunza kusema hapana. Kwanza, acha tufikirie mambo kadhaa kuhusu kusema hapana.

UNACHOPASWA KUJUA

Kusema hapana si ukatili. Huenda wazazi wengine wasikubaliane na hilo, wakisema kwamba unapaswa kuzungumza na mtoto wako, kujieleza, au hata kukubaliana naye. Wanadai kwamba ukisema hapana utafanya mtoto wako awe na kinyongo.

Ni kweli kwamba huenda mwanzoni mtoto wako hatafurahi unaposema “hapana.” Hata hivyo, hilo linamfundisha somo muhimu—katika ulimwengu, huwezi kupata chochote unachotaka. Lakini, ikiwa unampa mtoto wako kila kitu anachotaka, unadhoofisha mamlaka yako na kumfundisha kwamba anaweza kukushawishi akinuna kila anapotaka kitu fulani. Ukifanya hivyo, baada ya muda mtoto wako atashindwa kukuheshimu. Kwa kweli, mtoto anawezaje kumheshimu mzazi asiye na msimamo?

Kusema hapana humtayarisha mtoto kwa ajili ya kubalehe na utu uzima. Kunamfundisha faida za kujizuia. Mtoto anayejifunza somo hilo muhimu hatashawishiwa kwa urahisi kutumia dawa za kulevya au kufanya ngono wakati wa kubalehe.

Pia, kusema hapana kunamwandaa mtoto kuwa mtu mzima. “Ukweli ni kwamba, sisi [watu wazima] hatupati kila kitu tunachotaka,” anaandika Dakt. David Walsh. “Hivyo, hatuwasaidii watoto wetu tunapowafundisha kwamba wanaweza kupata chochote wanachotaka.”a

UNACHOWEZA KUFANYA

Kazia fikira lengo lako. Ungependa mtoto wako awe mtu mzima anayetegemeka na mwenye mafanikio. Lakini ni vigumu kufikia lengo hilo ikiwa unampa mtoto wako kila kitu anachoomba. Biblia inasema mtu ‘akibembelezwa tangu ujanani, katika maisha yake ya baadaye atakuwa mtu asiye na shukrani.’ (Methali 29:21) Kwa hiyo, kusema hapana ni sehemu ya nidhamu. Mazoezi hayo yatamsaidia mtoto wako, bali hayatamuumiza.—Kanuni ya Biblia: Methali 19:18.

Unaposema hapana, usilegeze msimamo. Mtoto wako hayuko sawa na wewe. Kwa hiyo, si lazima ujadiliane naye kana kwamba unahitaji ruhusa yake. Bila shaka, watoto wanapoendelea kukua, wanahitaji kusitawisha “nguvu zao za ufahamu” ili “kutofautisha yaliyo sawa na yaliyo makosa.” (Waebrania 5:14) Hivyo, si kosa kujadiliana na mtoto. Hata hivyo, usibishane na mtoto wako kuhusu sababu za kusema hapana. Ukizidi kubishana naye, atafikiri kwamba huna msimamo.—Kanuni ya Biblia: Waefeso 6:1.

Usibadili uamuzi wako. Mtoto wako anaweza kukushawishi kwa kununa au kulia-lia. Jambo hilo likitokea, utafanya nini? “Weka mpaka kati yako na mtoto wako,” kinashauri kitabu Loving Without Spoiling. “Mwambie, ‘Kama unasisitiza, ni sawa, lakini sitaki kukusikia. Nenda chumbani kwako. Lia mpaka utakaponyamaza.’” Mwanzoni, huenda ikawa vigumu kwako kufanya hivyo na pia kwa mtoto wako kukubali. Lakini ukishikamana na uamuzi wako, huenda akaacha kusisitiza.—Kanuni ya Biblia: Yakobo 5:12.

Usiseme hapana ili tu kuonyesha una mamlaka

Uwe na usawaziko. Usiseme hapana ili tu kuonyesha una mamlaka. Badala yake, acha ‘usawaziko wako ujulikane.’ (Wafilipi 4:5) Nyakati nyingine unaweza kukubaliana na mtoto wako—si kwamba unalegeza msimamo wako kwa kuwa mtoto analialia, bali kwa sababu maombi yake ni halali.—Kanuni ya Biblia: Wakolosai 3:21.

a Kulingana na kitabu No: Why Kids—of All Ages—Need to Hear It and Ways Parents Can Say It.

MAANDIKO MUHIMU

  • “Mtie mwana wako adabu wakati bado kuna tumaini.”—Methali 19:18.

  • “Enyi watoto, watiini wazazi wenu.”—Waefeso 6:1.

  • “Acheni Ndiyo yenu imaanishe Ndiyo, na Siyo yenu, Siyo.”—Yakobo 5:12.

  • “Msiwe mkiwakasirisha watoto wenu, ili wasivunjike moyo.” —Wakolosai 3:21.

FAIDA ZA KUSEMA HAPANA

“Kwa kawaida wazazi hupenda kuona watoto wao wakitabasamu na kuchangamka. Lakini kumbuka jambo hili: Ikiwa mara zote tunafanya mambo yanayowafurahisha watoto wetu, huenda ni ishara kwamba hatutimizi jukumu letu tukiwa wazazi. Watoto wako watajuaje jinsi ya kukabiliana na mfadhaiko na kuvunjika moyo usipowazoeza? Watajifunzaje kujizuia usipowafundisha? Ni jukumu lako kuwafundisha masomo hayo muhimu kwa kusema hapana.”—Dakt. David Walsh.

    Maktaba Kwenye Mtandao (1980-2025)
    Toka
    Ingia
    • Kiswahili
    • Shiriki
    • Mapendezi
    • Copyright © 2025 Watch Tower Bible and Tract Society of Pennsylvania
    • Masharti ya Utumiaji
    • Sera ya Faragha
    • Mpangilio wa Faragha
    • JW.ORG
    • Ingia
    Shiriki