Watchtower MAKTABA KWENYE MTANDAO
Watchtower
MAKTABA KWENYE MTANDAO
Kiswahili
  • BIBLIA
  • MACHAPISHO
  • MIKUTANO
  • g 11/15 kur. 7-9
  • Kuishi Bila Kuona

Hakuna video yoyote kwa sasa.

Samahani, haikuwezekana kupakia video.

  • Kuishi Bila Kuona
  • Amkeni!—2015
  • Habari Zinazolingana
  • Wasaidie Vipofu Wajifunze Kumhusu Yehova
    Huduma Yetu ya Ufalme—2015
  • Maandishi ya Vipofu Yanabadili Maisha
    Jinsi Michango Yako Inavyotumiwa
  • Kuboresha Ustadi Wetu Katika Huduma​—Kuwahubiria Vipofu
    Daftari la Mkutano wa Huduma na Maisha Yetu ya Kikristo—2020
  • Louis Braille—Kuwaangazia Nuru Wafungwa wa Giza
    Amkeni!—2000
Pata Habari Zaidi
Amkeni!—2015
g 11/15 kur. 7-9
Paqui na mume wake

Kuishi Bila Kuona

“Nilipoteza uwezo mkubwa wa kuona nilipozaliwa na kutiwa matone ya dawa kali machoni. Nilipokuwa kijana nikawa kipofu na nikashuka moyo sana.”—Paqui, mwanamke wa makamo ambaye mume wake pia ni kipofu.

UPOFU au matatizo ya kutoona vizuri yanaweza kusababishwa na mambo mengi, kutia ndani majeraha au ugonjwa. Mambo hayo yanaweza kuathiri jicho, neva za jicho, au ubongo. Mara nyingi, watu ambao hupoteza uwezo wao wa kuona kabisa au kwa kiasi kikubwa, hupatwa na wasiwasi, huzuni, na inakuwa vigumu kwao kukubali hali yao. Hata hivyo, wengi hujifunza kukabiliana na hali hizo na hivyo kuishi maisha yenye kuridhisha.

Kwa kawaida macho ndiyo njia kuu tunayotumia ili kutambua mazingira yetu. Hivyo mtu anapopoteza uwezo wake wa kuona yeye hutegemea hisi zingine, yaani, kusikia, kunusa, kugusa, na kuonja.

Kulingana na gazeti Scientific American, uchunguzi uliofanywa kuhusu mabadiliko katika utendaji wa chembe za neva (neuroplasticity) unaonyesha kwamba ubongo una uwezo wa “kubadilikana kulingana na hali.” Gazeti hilo likaendelea kusema: “Uchunguzi mwingi unaonyesha kwamba wakati ambapo hisi moja inaacha kutenda, ubongo una uwezo wa kubadili utendaji wake ili kutegemeza na kuongeza uwezo wa hisi zile nyingine.” Fikiria mambo yafuatayo.

Kusikia: Sauti mbalimbali zinaweza kuchora picha fulani akilini, iwe ni sauti inayotokezwa mtu anapozungumza au anapotembea. Fernando mwanamume ambaye ni kipofu anasema, “Ninaweza kuwakumbuka na kuwatambua watu kutokana na sauti wanayotokeza wanapotembea au kuzungumza.” Juan, ambaye pia ni kipofu anasema, “Kipofu hutumia sauti kuwatofautisha watu.” Na kama ilivyo kwa watu wengine, vipofu wanaweza kutambua hisia ya mtu kwa kutegemea jinsi anavyozungumza.

Kipofu aliyezoea kutofautisha sauti mbalimbali anaweza kutambua mambo yanayomzunguka, iwe ni upande ambao magari yanaelekea, ukubwa wa chumba anachoingia, au umbali wa vitu vinavyoweza kumwangusha.

Kunusa: Uwezo wa kunusa unaweza pia kumsaidia kipofu kupata habari nyingi mbali tu na kujua chanzo cha harufu hiyo. Kwa mfano, kipofu anapotembea njiani, harufu humwezesha kuchora ramani akilini inayomsaidia kutambua mahali palipo na mkahawa, soko, na kadhalika. Naye huboresha ramani hiyo anapogusa vitu na kusikia sauti anazofahamu.

Kugusa: Francisco anasema, “Vidole vyangu ndiyo macho yangu.” Fimbo inayotumiwa na vipofu inaweza kuongeza uwezo huo wa “kuona” kwa kutumia hisi ya kugusa. Manasés aliyezaliwa akiwa kipofu na kujifunza tangu utotoni kutumia fimbo ya vipofu, alisema, “Ninatambua kabisa mahali nilipo kupitia kumbukumbu, fimbo yangu, na hisi zangu nyingine.”

Mtu akisoma gazeti Mnara wa Mlinzi katika maandishi ya vipofu

Kusoma gazeti la Mnara wa mlinzi katika maandishi ya vipofu

Hisi ya kugusa huwasaidia pia vipofu wengi kusoma wakitumia machapisho katika maandishi ya vipofu. Siku hizi pia kuna maandalizi kadhaa yanayoweza kumsaidia kipofu kuboresha ujuzi wake na hali yake ya kiroho. Mbali na machapisho yaliyo katika maandishi ya vipofu, maandalizi hayo yanatia ndani, rekodi za sauti na teknolojia ya kompyuta kwa ajili ya vipofu. Wanaweza kutumia vifaa hivyo kusoma Biblia na machapisho mbalimbali yanayotegemea Biblia.a

Paqui na mume wake, waliotajwa mwanzoni, wamepata tumaini na faraja isiyo na kifani kutokana na maandalizi hayo ya kiroho. Pia, wamepata msaada kutoka kwa kutaniko lao la Kikristo la Mashahidi wa Yehova, ambalo ni familia yao ya kiroho. Paqui anasema, “Sasa tunafurahia maisha na tunaweza kujitegemea kwa kadiri kubwa.”

Kwa kweli, upofu una changamoto nyingi. Lakini watu wanapokabiliana na hali hiyo na kuendelea kufurahia maisha, wanatuthibitishia jinsi mwanadamu alivyo na uwezo wa kubadilikana na hali bila kukata tamaa!

a Mashahidi wa Yehova huchapisha machapisho yanayotegemea Biblia katika maandishi ya vipofu kwa lugha zaidi ya 25.

Ingawa Mimi Ni Kipofu, Maisha Yangu Yanaridhisha

Marco Antonio na mbwa wake, Dante

Marco Antonio ni mume, baba, na mfanyabiashara. Alizaliwa akiwa kipofu. Alizungumza na mwandishi wa Amkeni! kuhusu mambo anayofurahia na changamoto anazokabili.

Unaendeshaje biashara yako?

Kazini, ninashughulikia maswali yanayoulizwa kupitia simu, nazungumza na wanunuzi na wauzaji, na kushughulikia masuala ya benki.

Unafanya nini ili kujiburudisha?

Ninapenda muziki kwa kuwa unaniliwaza. Ninacheza piano, ingawa si rahisi kwa sababu siwezi kusoma muziki ulioandikwa katika maandishi ya vipofu na wakati huohuo nicheze piano nikitumia mikono yote. Ninapocheza muziki fulani kwa mara ya kwanza, ninasoma maandishi kwa mkono wa kulia na kucheza nikitumia mkono wa kushoto. Kisha ninarudia nikitumia mkono ule mwingine. Ninapoukariri muziki wote, ninatumia mikono yote.

Je, umekabili changamoto zozote?

Tangu utotoni wazazi wangu na ndugu zangu walinitunza vizuri, na walinitendea kana kwamba ninaona. Mara nyingi nilijigonga na kuanguka, lakini nilizoea kufanya mambo ambayo hufanywa na mtu anayeweza kuona. Nilipokuwa mtu mzima, jambo lililoniudhi hasa ni kushindwa kuendesha gari.

Mimi ni mume na pia baba. Ninajitahidi kuitunza familia yangu ambayo inanipenda na kunitunza vizuri. Mwana wangu mpendwa, David, amerithi tatizo langu la kudhoofika kwa neva kuu ya jicho. Lakini ninajaribu kumwekea mfano mzuri. Ninataka ajifunze kwamba akiwa na subira na bidii anaweza kutimiza mengi.

Kwa nini uliamua kuwa na mbwa wa kukuongoza?

Ninapoambatana na mbwa wangu anayeitwa Dante ninakuwa salama na ninaweza kutembea haraka zaidi. Ninapoenda mahali fulani kwa mara ya kwanza, mke wangu Loli ambaye si kipofu huambatana nasi na hivyo mimi na Dante hukariri njia. Niseme wazi kwamba mwanzoni haikuwa rahisi kujihisi salama nikiongozwa na mbwa, lakini sasa ninamwamini Dante kabisa. Hata jambo gani litukie barabarani, yeye hukazia fikira kazi yake. Lakini ninapomvua mkanda yeye hutenda kama mbwa wengine tu.

Kwa kuwa wewe ni Shahidi wa Yehova, unafanyaje funzo lako la Biblia?

Kabla ya maendeleo kufanywa katika teknolojia kwa ajili ya vipofu, Loli alikuwa akinisomea Biblia na machapisho yanayotegemea Biblia. Alikuwa msaada mkubwa sana kwangu. Kwa sababu hiyo, niliweza kutoa hotuba kwenye mikutano ya kutaniko. Hata hivyo, siku hizi ninaweza kujisomea Biblia na kusoma machapisho katika maandishi ya vipofu. Ninaweza pia kutembelea tovuti ya Mashahidi wa Yehova—jw.org—na kupakua rekodi za sauti. Vilevile, nina mashine ya maandishi ya vipofu inayoniwezesha kusoma maandishi yoyote yanayojitokeza kwenye kompyuta. Mashine hiyo ina vipini ambavyo hujipanga na kuunda herufi za maandishi ya vipofu. Ni ya pekee sana.

Jambo ninalofurahia hata zaidi ni kusaidia kutayarisha machapisho katika maandishi ya vipofu kwenye ofisi ya tawi ya Mashahidi wa Yehova iliyopo Madrid nchini Hispania. Ili kuongeza ubora wa machapisho ya maandishi ya vipofu, wale wanaoyaandaa huomba maoni kutoka kwa vipofu. Kwa kweli ninahisi kuwa ninapendwa na kuthaminiwa sana na ndugu na dada zangu wa kiroho.

Unapenda kuchangamana na wengine?

Ndiyo, hasa pamoja na familia yangu na Mashahidi wenzangu ninaoambatana nao kuhubiri nyumba kwa nyumba. Ndugu zangu wa kiroho hunitendea kama vile wanavyowatendea wengine. Hata wakati mwingine wanasahau mimi ni kipofu!

Kwa kuongezea, kuhubiri kunanisaidia kuwaeleza wengine kuhusu tumaini linalopatikana katika Biblia. Kwa mfano, katika andiko la Isaya 35:5 tunasoma kwamba Ufalme wa Mungu utakapoanza kutawala dunia, “macho ya vipofu yatafunguliwa.” Yesu Kristo alipokuwa duniani aliponya vipofu na hivyo kutusaidia kuwazia hali itavyokuwa wakati ujao. (Mathayo 15:30, 31) Kwa hiyo, upofu ni tatizo la muda tu, na ndivyo ilivyo na ulemavu mwingine wowote. Dunia itakapokuwa Paradiso hakuna atakayesema, ‘Mimi ni mgonjwa au mlemavu.’—Isaya 33:24; Luka 23:43.

    Maktaba Kwenye Mtandao (1980-2025)
    Toka
    Ingia
    • Kiswahili
    • Shiriki
    • Mapendezi
    • Copyright © 2025 Watch Tower Bible and Tract Society of Pennsylvania
    • Masharti ya Utumiaji
    • Sera ya Faragha
    • Mpangilio wa Faragha
    • JW.ORG
    • Ingia
    Shiriki