Wasaidie Vipofu Wajifunze Kumhusu Yehova
1. Yesu alionyeshaje huruma kwa vipofu?
1 Kifo cha Yesu kilikuwa kimekaribia sana. Alipokuwa akiondoka jiji la Yeriko, vipofu wawili waliokuwa wakiomba-omba walipaza sauti wakisema: “Bwana, uturehemu!” Ingawa majaribu yaliyokuwa mbele yake yalikuwa yakimhangaisha sana akilini, Yesu alisimama, akawaita wanaume hao, na akawaponya. (Mt. 20:29-34) Tunawezaje kuiga huruma ya Yesu kwa vipofu?
2. Tunawezaje kumhubiria kipofu tunayekutana naye katika maeneo ya umma?
2 Wasaidie: Unapokutana na kipofu, labda katika eneo la umma, jitambulishe kwake na umweleze kwamba ungependa kumsaidia. Kwa kuwa mara nyingi vipofu hutendewa vibaya, mwanzoni huenda mtu huyo akawa na wasiwasi. Lakini anaweza kutulia unapomwonyesha upendezi na urafiki wa kutoka moyoni. Pia, kumbuka kwamba kuna watu ambao hawajapoteza kabisa uwezo wao wa kuona ingawa wanatambuliwa kuwa vipofu, na hilo litakusaidia kujua jinsi ya kumsaidia. Baada ya kumsaidia, labda unaweza kumwambia kwamba unafanya kazi ya elimu ya Biblia. Mwambie kuwa ungependa kumsomea andiko fulani, kama vile Zaburi 146:8 au Isaya 35:5, 6. Iwapo anaweza kusoma maandishi ya vipofu, muulize kama angependa kupata chapisho la maandishi ya vipofu litakalomsaidia kujifunza mengi zaidi kuhusu Biblia. Unaweza pia kumsaidia kupata machapisho ya kusikiliza kutoka kwenye Tovuti ya jw.org. Ikiwa kompyuta yake ina programu ya kusoma kwa sauti maandishi yaliyo kwenye skrini, huenda atafurahia makala zilizo kwenye Tovuti hiyo, pamoja na machapisho yanayoweza kupakuliwa katika muundo wa RTF (Rich Text Format).—Ona sanduku “Unapomsaidia Kipofu . . .”
3. Tunawezaje kuwatafuta vipofu katika eneo letu?
3 Watafute Vipofu: Si kawaida kukutana na vipofu tunapohubiri nyumba kwa nyumba kwa sababu wengi wao hawajihisi huru kuzungumza na watu wasiowafahamu ambao wamewatembelea. Hivyo basi, tunahitaji kujitahidi sana ‘kuwatafuta’ vipofu na kuwatolea ushahidi. (Mt. 10:11) Je, unafanya kazi au kusoma pamoja na mtu aliye kipofu? Chukua hatua ya kwanza kuzungumza naye. Iwapo kuna shule ya vipofu katika eneo lenu, jitolee kuwapa machapisho ya maandishi ya vipofu ili yawekwe katika maktaba ya shule. Je, unamjua mtu yeyote aliye na mshiriki wa familia ambaye ni kipofu? Je, eneo lenu lina mashirika yanayotoa msaada kwa ajili ya vipofu au yaliyo na majengo ya makazi ambamo mna vipofu? Mweleze mshiriki huyo wa familia, au mtu aliye kwenye mapokezi ya jengo hilo la makazi, au msimamizi wa shirika hilo kwamba Mashahidi wa Yehova wanapenda sana kuwasaidia vipofu, na ujitolee kuwaletea machapisho ya vipofu au rekodi za kusikiliza. Mwonyeshe ahadi ya Biblia kwamba karibuni Mungu ataondoa upofu kabisa. Ukipenda, unaweza kumwonyesha video kutoka kwenye Tovuti ya jw.org yenye kichwa “Without It, I Would Feel Lost,” inayosimulia kisa cha mwanamume mmoja kipofu ambaye amefaidika kutokana na Biblia ya maandishi ya vipofu. Unapomweleza kusudi lako la kutaka kuwasiliana na vipofu, huenda ukapata fursa ya kuzungumza na mtu aliye kipofu.
4. Jambo lililoonwa na Janet linatufundisha nini?
4 Dada mmoja kipofu anayeitwa Janet alitembelea jengo lililo na wakazi ambao ni vipofu. Alianzisha mazungumzo na mwanamke mmoja mchanga. Janet alimwambia, “Yesu aliwaponya vipofu ili kuonyesha mambo atakayowafanyia watu wote walio vipofu.” Wakazungumzia andiko la Ufunuo 21:3, 4, na Janet akamweleza jinsi ahadi hiyo itakavyotimizwa na Ufalme wa Mungu. Mwanamke huyo alinyamaza kisha akasema: “Sijawahi kusikia jambo hilo kutoka kwa mtu aliye kipofu. Watu wengi walio na uwezo wa kuona huamini kwamba vipofu hupatwa na ulemavu huo kwa sababu ya jambo ambalo wao au mababu zao walifanya.” Janet alimtumia mwanamke huyo barua pepe ya kumwonyesha jinsi ya kupata kitabu Biblia Inafundisha kwenye jw.org, na sasa wanajifunza Biblia mara mbili kwa juma.
5. Ingawa hatuwezi kuwaponya vipofu kama alivyofanya Yesu, tukiwaonyesha upendezi tutapata baraka zipi?
5 Hatuwezi kuwaponya vipofu kama alivyofanya Yesu, lakini tunaweza kuwasaidia wote ambao wamepofushwa akili na mungu wa mfumo huu wa mambo, kutia ndani wale ambao ni vipofu halisi, waelewe kweli ya Neno la Mungu. (2 Kor. 4:4) Yesu aliwaponya wale wanaume wawili karibu na mji wa Yeriko kwa sababu ‘aliwasikitikia.’ (Mt. 20:34) Tukiwaonyesha vipofu upendezi kama huo, tutafurahia pendeleo la kuwasaidia wengine wajifunze kumhusu Yehova, ambaye atakomesha upofu milele.