Watchtower MAKTABA KWENYE MTANDAO
Watchtower
MAKTABA KWENYE MTANDAO
Kiswahili
  • BIBLIA
  • MACHAPISHO
  • MIKUTANO
  • w94 8/15 kur. 5-7
  • Kufumbua Macho ili Kuona Habari Njema

Hakuna video yoyote kwa sasa.

Samahani, haikuwezekana kupakia video.

  • Kufumbua Macho ili Kuona Habari Njema
  • Mnara wa Mlinzi Unaotangaza Ufalme wa Yehova—1994
  • Vichwa vidogo
  • Habari Zinazolingana
  • Kushinda Upofu wa Kiroho
  • Ponyo Pekee la Kudumu —Ufalme wa Mungu
  • Furaha Katika Ulimwengu Mpya wa Mungu
  • Wasaidie Vipofu Wajifunze Kumhusu Yehova
    Huduma Yetu ya Ufalme—2015
  • Kuna Tumaini Gani kwa Vipofu?
    Mnara wa Mlinzi Unaotangaza Ufalme wa Yehova—1994
  • Kuishi Bila Kuona
    Amkeni!—2015
  • Hakuna Fedha kwa Vipofu
    Amkeni!—1991
Pata Habari Zaidi
Mnara wa Mlinzi Unaotangaza Ufalme wa Yehova—1994
w94 8/15 kur. 5-7

Kufumbua Macho ili Kuona Habari Njema

“ANGA haipungui kuwa buluu kwa sababu mwanamume kipofu haioni,” yasema methali fulani ya Kidenmark. Lakini katika maisha zetu za kila siku zenye shughuli nyingi, je, kweli sisi huona kwamba anga ni buluu? Je! sisi huona wakati ujao tukiwa na uhakika? Je! kweli twaamini habari njema ambayo Neno la Mungu, Biblia, hutoa?

Katika makala inayotangulia, tulifikiria mambo mbalimbali kuhusiana na upofu halisi. Acheni sasa tuchunguze namna ya uwezo wa kuona iliyo ya maana zaidi. Hiyo yahusisha furaha yetu yenye kudumu pamoja na mataraja ya wapendwa wetu.

Bila shaka, twakabili “nyakati za hatari zilizo ngumu kushughulika nazo.” (2 Timotheo 3:1, New World Translation) Ni nini kinachotokea watu wanapong’ang’ana kupata riziki, kuvumilia magumu ya kiafya na matatizo ya familia, na kukabiliana na udhalimu wa kijamii na ukosefu wa upendo? Kwa kuhuzunisha, watu wengi hupata kwamba kutumaini kwao wanadamu wenzao, dini, na serikali, kwafifia. Wakiwa wanahisi kwamba hakuna suluhisho, wengine hukata maneno kwamba matatizo yao hayatasuluhishwa kamwe kwa njia ya kawaida. Katika gazeti la habari la Kibrazili Jornal da Tarde, Jacob Pinheiro Goldberg aonelea hivi: “Watu, wanapokabili uhalisi mkatili, huhisi kasirani sana kwa sababu ya makosa hivi kwamba hawasababu mambo kwa njia ya kiakili, nao hutegemea dini ya kifumbo inayokatisha tamaa.” Hata hivyo, hata mambo yanapoharibika, twataka kutumia fikira timamu, sivyo?

Ebu wazia kidogo kwamba wahitaji makao kwa ajili ya familia yako, na una pesa za kutosha. Labda watafuta huku na huku na kuzuru nyumba mbalimbali katika ujirani tofauti-tofauti. Ingawa wauzaji nyumba na nyanja wajaribu kuridhisha matakwa yako, huwezi kupata makao unayotamani. Hata hivyo, kwa kuwa uradhi na hali njema ya familia yako inahusika, wewe hukati tamaa, sivyo? Sasa ebu wazia ile furaha upatapo hatimaye ile nyumba uliyotamani sana.

Kama vile ungetumia wakati ukitafuta makao mapya, kwa nini usiichunguze Biblia ili kuona suluhisho la matatizo yako? Kama vile ni lazima tufikirie mambo ya hakika tufanyapo maamuzi juu ya makao, ndivyo tuhitajivyo kusababu kwa utimamu juu ya yale tusomayo katika Neno la Mungu. Na lenye manufaa hata zaidi ya kupata makao ni kuona na kukubali kwetu ile kweli kuhusu Yehova Mungu na Yesu Kristo. Yesu alisema hivi: “Uzima wa milele ndio huu, Wakujue wewe, Mungu wa pekee wa kweli, na Yesu Kristo uliyemtuma.”—Yohana 17:3.

Lakini ikiwa ujumbe wa Biblia ni wenye thamani hivyo, kwa nini wengi sana huendelea kuwa vipofu kuelekea habari yayo njema? Kwanza, na huenda hii ikawashangaza watu wengi, “dunia yote pia hukaa katika yule mwovu.” (1 Yohana 5:19) Kwa sababu hiyo, Shetani Ibilisi “amepofusha fikira zao wasioamini, isiwazukie nuru ya injili ya utukufu wake Kristo aliye sura yake Mungu.” (2 Wakorintho 4:4) Ingawa twaona kwa macho yetu, ni ubongo unaofafanua ile nuru inayoingia jichoni. Kwa hiyo, kuwa kipofu huelezwa pia kuwa “bila uwezo au bila nia ya kufahamu au kuamua.” Hilo latukumbusha usemi unaopendwa na wengi: “Hakuna walio vipofu zaidi ya wale wasiotaka kuona.”

Mtu aliye kipofu hawezi kuona vitu vilivyo mbele yake, kwa hiyo huenda akawa katika hatari ya kupata madhara. Upofu halisi wa walio wengi hauwezi kuponywa kwa sasa, hata hivyo hakuna alazimikaye kuendelea akiwa kipofu kiroho.

Kushinda Upofu wa Kiroho

Kama vile hali zisizo safi vya kutosha ziwezavyo kudhoofisha uwezo wa kuona, mazingira yaliyoshuka kiadili yaweza kuchangia upofu wa kiadili. Zaidi ya hayo, Yesu Kristo alionya dhidi ya mafundisho na mapokeo yaliyofanyizwa na wanadamu. Alieleza wazi kwamba viongozi wa kidini wa wakati huo wa nyuma walikuwa wakiongoza vibaya kundi lao: “Hao ni viongozi vipofu wa vipofu. Na kipofu akimwongoza kipofu mwenzake, watatumbukia shimoni wote wawili.”—Mathayo 15:14.

Badala ya kudanganywa na viongozi vipofu, wale wafumbuao macho yao ili kuona habari njema kuhusu Ufalme wa Mungu ni wenye furaha kama nini! Yesu alijulisha hivi: “Mimi nimekuja ulimwenguni humu kwa hukumu, ili wao wasioona waone.” (Yohana 9:39) Lakini, wale walio vipofu kiroho wanaweza kupataje kuona? Basi, acheni tuendeleze mazungumzo yetu kuhusu upofu halisi.

Maandalizi mbalimbali yanapatikana sasa kwa wale wenye kasoro ya macho. Hali haikuwa hivyo sikuzote. Kabla ya Valentin Haüy kuanzisha shule ya pekee kwa ajili ya vipofu katika 1784, hakukuwa na jitihada kubwa za kuwasaidia vipofu. Baadaye, Louis Braille alibuni mfumo uitwao kwa jina lake; alifanya hivyo ili kusaidia wale wenye kasoro ya macho kusoma.

Namna gani wale walio vipofu kiroho? Katika miaka ya karibuni jitihada kubwa zimefanywa ili kujulisha habari njema hata katika sehemu za mbali zaidi za dunia. (Mathayo 24:14) Mashahidi wa Yehova wanafurahi kuwaletea tumaini wale wenye upofu wa mfano na pia wale wenye upofu wa kimwili.

Mwanamke fulani Mbrazili aliandika hivi: “Nataka kusema kwamba kujapokuwa kupungukiwa kwangu kimwili, naweza kuona—kiroho. Ni Mungu wa ajabu kama nini! Tunafurahi kujua kwamba ‘Yehova atafumbua mkono wake na kushibisha kila kilicho hai matakwa yake.’” (Zaburi 145:16) Na Jorge, aliye kipofu kimwili, akumbuka hivi: “Kwa hakika maisha yangu yaweza kugawanywa katika sehemu mbili: kabla na baada ya Mashahidi. . . . Kupitia wao, nilianza kuona ulimwengu kwa uwazi na uangavu. Nasikilizana vizuri sana na kila mtu kutanikoni.” Ingawaje hilo ni jambo la kupendeza sana, Biblia hutupa sisi uhakikishio kwamba karibuni hakuna yeyote duniani atakayekuwa kipofu—kihalisi wala kiroho. Hilo litakuwaje? Itathibitikaje kuwa kweli kotekote duniani kwamba “BWANA huwafumbua macho waliopofuka”?—Zaburi 146:8.

Ponyo Pekee la Kudumu —Ufalme wa Mungu

Ujapokuwa ujuzi ulioongezeka wa kitiba, magonjwa mengi huendelea kusababisha upofu, umivu, na kifo. Ni nini basi, kinachohitajiwa ili kufutilia mbali utapia mlo, hali zisizo safi vya kutosha, na msononeko unaoondolea mbali uwezo wa kuona na pia shangwe ya uhai? Kule kuwaponya vipofu na wengine kwa Yesu kulikuwa kigezo cha kadiri ndogo kwa wakati ujao. Kwa furaha, kazi yake ya kufundisha na kuponya ilifananisha baraka ambazo zingeenezwa duniani chini ya serikali ya Ufalme wa Mungu.

Uponyaji wa kadiri ya ulimwenguni pote uko karibu.a Programu hii ya uponyaji wa kimungu inaonyeshwa vizuri na mtume Yohana: “Akanionyesha mto wa maji ya uzima, wenye kung’aa kama bilauri, ukitoka katika kiti cha enzi cha Mungu na cha Mwana-Kondoo, katikati ya njia kuu yake. Na upande huu na upande huu wa ule mto, ulikuwapo mti wa [“miti ya,” NW] uzima, uzaao matunda, aina kumi na mbili wenye kutoa matunda yake kila mwezi; na majani ya mti huo ni kuwaponya mataifa.”—Ufunuo 22:1, 2.

Semi kama vile “maji ya uzima” na “mti wa [“miti ya,” NW] uzima” yaonyesha kwamba baada ya mfumo mbovu wa leo kukoma, maandalizi ya uponyaji ya Ufalme wa Mungu yatainua wanadamu hatua kwa hatua hadi ukamilifu. Kwa kweli, manufaa za dhabihu ya fidia ya Yesu (kutia na msamaha kamili wa dhambi), pamoja na ujuzi kuhusu Yesu Kristo na Baba yake, utaleta afya kamilifu na uhai udumuo milele.—Yohana 3:16.

Furaha Katika Ulimwengu Mpya wa Mungu

Wazia basi, dunia bila uhalifu, uchafuzi, wala umaskini. Ona akilini familia yako ikiishi kwa amani katika Paradiso itakayorudishwa. (Isaya 32:17, 18) Litakuwa jambo lenye kupendeza kama nini kuona unamnanamna wa rangi ukiwa na akili na hisi kamilifu!

“Hali ya asili ya mwanadamu ni kuishi katika mazingira yanayobadilika daima—ya nuru, rangi, maumbo. Katika maumbile hakuna mazingira yanayokaa daima bila kubadilika,” asema Faber Birren. “Rangi ni mojapo mambo ya asili yenye kufurahisha katika ulimwengu huu. Ni jambo la kawaida la maumbile, na sehemu kubwa ya maisha yenye kufurahisha huitegemea.”

Zawadi ya uwezo wa kuona ni yenye thamani kama nini! Itakuwa shangwe iliyoje wakati macho yaliyokuwa kipofu wakati mmoja—kihalisi au kiroho—yatakapoona!

Ndiyo, katika Paradiso itakayorudishwa inayokuja, upofu na ulemavu mwingine-mwingine hautasababisha huzuni tena! Hakuna atakayeongozwa vibaya tena. Kwa kuwa upendo wa kweli utaenea, wote watanurishwa kiroho. Hayo na mengi zaidi, yako huko mbele tu, lakini sasa hivi ni wakati wa kuwa mwenye kukubalika kwa Yeye atakayetimiza ahadi yake ya kiunabii: “Ndipo macho ya vipofu yatafumbuliwa”!—Isaya 35:5.

[Maelezo ya Chini]

a Tafadhali chunguza uthibitisho unaotolewa katika kitabu Unaweza Kuishi Milele Katika Paradiso Duniani, sura 18, kilichotangazwa na Watchtower Bible and Tract Society of New York, Inc.

[Picha katika ukurasa wa 7]

Ndipo macho ya vipofu yatafumbuliwa!

    Maktaba Kwenye Mtandao (1980-2025)
    Toka
    Ingia
    • Kiswahili
    • Shiriki
    • Mapendezi
    • Copyright © 2025 Watch Tower Bible and Tract Society of Pennsylvania
    • Masharti ya Utumiaji
    • Sera ya Faragha
    • Mpangilio wa Faragha
    • JW.ORG
    • Ingia
    Shiriki