Sura ya 22
Ibada ya Kweli Njia ya Maisha
1. Ni tumaini gani lililo mbele yetu, lakini ni lazima tufanye nini ili tulipate?
UNALO tumaini la uzima wa milele mbele yako chini ya ufalme wa Mungu. Kama ulivyokwisha kuona, tumaini hili limewekwa imara juu ya kweli ya Neno la Mungu mwenyewe. Utaweza kulifikia ikiwa kweli unampenda Mungu na kumwabudu yeye kwa ‘kuenenda katika kweli.”-2 Yohana 1-4.
2. Ni kwa maneno gani ibada ya kweli ilijulikana miongoni mwa Wakristo wa kwanza? Kwa nini?
2 Ibada ya kweli inamaanisha zaidi kuliko kujua kweli tu. umaanisha hata zaidi kuliko kusema na kutangaza kweli kwa wengine. Humaanisha kusadiki na kutenda juu ya kweli ‘kuenenda katika kweli’ kwa kuitumia katika maisha zetu za kila siku. (Yakobo 1:22-25) Ibada ya kweli iliongoza sana maisha za kila siku za Wakristo wa kwanza hata ikajulikana kama “Njia hii” na “njia ya kweli.” (Matendo 9:2; 2 Petro 2:2) Ndiyo “njia” iliyoonyeshwa na Mungu kwa waabudu wote wa kweli kuishi maisha zao kadiri washindaniavyo mradi wa uzima wa milele.
3. Kwa nini ni lazima tutumie kweli ya Neno la Mungu katika kila utendaji wa maisha?
3 Hivyo, ibada yetu ya Yehova Mungu haiwezi kuwa kitu fulani kilicho mbali na yanayobaki ya maisha yetu. Badala yake, lazima tuitumie kweli ya Neno lake katika kila utendaji wa maisha. “Mlapo, au mnywapo, au mtendapo neno lo lote, fanyeni yote kwa utukufu wa Mungu.” (1 Wakorintho 10:31; tazama pia Wakolosai 3:17.) Kila tendo letu lapaswa lipatane na kweli ya Neno la Mungu, na hivyo lilete utukufu kwa Mungu. Jambo hili litakuwa kwa furaha yetu idumuyo. Kanuni za haki za Neno lake hazibadiliki kupatana na mahali pa kukaa au hali za mtu peke yake. Sikuzote ni za kweli, sikuzote ni za haki.—Zaburi 119:142.
4. Ni jambo gani lililomo katika kuuvaa utu mpya?
4 Ikiwa kweli unafuata ibada ya kweli, itakuwa na maana gani kwako sasa? Italeta maisha yako yote katika upatano na njia ya Mungu. Neno Lake linatuambia hivi: “Mvue kwa habari ya mwenendo wa kwanza utu wa zamani . . . mfanywe wapya katika roho ya nia zenu; mkavae utu mpya, ulioumbwa kwa namna ya Mungu katika haki na utakatifu wa kweli.” (Waefeso 4:22-24) Kuvaa utu mpya maana yake ni kuacha kabisa msemo wa matusi na msemo wa uongo kwa kupendelea msemo ulio safi na wa kweli. Maana yake ni kuweka mwenendo wa unyofu na wenye kustahiki badala ya ulevi na uasherati. Maana yake ni kusitawisha, si ulapupa, bali kufikiria wengine na ukarimu.—Wakolosai 3:5-10.
5. Je! inawezekana kudhihirisha sifa za kimungu katika nyakati zote? Jinsi gani?
5 Jinsi inavyoburudisha wakati sifa za kimungu zinapoonyeshwa katika njia ambayo mtu hushughulika na watu wengine katika maisha yake ya kila siku —na washiriki wa jamaa, wenzi wa kazi, watu ambao anawajua sana na wageni! (Wakolosai 3:12-14, 18-23) Lakini, je! wewe wafikiri ni vigumu kufanya badiliko hili, na kulidumisha kila siku? Kwa msaada wa roho ya Mungu unaweza. Kupitia kwa ibada ya kweli unaweza kuzaa matunda ya roho ya Mungu katika maisha yako.—Wagalatia 5:19-24.
6. (a) Jinsi gani ibada ya kweli huvuta kufanywa kwa uamuzi wa mtu? (b) Eleza jinsi ibada ya kweli huvuta kazi ya Mkristo na michezo yake.
6 Wakati ibada ya kweli inapokuwa ndiyo njia yako ya maisha itakuwa uongozi wako wa sikuzote. Katika kufanya maamuzi, makubwa au madogo, utajifunza kujiuliza mwenyewe: “Ni jambo gani litakalokuwa lenye kupendeza kwa Yehova Mungu? Kanuni katika Neno lake zinaonyesha ni nini ulio mwendo mwema na wa hekima?” (Zaburi 119:105; Mithali 3:1-6) Kwa mfano, Mkristo wa kweli ataangalia kwamba kazi yake ya kimwili haizuii utumishi wake kwa Yehova Mungu, au haihusu kazi au mazoea ambayo Biblia hulaumu. (Waebrania 13:5, 18; Isaya 2:3, 4; Ufunuo 18:4) Hata wakati inapokuja kwa michezo, lazima Neno la Mungu liongoze katika kuchagua jambo fulani lenye kujenga, nzuri. (Wafilipi 4:8) Hakuna jambo katika maisha yako ambalo halitavutwa na ibada ya kweli katika njia ya kufaa.
THAWABU YA FURAHA KWA USTAIHMILIVU
7. (a) Kwa nini huenda isiwe rahisi kuendelea kuenenda katika “njia ya kweli”? (b) Wakati wa kukabiliwa na kupinga, ni nini ulio mwendo mwema, kwa sababu ya Waebrania 10:36?
7 Walakini, kwa sababu ya mikazo ambayo ulimwengu huleta juu ya Wakristo wa kweli, huenda isiwe rahisi kuendelea kuenenda kwa uaminifu katika “njia ya kweli.” Yesu alionya kwamba waabudu wa kweli wangechukiwa na kuteswa, kama yeye alivyochukiwa na kuteswa. (Yohana 15:18-20; 2 Timotheo 3:12) Huenda zikazuka hali zitakazotisha kuzuia funzo lako la kawaida la Biblia au ushirika wako na Wakristo wenzako penye mikutano ya kundi. Huenda kupinga kukafanya kazi ya kuhubiri kuwa yenye shida, hata kuwa yenye hatari. Je! wewe utafanya nini? Biblia inashauri hivi: “Mna haja ya ustahimilivu, ili mkiisha kuyafanya mapenzi ya Mungu, mpate kupokea utimizo wa ahadi.” (Waebrania 10:36, NW) Hivyo, mwendo wa pekee wa haki ni kuendelea mbele kwa ujasiri katika utumishi wa Mungu, ukimtumainia Yeye kukutegemeza.—Zaburi 55:22; Waebrania 6:11, 12.
8. Kwa nini tunaweza kuwa na furaha ya kweli ikiwa tunashinda jaribu la imani yetu liletwalo na kupinga?
8 Kwa Wakristo wa kwanza, mwanafunzi Yakobo aliandika hivi: “Ndugu zangu, hesabuni ya kuwa ni furaha tupu, mkiangukia katika majaribu mbalimbali; mkifahamu ya kuwa kujaribiwa kwa imani yenu huleta [ustahimilivu].” (Yakobo 1:2, 3) Naam, twaweza kuwa na furaha ya kweli ikiwa, chini ya kupinga, tunashinda jaribu la imani yetu. Kwa nini? Kwa sababu kwa kustahimili tunategemeza upande wa Baba yetu wa mbinguni katika swali kubwa la maana sana lililotokezwa mbele ya ulimwengu. wote. Tena, Mwana wa Mungu hutuhakikishia hivi: “Kwa ustahimilivu kwa upande wenu mtajipatia nafsi zenu.” Naam, kwa ustahimilivu utapata thawabu ya uzima wa milele.—Luka 21:16-19, NW; 1 Petro 2:21-23; 2 Wathesalonike 1:4, 5.
9. (a) Kwa nini tunaishi katika wakati wenye baraka zaidi wa historia yote ya kibinadamu? (b) Ni tumaini gani lenye furaha lililoko mbele ya wale wasioiacha kamwe njia ya kweli?
9 Tunaishi katika wakati wenye baraka zaidi kuliko wakati wo wote mwingine wa historia yote ya kibinadamu. Karibuni sasa Yehova na Mwanawe, Kristo Yesu, watausafisha ulimwengu wote kwa kuondoa adui wote wa ufalme wa Mungu. Lo! itakuwa furaha namna gani, baada ya vita hiyo, kuishi chini ya hali zenye haki katika dunia ya paradiso, itakayokuwa huru na maumivu, huzuni na mauti! Wewe waweza kuwa na uhakika kamili katika tumaini hilo, kwa sababu “Mungu . . . hawezi kusema uongo.” (Tito 1:2, NW) Basi, tazama mbele kwenye tumaini hilo lenye baraka, na usiiache kamwe ibada ya Yehova, Mungu wa kweli. Endelea katika njia ya kweli, kwa maana “ulimwengu unatoweka na ndivyo na tamaa yake lakini yeye ambaye hufanya mapenzi ya Mungu hudumu milele.”—1 Yohana 2:17, NW.