Ibada ya Kweli Ni Njia ya Maisha Yenye Kufaulu
“Lazima ukumbuke [kitabu hiki cha torati] mchana na usiku ili upate kuyashika kwa bidii yote yaliyoandikwa ndani yacho. Ndipo utafanikiwa na kufaulu katika yote uyafanyayo.”—Yos. 1:8, “New English Bible.”
1. (a) Dini nyingi zaidi zinategemea ibada ya namna gani? (b) Tofautisha hilo na ibada ya kweli.
DINI nyingi hukazia sherehe zilizo takatifu sana za ibada, huku wakitaja kwa mdomo tu kwamba ibada yapaswa kubadili njia ya mtu ya maisha. Hivyo programu zao za kidini zinarudia-rudia ibada zile zile za sherehe na kuomba pesa za kununua vifaa vinavyotumiwa katika ibada hiyo. Ibada ya kweli haikazii sherehe za kidesturi tu. Ingawa ibada ya kweli inafanya waabudu washirikiane na wenzao, inahusu pia kila upande mwingine wa maisha ya mtu. Ni kielelezo cha maisha, njia ya maisha. Ndiyo sababu Biblia yataja Ukristo wa kweli kuwa “Njia hii” na “njia ya kweli.”—Matendo 9:2; 19:9; 2 Pet. 2:2.
2. (a) Yesu alionyeshaje kwamba ibada si sherehe tu? (b) Maana yake nini kuabudu “kwa roho”?
2 Yesu alionyesha pia kwamba ibada ya kweli ni njia ya maisha wakati alipomwambia mwanamke Msamaria hivi “Waabuduo halisi watamwabudu Baba katika roho na kweli . . . wamwabuduo yeye imewapasa kumwabudu katika roho na kweli.” (Yohana 4:23, 24) Yesu alitia mkazo ule ule juu ya ‘kuabudu kwa roho’ na ‘kuabudu kwa kweli,’ kuonyesha upande mwingine wa maana katika ibada. Maana yake nini ‘kuabudu kwa roho’? Katika maneno yanayozunguka mazungumzo yake na mwanamke Msamaria, Yesu alitofautisha ibada hiyo na ile inayotumia vitu vionekanavyo, kama mlima au mji. (Mstari 21) Badala ya kutegemea vitu hivyo, vinavyoonekana au kuguswa, mwabudu wa kweli huonyesha imani na kuendelea kuwa na “roho” ya kuabudu, akiabudu kwa uchangamfu au akifuata roho ya ibada yenyewe. Kwa njia hiyo anaabudu kwa roho, akiongozwa na maono yake ya moyoni amtumikie Mungu kupatana na kweli inayokaa akilini mwake nyakati zote na kumwongoza katika yote anayofanya.—2 Kor. 5:7.
3. Yehova alitaka kuabudiwaje tangu mwanzo?
3 Hiyo yapatana na vile Mungu alivyokusudia ibada iwe tangu mwanzo. Yeye hakuagiza viumbe wa kwanza wa kibinadamu wafuate sherehe fulani au desturi fulani wanapomwabudu. Walipaswa kumtumikia au kumwabudu Muumba wao kwa kufanya mapenzi yake kwa uaminifu hasa. Mungu aliwafunulia “mapenzi” hayo ili waweze kuishi kupatana na mambo halisi ya maisha. (Mwa. 1:28, 29; 2:16, 17, 19-25; Mt. 19:4, 5) Bila shaka, wakati ulipozidi kupita, Mungu aliwaeleza kweli zaidi zilizokuwa za lazima kuwawezesha wapanue vizuri makao yao ya dunia, wapanue jamaa yao na utendaji wao. Kama wangalitii maagizo hayo wangalitimiza matakwa makuu ya ibada ya kweli. Kama wanadamu wawili wa kwanza wangalichagua kufuata mwendo huo, kweli hizo zingalikuwa njia ya maisha kwao na wazao wao. Njia yao ya maisha ingalifaulu; isingalishindwa, kwa sababu ilipatana na kweli, mambo halisi, kutia na uhakika wa kwamba Yehova ndiye mwenye enzi kuu na ana uwezo wa kuwapa watu uzima.
DHAMBI YAONGEZA MAMBO KATIKA IBADA
4. Kwa sababu gani sherehe fulani zikawa za lazima katika ibada?
4 Lakini, dhambi na kutokutii ilipoingia, ikawa lazima ibada ya kweli iwe na mambo mapya ili ipatane na magumu mapya yaliyopata wanadamu. Mambo mapya hayo ya ibada, yalikuwa na sherehe fulani, tena yalikuwa na kusudi la muda lakini la lazima, lenye kufananisha jambo fulani. Sasa kizuizi kiliingia kati ya wanadamu wasiokamilika na Muumba mkamilifu. Wazao wa Adamu walipaswa kuelezwa wazi uhusiano huu mpya pamoja na njia ya Mungu ya kumaliza mtengano huo. Kwa hiyo, kukawa na dhabihu, ukuhani na mahali patakatifu baadaye, ili kufananisha “kweli” hizo, uhalisi wa mambo ambao sasa ulikuwa kati ya wanadamu na Muumba wao.
5. (a) Biblia yaelezaje kusudi la sherehe zilizokuwa chini ya Torati? (b) Zilikwisha wakati gani na jinsi gani?
5 Lakini, mtume Paulo aandika kwamba mipango yote hiyo ilikuwa “kivuli cha mema yatakayokuwa, wala si sura yenyewe ya mambo hayo.” (Ebr. 10:1) Basi, desturi na dhabihu peke yake hazikuwa ukweli wote. Lakini zilisaidia kuelewesha watu kweli na kuwafanya waikubali “wakati” ulipowekwa ulipofika kuelewesha hilo wazi kupitia kwa Kristo Yesu. “[Mahali patakatifu hapa] ndiyo mfano wa wakati huu uliopo sasa; wakati huo sadaka na dhabihu zinatolewa, zisizoweza kwa jinsi ya dhamiri kumkamilisha mtu aabuduye, kwa kuwa ni sheria za jinsi ya mwili tu . . . zilizoamriwa hata wakati wa matengenezo mapya.” (Ebr. 9:9, 10) Hivyo kusudi la “sheria” hizi lilipotimizwa Yesu alipofika, ibada ya sherehe iliacha kustahili machoni pa Mungu. Ilikuwa lazima mahali pake pachukuliwe na mambo halisi, kwa maana “mambo hayo ni kivuli cha mambo yajayo; bali mwili ni wa Kristo.” (Kol. 2:16, 17) Ndipo Yesu mwenyewe akawa “njia, na kweli.”—Yohana 14:6; 1:17.
KWELI ZISIZOBADILIKA ZATAKIWA SIKUZOTE
6. Sikuzote ni nini imekuwa sehemu ya lazima ya ibada ya kweli?
6 Ingawa “sheria” hizo walizopewa Waisraeli zilikuwa za lazima kwa muda, jambo kuu katika ibada ya Yehova ambalo limetiliwa mkazo sikuzote ni kuishi kulingana na kweli zisizobadilika. Sikuzote imani, haki, kutokuwa na hatia ya damu, ukweli na utii kwa mapenzi ya Mungu ndiyo mambo ya maana zaidi yatakayotakiwa ili kuweza kumfikia. Sikuzote mtu “aliye na mikono safi na moyo mweupe” ndiye ameweza kupanda mlimani kwa Yehova, si yule mwenye kumtolea Mungu zawadi tu. (Zab. 24:3-6; 15:1-4; Mit. 3:32) Kanuni hizi kuu za kweli ni njia ya maisha ambayo haikubadilika tangu mwanzo. Mika auliza hivi: “Nimkaribie [Yehova] na kitu gani, na kuinama mbele za Mungu aliye juu? Je! nimkaribie na sadaka za kuteketezwa, na ndama za umri wa mwaka mmoja? . . . Ee mwanadamu, yeye amekuonyesha yaliyo mema; na [Yehova] anataka nini kwako, ila kutenda haki, na kupenda rehema, na kwenda kwa unyenyekevu na Mungu wako!”—Mik. 6:6-8; Hos. 6:6; 1 Sam. 15:22.
7. (a) Yehova ataka nini hasa kutoka kwetu? (b) Kwa sababu gani mtu avutwa kwa urahisi na njia ya Yehova?
7 Yehova hatuwekei matakwa kwa ukatili wala bila kufikiri sawasawa. Yeye huagiza viumbe wake wafanye mambo wanayopaswa kuwa wakimfanyia yeye na wanadamu wenzao. ‘Kwenda na Mungu wetu’ katika njia ya kweli kunapatana na ‘sheria iliyoandikwa mioyoni mwetu’ na Yehova alipoumba wazee wetu wa kwanza. (Rum. 2:14, 15) Dhamiri hiyo au maono ya ndani ya kujua yaliyo haki na makosa inavutwa kwa urahisi na njia ya kweli. Kwa hiyo watu wanasikia na kuona kwamba kweli inafaa kwa sababu ya mabaki ya dhamiri waliyorithi. Hivyo Paulo angeweza kusema hivi: “Tumekataa mambo ya aibu yaliyositirika [kusema uongo], . . . bali kwa kuidhihirisha iliyo kweli twajionyesha kuwa na haki, dhamiri za watu zikitushuhudia mbele za Mungu.”—2 Kor. 4:2; 5:11; 6:4-10.
NJIA YA MAISHA YENYE KUFAULU
8. Ni nini kinachotofautisha kweli na mambo ya kuwaziwa tu? Toa mfano.
8 Wale wanaochagua kutembea katika kweli kama njia ya maisha wanafaidika sana. Kweli inafaulu inapozoewa. Wanasayansi wakigundua jambo na kulidhania kuwa kanuni ya kisayansi, lazima kwanza lijaribiwe kwa kuzoewa kabisa ndipo liweze kutambuliwa kwamba si kisio tu. Lazima lifaulu katika njia zinazotumika: katika mwundo, katika kuponya ugonjwa, na kadhalika. Lakini, katika maisha, watu wenye akili, wanafilosofia na viongozi wa dini wanaobadili sana kuwaza na mwenendo wa watu leo wameshindwa wenyewe katika jaribu hili. Mara nyingi wanayosema na kuandika yanasikika kuwa mema. Huenda wakasihi watu kwa maneno hayo na kutoa sababu nyingi zenye maneno mazuri. Lakini mafundisho mengi yao juu ya maisha si ya kweli. Kwa sababu gani? Mafundisho hayo hayasaidii! Matokeo yenye kusikitisha ya filosofia zao yanatuzunguka kila mahali.
9. Ni nini kinachohakikisha kwamba ibada ya kweli hufanya njia ya maisha ifaulu?
9 Lakini kumbukumbu la Biblia linaloonyesha maisha yenye tumaini hakika na kusudi ya watumishi wa Mungu wa zamani na vilevile ya wale wanaozoea kweli leo, lahakikisha kwamba ibada ya kweli ndiyo njia ya pekee ya maisha yenye kufaulu. Utii kwa amri za Mungu umetofautisha sikuzote waabudu wa kweli na watu wa vizazi vyao. Kama tulivyozungumza katika makala iliyotangulia, Israeli wa kale walikuwa bora kuliko mataifa ya siku hizo, waliposhikamana kwa uaminifu na “namna ya maarifa na ya kweli katika torati” waliyopewa kupitia kwa Musa. (Rum. 2:20; Yos. 1:8; Neh. 9:13) Ukristo wa karne ya kwanza ulibadili sana pia njia ya maisha ya walioukubali. Mwanahistoria mashuhuri John Lord aliandika katika kitabu chake The Old Roman World akasema:
“Ushindi wa kweli wa Ukristo ulionekana kwa kufanya wenye kufuata mafundisho yake wawe watu wema . . . Sisi tuna ushuhuda kwamba maisha zao hazikuwa na lawama, tabia zao zisingeweza kulaumiwa, walikuwa raia wema, na walikuwa na fadhili za Kikristo.”
Walifaulu katika “njia ya kweli,” na leo wenye kuifuata wanafaulu pia.—2 Pet. 2:2.
JINSI KWELI INAVYOFAULU
10, 11. (a) Viongozi wengi wa dini wanaonaje kanuni za adili za Biblia kama njia ya maisha? (b) Onyesha sababu maoni yao hayafai.
10 Wanafilosofia na viongozi wa dini wa kisasa wanajaribu kudhoofisha kanuni za kweli za Biblia, wakitetea “adili mpya.” Sheria ya Mungu yasema kwamba uasherati na uzinzi ni mbaya kila mara. (1 Kor. 6:18; 1 The. 4:3; Kut. 20:14) Lakini mawazo ya viongozi wa dini yanaonekana kutokana na yaliyoandikwa na kasisi Mkatoliki wa St. Mary’s Chapel katika Chuo Kikuu cha Michigan. Alipokuwa akishauri kijana na msichana waliochumbiana waliokuwa wameahirisha kuoana ili ‘wafikirie mambo’ kadha, ‘wakawa wakifanya ngono mara kwa mara,’ kasisi huyo alisema: “Tungeweza kuwaita waasherati na kuwahukumu hivyo kwa urahisi . . . Pengine wamevunja sheria, lakini je! wamevunja ubora wa sheria hiyo? Je! ni wazinzi? Hata! . . . Ni nani kati yetu asiyejitosheleza kwa njia fulani isiyo haki kabisa ili kujifariji moyoni mwake?” Bila shaka wengi wanaoongozwa na kasisi huyo na viongozi wengine wa dini walio kama yeye wanafanya mambo ya kujitosheleza ‘yasiyo haki kabisa.’ Lakini je! njia yao ya maisha inafaulu?
11 Njia ya kweli inayoelezwa katika sheria za Mungu haiwezi kudhihakiwa! Wenye kufuata maongozi ya mawazo hayo ya wanadamu wanavuna talaka na kuwa na jamaa zenye migawanyiko, kupatwa na kisonono na kaswende yenye kuenea sana, na matatizo mengine mengi yanayosababishwa na kutoaminika na kutofuata ndoa yenye heshima. (Gal. 6:7, 8; Ebr. 13:4) Akionyesha upande mmoja wa jambo hili, daktari mmoja ametoa onyo katika Medical World News, akasema kwamba uhuru wa kufanya ngono “hauongozi kwenye uhuru kila mara, na ukiongoza, unaharibu uhuru mwingine,” kama vile uhuru wa kutokuwa na magonjwa. Alithibitisha kwamba “adili zinaleta afya mara nyingi.”
12, 13. Onyesha sababu gani kweli kama njia ya maisha yafaulu inapotumiwa kuhusu (a) matumizi ya tumbako, (b) kutiwa damu mishipani.
12 Kutumia kanuni za Biblia juu ya kuweka miili yetu katika hali ya usafi kwaonyesha pia jinsi kweli ifaidivyo sana watu. Waabudu wa kweli wanaepuka madhara ya uchafu ambao tumbako inaingiza katika mwili wa mwenye kuizoea. (2 Kor. 7:1; Rum. 12:1) Dkt. Robert Dupont, msimamizi wa U.S. National Institute of Drug Abuse, hivi karibuni alisema tumbako “pengine ndiyo dawa ya kulevya yenye kuua watu zaidi katika jamii yetu . . . Watu wanaovuta sigareti wana tatizo lile lile kama wavuta bangi” kwa sababu wana mazoea ambayo ni vigumu kuyamaliza. Kuna hatari kubwa sana ya kupatwa na cancer ya mapafu, ya mdomo na kooni na vilevile ugonjwa wa moyo. Uchunguzi wa karibuni umeonyesha kuvuta sigareti kunaleta vidonda vya tumboni na kupoozesha ubongo. Watoto wanaozaliwa na mama wavutaji huwa wafupi zaidi, wenye ratili chache zaidi na wasio na akili sana wakilinganishwa na wengine. Wanakuwa katika hatari kubwa ya kuwa na kasoro za moyo na ya kufa wakati wa kuzaliwa. Je! “njia ya kweli” siyo inayofaulu zaidi?
13 Maarifa yameongezeka kuonyesha kuna hatari za kutiwa damu mishipani na kwamba kuna faida za kupasuliwa bila kutiwa damu, na hiyo inahakikisha ukweli wa amri ya Biblia ‘kujiepusha na damu.’ (Matendo 15:20, 28, 29) Faida za kupasua kwa njia hiyo zinaonyeshwa na wapasuaji wawili wa St. Barnabas Hospital katika mji wa New York:
“Tena, ni furaha mtu asipokuwa na haja ya kuwa na wasiwasi wa kupatwa na madhara yanayotokana na kutiwa damu mishipani kama kuharibika kwa chembe nyekundu za damu, kuharibika kwa figo, na kufura maini.”—New York State Journal of Medicine.
Hakika, njia ya kweli inafaulu inapozoewa!
14, 15. Tofautisha kufaulu kwa ibada ya kweli na ya uongo kuhusu mapigano ya kijeshi.
14 Kweli nyingine ambayo imejaribiwa ikaonekana yafaa ni ile aliyotaja Yesu: “Wote waushikao upanga, wataangamia kwa upanga.” Kweli hiyo yapatana na neno hili mkataa: “Wote watatambua ya kuwa ninyi mmekuwa wanafunzi wangu, mkiwa na upendo ninyi kwa ninyi.” (Mt. 26:52; Yohana 13:35) Lakini New Cathotic Encyclopedia (chapa ya mwaka 1967) chasema kuna njia nyingine, na kudai kwamba “vita ya haki haipingani na amri ya Kristo kwamba tupende adui zetu. Vita ya haki yaonyesha linalochukiwa ni tendo ovu si mwenye kulitenda. . . . Wakatoliki wako huru kabisa kujitungia maoni yao wenyewe kama watatetea hali zinazoelekea kuwa zahitaji kutetewa.” Uongozi wa namna hiyo unafaaje?
15 Wakatoliki na Waprotestanti ‘walijitungia maoni yao wenyewe’ yenye kupingana pande zote mbili wakati wa vita viwili vya ulimwengu, kinyume cha njia ya kweli. Matokeo yakawaje? Hawakufaulu. Wakatoliki walichinja mamilioni ya Wakatoliki wenzao na Waprotestanti wakafanya vivyo hivyo, kuhakikisha kabisa wao si wanafunzi wenye upendo wa Kristo, wala hawamo katika kweli. Hata hivyo, katika kitabu The Nazi Persecution of the Churches mwana historia J. S. Conway asema hivi:
“Makanisa makubwa yaliacha kufuata haki yalipopingwa na wapinzani, lakini Mashahidi wa Yehova walishikilia mafundisho yao kwa ushupavu [mpaka kufa]. Ilikuwa vigumu sana kuona makanisa mengine yakisimama imara kama Mashahidi. . . . Walikataa kuchukua silaha kwa sababu ya amri za Biblia.. . . Hakuna madhehebu nyingine iliyojikaza hivyo ilipotishwa sana na Gestapo.”—Kur. 196, 198, 199.
Ni watu gani peke yao ambao wangeweza kusema walifuata njia ya kweli baada ya vita hivyo viwili vyenye kuchacha zaidi katika historia yote?
16, 17. (a) Kweli ya Biblia juu ya serikali yaonyeshwaje? (b) Kwa sababu gani serikali ya Ufalme wa Mungu inafaulu? Toa mfano.
16 Kanuni za Biblia juu ya suala kuu linalokabili wanadamu leo, yaani, serikali ya ulimwengu, zinakuwa za kweli pia. Kanuni zifuatazo zilizotajwa zamani za kale ni za kweli, “Mtu mmoja anayo mamlaka juu ya mwenziwe kwa hasara yake,” na “kuelekeza hatua zake si katika uwezo wa mwanadamu.” (Mhu. 8:9; Yer. 10:23) Matatizo ya maisha ya mwanadamu yanahitaji serikali bora kuliko iwezayo kutokezwa na wanadamu. Maelfu ya miaka ya historia ya kibinadamu yamehakikisha hilo kabisa. Sasa, kama vile New York Times lilivyoomboleza: “Ni wazi kwamba viongozi kila mahali wamepoteza mamlaka na imani. . . . serikali za namna zote, katika nchi za namna zote, zimo taabuni kwa sababu hazisadikishi watu kwamba zinaweza kutatua matatizo yenye kuhangaisha zaidi watu wao.”—Mei 15, 1974, uk. 2.
17 Hata hivyo leo kuna serikali inayofaulu wakati nyingine zote zinaposhindwa. Kwa sababu gani? Kwa sababu si serikali ya wanadamu. Ni serikali ya Ufalme wa Mungu, nayo sasa inapanga kuwe na usimamizi wa njia ya kweli duniani. Raia milioni mbili wenye kushikamana nayo wanaunga mkono kanuni zake kwa hiari na shauku katika nchi zaidi ya 200, kwa miili yao, akili zao na mali zao. Katiba yake na kitabu chake cha sheria (Biblia) inatiliwa mkazo kupitia kwa makundi yaliyo kama miji, tena inafaulu zaidi sana kuliko sheria zo zote za serikali za dunia. Hivyo kundi la Kikristo linatenda kama “nguzo na msingi wa kweli,” likisaidia watu wawe watii au kuondoa wo wote wasiotaka kubaki katika njia ya kweli. (1 Tim. 3:15; 1 Kor. 5:6-13) Raia za serikali hiyo ya Ufalme wanapokea elimu isiyo na kifani juu ya kweli kupitia kwa vitabu sita ambavyo ni baadhi ya vitabu kumi vya ulimwengu vyenye kuuzwa zaidi ya vingine vyote.a Serikali hii ya Ufalme inafaulu, nayo inaendelea kufaulu kila siku, kwa sababu msingi wake ndiyo kweli.
NJIA YA KUFAULU
18. Kuna faida gani za kufuata kweli kama njia ya maisha?
18 Wale wanaochagua kufanya kweli iwe njia yao ya maisha wanapambana na matatizo. Kufahamu kweli juu ya hali ya wanadamu kunawasaidia Wakristo hawa wapende wanadamu wenzao wanaohitaji msaada. Jamaa zao zinaonyesha pia faida zinazotokana na kufuata mashauri ya kweli ya Biblia juu ya ukichwa wa jamaa na kulea watoto. (1 Pet. 2:12; Efe. 5:33; 6:1-4) Kujua kweli juu ya wakati ujao kutokana na unabii wa Biblia kunawafanya wasifadhaike na kunawapa matumaini yenye hakika na furaha, bila hofu.—Mit. 3:25, 26.
19, 20. (a) Wengine huonaje njia ya maisha ya Wakristo wa kweli? (b) Kwa sababu gani wale wanaosifu Mashahidi wa Yehova, kisha wanalaumu imani zao, ni wapumbavu? (c) Yatupasa tusalije?
19 Mara nyingi wengine huona kwamba njia hii ya maisha inafaulu. Kitu kinachowafanya wafaulu kinaonyeshwa na maoni yaliyotolewa juu ya Wakristo hawa katika gazeti la Washington, D.C., wakati wa kusanyiko la Mashahidi wa Yehova:
“Kuthamini kwao mwenendo mwema kunafurahisha sana mji . . . Wao wanasema hawaji hapa kuomba cho chote, hali ‘wako hapa kutetea Biblia na kanuni zake kama suluhisho la pekee la matatizo ya wanadamu.’”
Hiyo ndiyo njia ya kufaulu! Neno la Mungu, Biblia, linasaidia. Linafaulu linapozoewa.
20 Kabla ya kusema kwamba “Mashahidi huonyesha wanaishi kila siku kulingana na dini yao” makala iliyokuwa katika gazeti Democrat and Chronicle la Rochester, New York, ilisema: “Hata watu wa imani nyingine wapinge namna gani jinsi Mashahidi wanavyofasiri Biblia, wao wanashikamana sana na imani zao kwa unyofu.” Je! si upumbavu kwamba watu wale wale wanaosifu Mashahidi wa Yehova mara nyingi kwa sababu ya mwenendo wao ndio wenye kulaumu ‘tafsiri’ zao? Ni nini hufanya mwenendo wa Mashahidi wa Yehova uwe tofauti na wa watu wengine? Hawakuzaliwa wakiwa hivyo. Mashahidi wa Yehova wako walivyo kwa sababu ya ‘tafsiri’ izo hizo. Imani zao ni kweli inayotokana na Biblia tena ni njia yao ya maisha. Ndiyo sababu wanafaulu wakati wengine wanaposhindwa. Hivyo Mashahidi wa Yehova wana sababu kamili za kusali wakiwa na hakika kama mtunga Zaburi: “Ee [Yehova], unifundishe njia yako; nitakwenda katika kweli yako.” “Uniongoze katika kweli yako, na kunifundisha.” Mtunga zaburi asema yafuatayo juu ya mtu atembeaye hivyo: “[Yehova] atamfundisha katika njia anayoichagua. Nafsi yake itakaa hali ya kufanikiwa; wazao wake watairithi nchi.”—Zab. 86:11; 25:5, 12, 13.
Kutoka The Watchtower, April 1, 1976.
[Maelezo ya Chini]
a Kweli Iongozayo Kwenye Uzima wa Milele, “Let God Be True,” Kutoka Paradiso Iliyopotea Mpaka Paradiso Iliyopatikana, Did Man Get Here by Evolution or by Creation?, Is the Bible Really the Word of God? “Mambo Mawili Yasiyobadilika Asiyoweza Mungu Kusema Uongo.”