Watchtower MAKTABA KWENYE MTANDAO
Watchtower
MAKTABA KWENYE MTANDAO
Kiswahili
  • BIBLIA
  • MACHAPISHO
  • MIKUTANO
  • w77 4/15 kur. 173-178
  • Ibada ya Yehova Ndiyo Kweli

Hakuna video yoyote kwa sasa.

Samahani, haikuwezekana kupakia video.

  • Ibada ya Yehova Ndiyo Kweli
  • Mnara wa Mlinzi Unaotangaza Ufalme wa Yehova—1977
  • Vichwa vidogo
  • Habari Zinazolingana
  • JINSI ‘BABA ANAVYOTAFUTA’ WAABUDU WA KWELI
  • “KWELI” NI HAKIKA, SI UONGO
  • IBADA YA UONGO NA HADITHI
  • MIUNGU YA UONGO YASHUSHA TABIA ZA WANADAMU
  • Ibada ya Kweli Ni Njia ya Maisha Yenye Kufaulu
    Mnara wa Mlinzi Unaotangaza Ufalme wa Yehova—1977
  • Wakristo Huabudu kwa Roho na Kweli
    Mnara wa Mlinzi Unaotangaza Ufalme wa Yehova—2002
  • Ni Ibada ya Nani Anayoikubali Mungu?
    Ujuzi Uongozao Kwenye Uhai Udumuo Milele
  • Nyuzi Zile Zile Katika Ngano
    Jitihada ya Ainabinadamu ya Kutafuta Mungu
Pata Habari Zaidi
Mnara wa Mlinzi Unaotangaza Ufalme wa Yehova—1977
w77 4/15 kur. 173-178

Ibada ya Yehova Ndiyo Kweli

“Waabuduo halisi watamwabudu Baba katika roho na kweli. Kwa maana . . . wamwabuduo yeye imewapasa kumwabudu katika roho na kweli.”​—Yohana 4:23, 24.

1. Ni jambo gani linalotofautisha ibada ya kweli na ya uongo?

NI NINI kinachopaswa kuinua ibada ya kweli juu ya ibada nyingine zote? Je! si KWELI? Msingi wa ibada ya kweli wapaswa kuwa mambo ya hakika, yapaswa kupatana na jinsi mambo yalivyo hasa, badala ya kutegemea makisio au mambo ya kuwaziwa tu na waabudu. Je! Ibada nyingine yo yote isingekuwa ya bandia tu, na kumletea dharau Yeye ajulikanaye kuwa “Mungu wa kweli”?​—Zab. 31:5; Kut. 34:6.

2. Kwa sababu gani mtu hawezi kuabudu apendavyo tu?

2 Kweli inahusiana na maarifa kama vile uongo unavyohusiana na ujinga. Lingekuwa jambo la akili kama Muumba wa akili ya mwanadamu yenye maajabu angeacha ‘kweli na akili timamu’ iache kutumiwa katika ibada? (Matendo 26:25) Badala ya hivyo, wenye kufuata ibada ya i kweli wapaswa waweze kuambia waabudu wengine kama Yesu: “Ninyi mnaabudu msichokijua; sisi tunaabudu tukijuacho.” (Yohana 4:22) Bila shaka, wanadamu wenye kufa hawawezi kujua kila jambo juu ya Mungu asiyekufa, lakini wanayojua hayapaswi kuwa makosa, tena hayapaswi kamwe kuwa ya uongo. Mtume Yohana asema, “Hapana uongo wo wote utokao katika hiyo kweli.” (1 Yohana 2:21) Yesu aliendelea kusema kwamba ‘kuijua’ kweli ni kwa lazima katika ibada inayokubaliwa na Mungu: “Waabuduo halisi . . . imewapasa kumwabudu katika roho na kweli.” Ukristo wa karne ya kwanza hata uliitwa “njia ya kweli.” Je! nayo ibada inayokubalika leo haistahili kuitwa “kweli”? Je! wewe wadhani ibada yako ni ya kweli?​—Yohana 4:23, 24; 2 Pet. 2:2; Yos. 24:14.

3. Twajuaje kwamba kweli yaweza kupatikana?

3 Wakati Yesu alipoyanena maneno hayo juu ya ubora wa kuabudu kwa kweli, aliendelea kusema kwamba “Baba awatafuta watu kama hao wamwabudu.” “Hiyo ndiyo aina ya mwabudu atakayo Baba.” (Yohana 4:23, Jerusalem Bible) Ikiwa Baba ‘ataka’ au ‘anatafuta’ wale wanaotaka kumwabudu ‘kwa kweli,’ basi bila shaka ameonyesha njia ya kuijua kweli. Njia hiyo inavuta ‘aina hiyo’ tu ya watu wanyofu wafuate ibada ya kweli. Namna gani?

JINSI ‘BABA ANAVYOTAFUTA’ WAABUDU WA KWELI

4. Njia moja ya kujifunza kweli ni nini?

4 Kwanza, maajabu ya uumbaji yanashuhudia kweli fulani, na kufanya watu wenye akili wapendezwe na Muumba wao. (Zab. 111:7; Dan. 4:37) “Kwa maana yote ambayo huenda yakawa yanajulikana juu ya Mungu na wanadamu yako wazi mbele ya macho yao . . . Sifa Zake zisizoonekana, ndiyo kusema uwezo wake na uungu wake wa milele, umekuwa ukionekana, tangu ulimwengu ulipoanza, kwa jicho la akili, katika vitu ambavyo amefanya.” Kwa kutazama hekima iliyo wazi ya uumbaji, “jicho la akili,” yaani, yale maono ya ndani yenye kuona kweli, laweza kuona kwamba Mungu yuko na ana sifa nyingi. Hata hivyo, kama Biblia isemavyo, wengine “waliibadili kweli ya Mungu kuwa uongo,” wakajianzia namna za ibada zisizotambua kweli juu ya “sifa zisizoonekana” za Mungu.​—Rum. 1:19, 20, NE; 1:25, NW.

5, 6. Kanuni za uumbaji zaonyesha nini juu ya kweli?

5 Hata uumbaji wenyewe unashuhudia kwamba nyakati zote ni lazima Mungu atumie kweli katika shughuli zake, na kwa hiyo ni ya lazima katika ibada. Namna gani? Kwa sababu ya vile inavyoonyesha kanuni Zake zisizobadilika. Vitu vilivyoumbwa na Mungu vina kanuni zinazoonyesha vilifanywa kwa njia yenye kupatana na kwamba vinafanya kazi kwa mapatano, tena vina rangi na maumbo mbalimbali, Juu ya kanuni hizo za ajabu Encyclopcedia Britannica chasema hivi:

“Mambo yaliyotimizwa na wanadamu [katika kusawazika]. . . yanakuwa hafifu yakilinganishwa na kanuni za maumbile, Makundi ya nyota, mizunguko ya sayari, tabia zisizobadilika . . . zilizo katika vitu vilivyoumbwa, mizunguko ya nguvu za umeme zilizomo katika atom au chembe, ni mifano michache ya kusawazika kwa ajabu kwa maumbile.”​—Chapa ya 1959, Vol. 21, kur. 306, 307.

6 Basi, kusawazika huko kunaonyesha kweli juu ya vitu ambavyo Mungu amefanya. Hakuwa akikisia au kuwazia tu alipokuwa akivifanya. Kila kitu kilichoumbwa kiko kama kilivyokusudiwa. Bila shaka kanuni hizi za hakika na zenye kutegemeka zinazoonyeshwa katika uumbaji zinafanya “jicho la akili” likate maneno kwamba ziko pia kanuni za kweli zinazopaswa kuongoza mwenendo wa viumbe vyenye akili na uhusiano wavyo na Muumba wao. Lakini kanuni hizo hazikutiwa ndani ya mwanadamu zimwongoze bila ya yeye kutaka kama vile tabia za asili zinavyoongoza uumbaji mwingine wa Mungu. Sisi twaweza kuchagua kukubali kanuni za Mungu za kweli au kuzikataa.

7. Njia nyingine ya kupata kweli ni nini?

7 Hii yatuonyesha njia nyingine ambavyo Mungu ‘anatafuta’ waabudu wa kweli. Ameeleza kanuni zake za kweli za mwenendo na ibada kwa kuziandikisha katika Biblia. Mtunga zaburi asema: “Jumla ya neno lako ni kweli.” (Zab. 119:160, 142, 151) Maneno yake yanavuta namna ya watu wanaotaka kuabudu ‘kwa kweli.’ Biblia iliongozwa na Mungu ‘ifundishe kweli na kupinga makosa.’​—Yohana 4:24; 2 Tim. 3:16, NE; Yohana 17:17.

8, 9. (a) Je! mtu akijidai kwamba, atumia Biblia hiyo yamaanisha ana kweli? (b) Ni nini kinachohakikisha kwamba Yehova ‘atafuta’ waabudu wa kweli?

8 Biblia peke yake ndiyo inayoonyesha ibada ya Mungu Yehova kuwa kweli. Kwa hiyo, wale wanaojidai kwamba wanatumia Biblia, lakini wanashindwa kuendeleza ibada ya Yehova, wamekosa kusudi lake​—⁠tena wameikosa kweli. (Yer. 10:10, 23-25) Ingawa wengi wameikosa kweli kwa njia hiyo, bado ni jambo la maana kuangalia kwamba kitabu kinachoendeleza ibada ya Yehova ndicho kinachopatikana kwa wingi zaidi kuliko vitabu vingine vyote vya kidini. (Linganisha Wafilipi 1:15, 18.) Kinapatikana kwa wingi zaidi, katika lugha nyingi zaidi na nchi nyingi zaidi kuliko kitabu kinginecho chote katika historia​—kinavipita vyote kwa mbali! Yehova peke yake ndiye angeweza kufanya hilo litukie! Yeye ndiye anayechukua hatua ya kwanza ‘kutafuta’ waabudu wanaothamini kweli.

9 Hiyo yaonekana wazi zaidi tufikiriapo kwamba Ufalme wake ulioahidiwa sasa ‘unahubiriwa katika dunia yote kuwa ushuhuda’ kwa njia isiyolinganika, nao unahubiriwa kuhusiana na ibada ya Yehova. (Mt. 24:14) Ni ibada gani nyingine yenye mashahidi milioni mbili wanaopelekea watu ibada hiyo kwao wenyewe, katika nchi na visiwa vya bahari zaidi ya 200? Hakuna ibada nyingine yo yote inayofikia watu katika eneo kubwa hivyo. Hilo peke yake lapaswa kuonyesha watu wanaotaka kuabudu ‘kwa kweli’ kwamba mkono wa Yehova unafanya kazi. Lakini, yako mambo mengine mengi yanayoonyesha kweli ya ibada ya Yehova.

“KWELI” NI HAKIKA, SI UONGO

10. Alama moja yenye kutambulisha kweli ni nini?

10 Mtume Petro alionyesha tofauti kubwa kati ya ibada ya Yehova na namna nyingine za ibada aliposimulia jinsi alivyoweza kusadikisha wengine kweli juu ya Yesu: “Maana hatukufuata hadithi zilizotungwa kwa werevu,” au, kama vile New American Bible ya Kikatoliki inavyosema, kwa “hadithi zilizofanyizwa kwa werevu;” bali, “tulikuwa tumeuona wenyewe ukuu wake.” Hiyo ni alama moja yenye kutambulisha ibada ya kweli. Ibada ya kweli inaungwa mkono kwa kawaida na mambo au matukio halisi yaliyoonekana na watu. Ibada nyingine zimejawa na hadithi za werevu zilizotungwa na wanadamu.​—2 Pet. 1-16.

11, 12 (a) Kuna uhusiano gani kati ya Biblia na historia? (b) Ni nini kinachohakikisha sana historia ya Biblia?

11 Kati ya vitabu vya kidini, Biblia ndiyo sahihi kabisa na ndiyo yenye kueleza historia kwa unyofu. Ndiyo sababu mambo mengi ya hakika na matukio yaliyomo ndani yake yanahakikishwa na historia ya kilimwengu, ingawa hayaitegemei Biblia imejawa na mambo ya hakika na historia, nayo mambo hayo ndiyo yanayohakikisha ujumbe uliomo wa Mungu atendaye matendo ya kweli. Masimulizi ya Biblia yanapohusu utamaduni, desturi, vyeo vya wakuu, mambo ya kisheria na hata ya kisayansi, yanakuwa sahihi kabisa kulingana na historia, nayo hayawezi kupingwa.

12 Uangalifu wa waandikaji wa Biblia walipokuwa wakitoa maelezo ya vizazi kwa urefu, majina barabara ya watu na mahali, umri halisi, tarehe na kiasi cha vitu, waonyesha haikuwa ‘hadithi iliyofanyizwa kwa werevu.’ Habari zilizo wazi kama hizo zingalipingwa na watu wengine walioishi nyakati hizo kama zisingalikuwa sahihi. Waandikaji wenye kufanyiza hadithi wangaliepuka kutaja mambo waziwazi; hadithi na vitabu vingine vya kidini hufanya hivyo. Uamuzi wenye akili ni kwamba waandikaji wa Biblia bila shaka waliandika mambo waliyoona au waliyojua kuwa kweli. Mchimbuzi wa vitu vya kale G. Ernst Wright aliongozwa na uvumbuzi wake kusema hivi: “Inasisimua na kuthawabisha kujua kwamba Biblia si maandiko ya imani tu, bali ni maandiko yaliyotokea kuhusiana na watu na matukio halisi.”

13. Je! uhakika wa kwamba wanadamu waliandika Biblia, unafanya isifae? Kwa sababu gani?

13 Ni kweli kwamba Biblia iliandikwa na wanadamu wa kawaida walioona na kushiriki katika matukio hayo, lakini hiyo haiifanyi hata kidogo isiwe neno la Yehova la kweli. Kwa kweli, hiyo yaongeza ukweli wa Biblia kama neno la Mungu. Humo twasoma habari za watu kama Daudi, Yeremia, Paulo na Ayubu. Twaona jinsi walivyofanya makosa na kupatwa na majaribu na magumu, na jinsi maisha yanavyoonyeshwa kihalisi​—⁠pamoja na hofu zake, mambo yake yenye kukatisha tamaa, huzuni na furaha zake. Hivyo tunasadikishwa hata zaidi kwamba watu hao waliishi kweli wakapatwa na mambo wanayoeleza. Si namna ya watu ambao wangejitungia masimulizi ya kihistoria wanayoeleza, wala wasingejitungia mambo ya kweli waliyofanya na Mungu. Badala yake, tunaongozwa bila kizuizi tuamue kama watu wa Thesalonike kwamba, lazima ujumbe wa Biblia uonwe, “si kama neno la wanadamu, bali kama neno la Mungu; na ndivyo lilivyo kweli kweli.”​—1 The. 2:13.

14. Ni nani mteteaji mkuu wa ibada ya kweli? Twajuaje?

14 Mmojawapo wa shuhuda zenye kueleza mengi kwa ajili ya ibada ya Yehova ni ule wa Yesu Kristo. Uhakika wa kwamba aliishi na mafundisho yake yalisaidia sana wanafunzi wake wa kwanza hauwezi kufanyiwa ubishi. Uhakika huo umeonyeshwa katika kalenda nyingi za leo: Kutokea kwa Yesu duniani ndiko kunakoonyesha kipindi kipya cha historia. Akiwa mbinguni, yeye mwenyewe aliona matukio ya zamani yaliyoandikwa katika Biblia, alipokuwa hajawa mwanadamu. Alijua hayakuwa hadithi. Hivyo alitumia matukio hayo kueleza mafundisho yake mwenyewe mara nyingi, kwa mfano kuhusu talaka na mwisho unaokuja wa taratibu ya mambo. (Mt. 19:4; Mwa. 1:27; Mt. 24:3, 37-39; Mwa. 6 na 7) Yesu ndiye aliyekuwa wakili mkuu kuliko wote wa ibada ya Yehova, akajulisha jina hilo na maana yake, kama sehemu kuu ya ‘kushuhudia kwake kweli.’​—⁠Yohana 17:4, 6, 26; 18:37.

IBADA YA UONGO NA HADITHI

15. Mtu awezaje kujua hadithi ya uongo?

15 Hata ibada inayodai inatumia Biblia huwa mara nyingi na “hadithi zilizofanyizwa kwa werevu” badala ya kuwa na usahihi unaolingana na historia. Juu ya wenye kujidai kuwa Wakristo, ilitabiriwa hivi: “Watajiepusha wasisikie yaliyo kweli, na kuzigeukia hadithi za uongo.”​—2 Tim. 4:4.

16, 17. Toa mifano ya hadithi za uongo katika Ukatoliki na Uprotestanti.

16 Jumuiya ya Wakristo ‘imegeukia hadithi za uongo,’ kwa mfano kwa kuunga mkono ibada ya Mariamu na watakatifu. Mfano mmoja ni kijitabu kilichoandikwa na Mjesuit (Mkatoliki) kinachoitwa “Wakati Mariamu Alipotembea Duniani,” ambacho pia kimeonyeshwa ndani kwamba kinaweza kusomwa kwa ruhusa ya askofu mkuu. Utangulizi wa kijitabu hicho unakubali hivi: “Mambo yaliyosimuliwa katika kurasa zinazofuata si ya kihistoria. Pengine hayakutukia.” Kwa habari ya “Mtakatifu” Patrick wa Kikatoliki, Dkt. Joseph F. Kelly wa John Carrol University asema: “Hadithi zote zinazohusu Patrick huenda zikawa si za kweli, lakini hiyo haimaanishi hazina ubora.” Watu wengi wenye njaa ya kweli wanaolishwa ‘hadithi hizo zilizofanyizwa’ hata hawajasikia masimulizi yote ya kweli yaliyomo katika Biblia. Hadithi za uongo zawezaje kuwapa msingi wa kuabudu ‘kwa kweli’?

17 Hata Uprotestanti una hatia ya ‘kugeukia hadithi za uongo.’ Encyclopedia yo yote iliyo kamili yaweza kutoa uhakikisho wa kutosha kwamba mambo mengi wanayofundisha juu ya Utatu, moto wa mateso, nafsi, Krismasi, msalaba, Pasaka na imani nyingine ni hadithi tu. Ili kutetea kweli, Biblia yasema “mkatengwe nao” na “msiguse kitu kilicho kichafu.”​—2 Kor. 6:14-17.

18. Je! dini ya Wayahudi haina hadithi za uongo? Kwa sababu gani unajibu hivyo?

18 Hata Wayahudi ‘walijiepusha na kweli’ wakajitungia “hadithi za Kiyahudi,” ingawa walikuwa na Biblia. Walizikusanya wakaziita “Talmud.” (Tito 1:14) Mkuu Myahudi Nathan Ausubel aandika katika The Book of Jewish Knowledge kwamba Talmud kina “mambo mengi ya ujinga, miiko ya kutofanya mambo, ushirikina, maarifa ya kishetani, hadithi za uongo,” na kadhalika. Ausubel aonekana kama kwamba anatetea hadithi hizo za uongo anaposema kwamba mambo “yanayoharibu Talmud yaweza pia kupatikana katika vitabu vya kidini na vya filosofia vya Wagiriki na Warumi, vya Mababa wa Kanisa na Waalimu Wakristo wa kale.” Lakini, badala ya kutetea hadithi za uongo za dini ya Wayahudi, je! sababu anayotoa hailaumu dini nyingine zote kwa sababu ‘ziliibadili kweli ya Mungu kuwa uongo’?​—Rum. 1:25.

19, 20. (a) Ni hadithi gani ya uongo inayohusu wengi wa waabudu wa uongo? (b) Toa ushuhuda wa hadithi ya uongo katika dini nyingine kuu.

19 Hadithi nyingine ya uongo inayohusu mamia ya mamilioni ya watu, katika Jumuiya ya Wakristo na nje yake, ni dai la kwamba sanamu zinasaidia watu katika ibada ya kweli. Wakijumlishwa pamoja, Wakatoliki, wafuasi wa Buddha, Mabanyani na wengine hutumia mamia ya mamilioni ya sanamu hizo katika ibada, nazo mara nyingi huwa za pesa nyingi sana. Hata hivyo, Biblia yasema juu ya sanamu hizo hivi: “Ni ubatili tu, ni kazi za udanganyifu.” (Yer. 10:14, 15) Kwa hiyo, kwa kuwa Biblia yaeleza sanamu kuwa “ubatili tu,” hizo pia ni “hadithi zilizofanyizwa.” Hivyo Mungu aziona kuwa “kazi za udanganyifu” tu.

20 Ni wazi kabisa kwamba dini nyingi “kuu” za ulimwengu zinashikilia sana mapokeo na hadithi za uongo. Kwa kweli, kitabu Encyclopaedia Britannica cha 1974 kinapoeleza kila dini mojawapo kinatumia vichwa vikubwa vinavyosema “Hadithi za Uongo” au “Hadithi za Uongo na Mapokeo.” Kwa mfano, chini ya “Dini ya Mabanyani,” kichwa hicho kinasema kwamba “Hakuna upande wa maisha ya Kibanyani usiohusiana na hadithi za uongo.” Kwa habari ya dini ya Buddha, ambayo ni filosofia inayohusiana na Ubanyani, chasema hivi: “Hadithi za uongo zimedumu katika dini ya Buddha.” Kwa habari ya Uislamu, kitabu hicho kinasema habari za mapokeo ya zamani yanayohusu Muhamadi na jamaa yake kwamba “hayapatani na matukio halisi ya historia,” na kwamba ingawa Waislamu wanakana rasmi kwamba hawana hadithi hizo za uongo, “Mapokeo yapendwayo na watu wengi yanayohusu Nabii na watakatifu yanapatikana bado kwa wingi.”

21. (a) Kweli ya Biblia ni bora namna gani kuliko hadithi za uongo? (b) Kwa sababu gani wanadamu huepuka kweli?

21 Wakati mambo yote ya uongo yaliyotungwa na wanadamu yanapolinganishwa na maoni ya kweli ya Biblia juu ya wanadamu na kazi za Muumba, yanaonekana kuwa ovyo na yasiyo na maana. Yaonyesha wanajitahidi kuepuka kweli halisi ya Mungu na wajibu walio nao Kwake. (Yohana 8:46, 47) Kwa upande mwingine, masimulizi ya wazi ya Biblia yanaonyesha Mungu ndiye Mbuni Mkuu Zaidi wa uumbaji wenye utaratibu, na kutuonyesha wazi wajibu tulio nao Kwake. (Mwa. 1:1-28; 2:15-17) Waabudu wa kweli wamefanya haki kwa kutosheka kabisa wakijua kwamba msingi imara wa ibada yao ni kweli hiyo. Ni kama vile mtunga zaburi alivyopaza sauti: “Maana miungu yote ya watu si kitu, lakini [Yehova] ndiye aliyezifanya mbingu. . . . Mpeni [Yehova] utukufu wa jina lake.”​—Zab. 96:5, 8.

MIUNGU YA UONGO YASHUSHA TABIA ZA WANADAMU

22. (a) Eleza tabia kuu ya miungu ya kubuniwa. (b) Matokeo ya miungu hiyo ni nini juu ya waabudu wake?

22 Ni wazi kwamba miungu ya wanadamu iko sawa na wanadamu wenye kuifanya. Mchunguzi wa akili William Sargent aliona hivyo, akaandika katika kitabu chake The Mind Possessed kwamba mwanadamu amefanya miungu kwa mfano wake mwenyewe, “yenye kuonyesha mawazo yake, tamaa na hofu zake zenye kutofautiana.” Mtume Paulo anatoa maelezo zaidi. Anasema kwamba ‘wameubadili utukufu wa Mungu asiye na uharibifu kwa mfano wa sura ya binadamu aliye na uharibifu’ na ya viumbe vingine. (Rum. 1:23) Hivyo mara nyingi miungu ya hadithi za uongo huonyesha udhaifu wa kibinadamu na sifa za upotovu, na hiyo yaonyesha hakika kwamba ni “akili za wanadamu.” (Matendo 17:29) Kwa mfano, miungu mbali-mbali ya kiume na ya kike ya Wamisri ilisemekana ilikuwa ikipatwa na maumivu ndani ya mwili na kichwani; ilitaka sana kuona damu ikimwagwa, tena ilikuwa miungu yenye kulewa na kupiga punyeto (kusugua viungo vyao vya uzazi ili kuwasha tamaa). Nacho kitabu Jews, Gods and History chasema kwamba “miungu ya Kigiriki iliweka kielelezo cha kuwa na tamaa ya uzinzi isiyozuiliwa na vilevile upotovu wa tabia ambao mwishowe ulifanya watu wadhoofike katika adili.” Wenye kuabudu miungu ya namna hiyo wanafuata tabia zao mbovu.​—Rum. 1:18, 25-32.

23. (a) Tofautisha Yehova na waabudu wake na miungu ya kubuniwa na waabudu wake. (b) Toa mfano wa matokeo ya kweli juu ya waabudu wa Yehova.

23 Ibada ya Yehova iko tofauti sana. Yeye haonyeshwi kuwa dhaifu kwa njia yo yote, wala haonyeshwi kuwa mfisadi. Yeye ni mkamilifu na wa milele, mwenye kutumia sifa za upendo unaoongozwa na kanuni, hekima, uwezo na haki ya hukumu katika matendo yake yote. Hivyo waabudu wake waaminifu wanatukuzwa​—hawashushwi kamwe. Hata wakati waabudu wa kweli walipozungukwa na maongozi yenye kupotoa ya miungu mingine iliyoabudiwa na watu wa nyakati zao, wao hawakujiunga nao. Kwa mfano, muda mwingi wa historia yao, Israeli walizungukwa na hadithi potovu za kipagani walipokuwa wakikua wawe taifa. Hata hivyo kanuni bora za maandiko yao matakatifu na ibada ya Yehova Mungu hazikuharibiwa. Kitabu kimoja chasema: “Haiwezekani kujua sababu gani historia ya Israeli yenye vyanzo kama vya . . . Wamoabu, imekuwa na matokeo tofauti sana hivyo!” Lakini je! “vyanzo” vyao vilikuwa vimoja? Hapana! Ibada katika Israeli ilikuwa na chanzo tofauti. Haikutungwa na wanadamu. Ilikuwa dini iliyofunuliwa na Mungu. Ilikuwa ndiyo kweli!​—Neh. 9:13.

24. Jumuiya ya Wakristo imefuataje mungu wake yenyewe?

24 Kwa upande mwingine, watu wengi leo hujionyesha kuwa waabudu wa Mungu wa Biblia, lakini wako kama Wayahudi wa nyakati zilizofuata wenye kurudi nyuma, kwa maana ibada yao ‘si ya kweli.’ (Isa. 48:1) Viongozi wa dini wamejifanyia mungu wao, kwa mfano wao wenyewe. Fundisho lao la kipagani la Utatu lamwonyesha Mungu kuwa “fumbo” (siri). Kwa sababu wanafuata “hadithi zilizotungwa kwa werevu,” waabudu wanamchukua Yeye kuwa dhaifu au kigeugeu, asiye na kanuni zo zote, mwenye kuwaruhusu wafuate namna zote za ufisadi. (Yuda 4) Wanamwonyesha kuwa mungu wa vita anayefanya aagizwavyo na wanasiasa na viongozi wa dini pia. Nyakati za vita, mungu wao hupigania kiongozi ye yote wa kisiasa anayetumikiwa na viongozi wa dini wakati huo. Je! ni ajabu kwamba waabudu wake wamekuwa kama mungu wao?​—2 The. 2:10-12; 1 Yohana 4:5, 6.

25, 26. (a) Ni jambo gani linaloongoza waabudu wa kweli? (b) Ni katika maana gani Mungu anaumba wale wanaolichukua jina lake?

25 Lakini waabudu wa kweli wanaijua kweli juu ya Mungu wao Yehova na wanaishi kupatana na kanuni zake zisizobadilika. Wanamjua kwa sababu wamejifunza kweli juu yake kwa kuchunguza Neno lake, Biblia. (Zab. 86:11) Neno hilo lenye kuwatukuza linawafanya waige Muumba wao mkamilifu, badala ya kuiga mungu dhaifu na mpotovu aliyefanywa na wanadamu. Katika upungufu wao, wanajifunza kufuata sifa zake za kweli zenye uchangamfu, zenye upendo na safi.​—Mt. 5:44-48; Efe. 5:1.

26 Kwa njia hiyo, inaweza kusemwa kwamba Mungu alifanya au aliumba wale wanaomwabudu yeye. Wanaumbwa na mfano wa Yehova na roho yake. Kwa hiyo Yehova asema katika Isaya 43:7 na 10: “Kila moja aliyeitwa kwa jina langu, niliyemwumba kwa ajili ya utukufu wangu; mimi nimemwumba, naam, mimi nimemfanya . . . Ninyi ni mashahidi wangu.” (Linganisha Yakobo 1:18.) Uhai wenyewe na maisha ya waabudu wa kweli ‘wanaoitwa kwa jina lake’ unashuhudia kweli juu ya Mungu. Hivyo, inaweza kusemwa kwa kufaa kwamba ibada ya Yehova ndiyo kweli!

    Maktaba Kwenye Mtandao (1980-2025)
    Toka
    Ingia
    • Kiswahili
    • Shiriki
    • Mapendezi
    • Copyright © 2025 Watch Tower Bible and Tract Society of Pennsylvania
    • Masharti ya Utumiaji
    • Sera ya Faragha
    • Mpangilio wa Faragha
    • JW.ORG
    • Ingia
    Shiriki