Sura ya 20
Watoto Wafufuliwa kwa Wafu
JE! SI vizuri sana kujua kwamba fulani akupenda?— Ni jambo zuri kuwa na watu ambao kweli wanakuangalia. Lakini wajua kwamba kuna fulani akupendaye zaidi kuliko ye yote duniani?— Huyo ni Yehova.
Yehova atupenda sisi kadiri gani?— Je! yeye anatufikiria wakati tupo hapa tu, kisha anatusahau wakati hatupo? Au je! kweli anatukumbuka sisi?— Biblia inasema wala ‘mauti wala uzima, wala yaliyopo, wala yatakayokuwapo, hayataweza kututenga na upendo wa Mungu.’—Warumi 8:38, 39.
Hivyo Mungu hasahau. Yeye anawakumbuka watu wanaomtumikia, tena anakumbuka watoto wao wadogo. Hata ikiwa labda wanakufa, yeye atawarudisha tena kwenye uzima.
Wakati Mwana wa Mungu Yesu alipokuwapo duniani, alionyesha kwamba Yehova anawaangalia watoto wadogo. Yesu angepata nafasi ya kuzungumza na watoto juu ya Mungu. Hata alitumia nguvu ya Mungu kuwarudisha watoto kutoka kwa wafu! Ungependa kusikia namna Yesu alivyofanya hili kwa jamaa moja?—
Kulikuwako mtu mmoja jina lake Yairo. Yeye na mke wake na binti yao mwenye umri wa miaka kumi na miwili waliishi kama mwendo mfupi kutoka Bahari ya Galilaya. Baba na mama walimpenda binti yao sana. Alikuwa ndiye mtoto wao pekee.
Basi unaweza kuwazia namna walivyohuzunika wakati binti yao mdogo alipokuwa mgonjwa sana. Walifanya kila kitu kadiri walivyoweza apate kupona, lakini akazidiwa. Yairo aliweza kuona kwamba binti yake atakufa. Na hapakuwa na neno ambalo yeye au madaktari waliweza kufanya wamsaidie.
Pengine Yesu angeweza kusaidia. Yairo alikuwa amesikia juu ya mtu huyu wa ajabu na namna alivyoweza kuponya watu. Basi Yairo alitoka kwenda kumtafuta. Akamwona Yesu pwani ya Bahari ya Galilaya akifundisha watu wengi.
Yairo alipita kati ya watu wote wengi akaanguka miguuni pa Yesu. Akamwambia: ‘Binti yangu mdogo ni mgonjwa sana. Tafadhali njoo umsaidie. Nakuomba uje.’
Mara hiyo Yesu alikwenda na Yairo. Watu wengi waliokuwa wamekuja kumwona Mwalimu Mkuu nao wakafuata. Lakini walipotembea mwendo kidogo, watu fulani wakatoka katika nyumba ya Yairo, wakamwambia: “Binti yako amekwisha kufa; kwani kuzidi kumsumbua mwalimu?”
Yesu aliwasikia watu wakisema hivi. Akajua namna Yairo alivyokuwa mwenye huzuni kupoteza mtoto wake wa pekee. Basi akamwambia: ‘Usiogope. Mwamini Mungu tu. Binti yako atapona.’
Basi wakaendelea na safari mpaka wakaja nyumbani kwa Yairo. Hapa rafiki za jamaa walikuwa wakilia. Walihuzunika sana kwa sababu rafiki yao mdogo alikuwa amekufa. Lakini Yesu akawaambia: ‘Acheni kulia. Kijana hakufa, bali amelala tu.’
Yesu aliposema hivi, watu walianza kumcheka. Maana walijua kijana wa kike alikuwa amekufa. Lakini Yesu alisema kijana wa kike alikuwa akilala tu ili awafundishe watu hao somo. Alitaka wajue kwamba kwa nguvu za Mungu yeye angeweza kurudisha wafu kwenye uzima kwa vyepesi kama vile tungeweza kumwamsha mtu kutoka katika usingizi.
Kwanza Yesu alimwambia kila mtu aondoke chumbani isipokuwa watatu wa mitume wake na baba na mama ya kijana wa kike. Akaingia mahali kijana alipokuwa. Akamshika mkono, akasema: ‘Kijana wa kike, inuka!’ Na mara hiyo akasimama akaanza kutembea! Baba na mama walijaa furaha wee.—Marko 5:21-24, 35-43; Luka 8:40-42, 49-56.
Umepata kuwa na rafiki aliyekufa?— Ungependa ikiwa mtu huyo angeweza kurudi kwenye uzima hata ungeweza kujifurahisha tena urafiki wake?— Unafikiri hili laweza kutukia?—
Kwa kuwa Yesu aliweza kumrudisha yule kijana wa kike kwenye uzima, yeye aweza kufanya yale yale kwa wengine, sivyo?— Lakini je! kweli atafanya hivyo?— Ndiyo, kwa sababu Yesu mwenyewe alisema: “Sao yaja, ambayo watu wote waliomo makaburini wataisikia sauti yake. Nao watatoka.” Na wakati huo unakuja upesi, chini ya utawala wa ufalme wa Mungu.—Yohana 5:28, 29.
Ebu fikiri namna itakavyokuwa vizuri sana kukaribisha watu kurudi kwenye uzima! Wengine kati yao watakuwa watu tuliojua. Nasi tutajua ni akina nani wakati wanarudi kutoka kwa wafu, kama vile Yairo alivyomjua binti yake wakati Yesu alipomfufua. Wengine watakuwa watu waliokufa kwa maelfu ya miaka iliyopita. Lakini kwa vile waliishi zamani, Mungu hatawasahau.
Je! si ajabu kujua kwamba Yehova Mungu na Mwana wake Yesu wanatupenda hivyo sana?— Wao wanataka tuishi, si miaka michache tu, bali milele!
(Juu ya tumaini la ajabu la Biblia kwa wafu, soma tena Matendo 24:15, 1 Wakorintho 15:20-22 na Isaya 25:8.)