Maisha na Huduma ya Yesu
Machozi Yakabadilika Kuwa Pindi Yenye Furaha
YAIRO anapomwona yule mwanamke mwenye mtiririko wa damu amepona, uhakika wake katika nguvu za kimuujiza za Yesu bila shaka unaongezeka. Mapema siku hiyo Yesu alikuwa ameulizwa na Yairo aje na kumsaidia binti yake mpendwa mwenye umri wa miaka 12, aliyekuwa karibu kufa. Lakini wanapokuwa safarini kwenda kwa nyumba ya Yairo, ambayo ni karibu Kapernaumu, mwanamke ambaye anagusa tu upindo wa vazi la Yesu anaponywa.
Hata hivyo, wakati ule ule, jambo ambalo Yairo anaogopa sana linatukia. Yesu akiwa angali anazungumza pamoja na mwanamke huyo, wanaume fulani kutoka katika nyumba yake wanawasili na kumwambia Yairo hivi polepole: “Binti yako amekwisha kufa; kwani kuzidi kumsumbua Mwalimu?”
Habari hizo zinakuwa pigo kama nini! Ebu fikiria: Mwanamume huyu, aliyekuwa na heshima kubwa katika mtaa huo, sasa anakuwa hoi kabisa anapopata kujua juu ya kifo cha binti yake. Hata hivyo, Yesu anapata kuyasikia mazungumzo hayo. Hivyo, akimgeukia Yairo, anasema hivi kwa kumtia moyo: “Usiogope, amini tu.”
Yesu anaandamana na mtu huyo mwenye huzuni kurudi nyumbani kwake. Wanapowasili, wanapata makelele ya watu wakilia na kuomboleza. Makutano yamekusanyika, na wanajipiga-piga kwa huzuni. Yesu anapoingia ndani, anauliza: “Mbona mnafanya ghasia na kulia? Kijana hakufa, bali amelala tu.”
Wanapoyasikia maneno hayo watu wanaanza kumcheka Yesu kwa dharau kwa sababu wanajua kwamba kweli msichana huyo amekufa. Hata hivyo, Yesu anasema kwamba msichana analala tu, ili aonyeshe kwamba, kwa nguvu zake alizopewa na Mungu, watu wanaweza kurudishwa kutoka kifo kwa urahisi kama vile wanavyoweza kuamshwa kutoka katika usingizi mzito.
Yesu sasa anatoa watu wote nje isipokuwa Petro, Yohana, Yakobo, na mama na baba ya msichana aliyekufa. Anawachukua hao watano pamoja naye kwenye mahali ambapo msichana huyo kijana analala. Akimshika mkono wake, Yesu anasema: “Talʹi·tha cuʹmi,” maneno ambayo yakitafsiriwa yanamaanisha, “Msichana, nakuambia, Inuka.” Na mara moja msichana yule anainuka na anaanza kutembea! Wazazi wake wanapoona hivyo wanakuwa karibu kurukwa na akili kwa sababu ya furaha kubwa.
Baada ya kuamuru kwamba mtoto apewe chakula, Yesu anawaagiza Yairo na mke wake wasimwambie mtu ye yote jambo lililotukia. Lakini ijapokuwa yale ambayo Yesu anasema, mazungumzo kuhusu jambo hilo yanaenea katika ujirani huo wote. Huo ndio ufufuo wa pili ambao Yesu anafanya. Mathayo 9:18-26; Marko 5:35-43; Luka 8:41-56.
◆ Yairo anapokea habari gani, naye Yesu anamtiaje moyo?
◆ Hali inakuwaje wanapowasili nyumbani mwa Yairo?
◆ Kwa sababu gani Yesu anasema kwamba mtoto ambaye amekufa amelala tu?
◆ Ni nani hao watu watano waliokuwa pamoja na Yesu ambao wanaushuhudia ufufuo huo?