Sura ya 24
Msaada Kutoka kwa Malaika wa Mungu
WATU wengine wanasema wanaamini wanachoweza kuona tu. Lakini huo ni upumbavu. Kuna vitu vingi ambavyo hatujaona na macho yetu hata kidogo. Unaweza kutaja kimoja?—
Namna gani hewa? Tunaivuta. Je! twaweza kuisikia?— Nyosha mkono wako. Sasa nitapuliza juu yake. Uliisikia? — Ndiyo, lakini hatuwezi kuona hewa, sivyo?—
Je! kuna watu vile vile ambao hatuwezi kuona?— Ndiyo, Mungu ni mmojawapo. Mimi sijamwona hata kidogo, lakini nimeviona vitu ambavyo yeye amefanya. Umeona vitu hivyo hata wewe, sivyo?— Basi twajua kuna Mungu.
Na Biblia inasema kwamba Mungu alifanya watu wengi waishi naye mbinguni. Mungu aweza kuwaona, nao wanaweza kumwona Mungu. Lakini aliwafanya hivyo hata tusingeweza kuwaona. Aliwafanya tena kuwa wenye nguvu sana, wenye nguvu zaidi kuliko na wanadamu. Wanaitwa malaika.
Mwalimu Mkuu alijua juu ya malaika. Alipokuwa mbinguni alikuwa malaika. Naye aliishi pamoja na malaika wengine. Yeye alijua mamilioni yao. Na malaika hao wanapendezwa na sisi ikiwa tunamtumikia Yehova.
Palikuwa na mtu jina lake Danieli aliyemtumi-kia Yehova. Danieli aliishi katika Babeli. Watu wengi huko hawakumpenda Yehova. Hata waliagiza Danieli atupwe katika tundu la simba kwa sababu yeye hakuacha kusali kwa Yehova. Humo Danieli akawa pamoja na simba hao wote wenye njaa. Kungetukia nini? ‘Mungu alimtuma malaika wake akafumba vinywa vya simba.’ Danieli hakuumizwa hata kidogo! Malaika wanaweza kufanya maajabu.—Danieli 6:18-22.
Wakati mwingine Petro alikuwa katika kifungo. Petro alikuwa mtume wa Mwalimu Mkuu. Watu wengine hawakupenda alipowaambia kwamba Yesu alikuwa Mwana wa Mungu. Hivyo walimtia Petro katika kifungo. Askari walikuwa wakimlinda Petro kuhakikisha asije akatoroka. Je! alikuwako ye yote ambaye angeweza kumsaidia Petro?—
Petro alikuwa akilala kati ya askari wawili, na kulikuwako minyororo mikononi mwake. Lakini Biblia inasema: ‘Tazama! malaika wa Yehova akaja, na nuru ikaanza kumulika katika chumba cha jela. Akimgusa Petro ubavuni mwake, malaika akamwamsha Petro, akisema, “Ondoka upesi.”
Na hapo, minyororo ya Petro ikaanguka kutoka mikononi mwake! Na malaika akamwambia: ‘Jivike nguo yako, vaa viatu vyako ukanifuate.’ Askari hawakuweza kuwazuia kwa sababu malaika alimsaidia Petro. Sasa wakaja kwenye mlango wa chuma, na ajabu ikatukia. Mlango ulijifungua wenyewe! Petro na malaika wakatoka nje. Malaika yule alikuwa amemweka Petro huru.—Matendo 12:4-11.
Je! malaika watatusaidia na sisi?— Ndiyo. Je! maana yake hawatatuacha tujiumize hata kidogo?— Ikiwa ungekimbia barabarani mbele ya motokaa, je! malaika angekulinda?— Hapana. Malaika hawatuzuii tusijiumize ikiwa tunafanya mambo ya kipumbavu. Ikiwa ungeruka kutoka nyumba ndefu, je! malaika wangekushika?— Ibilisi alijaribu kumshawishi Yesu afanye hivyo mara moja. Lakini Yesu hakufanya. Twaweza kujifunza kwa hilo.—Luka 4:9-13.
Mungu amewapa malaika kazi ya pekee kufanya. Biblia inasema juu ya malaika ambaye anawaambia watu kila mahali wamwabudu Mungu.—Ufunuo 14:6, 7.
Malaika wanafanya hivyo namna gani? Je! wanapaza sauti kutoka mbinguni ili kila mtu aweze kuwasikia?— Hapana; bali Wakristo wa kweli duniani wanasema na wengine juu ya Mungu, nao malaika wanawaongoza katika kazi yao. Malaika wanahakikisha kwamba wale wanaotaka kweli kujua juu ya Mungu wanayo nafasi ya kusikia. Twaweza kushiriki katika kazi hiyo, nao malaika watatusaidia.
Lakini namna gani ikiwa watu wasiompenda Mungu wanatutaabisha? Namna gani ikiwa wangetutia kifungoni, kama walivyomfanya Petro? Je! malaika wangetuweka huru— Wanaweza. Lakini sivyo wanavyofanya sikuzote.
Wakati mmoja mtume Paulo alipokuwa mfungwa, malaika hawakumweka huru mara hiyo. Walikuwako watu kifungoni waliotaka kusikia juu ya Mungu na Kristo. Walikuwako watawala waliotaka kusikia vile vile. Paulo alipelekwa mbele yao, naye aliweza kuwahubiria. Lakini sikuzote malaika walijua mahali alipokuwa Paulo, nao walimsaidia. Watatusaidia sisi vile vile, ikiwa kweli tunamtumikia Mungu.— Matendo 27:23-25.
Kuna kazi kubwa nyingine ambayo malaika tena watafanya, nao wataifanya hivi karibuni. Wakati wa Mungu wa kuharibu waovu wote unakaribia sana. Wote wasiomwabudu Mungu wa kweli wataangamizwa. Wale wasemao hawaamini malaika kwa sababu hawawezi kuwaona watajua namna walivyo na kosa. Lakini itakuwa kuchelewa mno. Hakuna mmoja wa waovu atakayejificha. Malaika watawaona wote.—2 Wathesalonike 1:6-8.
Hiyo itakuwa na maana gani kwetu?— Tukiwako upande ule ule kama malaika, watakuwa kama ndugu zetu. Hakutakuwa na jambo la kuogopa. Watatusaidia.
Lakini je! sisi tuko upande huo?— Tuko ikiwa tunamtumikia Yehova. Na, ikiwa tunamtumikia Yehova, tutakuwa tukiwaambia watu wengine wamtumikie vile vile.
(Ili kujifunza zaidi juu ya namna malaika wanavuta maisha za wanadamu, soma Zaburi 34:7, Mathayo 18:10 na Matendo 8:26-31.)