Sura ya 29
Fanya Urafiki na Wale Wampendao Mungu
NIAMBIE ambao ni rafiki zako. Majina yao ni nani?—
Ni vizuri kuwa na rafiki. Ni watu ambao unapenda kukaa nao. Unapenda kusema nao na kufanya mambo pamoja.
Tena ni jambo la maana kuwa na rafiki za namna nzuri. Twawezaje kujua ikiwa ni namna nzuri au sivyo?—
Basi, nani ungesema ndiye mtu mkubwa kuliko wote katika maisha zetu?— Ni Yehova Mungu, sivyo? Uhai wetu, pumzi yetu na mambo yote mazuri yanatoka kwake. Hatutaki kabisa kufanya lo lote ambalo lingeharibu urafiki wetu na Mungu, sivyo? Lakini ulijua kwamba uchaguzi wetu wa rafiki ungeweza kuharibu urafiki huo? Ndiyo. Basi yatupasa tuchague rafiki kwa uangalifu.
Mwalimu Mkuu alituonyesha namna ya kufanya hivyo. Alikuwa na rafiki za namna nzuri. Akasema: “Ninyi mmekuwa rafiki zangu, mkitenda niwaamuruyo.” Sababu gani ilikuwa hivyo? Kwa sababu kila kitu ambacho Yesu aliwaambia watu kilitoka kwa Mungu. Basi Yesu alikuwa akisema kwamba rafiki zake walikuwa watu waliotenda ambayo Mungu alisema imewapasa watende.—Yohana 15:14.
Hii haina maana kwamba Yesu hakuwahurumia watu waliokuwa hawafanyi utumishi wa Mungu. Aliwahurumia. Hata alikwenda nyumbani kwao na kula pamoja nao. Watu wengine waliosikia juu ya hili walisema kwamba Yesu alikuwa ‘rafiki ya wenye dhambi.’ Lakini je! hii ilikuwa kweli?— Mathayo 11:19.
Hapana haikuwa kweli. Yesu hakwenda nyumbani kwao kwa sababu alipenda namna walivyoishi. Aliwatembelea ili aweze kusema nao juu ya Mungu. Alijaribu kuwasaidia wageuze njia zao mbaya wamtumikie Mungu.
Hii ilitukia siku moja katika mji wa Yeriko. Yesu alikuwa akipita tu akielekea Yerusalemu. Kulikuwako kundi la watu huko, na katika kundi alikuwako mtu jina lake Zakayo. Alitaka kumtazama Yesu. Lakini Zakayo alikuwa mfupi sana na asingeweza kuona kwa sababu ya kundi. Basi alikimbia akatangulia njiani akapanda mti ili amtazame vizuri Yesu anapopita karibu.
Yesu alipofika penye mti huo alitazama juu akasema: ‘Shuka upesi. Leo nitafika nyumbani kwako.’ Lakini Zakayo alikuwa tajiri aliyekuwa amefanya mabaya. Kwa sababu gani Yesu alitaka kwenda nyumbani kwa mtu huyo?—
Haikuwa kwa sababu Yesu alipenda namna mtu huyo alivyoishi. Alikwenda huko aseme na Zakayo juu ya Mungu. Aliona namna mtu huyo alivyojitahidi sana kumwona. Basi akajua kwamba labda Zakayo angesikiliza. Huu ungekuwa wakati mzuri kuzungumza naye juu ya namna Mungu asemavyo imetupasa tuishi.
Matokeo yalikuwa nini? Zakayo aligeuza njia zake mbaya. Alirudisha fedha ambazo haikuwa haki yake kuchukua, akawa mfuasi wa Yesu. Hapo tu ndipo Yesu na Zakayo wakawa rafiki.—Luka 19:1-10.
Basi, tukijifunza kwa Mwalimu Mkuu, je! tutatembea na watu ambao si rafiki zetu?— Ndiyo. Lakini hatutakwenda nyumbani kwao kwa sababu twapenda namna wanavyoishi. Na hatutafanya mabaya pamoja nao. Tutawatembelea ili tuseme nao juu ya Mungu.
Lakini zaidi tunapenda kukaa na rafiki zetu wa karibu. Tumeona kwamba ili wawe rafiki za namna nzuri, inawapasa wawe namna ambayo Mungu angependa. Lakini tunawezaje kujua ikiwa wako hivyo?—
Basi, njia moja nzuri ni kuwauliza: Je! unampenda Yehova? Huenda wengine kati yao hata wasijue Yehova ni nani. Lakini ikiwa wanataka kujifunza juu yake, twaweza kuwasaidia. Na ufikapo wakati ambapo wanampenda Yehova kama sisi, basi twaweza kuwa rafiki zao wa karibu.
Kuna njia nyingine ya kujua ikiwa mtu angekuwa rafiki mzuri. Tazama mambo ayafanyayo. Je! anawafanyia watu wengine mambo ya uka-tili halafu kucheka? Hivyo si vizuri, sivyo?— Je! sikuzote anapata matata? Sisi tusingetaka tupate matata pamoja naye, sivyo?— Au yeye anafanya mabaya kwa kusudi halafu anafikiri ni mwenye akili kwa sababu hakukamatwa? Hata ikiwa hakukamatwa, Mungu aliona alilofanya, sivyo?— Unafikiri watu wanaofanya mambo hayo wangekuwa rafiki wazuri?—
Sababu gani usichukue Biblia yako, tuone inasema nini juu ya namna wenzi wetu wavutavyo maisha zetu? Andiko liko katika 1 Wakorintho sura ya 15, mstari wa 33, NW. Unapaona?—
Panasema hivi: “Msipotezwe. Mashirika mabaya yanaharibu mazoea mazuri.” Maana yake tukienda na watu wabaya tutakuwa wabaya. Na tena ni kweli kwamba wenzi wazuri wanatusaidia kufanyiza mazoea mazuri.
Tusisahau kabisa kwamba mtu aliye mkubwa kuliko wote katika maisha yetu ni Yehova. Hatutaki tuharibu urafiki wetu naye, sivyo?— Basi inatupasa tuwe waangalifu kufanya urafiki na wale wampendao Mungu tu.
(Maana ya wenzi wa namna nzuri tena inaonyeshwa wazi katika1 Yohana 2:15, 2 Mambo ya Nyakati 19:2, Zaburi 119:115 na 2 Timotheo 2:2. Someni pamoja maandiko hayo.)