Sura ya 30
Watu Wawili Walioadhimisha Ukumbusho wa Siku ya Kuzaliwa
JE! UNAPENDA kuwa na karamu?— Ikiwa ni karamu nzuri, zaweza kupendeza sana.
Lakini si karamu zote ni nzuri. Karamu nyingine ni zenye kelele sana hata jirani wanakasirika. Na kuna karamu nyingine ambazo hata Mungu hazipendi. Ulijua hilo?— Ungependa kuhudhuria karamu ikiwa ungejua Mungu haipendi?—
Biblia inatuambia juu ya karamu. Siku moja Mwalimu Mkuu alihudhuria karamu, ndivyo na mitume wake. Ilikuwa karamu iliyoandaliwa wakati mtu fulani alipokuwa na arusi. Umepata kuhudhuria karamu ya namna hiyo?—
Biblia inatuambia vile vile juu ya karamu mbili za ukumbusho wa siku ya kuzaliwa. Je! mojawapo ilikuwa kuadhimisha ukumbusho wa siku ya kuzaliwa kwa Mwalimu Mkuu?— Hapana. Karamu mbili hizi za ukumbusho wa siku ya kuzaliwa zilikuwa za wanadamu ambao hawakumtumikia Yehova.
Mojawapo ya karamu za ukumbusho wa siku ya kuzaliwa ilikuwa ya Mfalme Herode Antipa. Alikuwa mtawala wa mkoa wa Galilaya wakati Yesu alipoishi huko.
Mfalme Herode alifanya mambo mengi mabaya. Alimchukua mke wa ndugu yake kuwa mke wake mwenyewe. Jina lake alikuwa Herodia. Yohana Mbatizaji mtumishi wa Mungu alimwambia Herode kwamba kufanya hivyo lilikuwa kosa. Herode hakupenda hilo. Basi akaagiza Yohana afungwe kifungoni.—Luka 3:19, 20.
Yohana alipokuwa kifungoni, ikaja siku ya kuadhimisha ukumbusho wa siku ya kuzaliwa kwa Herode. Herode akafanya karamu kubwa. Akawaalika watu wengi wakubwa. Wote wakala na kunywa wakajifurahisha.
Ndipo binti Herodia akaingia akawachezea. Kila mtu alipendezwa sana na kucheza kwake hata Mfalme Herode akataka kumpa zawadi kubwa. Alimwita akasema: ‘Lo lote utakaloniomba nitakupa, hata nusu ya ufalme wangu.’
Angeomba nini? Je! ingekuwa fedha? mavazi mazuri? awe na jumba lake mwenyewe? Yule binti hakujua la kusema. Basi alimwendea mama yake Herodia akasema: “Niombe nini?”
Sasa, Herodia alimchukia sana Yohana Mbatizaji. Basi akamwambia binti yake aombe kichwa chake. Binti akarudi kwa mfalme akasema: ‘Nataka unipe sasa hivi katika sahani kichwa cha Yohana Mbatizaji.’
Mfalme Herode hakutaka kumwua Yohana, kwa sababu alijua Yohana alikuwa mtu mzuri. Lakini Herode alikuwa amefanya ahadi, naye aliogopa ambavyo wengine karamuni wangefikiri ikiwa angegeuza nia yake. Basi alimtuma mtu kifungoni akakate kichwa cha Yohana. Mara akarudi mtu yule. Alikuwa na kichwa cha Yohana katika sahani, akampa binti. Ndipo binti akakimbia akampa mama yake. Je! hilo halikuwa jambo baya sana?—Marko 6:17-29.
Lakini namna gani karamu nyingine ya ukumbusho wa siku ya kuzaliwa ambayo Biblia inasimulia? Je! ilikuwa bora?—
Karamu hii ilikuwa ya mfalme wa Misri. Penye karamu yake vile vile aliagiza kichwa cha mtu fulani kikatwe. Ndipo alipomtundika ndege wamle.—Mwanzo 40:20-22.
Unafikiri Mungu alipendezwa na karamu hizo?— Wewe ungalitaka kuzihudhuria?—
Sasa, twajua kwamba kila kitu kilichomo katika Biblia kimo kwa sababu fulani. Inatuambia juu ya watu wazuri ili tuweze kuwa kama wao. Na inatuambia juu ya watu wabaya ili tusifanye waliyofanya. Biblia inatuambia juu ya karamu mbili tu za ukumbusho wa siku ya kuzaliwa, na mbili zote zilikuwa mbaya. Basi, ungesema Mungu anatuambia nini juu ya karamu za ukumbusho wa siku ya kuzaliwa? Je! Mungu anataka tuadhimishe ukumbusho wa siku ya kuzaliwa?—
Ni kweli kwamba penye karamu kama hizo leo watu hawakati kichwa cha mtu fulani. Lakini wazo lote la kuadhimisha ukumbusho wa siku ya kuzaliwa lilianzishwa na watu waliofanya mambo hayo. Walikuwa wapagani. Walikuwa watu ambao hawakumtumikia Yehova. Je! twataka kuwa kama wao?—
Namna gani Mwalimu Mkuu? Je! aliadhimisha ukumbusho wa siku ya kuzaliwa kwake?— Hapana. Hakuna mahali katika Biblia pasemapo lo lote juu ya karamu ya ukumbusho wa siku ya kuzaliwa ya Yesu.
Hata Yesu alipokwisha kufa, wafuasi wake wa kweli hawakuadhimisha ukumbusho wa siku ya kuzaliwa kwake. Hawakutaka wawe kama wapagani. Lakini mwisho walikuwako watu waliotaka kuadhimisha ukumbusho wa siku ya kuzaliwa kwa Yesu. Hawakuweza kutumia tarehe ya kweli ya kuzaliwa kwa Yesu, kwa sababu Biblia haisemi ilikuwa tarehe gani. Basi walichagua tarehe wakati wapagani walipokuwa na sikukuu. Ilikuwa Desemba 25. Hata leo, ndio wakati ambao watu wanaadhimisha Krismas. Unafikiri Mungu anapendezwa na hilo?—
Basi, tunapokuwa na karamu tunataka tuhakikishe kwamba ni nzuri. Si lazima tungojee siku ya pekee. Twaweza kula chakula fulani cha pekee na kujifurahisha michezo. Ungependa kufanya hivyo? — Lakini mbele ya kufanya mipango yetu, na tuhakikishe kwamba ni karamu ya namna nzuri ambayo Mungu atapendezwa nayo.
(Maana ya kufanya sikuzote ambayo Mungu anapendezwa nayo vile vile inaonyeshwa katika Yohana 8:29, Warumi 12:2, Mithali 12:2 na 1 Yohana 3:22.)