Sura ya 31
Maji Yachukua Ulimwengu
JE! UNAPENDA kucheza michezo?— Mimi napenda. Inaweza kufurahisha sana, sivyo?— Lakini ulijua kwamba kuna hatari katika kushughulika mno na michezo?— Ndiyo. Huenda tukakosa wakati wa kumsikiliza Mungu. Ulijua hilo?—
Mwalimu Mkuu alijua hili lilikuwa limetukia kwa Ulimwengu mzima wa watu hapo zamani. Alisema: ‘Watu hao walikuwa wakila. Walikuwa wakinywa. Walikuwa wakioa na kuolewa.’ Si vibaya kula na kunywa au kuoa na kuolewa. Lakini wao walishughulika mno na mambo hayo hata hawakuwa na nafasi ya kumsikiliza Mungu. Hilo lilikuwa baya.
Jambo gani liliwapata watu hao?— Yesu akasema: “Wasitambue, hata Gharika ikaja, ikawachukua wote.” Yesu alikuwa akisema juu ya watu waliokufa katika siku za Nuhu. Wakati huo maji ya gharika yalifunika dunia nzima.—Mathayo 24:37-39.
Yesu alisema kwamba yaliyowapata watu hao ni onyo kwetu leo. Basi inafaa tujue yote juu ya gharika ya siku za Nuhu.
Kwanza, sababu gani Yehova Mungu alileta Gharika?— Ni kwa sababu watu walikuwa wakifanya mabaya. Hata hivyo alikuwako mtu mmoja aliyepata kibali cha Mungu. Alikuwa nani?— Alikuwa Nuhu. Nuhu alimpenda Yehova Mungu. Yeye hakuwa na shughuli mno hata asimsikilize Mungu. Je! sivyo imetupasa sisi vile vile tuwe?
Siku moja Yehova alimwambia Nuhu kwamba Yeye atawaharibu watu wote walioendelea kufanya mabaya. Mungu angenyesha mvua sana hata maji yangeifunika dunia nzima, hata milima.
Je! Nuhu vile vile angekufa wakati maji yote hayo yangeanguka? Hapana; Yehova angemwokoa. Yehova alimwambia Nuhu ajenge safina kubwa. Safina ni kama chombo, lakini inaonekana zaidi kama sanduku kubwa refu. Inaelea juu ya maji. Mungu alimwambia Nuhu ajenge safina kubwa sana ili yeye na jamaa yake na wengi wa wanyama wawe salama ndani yake.
Sasa, Nuhu hakuwa amepata kujenga safina hapo zamani. Lakini Mungu alimwambia namna ya kufanya. Nuhu na jamaa yake walifanya kazi sana. Wakakata miti mikubwa. Kwa mbao kutoka kwa miti hii wakaanza kujenga safina. Hii ilichukua miaka mingi sana, kwa sababu safina ilikuwa kubwa sana.
Je! Yehova aliwapa watu wengine nafasi ya kuingia katika safina waokoke?— Ndiyo. Yehova alimwambia Nuhu kuhubiri. Basi kwa muda wa miaka ambayo safina ilikuwa ikijengwa, Nuhu aliwaonya watu juu ya gharika itakayokuja.
Je! ye yote kati yao alisikiliza?— Jamaa ya Nuhu tu ndio waliosikiliza. Wote wanaobaki walikuwa wenye shughuli mno wakifanya mam–bo mengine. Hawakufikiri walikuwa wabaya sana, na hawakupata nafasi ya kusikiliza.
Mwisho, wanyama wote ambao Yehova alitaka waokolewe waliingizwa katika safina. Sasa ukawa wakati kwa watu kuingia ndani. Nuhu na jamaa yake waliingia ndani yake. Ndipo Yehova akafunga mlango. Ilikuwa kuchelewa mno kwa mwingine ye yote kuingia.
Watu waliokuwa nje bado hawakuamini kwamba kungekuja gharika. Lakini kwa ghafula maji yakaanza kuanguka! Nuhu alisema kweli!
Haikuwa mvua tu ya kawaida. Yalikuwa mafuriko! Upesi maji yakawa kama mito mikubwa, yakivuma sana. Yakaangusha na miti mikubwa na kuviringisha mawe makubwa kana kwamba yalikuwa changarawe.
Namna gani watu waliokuwa nje ya safina? Yesu akasema: “Gharika ikaja, ikawachukua wote.” Hata ikiwa walipanda kilima, wapi. Mafuriko hayakuacha kwa siku 40 mchana na usiku. Mwisho dunia nzima ikafunikwa maji. Watu wote waliokuwa nje ya safina sasa wakafa. Kwa sababu gani?— Kama Yesu alivyosema, ‘Hawakusikiliza!’
Lakini safina ilikuwa ikielea juu ya maji. Nuhu, jamaa yake na wanyama walikuwa salama ndani. Yehova aliokoa watu waliomsikiliza Yeye.—Mwanzo 6:5-7:24.
Sasa, kwa sababu gani imetupasa tujue juu ya yaliyotukia katika siku za Nuhu? Unakumbuka aliyosema Yesu? Alisema yaliyotukia wakati huo ni onyo kwetu. Tena Yehova atawaharibu watu wabaya wote, lakini wakati huu hatatumia gharika. Wakati wake kufanya hivi uko karibu.
Mungu afanyapo hivi, ni watu gani ambao Mungu ataokoa? Je! watakuwa watu waliokuwa wenye kushughulika mno na mambo mengine hata hawakutaka kabisa kujifunza juu ya Mungu? Je! watakuwa watu ambao sikuzote walikuwa wenye shughuli mno hata wasijifunze Biblia?—Je! watakuwa wale ambao hawakutaka kabisa kwenda kwenye mikutano ambako watu walijifunza mapenzi ya Mungu? Unaonaje?—
Sisi twataka tuwe kati ya watu hao ambao Mungu ataokoa, sivyo?— Je! isingekuwa vizuri sana ikiwa jamaa yetu ingeweza kuwa kama ya Nuhu hata Mungu angeweza kutuokoa sisi sote? Sikuzote na tusaidiane tuwe waaminifu kwa Mungu ili aje atuokoe sisi sote.
(Yatupasa tutafute wakati katika maisha zetu ili tumsikilize Mungu. Soma yanayosemwa juu ya hili katika Hosea 4:6, Mathayo 13:18-22 na Kumbukumbu la Torati 30:15, 16.)