Sura ya 42
Kaburi Tupu
JE! KWELI Mwalimu Mkuu alikufa penye mti wa mateso?— Ndiyo. Watu wengi waliona ikitukia. Wengine hata walimwona askari akitokea na kuchoma mkuki wake katika ubavu wa Yesu. Waliona damu ikitoka. Ndiyo, Mwalimu Mkuu alikuwa amekufa.
Wakati uliofuata, mtu mmoja jina lake Yusufu alikwenda kwa gavana wa Kirumi. Yusufu alimwamini Mwalimu Mkuu. Alisema hivi: ‘Tafadhali uniruhusu niuondoe mwili wa Yesu katika mti niuzike?’ Gavana akasema: ‘Haya. Uondoe.’ Basi Yusufu akaupeleka mwili wa Yesu kwenye bustani mahali lilikuwako kaburi. Unajua kaburi lilivyo?—
Ni mahali ambapo maiti zinapowekwa. Basi, mwili wa Yesu uliwekwa ndani ya kaburi. Halafu jiwe kubwa la mviringo liliviringishwa mbele ya mlango wa kaburi. Kaburi lilifunikwa.
Yesu alikuwa amekufa. Lakini Yesu alikuwa amewaambia wanafunzi wake kwamba Mungu angemfanya awe hai tena. Wakati gani? Yesu alikuwa amesema hivi: ‘Siku ya tatu nikiisha kufa.’ Je! ndivyo ilivyotukia? Ebu tuone.
Ni mapema sana asubuhi, mbele ya kucha. Basi kungali ni usiku. Askari wengine wako huko wakilinda kaburi. Makuhani wakuu waliwatuma kufanya hivyo. Kwa sababu gani? Ili kuzuia wanafunzi wa Yesu wasiende karibu. Lakini sasa jambo la kustaajabisha linatukia.
Kwa ghafula ardhi inaanza kutetemeka. Katika giza kuna mwako wa nuru. Tazama! Ni malaika wa Yehova! Askari wanaogopa sana hawawezi kwenda. Malaika anakwenda kwenye kaburi. Analiondoa jiwe. Tazama ndani. Kaburi ni tupu!
Ndiyo, Yehova Mungu amemrudisha Yesu kwenye uzima. Lakini Yeye amemfanya Yesu hai kwa mwili kama ule ambao Yesu alikuwa nao mbele ya kuja duniani. Je! unakumbuka huo ulikuwa mwili wa namna gani? Ulikuwa mwili kama ule walio nao malaika, mwili wa kiroho.—1 Petro 3:18.
Unaweza kuona mwili wa kiroho?— Hapana. Basi, ikiwa malaika alitaka watu wamwone ilimpasa ajifanyie mwili kama mwili wetu. Ndipo watu wangeweza kumwona. Kisha malaika angetoweka.
Sasa jua linapanda. Askari wamekwenda. Na wanawake wengine waliompenda Yesu wanakuja kwenye kaburi. Wanajiuliza wenyewe hivi: ‘Ni nani atatuondolea jiwe zito?’ Lakini wakati wanapotazama, kumbe jiwe limekwisha kuviringishwa. Na tazama, kaburi ni tupu! Maiti ya Yesu imetoweka! Mara hiyo mmoja wa wanawake anakimbia kwenda kuwaambia wengine wa mitume wa Yesu.
Wanawake wengine wanabaki karibu na kaburi. Wanasema: ‘Mwili wa Yesu unaweza kuwa wapi?’ Kwa ghafula wanaume wawili katika mavazi yenye kung’aa wanatokea. Ni malaika! Wanasema hivi kwa wanawake: ‘Sababu gani ninyi mnamtafuta Yesu hapa? Amefufuka. Nendeni upesi mkawaambie wanafunzi wake.’
Basi, unaweza kuwazia namna wanawake wanavyokimbia sana! Njiani mwanamume mmoja anakutana nao. Unajua ni nani?— Ni Yesu! Yeye vile vile anawaambia wanawake hivi: ‘Nendeni mkawaambie wanafunzi wangu.’
Wanawake wanakuwa na wasiwasi. Wanawakuta wanafunzi na kuwaambia hivi: ‘Yesu yuko hai! Tulimwona!’
Kwanza wanafunzi wanaona jambo hili halisadikiki. Hata hivyo, wanajua kaburi ni tupu. Petro na Yohana wamekwenda huko wakaona ni tupu. Wanafunzi wanataka kuamini kwamba Yesu yuko hai tena. Lakini inaonekana haisadikiki. Jambo gani litawafanya wasadiki?
Kisha Yesu anaonekana kwa wengine wa wanafunzi hao. Wakati wawili wao wanapotembea njiani, Yesu anaanza kutembea nao. Anasema nao kisha anatoweka. Anaonekana kwa Petro vile vile.
Halafu siku ile ile wanafunzi wengi wanakusanyika katika chumba. Milango inatiwa kufuli, kwa sababu wanaogopa makuhani. Kwa ghafula Yesu yuko umo humo chumbani pamoja na wao! Sasa wanajua kweli Mwalimu Mkuu yuko hai tena. Wazia namna wanavyofurahi!—Ma-thayo 28:1-15; Luka 24:1-49; Yohana 19:38-20:21.
Wakati kunapita siku nyingi, Yesu anatoka duniani anarudi kwa Baba yake mbinguni. Upesi wanafunzi wanaanza kumsimulia kila mtu kwamba Mungu alimfufua Yesu kutoka kwa wafu. Watu wengi wanaamini na kuwa wanafunzi.
Jambo hili linawakasirisha makuhani wakuu. Wanaagiza mitume wakamatwe. Wanawaambia hivi: ‘Acheni kuwaambia watu mambo haya!’ Hata wanaagiza mitume wapigwe viboko. Je! wanaacha kufundisha watu? Wewe ungalifanya nini?—
Mitume hawaachi. Hawaogopi sasa. Hata wana nia ya kufa ikiwa ni lazima. Wanajua kwamba Mungu alimfanya Yesu hai tena. Walimwona Yesu alipokwisha kufufuka kutoka kwa wafu. Wana hakika kwamba Mungu anaweza kuwafanya hai tena vile vile ikiwa wanakufa wakiwa waaminifu kwake.—Matendo 1:3-11; 5:40-42.
Sisi tunaweza kuwa kama wanafunzi wa Yesu. Tunaweza kuwaambia watu jambo la ajabu ambalo Mungu alifanya wakati alipomfanya Mwana wake hai tena. Tunaweza kumtii Mungu kama Yesu. Lakini namna gani ikiwa tunakufa kwa sababu ya kumtii Mungu, kama Yesu alivyokufa?— Si lazima kuogopa hata kidogo. Yehova anaweza kutufanya sisi hai tena chini ya ufalme wake wa haki.
(lmani katika kufufuka kwa Yesu imepaswa itupe sisi tumaini imara na kutia nguvu imani yetu. Soma 1 Wakorintho 15:3-8, 20-23; Matendo 2:22-36; 4:18-20.)