Chanzo cha Kimungu cha Roho Takatifu
(Funzo la Kitabu)
1. Kwa sababu gani roho takatifu ilikuwa ikitenda kazi katika Bustani ya Edeni wakati mwanamume na mwanamke walipokutana mara ya kwanza?
WAKATI mwanamume na mwanamke walipokutana mara ya kwanza, waliona nguvu fulani ndani yao—nguvu ya mapenzi. Walipendana wakati uo huo. Mwanamume na mwanamke wa kwanza walikuwa watakatifu ingawa walikuwa uchi, bila mavazi. Ndiyo kusema, walikuwa waking’aa, safi, wenye kutakata, wenye mwili mzima, akili nzima na moyo mzima. Kwa hiyo hawakuona haya na wangeweza kuwa na uhusiano (urafiki) na Muumba wao, Mungu, bila vizuizi. Walifurahia uhusiano wao na Yeye wakiwa kama watoto katika mahali safi na patakatifu. Palikuwa mahali pa raha tu, palipoitwa kwa kufaa Bustani ya Edeni au Paradiso ya Raha. Roho takatifu, yaani, nguvu takatifu ya utendaji ya Mungu, ilikuwa ikifanya kazi sana hapo.
2. Kwa sababu gani Chanzo cha roho takatifu kikawa cha kimungu?
2 Mwanamume na mwanamke, yaani, wazazi wetu wa kwanza wa kidunia, walikuwa wanadamu, yaani, walikuwa wa duniani, walifanyizwa kwa vitu vinavyopatikana hapa duniani. Lakini namna gani Muumba wao, Mungu? Huyu alipaswa kuwa wa kimungu. Alikuwa mwenye cheo bora pia kwa vile alivyokuwa Mtu mwenye akili zaidi. Kwa ufupi, alikuwa bora kuliko mwanadamu. Ndiyo sababu mwanadamu hakuweza kumwona, maana maono yake hayafiki mbali. Basi, mwanamume na mwanamke wa kwanza hawakumwona Muumba wao, Mpaji-Uzima wao, Baba yao wa mbinguni. Kwa kuwa yeye alikuwa mbinguni bila kuonekana, alikuwa ile tunayoita “roho” leo. Kwa kuwa yeye ni Mtu mmoja, kama kiumbe wake mwanadamu, Muumba aweza kuitwa “Roho.” Kwa kutofautishwa yeye ndiye Ile Roho. Yeye ndiye Chanzo kisichoonekana cha roho takatifu, kwa maana Yeye mwenyewe ni mtakatifu.
3. Mwanzo 1:1 yaeleza utendaji wa nani?
3 Kabla dunia yetu na mbingu hazijakuwako, Mtu huyu wa kiroho alikuwa akifanya kazi. Kitabu kitakatifu kinachotueleza habari zote kabla mwanadamu hajakuwako kinaanza kwa kusema waziwazi hivi: “Hapo mwanzo Mungu aliziumba mbingu na nchi.”—Mwanzo, sura ya 1, mstari wa 1.
4, 5. Kwa sababu gani si lazima Mungu aabudiwe katika jengo lo lote la wanadamu mahali po pote duniani?
4 Mungu huyo aliye Muumba yuko juu zaidi hata kuliko mbingu alizoziumba na kwa hiyo yuko juu zaidi kuliko mwanadamu wa dunia. Kwa hiyo yeye ni roho. Maelfu ya miaka baada ya mwanadamu kuumbwa, Mwanzishi wa Ukristo wa kweli alieleza jambo ilo hilo. Alipokuwa karibu na kisima chini ya Mlima Gerazimu katika Samaria wa kale, alimwambia mwanamke Msamaria hivi: “Mungu ni Roho, nao wamwabuduo yeye imewapasa kumwabudu katika roho na kweli.” (Injili ya Yohana sura ya 4, mstari wa 24) Si lazima Mungu wa kweli aabudiwe katika jengo la kidini la wanadamu mahali po pote duniani, hata Yerusalemu katika Mashariki ya Kati. Muda unaopungua miaka 20 baada ya maneno yaliyotangulia kutajwa, mtume Mkristo alisimama mbele ya Baraza Kuu Zaidi ya mji wa Athene, ambako kulikuwa na mahekalu mengi, ya miungu-waume na miungu-wake wa dini yao. Alisema:
5 “Mungu aliyefanya ulimwengu na vitu vyote vilivyomo, yeye, kwa kuwa ni Bwana wa mbingu na nchi, hakai katika hekalu zilizojengwa kwa mkono; wala hatumikiwi kwa mikono ya wanadamu kama kwamba anahitaji kitu cho chote; kwa maana ndiye anayewapa wote uzima na pumzi na vitu vyote. Naye alifanya kila taifa la wanadamu kutoka katika [mtu] mmoja, wakae juu ya uso wa nchi yote.”—Matendo 17:24-27.
6. Mjenzi wa hekalu la kwanza Yerusalemu alionyeshaje kwamba alijua hivyo juu ya kuabudu Mungu?
6 Zaidi ya miaka elfu moja kabla ya hapo mjenzi wa hekalu la kwanza lijulikanalo Yerusalemu katika Mashariki ya Kati alijua hivyo juu ya Mungu wa kweli, ambaye ni Roho asiye wa kidunia. Mfalme wa Yerusalemu wakati huo alisali Kwake alipokuwa akiweka wakf hekalu hilo alilojenga kwa ajili ya jina la Mungu akamwambia: “Lakini Mungu je! atakaa kweli juu ya nchi? Tazama, mbingu hazikutoshi, wala mbingu za mbingu; sembuse nyumba hii niliyoijenga!”—1 Wafalme 8:27.
MUNGU NDIYE CHANZO CHA NGUVU ZOTE
7. Ni kwa njia gani Mungu hawezi kuenea hata katika “mbingu za mbingu”
7 Mwenye kusema maneno yaliyotangulia, Sulemani mwana wa Mfalme Daudi, ndiye aliyekuwa mwanasayansi mwenye hekima zaidi ya wote kabla ya Wakati wetu wa Kawaida. Alisema kweli kwamba Mungu aliyemjengea hekalu asingeweza kuenea hata katika mbingu ya mbingu. Dunia yetu ni kisehemu kidogo sana cha ulimwengu wote ulio mkubwa sana hata wanasayansi hawawezi kuona miisho yake wakitumia darubini zenye nguvu zaidi leo. Hata hivyo, Mungu wa kweli hawezi kuenea katika ulimwengu wote huu usiopimika mpaka sasa. Mungu aweza kupita kitu cho chote cha ulimwengu wote, kionekanacho na kisichoonekana. Aweza kwenda mbali zaidi kukipita na kuumba vitu vingine zaidi vya kupanua ulimwengu wote, nje kabisa ya anga lisilo na miisho. Hiyo yamaanishaje?
8. Uungu wa Muumba ni wa mpaka wakati gani, na kwa sababu gani hakuna lisilowezekana Kwake?
8 Yamaanisha kwamba Mungu hawekewi mipaka na wakati wala anga. Uhai wake nyakati zilizopita haukuwa na mipaka. Maisha yake wakati ujao hayana mipaka. Musa, mpaji sheria mkuu zaidi aliyeishi kabla ya Ukristo, alimwambia Huyu asiyewekewa mipaka hivi: “Tangu milele hata milele ndiwe Mungu.” (Zaburi 90:2) Mungu huyu aishi milele, kwa kusudi la kuendelea kupanua ulimwengu wa sasa. Hiyo yaonyesha yeye ndiye akiba isiyo na mwisho ya nguvu zote. Vitu vyote vilivyo katika ulimwengu wote ni visehemu tu vya nguvu zitokazo kwake. Vimeunganishwa pamoja vikawa vitu vyenye uzito mkubwa na mdogo. Mwanasayansi Albert Einstein wa karne ya 20 alionyesha kwamba: nguvu za vitu vinaweza kujulikana kwa kuzidisha uzito wake na mwendo wa nuru mara mbili. Basi, si ajabu kwamba Mungu aliye chanzo hicho cha nguvu zote aweza mambo yote.
9, 10. Ni kwa njia gani Mungu aleta nje “hesabu” ya jeshi la nyota na hapana hata moja “isiyokuwapo”?
9 Kwa mfano, angalia vile Yeye anavyojitaja kuwa kwa njia inayoelekea kutoaminika, atuambiapo tuinue macho yetu angani usiku tuzitazame nyota. Asema: “Inueni macho yenu juu, mkaone; ni nani aliyeziumba hivi; aletaye nje jeshi lao kwa hesabu; aziita zote kwa majina; kwa ukuu wa uweza wake, na kwa kuwa yeye ni hodari kwa nguvu zake; hapana moja isiyokuwapo mahali pake.”—Isaya 40:26.
10 Watu wenye elimu za nyota leo wanaweza kukadiri tu hesabu ya nyota wanazoweza kuona kwa kutumia darubini zao zenye nguvu zaidi. Sivyo alivyo Muumba mbingu na dunia. “Huihesabu idadi ya nyota, huzipa zote majina.” (Zaburi 147:4) Afananisha nyota zote za mbingu na jeshi kubwa sana. Yeye ajua kila mshiriki wa jeshi hili kwa jina. Aweza kuziita zote kwa majina. Aziitapo nyota hizi, hakuna moja inayokosa kuitika. Kila moja inaitika iitwapo na kueleza inavyofanya kazi. Anakuta kila moja ikitimiza kusudi la kuumbwa kwake. Hakuna inayokosekana.
11. Kwa sababu gani Muumba hachoki wala hataacha ulimwengu wote uharibike?
11 Mungu ana “ukuu wa uweza” usiopimika. Haumaliziki. Tufikiripo tu juu ya nguvu zilizomo katika jua lenye kuongoza zile sayari tisa, ambalo ni tanuru yenye milipuko ya atomiki iliyo kama mlipuko wa makombora ya haidrojeni, tunashangaa kabisa. Halafu tunapofikiria mamilioni mamilioni yasiyohesabika ya nyota nyingi ambazo ni kubwa kuliko jua letu, tunapata kiwazo kidogo juu ya nguvu nyingi ajabu zitokazo kwa Mungu anayewakilishwa na nyota. Hata hivyo ni kweli kabisa: “Huwapa nguvu wazimiao, humwongezea nguvu yeye asiyekuwa na uwezo.” (Isaya 40:29) Hataacha kamwe ulimwengu wetu wenye kupanuka uharibike. Utaendelea kuwako milele utumize kusudi la kuumbwa kwake. Mtazama nyota wa kale alitumia usemi wa mashairi akasema: “Mbingu zauhubiri utukufu wa Mungu, na anga laitangaza kazi ya mikono yake. Mchana husemezana na mchana, usiku hutolea usiku maarifa.”—Zaburi 19:1, 2.
12. Kwa sababu gani wanadamu hawawezi kuwa na sababu ya kumpuza Mungu na wajibu walio nao Kwake?
12 Tunafaidika kwa sababu wanadamu hawawezi kumwona Mungu. Hata hivyo, yeye anatupa ushuhuda mwingi sana kutuonyesha yuko hata wanadamu hawana sababu ya kukataa au kupuza kuwako kwake na wajibu walio nao kwake. “Kwa sababu,” kama mwandikaji mmoja wa Biblia alivyoandika, “mambo yake yasiyoonekana tangu kuumbwa ulimwengu yanaonekana, na kufahamika kwa kazi zake; yaani, uweza wake wa milele na Uungu wake; hata wasiwe na udhuru; kwa sababu, walipomjua Mungu hawakumtukuza kama ndiye Mungu.” (Rum. 1:20, 21) Kwa sababu ya ushuhuda wote uliopo, hawawezi kubisha kwamba Mungu hayuko wala hawawezi kubisha wakisema “Mungu amekufa.” Yeye angali hai tena ana nguvu nyingi ajabu na kumbukumbu kamili la kutimizia makusudi aliyotaja, ambayo yametangazwa na kuhubiriwa miaka elfu sita sasa. Jinsi tunavyoweza kushukuru kwa jambo hili!
13. Zaidi ya nguvu nyingi ajabu, Mungu ni Chanzo cha kitu gani kingine, na kwa sababu gani?
13 Sisi hatujiungi na wanasayansi wa kisasa kukana tukisema Mungu siye Chanzo cha nguvu zote zinazofanya kazi sasa. Twajua yeye ndiye Chanzo cha kitu kingine pia kinachokanwa na, wanasayansi, bila ya kujua habari zake. Kitu gani? Ni “roho.” Kwa sababu gani asiwe ndiye Chanzo cha roho? “Mungu ni roho,” kama Yesu Kristo alivyoonyesha karne kumi na tisa zilizopita.—Yohana 4:24, na maelezo ya pambizoni.
14. “Roho takatifu” ni nini, na ni nani aitoaye?
14 Mungu anatokeza nguvu ya utendaji isiyoonekana anayotimizia mapenzi yake., Nguvu hiyo si maongozi tu kama yale ambayo mwanadamu aweza kutumia juu ya wengine kwa mamlaka. Ni nguvu yenye kutenda kazi, nayo inatoka kwa Mungu aliye mtakatifu, yaani, aliye safi na mwenye haki kabisa. Yeye anaipeleka ikatimize mambo yaliyo matakatifu. Kwa hiyo inaitwa kwa kufaa “roho takatifu.” Ndivyo inavyoitwa katika Neno la Mungu lililoandikwa. Yesu Kristo mwenyewe alimtambua Mungu kuwa ndiye Chanzo cha roho takatifu. Alishuhudia hilo alipowaambia baba zake wanadamu wa siku zake hivi: “Ikiwa ninyi mlio waovu mnajua kuwapa watoto wenu vipawa vyema, je! Baba aliye mbinguni hatazidi sana kuwapa [roho takatifu] hao wamwombao?”—Luka 11:13.
15. Sisi tungetaka roho gani itende kazi juu yetu, kama Mfalme Daudi?
15 Babu wa Kristo aliyekuwa mfalme alikubali pia kwamba Mungu ndiye Chanzo cha roho takatifu. Ilionekana wazi kwamba alikubali hivyo alipokiri kosa lake mbele za Mungu, akamwomba msamaha na kusema: “Usinitenge na uso wako, wala roho yako [takatifu] usiniondolee.” (Zab. 51:11) Kama Mfalme Daudi angalinyimwa roho takatifu angalikuwa ametengwa na Chanzo chake. Matokeo yangalikuwa mabaya sana, yenye msiba. Ikiwa sisi leo twaamini Mungu yuko na ndiye Chanzo cha roho takatifu, tukimwomba roho hiyo, atatupa. Hiyo ndiyo nguvu tunayotaka itende kazi juu yetu, sivyo? Ikiwa twataka hivyo, Mungu ataweza kututumia kufanya mambo mengi yenye faida na kuendelea kutufanya watakatifu katika ulimwengu mchafu sana.
NI NGUVU, SI MTU
16. Yaonyeshwaje kwamba neno la Kiebrania la “roho” linatoa maelezo mengi?
16 Katika Neno la Mungu lililoandikwa, Maandiko Matakatifu, neno lililochaguliwa kama jina la nguvu hii ya utendaji isiyoonekana itokayo kwa Mungu linafaa, kwa maana linatoa maelezo mengi. Katika kitabu cha mwanzo cha Maandiko hayo inaitwa ruʹahh. Tafsiri ya zamani zaidi ya Kigiriki ya kitabu cha kwanza cha Biblia iliiita pneuʹma. Kwa sababu neno la Kiebrania ruʹahh lamaanisha kitendo na mwenendo, watafsiri Waingereza wamelitafsiri kuwa “mpulizo, pumzi, upepo, tufani, nguvu ya utendaji,” na vilevile “roho.” Kwa sababu hiyo maneno yanayozunguka neno hilo la Kiebrania ndiyo yanayosaidia kuamua kama neno hilo lapaswa kutafsiriwa kuwa “roho” au vingine.
17. An American Translation yasema nini mahali pa ‘‘Roho ya Mungu” katika Mwanzo 1:1, 2, na hivyo yaonyesha nini juu ya ruʹahh?
17 Kwa mfano, katika mstari wa pili wa Maandiko Matakatifu neno ruʹahh lapatikana kwa mara ya kwanza. Lapaswa kutafsiriwaje katika lugha nyingine? Tafsiri ijulikanayo sana ya Biblia ya Kiingereza, King James Authorized Version, yatafsiri Mwanzo 1:1, 2 hivi: “Katika mwanzo Mungu aliiumba mbingu na dunia. Nayo dunia ilikuwa bila umbo, na utupu; na giza lilikuwa juu ya uso wa kilindi. Nayo Roho ya Mungu ilienenda juu ya uso wa maji.” Lakini, An American Translation, iliyotafsiriwa na University of Chicago mwaka 1939, yasema hivi: “Wakati Mungu alipoanza kuziumba mbingu na dunia, dunia ilikuwa ukiwa, yenye giza lenye kufunika lile shimo kubwa sana na upepo wa namna ya tufani ulikuwa ukipita kwa nguvu nyingi sana juu ya uso wa maji.” Hapa neno “upepo” limetumiwa mahali pa neno “Roho,” nayo maneno “Roho ya Mungu” yametafsiriwa kuwa “upepo wa namna ya tufani.” Hivyo An American Translation yaonyesha kwamba neno ruʹahh lamaanisha kitu kisichoonekana chenye kuenenda au kutenda.
18. New World Translation of the Holy Scriptures yaonyeshaje kwamba hakuna mtu aitwaye “Roho” aliyeenenda juu ya maji?
18 Tafsiri New World Translation of the Holy Scriptures inashikamana na maoni hayo ya kwamba ruʹahh lamaanisha nguvu isiyoonekana yenye kutenda kazi na kutafsiri Mwanzo 1:1, 2 kwa Kiingereza hivi: “Katika mwanzo Mungu aliziumba mbingu na dunia. Sasa dunia ilikuwa haina umbo na ukiwa na kulikuwa na giza juu ya uso wa kilindi chenye maji, na nguvu ya utendaji ya Mungu ilikuwa ikienenda huko na huku juu ya uso wa maji.” Hivyo tafsiri hii na vilevile An American Translation yaonyesha kwamba hakuna mtu aitwaye “Roho” aliyekuwa akienenda bila kuonekana juu ya maji yaliyofunika dunia yote. Bali, nguvu ya utendaji ya Mungu ambayo haina utu ndiyo iliyokuwa ikienenda huko na huku juu ya uso wa maji usiokuwa na nuru.
19. Tutasemaje juu ya kama roho ya Mungu au nguvu ya utendaji ilikuwa ikienenda juu ya maji bila sababu?
19 Hatujui namna nguvu ya utendaji ya Mungu isiyoonekana ilivyojionyesha kuwa; maandishi ya kwanza hayatoi maelezo mengi. Hata hivyo, ni hakika kwamba nguvu ya utendaji ya Mungu haikuwa ikienenda huko na huku bila sababu, bila matokeo mema: Inaelekea kuwa iliondoa wingu lo lote lenye mavumbi ya miale ya jua ambayo labda yaliizunguka dunia yakazuia nuru ya jua letu isifike usoni pa kilindi chenye maji kilichozunguka dunia yote.a
20. Mungu aliendeleaje na kusudi lake kwamba wazazi wetu wa duniani watumie nuru ya Mchana kuona?
20 Kwa vyo yote, baada ya nguvu ya utendaji ya Mungu kuenenda hivyo huku na huko juu ya uso wa kilindi chenye maji, kwa muda usiotajwa, amri ya kimungu ilitolewa: “Mungu akasema, Iwe nuru; ikawa nuru. Mungu akaiona nuru, ya kuwa ni njema; Mungu akatenga nuru na giza. Mungu akaiita nuru Mchana, na giza akaliita Usiku. Ikawa jioni ikawa asubuhi, siku moja.” (Mwanzo 1:3-5) Hivyo, nguvu ya utendaji ya Mungu ilitenda kazi kwa njia njema, kwa kusudi jema, kupatana na utakatifu wa Mungu. Ilikuwa “roho takatifu.” Mungu aliitumia kuendeleza kusudi lake kwamba wazazi wetu wa kwanza duniani watumie nuru ya Mchana kuona.
21. Kwa vile Mungu ametendesha kazi roho takatifu yake, kwa sababu gani tunaongozwa tujisikie kama mwandikaji wa Zaburi 143:10?
21 Tangu nguvu ya utendaji ya Mungu ilipotajwa mara ya kwanza, yeye ameitumia kufaidi wanadamu. Tunapofahamu hivyo tunapendezwa na Chanzo cha mbinguni cha roho takatifu. Maandishi ya Biblia yanayoonyesha ilivyotenda kazi maelfu ya miaka yafunua kwamba Mungu ameitumia sikuzote kwa njia takatifu. Imetimiza kusudi la Mungu lenye haki. Haitupasi kutaka kuipinga nguvu ya utendaji hiyo isiyoonekana ya Mungu Mwenye Nguvu Zote. Yatupasa kujisikia kama mwandikaji Biblia aliyemwambia hivi: “Unifundishe kuyatenda mapenzi yako, kwa maana ndiwe Mungu wangu; roho yako [njema inihuishe] kwenye nchi sawa.”—Zaburi 143:10. —Kutoka Holy Spirit—the Force Behind the Coming New Order sura ya 1.
[Maelezo ya Chini]
a Tazama Mwanzo 8:1, ambapo neno la Kiebrania ruʹahh limetafsiriwa “upepo,” si “roho.”