Sura ya 7
Mavazi na Sura Yako Huonyesha Ulivyo WEWE
1-4. Ni kwa sababu gani kuvaa kwetu kunaonyesha utu wetu wa ndani? Toa mifano.
UMEPATA kustaajabia rangi za namna nyingi zenye kupendeza katika maua ya masika au kustaajabia namna namna zenye kupendeza za samaki wanaokaa katika maji ya chumvi ya bahari? Kutazama vitu hivi kunatusadikisha kwamba Muumba wetu anapendezwa sana na namna namna ya vitu na uzuri wavyo. Hataki kila kitu kiwe kisichopendeza au kuwa cha namna ile ile. Na inapendeza kama nini kuona mitindo ya namna nyingi sana kati ya watu ulimwenguni pote! Lakini umepata kufikiri kidogo namna sura yako inavyoonyesha sana utu wako wa ndani?
2 Ulipokuwa mtoto mdogo sana labda mavazi yako hayakuonyesha sana namna ulivyokuwa. Wazazi wako walikuwa wakikuvika mavazi na kukuchanua nywele. Lakini ulipogeuka kuwa mtu mzima wakakuacha uchague mwenyewe mavazi yako, uchanue nywele namna upendavyo na mambo kama hayo. Sasa uhuru wako wa kuchagua ukaonekana wazi. Na sura yako mwenyewe ikaanza kuonyesha zaidi na zaidi utu wako wa ndani. Mavazi yako na sura yako vinaonyesha ukoje ndani yako?
KUTUNZA USAWA WAKO
3 Mara nyingi watu wanaojivuna sana wanaonyesha hivyo kwa kupenda mitindo kupita kiasi. Wanataka kumshinda kila mtu mwingine kwa mavazi au kwa sura yao. Lakini kujivuna au choyo chaweza kuonyeshwa vilevile kwa kuwa mzembe sana. Kwa sababu gani? Kwa sababu ijapokuwa huenda mzembe akawa mvivu tu, anaweza vilevile kuwa na moyo wenye choyo wa kutofikiria kama sura yake inawachukiza wengine au sivyo. Mtu asiyejivuna na anayefikiria wengine anakuwa mwenye kiasi katika mambo hayo. Sura yake itaonyesha kwa kuchagua vizuri bila kupita kiasi.
4 Vijana wengine wanadhani ni lazima kufuata mitindo yote ya kisasa ili wasionekane kuwa “watu wa mashambani” (wasio na maendeleo). Lakini kuna kiasi kati ya kushikilia mitindo ya kale kupita kiasi na kufuata mitindo ya kisasa kupita kiasi. Ukiwa hivyo, hapo utakuwa mtu mwenye kuvalia vizuri sikuzote na hutafuata kila mtindo unaotokea, kama kitoto cha bandia kinachogutuka kila mara kamba inapovutwa.
5-7. (a) Ni nani wanaopata sana faida wakati mtu anapotaka kufuata mitindo yote ya mavazi? (b) Mtu anawezaje kuonyesha kwamba anajiheshimu hata asipokuwa na fedha nyingi? (c) Kanuni zinazopatikana katika Wafilipi 2:3, 4 na Warumi 15:2 zinaweza kutumiwa namna gani juu ya kuvaa kwetu?
5 Jiulize mwenyewe: Ni nani anayepata faida ninapopenda sana mitindo? Ni watu wa biashara wanaoanzisha na kutia watu moyo wafuate mitindo. Kuna jambo moja kubwa linalowapendeza: kuchuma fedha. Ukidanganywa nao sikuzote utawapa faida, lakini wewe mwenyewe hupati faida katika njia yo yote ya kweli.
6 Pengine uzembe hautakuletea hasara ya fedha nyingi lakini unaweza kukuletea hasara sana katika njia nyingine. Unaweza kukufanya ukose kazi au ukose kuheshimiwa na wengine. Kama mtu anatunza mavazi yake vizuri na kuwa safi hata yajapokuwa si yenye fedha nyingi, kufanya hivyo kunaonyesha anajiheshimu. Watu wengine wanamheshimu zaidi na kumtumaini zaidi.
7 Kanuni nzuri ya kufuata mambo yote ya maisha inapatikana katika Biblia katika Warumi 15:2: “Kila mtu miongoni mwetu na ampendeze jirani yake, apate wema, akajengwe.” Watu wengine wanatutazama zaidi kuliko tunavyojitazama. Kwa hiyo, je! tusijaribu kuwapa kitu kitakachowapendeza kutazama? Si kitu ambacho kwa sababu ya sura yao kitawafanya waone haya, bali kitu kinachoonyesha tunafikiria maoni yao.
WAJULIKANA KWA MAVAZI
8-11. (a) Watu mbalimbali wanajulikana namna gani kwa mavazi yao? (b) Kwa hiyo huenda watu wakadhania nini kwa kuona mtu anavyovaa, na huenda hili likaleta magumu namna gani?
8 Kuvaa kwako kwaonyesha namna ulivyo katika njia nyingine. Kunaweza kuonyesha wewe kuwa mtu wa kikundi fulani. Hivi ndivyo ilivyokuwa hata maelfu ya miaka iliyopita, wakati Biblia ilipokuwa ikiandikwa. Kwa mfano, tunasoma katika kitabu cha Pili cha Wafalme juu ya watu waliotumwa wakirudi kumpasha Mfalme Ahazia habari na kumwambia walivyokutana na mtu aliyewapa ujumbe fulani. Mfalme aliuliza hivi: “Alikuwa mtu wa [sura] gani?” Walipoeleza juu ya mavazi yake, mara hiyo mfalme akasema: “Ndiye yule Eliya.” Alijuaje? Kwa sababu Eliya alivaa vazi la pekee la nabii.—2 Fal. 1:2, 5-8.
9 Lilikuwa jambo lenye heshima kujulikana kama nabii. Lakini mfano mwingine wa Biblia waonyesha kwamba vazi la mtu laweza kumshirikisha vilevile na kitu kisicho cha heshima. Ili Tamari, binti-mkwe wa Yuda atimize kusudi fulani, alivua mavazi ya ujane wake akavaa shela na nguo ya kujifunika usoni, akaketi kando ya njia. Yuda alipokuwa akipita njia hiyo, habari yasema kwamba “alimdhania kuwa ni kahaba, maana amejifunika uso [kwa shela].” Vazi lake lilimfanya awe na sura ya kahaba wa wakati huo.—Mwanzo 38:13-15.
10 Kama ilivyokuwa hapo kale, leo kuvaa kwetu kwaweza kutushirikisha na vikundi fulani vya watu hata tusipofuata mazoea yao au kuwa na imani yao. Watu wanadhani kwamba bila shaka tunaunga mkono kikundi cha watu wanaovaa namna hiyo. Je! twaweza kuwalaumu?
11 Mtindo wa mavazi unatambulisha si mapolisi, wazima moto au wauguzi tu; unatambulisha vile-vile watu wanaofanya kazi isiyo ya heshima. Leo makahaba hawavai sana shela kama wale waliokuwa katika Kanaani yapata miaka 3,500 iliyopita. Walakini, sasa mavazi yao yenye kuonyesha uchi sana na kuvuta tamaa yanaonyesha waziwazi hata zaidi kazi yao wanayofanya. Vilevile wengine kati ya wanaume wanaopendelea kuasi au kupindua serikali wamevaa mitindo ya pekee, na vivyo hivyo hata wanaume na wanawake wanaofanya ngono wao kwa wao. Je! twataka tushirikishwe na watu hao? Je! tushangae tukikosa kuona kazi tunapoitafuta au tusipopendekezwa kwenye mapendeleo fulani katika kundi la Kikristo kwa sababu tunavaa kama watu hao?
LINALOAMUA JUU YA MITINDO YA NYWELE
12-15. (a) Unadhani ni mitindo ya namna gani ya nywele inayovuta sana macho ya watu siku hizi? Kwa sababu gani? (b) Kwa sababu gani shauri lililomo katika 1 Petro 3:3 lilitolewa? (c) 1 Wakorintho 11:14, 15 linamaanisha nini? Ungetumiaje andiko hilo juu ya mitindo ya kisasa? (d) Wanaume wakifuata wanawake kwa namna wanavyoacha nywele zao ziwe ndefu sana, huenda wengine wakadhania mambo gani?
12 Kuna mitindo mingi ya kusukia nywele zako. Mitindo ya nywele karne zote imekuwa tofauti na ile ya nchi nyingine na vipindi mbalimbali vilevile. Je! kuna tofauti yo yote juu ya mtindo wa nywele unaochagua? Ndiyo, iko. Mara nyingine mitindo ya nywele yenye kupita kiasi sana imefanyizwa kwa sababu ya kiburi cha wanadamu. Mtume Paulo na mtume Petro waliona ni lazima wawashauri wanawake Wakristo kwa sababu hiyo, wasifuate kupita kiasi au wasitie maana kupita kiasi juu ya mitindo ya nywele. Petro aliandika hivi: “Kujipamba kwenu, kusiwe kujipamba kwa nje, yaani, kusuka nywele; na kujitia dhahabu.”—1 Petro 3:3.
13 Walakini, miaka ya karibuni mitindo ya nywele ya vijana, sana sana ile ya kuacha nywele ziwe ndefu sana na masharafa (nywele au ndevu za mashavuni), zimevuta sana macho ya watu. Hata hivyo, je! haikuwa kawaida ya wanaume katika nyakati za Biblia kuacha nywele zao ziwe ndefu kuliko ilivyo kawaida ya nchi nyingi leo? Bila shaka. Lakini kuna jambo jingine la hakika vile-vile. Jambo gani? Bado nywele za wanaume zilikuwa fupi kuliko za wanawake. Ndiyo sababu mtume Paulo aliweza kuliandikia kundi katika Korintho, Ugiriki, akisema hivi: “Je! hayo maumbile yenyewe hayawafundishi ya kwamba mwanamume akiwa na nywele ndefu ni aibu kwake? Lakini mwanamke akiwa na nywele ndefu ni fahari kwake.” (1 Wakorintho 11:14, 15) “Maumbile” yanatufundishaje jambo hili?
14 Kwanza, kati ya watu wenye nywele za singa kama vile Wayahudi na Wazungu ambao Paulo alikuwa akiandikia, kuna tofauti kubwa kati ya urefu wa nywele za wanaume na nywele za wanawake. Kwa kawaida nywele za wanaume ni fupi kuliko za wanawake. Watu wamefahamu vilevile kwamba hili ndilo jambo la “maumbile” na jambo linalowafaa wanaume kukata nywele ziwe fupi kuliko zile za wanawake. Si jambo la asili mwanamume au mvulana kuacha nywele zake ziwe ndefu hata sura yake iwe kama sura ya msichana. Badala yake, nywele ndefu zaidi zinaonyesha namna kizazi kilivyo (na nchi zile) ambamo ngono za wanaume kwa wanaume na wanawake kwa wanawake zinaongezeka. Biblia inaonyesha kwamba ngono za wanaume kwa wanaume na wanawake kwa wanawake ni “matumizi yasiyo ya asili,” hayafai tena ni yenye kuchukiza machoni pa Mungu.—Warumi 1:26, 27.
15 Je! jambo hili linatuzuia sana? Hapana, kwa maana kama yalivyo mavazi, ndivyo ilivyo na mitindo ya nywele, kuna njia za namna nyingi za kusukia nywele ambazo ni zenye kupendeza sana pasipo kupita kiasi au kutenda tofauti na njia ya asili. Bado zinaweza kuwako namna zenye kupendeza ambazo si mbaya machoni pa Mungu.
NAMNA GANI MARASHI (MANUKATO)?
16-19. (a) Wewe waonaje matumizi ya marashi? (b) Mara nyingine yana ubaya gani? (c) Kanuni za Biblia zinatoaje uongozi uliosawazika katika jambo hilo?
16 Biblia inaonyesha kwamba, tangu nyakati za kale watu wametumia marashi. Twajua wanavaa mavazi, si kwa kusudi la kufunika mwili tu, bali kufanya sura ipendeze vilevile. Mara nyingi Waebrania wa kale walitumia manukato ili mwili wao upendeze hata zaidi. Vilevile, kuna ushuhuda unaoonyesha kwamba walitumia marashi fulani, sana sana mafuta ya kujipaka ili ngozi ya mwili isikauke na sura yao ipendeze zaidi.
17 Basi ni nini kitakachoongoza wanawake vijana leo wanaotaka kutenda yatakayofanya wakubaliwe na Mungu? Ni lazima wafuate shauri jema ili watende mambo yote “pamoja na adabu nzuri na moyo wa kiasi,” waache kujipamba kwao “kuwe utu wa moyoni usioonekana, katika mapambo yasiyoharibika; yaani, roho ya upole na utulivu, iliyo ya thamani kuu mbele za Mungu.”—1 Timotheo 2:9, 10; 1 Petro 3:3, 4.
18 Inafaa bila shaka wasichana wafahamu kwamba marashi yanaweza kuwafanyia mabaya kuliko mema. Yanaweza kuharibu sura nzuri au kuifanya iwe mbaya zaidi. Zaidi ya hayo, mara nyingi marashi yanaficha uzuri wa ujana unaopita sana uzuri wa kubandia tu unaofanyizwa na marashi.
19 Kutumia marashi kupita kiasi kunafanya mara nyingi hitilafu (tofauti) za wasichana zionekane. Yanaweza kuzuia zaidi uzuri wo wote wa utu (unaopendeza zaidi na kukaa muda mrefu kuliko sura nzuri) usionekane au usijulikane. Kutumia marashi kupita kiasi kunaweza kuharibu utu wako machoni pa wengine na mwishowe hata utu wako uwe wa bure.
KUFUATA MAONGOZI MEMA
20-22. (a) Tunapata nini katika Biblia badala ya sheria zinazokataza namna ya kuvaa na kujipamba? Basi ili tuyafuate hayo, twatakiwa tufanye nini? (Mithali 2:10, 11) (b) Sababu gani wazazi wana haki kuwekea watoto wao maongozi ya ziada?
20 Hakuna sheria zinazokataza mambo hayo katika Neno la Mungu, lakini yanatolewa maongozi mema. Imewapasa vijana wapate maoni yaliyosawazika, nayo Biblia itawasaidia wafanye hivyo.
21 Wazazi wako wana haki kuweka maongozi ya ziada. Kama nyumba unamoishi ingepakwa mchanganyiko wa rangi zisizofaa, watu wangewaza kwamba labda mwenye nyumba, au mke wake, hana akili. Au, kama nyumba isingetunzwa vizuri na kuharibika sura, wasingemheshimu sana mwenye nyumba. Wewe unawakilisha wazazi wako hata kuliko nyumba. Unachukua jina lao na, kama vile ufanyalo na usemalo linavyoonyesha namna walivyokulea na namna walivyo, ndivyo na sura yako inavyoonyesha. Zaidi ya hayo, ukijidai kuwa mmoja wa watumishi wa Mungu, unamwakilisha Yeye vilevile. Je! sura yako inapatana na vile unavyojidai?
22 Yafikirie maneno ya Yesu: “Mkiyajua hayo, heri ninyi mkiyatenda.” (Yohana 13:17) Je! unaweza kufahamu mwenyewe maana ya shauri hilo la Biblia? Kwa kutumia shauri la Biblia katika maisha yako, unaweza kuonyesha kwamba una busara ya kweli na nguvu ya utu wako. Ndipo utakapokuwa na furaha ya kujua kwamba unapendeza machoni pa Mungu, Mwanawe, na wote wanaompenda na kumtumikia.
[Blabu katika ukurasa wa 53]
Mavazi yako yanaonyesha ukoje?