Watchtower MAKTABA KWENYE MTANDAO
Watchtower
MAKTABA KWENYE MTANDAO
Kiswahili
  • BIBLIA
  • MACHAPISHO
  • MIKUTANO
  • be funzo 15 uku. 131-uku. 134 fu. 4
  • Kuwa Nadhifu

Hakuna video yoyote kwa sasa.

Samahani, haikuwezekana kupakia video.

  • Kuwa Nadhifu
  • Faidika na Elimu ya Shule ya Huduma ya Kitheokrasi
  • Habari Zinazolingana
  • Kwa Nini Mavazi na Mwonekano Wetu Ni Muhimu?
    Furahia Maisha Milele!—Masomo ya Kujifunza Biblia
  • Mavazi Yenye Mpangilio Mzuri Humstahi Mungu
    Huduma Yetu ya Ufalme—2003
  • Je, Mtindo Wako wa Mavazi Unamtukuza Mungu?
    Mnara wa Mlinzi Unaotangaza Ufalme wa Yehova (Funzo)—2016
  • Mavazi na Sura Yako Huonyesha Ulivyo WEWE
    Kupata Faida Zote za Ujana Wako
Pata Habari Zaidi
Faidika na Elimu ya Shule ya Huduma ya Kitheokrasi
be funzo 15 uku. 131-uku. 134 fu. 4

SOMO LA 15

Kuwa Nadhifu

Unahitaji kufanya nini?

Unahitaji kuvaa mavazi nadhifu, safi, na yenye kiasi. Unapaswa kuchana nywele vizuri. Uonekane makini.

Kwa Nini Ni Muhimu?

Maoni ya wengine juu ya imani yako na maisha yako ya Kikristo hutegemea jinsi unavyoonekana.

JINSI unavyoonekana huonyesha mengi juu yako. Ingawa Yehova huutazama moyo, kwa kawaida wanadamu hutazama “sura ya nje.” (1 Sam. 16:7) Ukiwa safi na nadhifu, inaelekea wengine watakuona kuwa mtu anayejiheshimu, na inaelekea kwamba watakusikiliza zaidi. Kuvalia vizuri pia kutaletea sifa tengenezo unalowakilisha na pia kutafanya wale wanaokusikiliza wamheshimu Mungu unayemwabudu.

Miongozo ya Kufuata. Biblia haiweki sheria nyingi juu ya jinsi unavyopaswa kuonekana. Lakini inaandaa kanuni zenye usawaziko zinazoweza kutusaidia kufanya maamuzi mazuri. Msingi wa kanuni hizo zote ni ‘kufanya mambo yote kwa utukufu wa Mungu.’ (1 Kor. 10:31) Kuna kanuni zipi zinazohusu unadhifu?

Kwanza, Biblia inatuhimiza kwamba mwili wetu na mavazi yetu yawe safi. Sheria ambayo Yehova aliwapa Israeli la kale ilikuwa na matakwa yanayohusu usafi. Kwa mfano, makuhani walipokuwa wakihudumu, walipaswa kuoga na kufua mavazi yao pindi fulani hususa. (Law. 16:4, 24, 26, 28) Ingawa Wakristo hawaongozwi na Sheria ya Musa, kanuni hizo zingali zinatumika. (Yn. 13:10; Ufu. 19:8) Mwili wetu, mdomo wetu, na mavazi yetu yanapaswa kuwa safi hasa tunapohudhuria mikutano au tunapokuwa katika huduma ya shambani ili tusije tukawaudhi wengine. Wale wanaotoa hotuba au maonyesho kutanikoni wanapaswa kuweka mfano mzuri wa usafi. Kuwa nadhifu kunamheshimu Yehova na tengenezo lake.

Pili, Biblia inatuhimiza tuwe wenye kiasi na utimamu wa akili. Mtume Paulo aliwahimiza wanawake Wakristo “wajirembe . . . na kiasi na utimamu wa akili, si kwa mitindo ya kusuka nywele na dhahabu au lulu au mvao ulio ghali sana, bali katika njia inayofaa wanawake wanaodai kumstahi Mungu.” (1 Tim. 2:9, 10) Wanaume pia wanapaswa kuvaa na kujitunza kwa kiasi na utimamu wa akili.

Mtu mwenye kiasi anatahadhari asiwaudhi wengine isivyofaa na kutojielekezea fikira mno. Utimamu wa akili hutokeza busara, au utambuzi. Mtu mwenye sifa hizi ana usawaziko kwa sababu anaheshimu kanuni za Mungu. Haimaanishi tusivae kwa njia inayovutia lakini sifa hizo zinatusaidia kuvaa kwa njia ya busara na kuepuka mavazi na mapambo yanayopita kiasi. (1 Yoh. 2:16) Tutumie kanuni hizi tuwe mikutanoni, katika huduma ya shambani, au katika utendaji mwingine wowote. Hata mavazi yetu ya kawaida yaonyeshe kiasi na utimamu wa akili. Tukiwa shuleni au kazini, tutapata fursa za kuhubiri kivivi-hivi. Ingawa huenda tusivae kama tunavyovaa tukihudhuria mikutano, na makusanyiko, bado tunapaswa kuvaa mavazi nadhifu, safi, na yenye kiasi.

Ni wazi kwamba sisi sote hatuvai kwa njia ileile moja wala hatutazamiwi kufanya hivyo. Watu wana mapendezi tofauti-tofauti na hiyo ni sawa. Lakini, nyakati zote tutumie kanuni za Biblia.

Mtume Petro alionyesha kwamba jambo muhimu zaidi kuliko hata mitindo ya kusuka nywele na mavazi ya nje ni “mtu wa siri wa moyoni.” (1 Pet. 3:3, 4) Mioyo yetu inapojaa upendo, shangwe, amani, fadhili, na imani thabiti, hizi sifa zitakuwa kama mavazi yetu ya kiroho ambayo yanamheshimu Mungu kwelikweli.

Tatu, Biblia inatuhimiza tufikirie kama mavazi yetu yana mpangilio mzuri. Andiko la 1 Timotheo 2:9 linataja “mavazi yenye mpangilio mzuri.” Ingawa mtume Paulo alirejelea mavazi ya wanawake, kanuni hiyo inahusu wanaume pia. Kitu ambacho kina mpangilio mzuri ni nadhifu. Tuwe matajiri au maskini, tunaweza kuwa nadhifu.

Mojawapo ya mambo ambayo wengine huona kwanza ni nywele zetu. Nywele zetu ziwe nadhifu, au zichanwe vizuri. Kwa kawaida watu huchana nywele zao kulingana na desturi za mahali wanapoishi au kulingana na jinsi nywele zao zilivyo. Andiko la 1 Wakorintho 11:14, 15, lina ushauri wa mtume Paulo kuhusu mitindo ya nywele, na inaonekana alifikiria mambo hayo mawili. Lakini, mtindo wa nywele za mtu ukidokeza kwamba anajaribu kufanana na watu wa jinsia tofauti, basi anakiuka kanuni za Biblia.—Kum. 22:5.

Unadhifu wa wanaume unatia ndani kunyoa ndevu. Katika sehemu ambazo masharubu yanakubalika, mtu yeyote mwenye masharubu ayatunze vizuri.

Nne, tusionyeshe kupenda ulimwengu na njia zake. Mtume Yohana alionya hivi: “Msiwe mkipenda ama ulimwengu ama vitu vilivyo katika ulimwengu.” (1 Yoh. 2:15-17) Ulimwengu umejaa tamaa nyingi za kufanya dhambi. Yohana anataja baadhi ya tamaa hizo kuwa tamaa ya mwili wenye dhambi na wonyesho wa mali. Pia Maandiko yanataja roho ya uasi, au kutotii wenye mamlaka. (Mit. 17:11; Efe. 2:2) Mara nyingi mavazi ya watu na mapambo yao huonyesha tamaa zao na fikira zao. Kwa hiyo wanaweza kuvaa kwa njia isiyo na kiasi, kwa njia inayochochea tamaa ya ngono, kwa kujionyesha, kwa kujiachilia, au kizembe. Tukiwa watumishi wa Yehova, sisi huepuka mitindo kama hiyo isiyo ya Kikristo.

Badala ya kuiga ulimwengu, ni afadhali kuiga mifano mizuri ya wanaume na wanawake wakomavu kiroho wa kutaniko la Kikristo kwa jinsi tunavyovaa na kujipamba. Vijana wanaotumaini kutoa hotuba za watu wote siku moja wanaweza kutazama mavazi ya wale ambao wanatoa hotuba za watu wote. Wote wanaweza kuiga mfano unaowekwa na wale ambao wamefanya kazi ya kuhubiri kwa miaka mingi.—1 Tim. 4:12; 1 Pet. 5:2, 3.

Tano, ili kuamua jambo linalofaa, tunapaswa kukumbuka kwamba “hata Kristo hakujipendeza mwenyewe.” (Rom. 15:3) Jambo kuu zaidi katika maisha ya Yesu lilikuwa kufanya mapenzi ya Mungu. Pia Yesu aliweka masilahi ya wengine mbele ya masilahi yake. Ikiwa aina fulani ya mavazi au kujipamba kwa njia fulani kunaweza kuwakwaza watu wa eneo tunamotumikia sasa, tufanyeje? Tukiiga roho ya unyenyekevu ya Kristo tutaweza kufanya uamuzi wenye hekima. Mtume Paulo alitaja kanuni hii: “Katika njia yoyote sisi hatutoi sababu yoyote ya kukwaza.” (2 Kor. 6:3) Kwa hiyo tunaweza kuacha mitindo fulani ya nywele au kuacha kuvaa mavazi ambayo yanaweza kuwazuia watu wasitusikilize.

Jinsi Unavyosimama. Unadhifu unatia ndani kusimama vizuri. Haiwezekani sisi sote tusimame kwa njia ileile moja, na hatujaribu kuiga njia fulani ya kusimama. Lakini, kulingana na Biblia, kusimama wima kunaonyesha heshima na usadikisho. (Law. 26:13; Luka 21:28) Hata hivyo, ndugu au dada anaweza kushindwa kusimama wima au anaweza kuhitaji kuegemea kitu fulani kwa sababu ya kufanya kazi kwa miaka mingi akiwa ameinama au kwa sababu ya uzee au kwa sababu ya kudhoofika kimwili. Lakini inapendekezwa kwamba wale ambao wanaweza kusimama wima wasimame hivyo ili watu wasidhani hawajali au kwamba wanajutia yale wanayosema. Na ingawa si vibaya kwa msemaji kuegemea kinara cha msemaji pindi kwa pindi, kwa kawaida wasikilizaji huvutiwa zaidi asipokiegemea.

Vifaa Nadhifu. Mbali na sisi wenyewe kuwa safi na nadhifu, vifaa tunavyotumia katika huduma viwe safi na nadhifu pia.

Ebu fikiria Biblia yako. Si rahisi kwa wengine kupata Biblia mpya wakati Biblia wanazotumia zinapochakaa. Lakini hata kama umetumia Biblia yako kwa muda gani, inapaswa kuwa wazi kwamba inatunzwa vizuri.

Unaweza kupanga vichapo kwa njia mbalimbali katika mkoba wa kuhubiri, lakini mkoba huo uwe nadhifu. Je, umewahi kuona karatasi zikitawanyika zikitoka katika Biblia ya mhubiri anapomsomea mwenye nyumba andiko fulani au labda ndugu anapotoa hotuba mbele ya kutaniko? Ulikengeushwa, sivyo? Kama karatasi zilizowekwa ndani ya Biblia zinakengeusha, labda kuweka karatasi hizo mahali pengine kunaweza kufanya vifaa vyako viwe nadhifu. Kumbuka pia kwamba kuweka Biblia yako au vichapo vingine vya dini sakafuni huonwa kuwa kukosa heshima katika jamii nyingine.

Tutilie maanani unadhifu. Unadhifu unawapa pia wengine picha ya jinsi tulivyo. Na jambo muhimu zaidi ni kwamba tunakuwa nadhifu kwa sababu tunataka “kuremba fundisho la Mwokozi wetu, Mungu, katika mambo yote.”—Tit. 2:10.

CHUNGUZA JINSI UNAVYOONEKANA

  • Je, kila kitu ni safi?

  • Je, jinsi unavyoonekana inaonyesha una kiasi na utambuzi?

  • Je, kila kitu kimepangwa vizuri?

  • Je, nywele zako ni nadhifu

  • Je, jinsi unavyoonekana inaonyesha kwa njia yoyote kwamba unapenda ulimwengu?

  • Je, kuna sababu nzuri ya kufikiria kwamba jinsi unavyoonekana inaweza kukwaza mtu?

MAZOEZI: Jichunguze kila siku katika juma lote, hata kama umepangia kufanya nini, ukitumia orodha inayosema “Chunguza Jinsi Unavyoonekana” iliyoko kwenye ukurasa wa 132.

    Maktaba Kwenye Mtandao (1980-2025)
    Toka
    Ingia
    • Kiswahili
    • Shiriki
    • Mapendezi
    • Copyright © 2025 Watch Tower Bible and Tract Society of Pennsylvania
    • Masharti ya Utumiaji
    • Sera ya Faragha
    • Mpangilio wa Faragha
    • JW.ORG
    • Ingia
    Shiriki