Watchtower MAKTABA KWENYE MTANDAO
Watchtower
MAKTABA KWENYE MTANDAO
Kiswahili
  • BIBLIA
  • MACHAPISHO
  • MIKUTANO
  • yy sura 9 kur. 66-71
  • Je! Unachoshwa Nyumbani?

Hakuna video yoyote kwa sasa.

Samahani, haikuwezekana kupakia video.

  • Je! Unachoshwa Nyumbani?
  • Kupata Faida Zote za Ujana Wako
  • Vichwa vidogo
  • Habari Zinazolingana
  • MAONI YAWEZA KULETA TOFAUTI
  • KUWA NA NIA YA KUANZA MAMBO NA KUWA NA MAMBO MENGI ZAIDI YENYE KUPENDEZA
  • Je, Ni Suluhisho Sahili kwa Ukimwa?
    Amkeni!—1995
  • Vipi Ikiwa Mtoto Wangu Anahisi Amechoshwa?
    Msaada kwa Ajili ya Familia
  • Kuchoshwa Kwaweza Kusababisha Mkazo na Kushuka Moyo
    Amkeni!—1990
  • Nifanye Nini Nikikosa Kitu cha Kufanya?
    Vijana Huuliza
Pata Habari Zaidi
Kupata Faida Zote za Ujana Wako
yy sura 9 kur. 66-71

Sura ya 9

Je! Unachoshwa Nyumbani?

1-3. (a) Unafikiri ni kitu gani kinacholeta uchovu katika nyumba nyingi? (b) Je! ni vibaya kupendezwa na mambo yasiyo ya nyumbani mwenu?

LEO tatizo la uchovu linapata vijana wengi ijapokuwa nyumba hazifanani. Haikuwa hivyo zamani. Miaka ya zamani, jamaa zilifanya kazi nyingi zaidi pamoja tena ziliungana sana kwa njia hiyo. Lakini leo vijana wengi wanaona “nyumbani kwao” ni mahali pa kula na kulala tu.

2 Je! umepata kusumbuliwa na uchovu? Kama ndivyo, basi unaweza kupunguza furaha ya nyumba yako. Labda unajiona nyakati nyingine unataka kuishi peke yako na kujitafutia maisha yenye kupendeza.

3 Hii ni kawaida inayowapata vijana. Unakuza maoni yako wakati unapoendelea kukua. Unatamani zaidi kujua mambo. Unapendezwa ujaribu kutumia vitu vipya. Ulizo ni hili, Utaonyeshaje maoni hayo makuu? Je! yatakufanya uchoke na nyumbani kwenu au uchoke na uongozi wa wazazi? Sana sana ni nini kinacholeta uchovu mwingi, na ni njia gani ya kuuondolea?

MAONI YAWEZA KULETA TOFAUTI

4-6. (a) Maoni ya mtu mwenyewe yanaamua sana namna gani kama anachoshwa au hachoshwi? (b) Wewe mwenyewe ungeweza kufanya nini ili hali ya nyumbani mwenu iwe bora? (Wafilipi 2:3, 4)

4 Ni kweli kwamba nyumba nyingine zina magumu yanayozuia amani na furaha. Lakini kwa kawaida ni maoni yako yanayoonyesha kama unaona maisha ya nyumbani kuwa yenye kupendeza au yenye kuchosha. Kwa sababu gani? Kwa sababu kuna vijana wenye hali izo hizo wanaofurahia maisha, huku wengine wenye hali izo hizo wakichoka nayo. Tofauti ni kwamba wengine wana maoni yaliyo bora juu ya maisha yao ya nyumbani. Hivyo kushinda uchovu na magumu mengine mengi kunategemea sana namna maoni yako mwenyewe yalivyo juu ya mambo hayo vilevile.

5 Sababu gani usione hivi: Kila jamaa ina hali yake. Hali hii haifanyizwi na mtu mmoja ye yote, ila kila mtu anashiriki kuongeza hali nzima ya jamaa. Jamaa yako ikoje? Je! nyumbani kwenu ni mahali penye furaha na uchangamshi? Je! mnafurahiana, mnazungumza kwa furaha wakati wa chakula, mnaona furaha ya kufanya kazi pamoja na kutumikiana? Au kila mmoja wenu anatenda kwa njia yake mwenyewe, bila kupendezwa sana na wenzake? Wewe ungependelea iwe namna gani?

6 Ni vyepesi kulaumu wengine mambo yakiwa tofauti na unavyotaka yawe. Lakini kabla ya kunung’unika, sababu gani usijiulize hivi kwanza: “Mimi mwenyewe nafanya nini ili nisaidie kuweko hali nzuri ya jamaa? Najitahidi kwa kadiri gani nilete maendeleo?” Kama merikebu inapigwa na mawimbi ya bahari yenye kuchafuka ni kazi bure nahodha kuketi pembeni na kunung’unika. Ni wakati wa wote kufanya kazi na kila mtu kusaidia ili merikebu isafiri salama mpaka kuifikilia nchi kavu.

7-9. Ni nini kinachoweza kutusaidia tuache kuchoshwa na kazi yo yote tunayopaswa kufanya?

7 Mara nyingi vijana wanaochoshwa hawaoni faida ya kazi wanazopewa kufanya. Jaribu kuhakikisha namna kazi zo zote unazogawiwa shuleni au nyumbani au unakofanya kazi zinavyopasa maisha yako na maisha za wengine vilevile, sasa na siku zijazo. Kama unaweza kufanya hivyo, utaweza kuzifanya kazi hizo ukiwa na kusudi. Jambo hili laweza kutofautisha kati ya kufurahia maisha na kuchoshwa.

8 Kwa kweli, zile kazi zenyewe unazoona zinachosha zingeweza kukusaidia usitawishe sifa na mazoea yenyewe yatakayokuwezesha zaidi sana uwe na maisha mazuri wakati ujao. Kwa mfano: Kama wewe ni kijana, je! umepata kuunda ndege-ulaya ya mfano? Kwanza, ilikupasa uunganishe vipande vingi vya vyuma kisha kuvifunika. Pengi-ne wakati wa kumalizika kwa ndege-ulaya vipande vilivyounganishwa havitaonekana. Lakini bila nguvu na kielezo chake, ndege-ulaya hiyo ingekuwa kazi bure. Au, kama wewe ni msichana, je! umepata kushona vazi la kike? Pengine vazi lilipomalizika mishono uliyopinda haikuonekana. Lakini bila mishono hiyo isiyoonekana, kusingekuwako vazi.

9 Ndivyo na yale unayojifunza shuleni au unayojifunza kwa kufanya kazi nyumbani. Ni sehemu ya kiolezo (mfano) chote kiwezacho kusaidia kuweka msingi wa kuwa na matokeo mazuri wakati ujao. Unaweza kujifunza uvumilivu na kukaza nia, hata kupata nguvu ya ndani kwa kufanya kazi mara nyingi ambazo ni nyepesi na zisizo na maana.

KUWA NA NIA YA KUANZA MAMBO NA KUWA NA MAMBO MENGI ZAIDI YENYE KUPENDEZA

10-12. (a) Mtu anaposema, “Hakuna la kufanya,” kwa kawaida mtu huyo hana nini? (b) Ni mambo gani ya kufurahisha yanayofanya akose hicho?

10 Mara nyingi wakati wa vipindi vyenye nafasi tele, mtu anasikiwa akinung’unika kwamba, “Hakuna la kufanya.” Kwa kawaida ugumu si kutokuwa na mambo yenye kupendeza na yanayofaa kufanywa, bali ni kutokuwa na nia ya kuanza mambo, na kutokuwa na akili ya kufikiri. Au pengine mwenye kunung’unika anaweza kuonyesha kwamba hana mambo mengi yanayompendeza.

11 Taratibu ya sasa haitii watu moyo wawe na nia ya kuanza mambo, sana sana nyumbani. Hata vijana leo wanazoea kuwa watazamaji kuliko kuwa watendaji. Je! ndivyo unavyotumia wakati mwingi nyumbani, ukitazama sinema, vipindi vya television, ukisikiliza muziki au kuwatazama wengine wakicheza michezo ya kushindana?

12 Hili ni jambo jepesi zaidi kuliko kufanya kazi mwenyewe, au kujifunza kufanya kazi. Lakini mwishowe inachosha vilevile. Jambo hili linakufanya utegemee sana furaha ya wengine; linakuacha katika hali ya kutoweza kujifanyia kazi ili ufanye maisha yapendeze. Jambo hili lawafaa watoto wachanga, lakini haliwafai wanaume na wanawake wanaokua wawe watu wazima.

13, 14. Ni kazi gani unazofurahia zinazotaka uwe na nia ya kuanza mambo au kushiriki?

13 Una mambo mangapi yenye kupendeza? Hakuna mwisho wa kazi zinazofaa na elimu zinazopaswa kuchunguzwa. Kusoma kunataka bidii zaidi kuliko kutazama television. Lakini kunaleta faida kubwa zaidi. Hakuna utendaji, hakuna kazi, hakuna mahali wala watu wala wanyama wasiozungumzwa katika vitabu. Unapozidi kusoma ndivyo furaha yako ya kusoma inavyozidi, na uwezo wa kufahamu maarifa unazidi vilevile. Lakini haitoshi kusoma kwa kusudi la kupisha wakati tu. Ni lazima uamue juu ya jambo litakalokuwa lenye faida. Ndipo unapoweza kusoma ukiwa na mradi utakaofanya maisha yako yawe yenye maana sasa na wakati ujao kwa kukutayarisha ufanye mambo.

14 Bila shaka, si kila mtu anayefurahia kufanya mambo ambayo wengine wanafurahia. Wengine wanafurahia kujifunza kufanya kazi ya mbao au ya vyuma, hali wengine wanapendelea kazi ya kupiga picha au kulima bustani. Labda wasichana wengine wanataka kazi ya kupika chakula, hali wengine wanapendelea kushona au kazi ya kusuka nywele. Lakini kujifunza kufanya mambo mapya, nyumbani au mahali pengine, na kusitawisha uwezo wa kufanya kazi bora kutaleta furaha na kufanya maisha yapendeze.

15-18. (a) Wakati mtu anapozoea kutumikia watu wengine, maisha yake yanakuwa namna gani? (Matendo 20:35) (b) Ni nini mojawapo la mambo yanayofaa sana ambalo kijana Mkristo aweza kufanyia watu wengine? (Mathayo 24:14; 1 Timotheo 4:16) (c) Kwa sababu gani ni vizuri zaidi kuendelea na bidii yo yote inayofaa?

15 Unapoona hupendi kufanya jambo kwa faida yako mwenyewe, sababu gani usimfanyie mtu mwingine, ukianzia nyumbani? Kazi isiyoweza kupendeza ambayo ungejifanyia mwenyewe yaweza kupendeza sana unapomfanyia mtu mwingine, mshiriki wa jamaa, rafiki, zaidi mtu aliye na shida. Jambo hili linafurahisha sana, na hakuna mwisho wa nafasi za kufanya hivyo. Usingojee kuambiwa kufanya jambo fulani. Unalofanya lisipotazamiwa na mtu mwingine, kule kushangaa kwake kutakuongezea furaha. Ebu jaribu.

16 Hiyo ni njia nyingine inayoweza kukupa faida kwa kuwatumikia wengine. Vijana wanaopendezwa sana na ahadi ya Mungu ya taratibu mpya wanaona kwamba kushiriki habari njema hizi pamoja na wengine kunayafanya maisha yao yawe yenye maana zaidi. Inaleta faida sana kupata watu wanaotafuta kweli sana na kuweza kuwasaidia. Ijapokuwa hao ni wengi kuliko wale wanaoikataa kweli, hilo halipunguzi matokeo yenye kuchangamsha ya utendaji huo. Badala yake, linaufanya utendaji huo uwe mgumu zaidi. Uvumilivu na imani vinahitajiwa. Hizi ni njia kubwa za kushinda kuchoshwa.

17 Mtume Paulo anaambia wale wanaomtumikia Mungu hivi: “Tusichoke katika kutenda mema; maana tutavuna kwa wakati wake, tusipozimia roho.” (Wagalatia 6:9) Vilevile, unapotaka kusitawisha uwezo wenye kusudi na faida ya kweli, imekupasa uendelee kufanya hivyo mpaka utakapoanza kupata matokeo ya kutaabika kwako.

18 Halafu unaweza kupanua uchunguzi wako wa uwezo mwingine ambao bado watakiwa kusitawishwa, na kwa sababu hiyo utakuwa mtu bora, mwenye kupendeza na mwenye kufaa zaidi. Wazazi wako na wengine nyumbani watafurahia kuwa karibu nawe, nawe hutachoshwa nyumbani.

[Picha katika ukurasa wa 68]

Taabu baharini yataka watu washirikiane sana. Je! matata yakiwako nyumbani, wewe unasaidia kuwe amani?

    Maktaba Kwenye Mtandao (1980-2025)
    Toka
    Ingia
    • Kiswahili
    • Shiriki
    • Mapendezi
    • Copyright © 2025 Watch Tower Bible and Tract Society of Pennsylvania
    • Masharti ya Utumiaji
    • Sera ya Faragha
    • Mpangilio wa Faragha
    • JW.ORG
    • Ingia
    Shiriki