Sura ya 11
Sababu Gani Ujifunze Shuleni?
1-3. (a) Wewe unaonaje shule? (b) Kanuni ya Biblia katika Wagalatia 6:7 inakupasaje masomo ya shule?
UNAKWENDA shuleni kwa sababu gani? Labda ni lazima katika nchi yenu kwenda shuleni mpaka kufikia umri fulani, upende usipende. Au labda wewe ni mchanga bado na kwa hiyo inakupasa ufanye unavyoagizwa na wazazi.
2 Walakini, je! unaona sababu nyingine zo zote za kuwa shuleni? Je! kuna faida zo zote zinazotokana na kufanya bidii sana shuleni au masomo unayopewa ukafanyie nyumbani? Bila shaka unawajua vijana wengi wanaojifunza ili waonekane tu kama wanajifunza, sivyo? Lakini, kwa kutokuitumia vizuri nafasi waliyonayo wajifunze wanajizuia wenyewe kwa muda wa maisha zao. Ni kwa sababu gani?
3 Kwa sababu jambo ambalo mtu anafanya wakati wa ujana wake linaonyesha analoweza kufanya akiwa mtu mzima. Kanuni hii ya Biblia inapasa hata shule: “Cho chote apandacho mtu, ndicho atakachovuna.” (Wagalatia 6:7) Lakini, labda utauliza hivi, ni faida gani zinazotokana na ‘kupanda’ wakati na bidii za kujifunza shuleni sasa?
MAFUNDISHO YANAYOFAA
4-6. (a) Kwa sababu gani ikiwa mtu anatumia vizuri nafasi zake za kujifunza shuleni ana hali njema zaidi? (b) Ni masomo gani yanayotolewa shuleni ambayo unadhani yangekufaa zaidi wakati wa maisha ya baadaye?
4 Ni lazima ujue kwamba kwa muda wa miaka michache inayobaki pengine itakupasa ujitegemee mwenyewe. Pengine mwishowe utakuwa na madaraka ya kuwa mume na baba, au kuwa mke na mama. Je! ungetaka kufanya madaraka hayo yawe mepesi na yenye kufurahisha zaidi? Ukitumia vizuri miaka yako ya kuwa shuleni, ukijifunza mambo yatakayofaa maisha yako ya mtu mzima, unaweza.
5 Kuna masomo yanayoweza kukufundisha mambo ya msingi ya kazi mbalimbali katika shule nyingi. Kwaweza kuwa na masomo ya wanaume vijana ya useremala, kazi ya umeme, kazi ya kuunganisha vyuma kwa moto, kazi ya uhasibu (hesabu) na masomo mengine. Wanawake vijana wanaweza kuchukua masomo ya kazi ya ukarani, kazi za nyumbani, kama kupika na kushona, na masomo mengine yenye maana.
6 Huenda mengi kati ya mafundisho haya yasipatikane vyepesi ukiisha kuacha shule. Ukiyapata baadaye, pengine yatakuwa yenye fedha nyingi sana. Au labda itakupasa ujifunze kwa kufanya kazi pamoja na wengine wasiotaka sana kukufundisha. Kwa hiyo, kwa nini usitumie nafasi uliyo nayo ujifunze machache kati ya mambo hayo wakati bado uko shuleni? Ndipo wakati mwingine unaweza kuzungumza na wazazi wako juu ya masomo ya shule unayotaka kuchagua. Kwa kufanya hivi utaweza kufaidika na ujuzi ambao wamepata katika maisha.
JIFUNZE KUSOMA VIZURI
7-11. (a) Kwa sababu gani uwezo wa kusoma vizuri ni wenye faida sana? (1 Timotheo 4:13; Yoshua 1:8) (b) Ni nini lingeweza kukusaidia kufanya uwezo wako wa kusoma uwe bora?
7 Ijapokuwa kuna mambo mengi ambayo ni bora unayoweza kujifunza shuleni, kuna jambo moja linaloweza kukufurahisha sana. Hilo litaongoza sana maisha yako mengine ya shuleni na vilevile maisha yako yote ya mtu mzima. Huo ndio uwezo wa kusoma—kusoma VIZURI. Ndiyo njia ya kukuongoza kwenye namna nyingi za maarifa, ufundi na furaha.
8 Kila siku unaona vitu vya kusoma kama: ishara, maandishi juu ya vibandiko, vitabu, magazeti, karatasi za kazi, na barua vilevile. Vyote hivi vinaweza kuwa kazi isiyopendeza wale wasiosoma vizuri. Walakini, kama unajifunza kusoma vizuri, utaona maisha yanafurahisha sana.
9 Utataka ujifunze kusoma vizuri sana sana kama wewe ni Mkristo ili uweze kujifunza yaliyomo katika Biblia, Neno la Mungu. Vilevile utaona kujua kusoma vizuri kuwa na thamani kuu unapowaambia wengine makusudi ya Mungu. Ndiyo, kusoma kuzuri na kuzungumza kuzuri, ni mambo yanayokamatana sana.
10 Ukiona ni vigumu kwako kusoma kama wengi wanavyoona, usivunjike moyo. Unatakiwa ujizoeze sana na kuwa mwangalifu wa kuona namna maneno yanavyoendelezwa. Nyakati nyingine usome kwa sauti kuu. Kufanya hivyo kutakusaidia ufahamu maana ya kweli upate kutumia uchangamfu unaofaa wakati wa kusoma. Ikiwezekana, mwombe mtu anayesoma vizuri asikilize wakati unaposoma. Kufanya hivyo kutakusaidia utengeneze makosa yo yote au mazoea mabaya yo yote unayositawisha.
11 Ni kweli kwamba bila kufanya bidii sana huwezi kuwa na uwezo wa kusoma bila kukosea-kosea. Lakini utapata faida mara nyingi ukifanya bidii sasa. Bidii hiyo itakusaidia upate faida zote za maisha.
FAIDA NYINGINE ZINAZOTOKANA NA KUJIFUNZA
12-14. (a) Masomo unayojifunza sasa shuleni yana faida gani? (b) Kujiadibisha upate kujifunza kutakupa faida namna gani maishani baadaye?
12 Pengine masomo fulani ya shule yataonekana hayana faida sana, lakini yanapanua maoni yako na ni yenye faida katika njia nyingine. Kujifunza historia, jiografia na lugha kunakuwezesha ujue watu wengine na mahali pengine. Elimu ya hesabu ambayo wengi wanaona kuwa somo gumu, inafaa sana katika kazi na mambo mengi. Ni yenye faida hata kwa mama anayehitaji kujua namna ya kutayarisha vyakula na kupanga atakavyotumia fedha zake.
13 Kuna faida nyingine ya kujifunza shuleni, hata kujifunza masomo yale usiyopenda. Kujifunza kunazoeza akili zako na kufanya uwezo wako wa kutumia akili uwe bora. Ni kama mishipa mwilini mwako—kadiri unavyozidi kuitumia ndivyo itakavyokufaa. Mwishowe utaona akili zinazoezwa zaidi na kuleta matokeo zaidi. Lakini usipotumia akili sana, zitakuwa dhaifu kama mishipa isiyotumiwa sana. Nani angetaka akili zake ziwe hivyo?
14 Je! kuna jambo jingine lo lote lenye faida sana linalotokana na kujitahidi na masomo yako shuleni? Ndiyo, unaweza kujifunza kujiadibisha. Pengine huku hakutakupendeza sasa. Lakini, kama unavyojua, huwezi kufanya sikuzote mambo unayopendelea kufanya tu maishani. Itakuwa hata hivyo zaidi utakapofika wakati wako wa kutwaa madaraka makubwa zaidi ya kujipatia mwenyewe riziki, au kutunza jamaa yako mwenyewe. Ikiwa unazoea kujiadibisha sasa kama mtu anayejizoeza michezo, kutakusaidia ujipatie adabu inayohitajiwa upate kutimiza madaraka ya mtu mzima. Kutakusaidia vilevile usitawishe uwezo wa kukaza fikira pamoja. Hilo ndilo jambo ambalo watu wengi sana wanaona sasa kwamba ingaliwafaa wajifunze kulisitawisha walipokuwa vijana.
ULINZI
15-18. (a) Kufanya bidii ili ujifunze kutakuwa ulinzi kwako katika njia gani? (Mithali 13:20) (b) Kwa nini imempasa kijana aliye Mkristo atake sana kuweka mfano mzuri shuleni? (Tito 2:6, 7, 10) (c) Wakristo wana tumaini gani la uzima ambalo limepaswa likutie moyo sana ujifunze na kujipatia ufundi unaofaa shuleni? (1 Yohana 2:15-17; 2 Petro 3:13)
15 Kwa habari ya kujitahidi sana katika masomo yako, bado kuna faida nyingine inayostahili kutajwa kwa pekee. Bidii ya kujifunza yaweza kukulinda. Katika njia gani?
16 Bila shaka umeona ushuhuda mwingi wa mwenendo mbaya katikati ya wanashule wenzako. Kuna uasherati mwingi na matumizi ya dawa za kulevya, na matokeo yake ni yenye kuhuzunisha sana. Tena, kuna roho ya uasi katikati ya vijana wengi.
17 Pengine utasumbuliwa ukishirikiana na watu wasioheshimu kanuni za Neno la Mungu zinazoongoza mwenendo mwema. Ijapokuwa huwezi kuepuka kukutana na watu hao, unaweza kuepuka kushirikiana nao ikiwa si wakati wa masomo ya shule. Na ukifanya sana bidii na masomo yako ya shule, hutakuwa na nafasi nyingi sana ya kushirikiana na watu wasio na adabu baada ya shule. Mwishowe watu hao watakuacha wakiona unataka sana kuendelea na masomo yako. Huu utakuwa ulinzi kwako.
18 Tena, kwa kufanya bidii na masomo yako ya shule, utaweka mfano mzuri kama unajulikana kuwa Mkristo wa kweli. Hiyo italeta sifa kwako, wazazi wako na kwa Mungu unayeabudu. Kama Mkristo kijana, utatiwa moyo na nguvu nyingi na jambo hili: Uwezo mwingi na ufundi ambao unasitawisha sasa utakuwa wenye manufaa hata baada ya taratibu hii ya sasa ya mambo. Kwa nini? Kwa sababu Biblia inahakikisha kwamba taratibu yote hii mbovu ya mambo inakaribia kwisha. Karibuni taratibu mpya ya Mungu yenye haki, ambamo watu wenye mioyo minyofu wataweza kufurahia uzima wa milele, itakaa mahali pa taratibu ya kale. Ahadi hii ya Mungu itatimizwa katika taratibu hiyo mpya: “Wachaguliwa wangu watafurahia kazi ya mikono yao muda wa siku nyingi.” (Isaya 65:22, ZSB) Kwa hiyo mazoea mazuri ya masomo na ya kufanya kazi unayojifunza sasa kama kijana yanaweza kuwa chanzo cha uradhi na furaha milele.
[Picha katika ukurasa wa 80]
Mafundisho yanayofaa yaweza kukuweka tayari kwa maisha ya baadaye