Sura ya 17
Nyimbo na Ngoma Unazochagua Kucheza
1-3. (a) Ni katika njia gain yaweza kusemwa kwamba Muumba alitia nyimbo katika mazingira (hali) yetu ya asili? (b) Toa mifano ya kuonyesha kwamba Biblia inakubalia kucheza ngoma.
MUUMBA alitia nyimbo katika mazingira (hali) ya wanadamu. Si ndege peke yao wanaosikiwa wakiimba kwa sauti za nyimbo tamu, bali hata kububujika kwa vijito vya maji, uvumi wa upepo katika miti, mlio wa nyenje, mkoromo wa vyura na sauti za viumbe vingine vya duniani. Basi, si ajabu kwamba kuundwa kwa vyombo vya nyimbo (muziki) kulianza tangu mwanzo wa historia ya wanadamu.
2 Vilevile kucheza ngoma (dansi) kulianza zamani sana. Katika Israeli, Miriamu dada ya Musa aliongoza wanawake “wenye matari na kucheza.”” Vilevile, Mungu alipokwisha kumsaidia Mfalme Daudi ashinde adui wabaya, “wanawake wakatoka katika miji yote ya Israeli, kwa kuimba na kucheza.” Vilevile ni wazi kwamba Yesu Kristo alikubali kucheza ngoma, maana alitaja kucheza ngoma kuwa sehemu ya sherehe inayofaa katika mfano wake juu ya mwana mpotevu. Yesu alitaja kwamba “sauti ya nyimbo na machezo” yalitayarishwa wakati mwana mpotevu aliporudi. Biblia inaonyesha kwamba ngoma nyingine zilichezwa na watu mmoja mmoja au na vikundi vya wanaume, au vya wanawake.—Kutoka 15:20; 1 Samweli 18:6; Luka 15:25.
3 Je! maana yake ni kwamba nyimbo na ngoma zote ni nzuri? Au yakupasa kuchagua nyimbo unazosikiliza na ngoma unazotaka kucheza? Ni nini kinachoweza kutusaidia tuamue? Sana sana jambo hili ni la maana namna gani?
KUCHAGUA KUCHEZA NGOMA (DANSI)
4-6. (a) Ni mambo gani yangeweza kufanya ngoma fulani zikataliwe na Wakristo? (Wakolosal 3:5, 6) (b) Ni kwa sababu gani ngoma fulani za kisasa zimelinganishwa na ngoma za kale za uzazi?
4 Kuna ngoma (dansi) za namna nyingi—kuanzia na ngoma nzuri za Kizungu za watu wawili wawili wakizunguka pamoja mpaka ngoma za kuchangamka wanazoita polka. Kuna ngoma za Latin-Amerika za aina ya conga, rumba, na samba, vilevile merengue, beguine na bossa nova, na nyingi za hizo zinatoka Afrika. Tena kuna ngoma inayoitwa rock ’n’ roll, na nyingine za kisasa. Je! kuna sababu nzuri ya kukufanya ukatae ngoma fulani kati ya hizo?
5 Ikiwa ngoma inaamsha nyege zako na kuleta kishawishi cha kufanya uasherati, hiyo ni sababu nzuri ya kuikataa. Inaweza kukuletea matatizo (magumu) mengi.
6 Kwa mfano, ngoma za kale za uzazi zilikusudiwa kuchochea nyege, na ngoma fulani za kisasa zimeonyesha mambo hayo. Miaka iliyopita gazeti Time lilieleza hivi:
“Hapo mwanzoni Twist ilikuwa ngoma nzuri. . . . Lakini vijana katika [nyumba fulani ya starehe ya chama huko New York] wameifufua Ngoma ya Twist na kuifanya kichekesho cha kuiga sherehe ya kale ya kubalehe inayohusu kabila.”
7-10. (a) Kama mtu angeshiriki ngoma hizo, yaelekea wengine wangevutiwa naye kwa sababu gani? Ikiwa wewe ni mvulana, ungetaka uvute wasichana kwa sababu hiyo, au kama wewe ni msichana? (b) Kwa sababu gani ni lazima kuwa mwangalifu hata katika ngoma za kukaribiana sana mwili?
7 Miaka ya karibuni kumetokea ngoma za namna nyingi kutokana na ile ya Twist. Wachezaji hawagusani, ila nyonga na mabega yanaelekea kuzunguka katika njia zinazoonyesha wanataka ngono. Huenda kijana akaamshwa nyege vyepesi kwa kutazama namna mwili unavyozunguka katika njia hizo. Kwa mfano, huenda msichana asifikiri lo lote, ila kujikuta anafuata mwendo wa ngoma. Lakini haimpasi akose kujua matokeo juu ya watazamaji na wanavyoweza kumfikiria, kama vile barua hii aliyopelekewa mhariri (mwandikaji) wa Times Magazine la New York inavyoeleza: “Na tutumaini kwamba miili ya wachezaji Twist wetu vijana (na si wachanga sana) inadanganya, kwamba katika akili zao hawafikirii kutenda mambo ambayo mifupa yao ya nyonga na vifua vyao vinatenda nje.”
8 Hata ijapokuwa huna makusudi mabaya, kama unashiriki ngoma hizo lingekuwa jambo la hekima ufikirie namna unavyoweza kuvuta vijana wengine kwa mwili wako. Kwa mfano, je! wanavutwa kwako kwa sababu unawaamsha nyege, namna ile ile wanavyoweza kuamshwa na watu wanaovaa mavazi yenye kubana sana, na kuzungusha nyonga zao na kufanya ishara mbalimbali za kuonyesha wanataka mahaba? Je! wataka umvute mtu kwa sababu hiyo tu? Au wamtaka mtu anayekupenda kwa sababu ya jinsi ulivyo? kwa sababu ya mambo unayoona kuwa ya maana katika maisha? anayekupenda awe akikufaa katika mazungumzo yako? Je! unapendezwa na mtu anayefurahia kukutumikia, au unapendezwa tu na yule anayetaka kile anachoweza kupata kutoka kwako?
9 Hata zile ngoma zenye mitikiso mizuri ya mwili ambazo wachezaji wanashikana, zaweza mara nyingine kuamsha nyege kwa sababu ya kukaribiana sana mwili. Basi, ikiwa unashiriki ngoma hizo, fahamu kwamba yawezekana mwenzako kuamshwa nyege isivyofaa ijapokuwa labda wewe hudhani mnakaribiana sana hata kuweza kusitawisha nyege kutokana na ngoma hiyo.
10 Ni kweli kwamba ngoma nyingi ambazo umeona zikichezwa katika jamii yenu haziwezi kuchezwa katika njia ya adabu na inayofaa. Kwa kuwa mara nyingi akili ya ngoma hizo inakamatana (inahusiana) na uzazi, hali hii inazifanya zichezwe katika njia inayovunja shauri la Neno la Mungu linalosema tuwe na mwenendo safi ulio mzuri.
KUCHAGUA NYIMBO (MUZIKI)
11, 12. Ni kwa njia gani nyimbo zina nguvu? Taja mifano.
11 Vilevile unahitaji uangalifu na busara katika kuchagua nyimbo unazosikiliza kama vile unavyouhitaji katika kuchagua ngoma za kucheza. Kwa sababu gani? Kwa sababu nyimbo zina nguvu. Kama nguvu nyingine yo yote, nyimbo zinaweza kufanya mema au mabaya.
12 Nguvu ya nyimbo inatokana na nini? Inatokana na uwezo wake wa kutia maoni na tabia fulani au roho fulani ndani ya watu. Nyimbo zinaweza kustarehesha na kutuliza, au kuburudisha na kuchangamsha. Unaweza kuona tofauti kati ya wimbo wenye kupiga-piga kwa nguvu na wimbo mpole wa kumwimbia mchumba usiku. Nyimbo zinaweza kuamsha maono yote ya moyoni ya wanadamu—upendo, huruma, heshima, huzuni, hasira, chuki na tamaa. Katika historia yote wanadamu wamefahamu nguvu za nyimbo na kuzitumia ili waongoze watu katika njia fulani. Kwa mfano, sehemu ya ushindi wa Mapinduzi ya Ufaransa inasemekana kuwa ililetwa na ule ambao mwandikaji mmoja anauita “mwito wa vita wenye kuogofya sana” wa wimbo La Marseillaise. Na mara nyingi shule zina “nyimbo za kuamsha moyo wa kushindana” wanazotumia kabla ya mashindano ya michezo.
13-16. (a) Shauri katika Mithali 4:23 linahusiana (linakamatana) namna gani na kuchagua nyimbo? (b) Nyimbo zinaweza kuwa kiunganishi namna gani, na mara nyingine zinawezaje kuleta mabaya yasiyokwisha?
13 Biblia inaonyesha kwamba moyo ndio unaoongoza mawazo na matendo ya mtu, kwa hiyo Neno la Mungu linashauri hivi: “Linda moyo wako kuliko yote uyalindayo; maana ndiko zitokako chem-chemi za uzima.” (Mithali 4:23) Kwa kuwa nyimbo zina nguvu ya kutia mawazo moyoni, tunatakiwa tuchague nyimbo zinazofaa ili kulinda mioyo yetu.
14 Ni kweli kwamba nyimbo zinaongoza moyo kwa muda tu. Lakini mara nyingi muda huo unatosha kuongoza mtu aamue kufanya jambo fulani, au alegeze hali yake ya kujiweza apatwapo na jambo la kumvuta au kumshawishi. Ikiwa ulijifunza somo la kemia (chemistry) shuleni ulijifunza habari za vitu vinavyoitwa catalysts, vinavyogeuza vitu vingine vinapochanganywa pamoja. Ulijifunza kwamba njia ya pekee ya kuunganisha vitu viwili au zaidi ni kuvichanganya na kitu kingine tofauti. Kitu cha namna hiyo kinaitwa catalyst. Basi, sisi sote tuna makosa na maelekeo fulani mabaya, na kwa sababu hiyo tunajiona kushawishwa mara nyingine tufanye mambo fulani yaliyo mabaya. Tuseme hali zimetokea zinazokufanya utake kutenda jambo baya. Nyimbo zaweza kuwa kiunganishi kitakachounganisha tamaa na hali zilizotokea na kutokeza jambo ambalo baadaye unaweza kulisikitikia sana. Mwanamke mmoja aliye mchunguzi wa tume moja ya serikali alichunguza maandishi na picha za umalaya kisha akasema hivi:
15 “Kwa kuvuta mawazo ya ndani ya msichana ili kuamsha mahaba yake, mara nyingi nyimbo zinakuwa kama kiunganishi cha mapenzi na hivyo zinaamsha nyege katika msichana. . . Nyimbo zinatokeza maoni hayo.”
16 Ndiyo, ijapokuwa nyimbo zinachochea mtu kwa muda mfupi tu, zinaweza kukufanya ufuate maisha ambayo hayataweza kugeuka hata kidogo. Basi, je! wewe huoni yakufaa sana uwe mwenye busara juu ya nyimbo?
UGUMU WA KUAMUA
17, 18. Kwa kusikiliza wimbo, unaweza kujua namna gani kama unakufaa au ni mbaya?
17 Hakika, hakuna mtu anayeweza kukupa orodha ya kukuonyesha waziwazi nyimbo ambazo ni nzuri na ambazo ni mbaya. Sababu yake ni kwamba kati ya karibu namna zote za nyimbo, hakuna namna moja inayoweza kutajwa kuwa “nzuri sana” wala “mbaya sana.” Inakupasa utumie akili na moyo wako upate kujua ubora wa wimbo fulani, na kuongozwa na kanuni kama zile tulizokwisha kuzungumza. Nao uchaguzi wako unawaonyesha wengine jinsi wewe ulivyo.
18 Zamani za kale Ayubu aliuliza hivi: “Je! sikio silo lijaribulo maneno, kama vile kaakaa lionjavyo chakula?” (Ayubu 12:11) Vivyo hivyo sikio lako laweza kujaribu nyimbo. Bila hata kuyasikia maneno unaweza mara nyingi kujua tabia au roho ambayo wimbo unakusudia kutokeza, na mwenendo ambao unakazia ufuatwe. Ndivyo ulivyokuwa wimbo ambao Musa alisikia alipokuwa akitelemka Mlima Sinai na kuikaribia kambi ya Israeli. Kama alivyomwambia Yoshua: “Hiyo si sauti ya watu wapigao kelele kwa sababu ya kushinda vitani [wimbo wa ushindi] , wala si sauti ya watu wapigao kelele kwa sababu ya kushindwa [wimbo wa maombolezo] ; bali kelele za watu waimbao ndizo ninazozisikia mimi.” Kwa kweli kuimba kwao kulionyesha walikuwa wakiendesha kazi mbaya, yenye fujo za uasherati na ibada ya sanamu.—Kutoka 32:15-19, 25.
19-22. (a) Wale wanaopenda nyimbo bora wanahitaji wajihadhari na nini? (b) Kwa habari ya matokeo ya nyimbo za aina ya jazz na rock, ni mambo gani yanayostahili kufikiriwa kwa makini?
19 Ebu ifikirie mifano ya kisasa. Kwa desturi, nyimbo za kale na zenye mafundisho bora mara nyingine zinaonyesha heshima na adhama. Lakini ijapokuwa nyingi zina matokeo bora katika mawazo ya mtu, nyingine kati ya hizo zinapasa maisha mabaya au ya kichoyo na hata zinayatukuza. Yafaa kukumbuka kwamba watungaji wengi mashuhuri wa nyimbo bora walikuwa wenye maisha ya ufisadi. Na ijapokuwa kwa desturi walitunga nyimbo kwa ajili ya wasikilizaji waliodhaniwa kuwa walithamini “mambo mazuri zaidi ya maisha,” bila shaka waliingiza maoni yao yaliyopotoka na mawazo yao ya ndani yaliyopotoka katika baadhi ya nyimbo zao zenye maneno au zi-sizo na maneno. Basi tukitaka kulinda afya ya akili na mioyo yetu, tusizikubali bila kufikiri hata zile nyimbo zinazosemekana kuwa hazina mambo ya upuzi.
20 Zaidi ya nyimbo bora za kale tunaona nyimbo nyingine zenye sauti ya makelele, aina ya jazz na rock. Hata katika hizi unaona nyimbo nyingine zenye sauti tamu na za kiasi. Lakini nyingine kati ya hizo hazionyeshi adabu na zina makelele mengi. Ndiyo sababu waimbaji wenyewe wanatofautisha kati ya nyimbo za aina ya jazz na rock ambazo ni “pole” na zile ambazo ni “zenye hasira,” “kali” au “zenye uchungu.” Unaweza kujua mwendo ambao wimbo unakazia ufuatwe—masikio yako, akili na moyo wako zitakuambia. Maneno au namna ya sauti ya nyimbo nyingine zinakuwa wazi sana hata watu wanajua vyepesi kwamba zinapasa mwenendo wa namna fulani au watu fulani. Kwa mfano, Biblia inasema juu ya “nyimbo za walevi” na “wimbo wa kahaba.” (Zaburi 69:12; Isaya 23:15, 16) Namna gani leo?
21 Kwa mfano, ukisoma katika gazeti juu ya tafrija ya kuimba nyimbo au juu ya sikukuu, nayo taarifa inasema kwamba watu walipiga makelele, wasichana wakizirai (kuzimia) , dawa za kulevya zikatumiwa hata ikawa lazima polisi waletwe ili kuzuia mahali pa michezo pasiharibiwe—ungedhani ni nyimbo za namna gani zilizokuwa zikiimbwa ? Ukisikia mwimbaji kijana au mutribu akifa kwa sababu ya kutumia dawa za kulevya kupita kiasi—ungedhani yeye alikuwa fundi wa kuimba nyimbo wa namna gani?
22 Labda unajua kwamba vijana wengi wanavutiwa na nyimbo za rock kwa sababu wanaamini kwamba mashairi yazo yanasimulia hali na matatizo yanayotokea karibu yao. Nyimbo za rock zinajaribu kukazia ujumbe huo kuliko nyimbo za namna nyingine yo yote zinazopendwa na watu wengi: zinakazia matatizo ya kukua, ukosefu wa uhusiano (ushirika) kati ya wazazi na watoto, dawa za kulevya, ngono, haki za raia, maoni yenye kutofautiana, umaskini, vita na mambo yanayofanana na hayo. Zinajaribu kuonyesha namna vijana wengi wanavyochukia matendo ya kuonea watu na mawazo yao ya kutaka ulimwengu bora. Lakini matokeo yamekuwa nini? Nyimbo hizo zimefanyia vijana wengi nini? Fikira zake zimewaletea matatuzi gani ya kweli? Ikiwa nyimbo hizo zinakusudiwa kuonyesha matatizo (magumu) yanayotokea, ni kwa sababu gani nyingi kati ya hizo zinaelekeza kwenye matumizi ya dawa za kulevya, mashairi mengine yakifahamika na watumiaji wa dawa za kulevya peke yao? Hayo ni maulizo ya kufikiria.
23-25. (a) Ni nini maana ya shauri linalozungumzwa katika Mhubiri 7:5? (b) Tufikirie nani tunapochagua nyimbo na ngoma tunazotaka kucheza? Kwa sababu gani? (1 Wakorintho 10:31-33; Wafilipi 1:9, 10) (c) Kwa hiyo kwa sababu gani si jambo la mchezo kuchagua nyimbo na ngoma tunazotaka?
23 Kwa hiyo, uchaguzi wako wa nyimbo si jambo la mchezo. Ukitaka kujiacha ufanyiwe uamuzi na wengine kwa kufuata mambo kwa sababu tu yanafanywa na wingi wa watu, hiyo ni juu yako mwenyewe. Lakini unaweza kutumia akili yako mwenyewe na kutumia uangalifu katika kuchagua, ukiongozwa na hekima isiyokwisha ipitayo hekima zote, inayopatikana katika Neno la Mungu. Mhubiri 7:5 asema hivi: “Heri kusikia laumu ya wenye hekima, kuliko mtu kusikia wimbo wa wapumbavu.” ‘Upumbavu’ unaosemwa na Biblia si ule wa kupungukiwa akili tu bali ni upumbavu wa kukosa tabia njema, kufuata mwendo unaoweza kuleta matata wakati ujao.
24 Labda unadhani kwamba unaweza kusikiliza nyimbo zilizo na maneno yasiyopatana na mambo ya kweli na mema au zenye kuamsha nyege na zisizoonyesha adabu na bado usivutwe nazo. Labda unadhani vivyo hivyo juu ya ngoma unazocheza. Lakini wewe ni mfano gani kwa wengine? Je! unajiona kama mtume Paulo alivyojiona, aliyesema kwamba alikuwa tayari kuacha hata mambo yanayofaa kama kula nyama ikiwa kwa kufanya hivyo angeweza kuepuka kuwa kwazo kwa wengine? Nyimbo unazochagua zinaonyesha wewe u mmoja wa watu gani?
25 Basi kuchagua nyimbo unazotaka kusikiliza na ngoma unazotaka kucheza kunaonyesha kama unapendezwa na tafrija tu au na maisha mema ya milele, ukiwa katika upendeleo wa Mungu.
[Picha katika ukurasa wa 124]
Kucheza ngoma kulianza zamani za kale