Watchtower MAKTABA KWENYE MTANDAO
Watchtower
MAKTABA KWENYE MTANDAO
Kiswahili
  • BIBLIA
  • MACHAPISHO
  • MIKUTANO
  • w84 3/15 kur. 8-13
  • Jihadhari na Muziki Unaovunja Heshima!

Hakuna video yoyote kwa sasa.

Samahani, haikuwezekana kupakia video.

  • Jihadhari na Muziki Unaovunja Heshima!
  • Mnara wa Mlinzi Unaotangaza Ufalme wa Yehova—1984
  • Vichwa vidogo
  • Habari Zinazolingana
  • Kwa Sababu Gani Kuna Uhitaji wa Kujihadhari?
  • Usiwe na Ushiriki Wo Wote Pamoja na Mashetani!
  • Epuka Roho ya Ulimwengu
  • Tofautisha Kati ya Mema na Mabaya
  • Ninaweza Kuwekaje Muziki Mahali Pao Panapofaa?
    Amkeni!—1993
  • Ninaweza Kuwa na Usawaziko Jinsi Gani Kuhusu Muziki?
    Maswali Ambayo Vijana Huuliza—Majibu Yafanyayo Kazi, Buku la 2
  • Je, ni Muhimu Kuchunguza Aina ya Muziki Ninaosikiliza?
    Vijana Huuliza
  • Kupata Shangwe Yamuziki—Ni Nini Ufunguo?
    Mnara wa Mlinzi Unaotangaza Ufalme wa Yehova—1989
Pata Habari Zaidi
Mnara wa Mlinzi Unaotangaza Ufalme wa Yehova—1984
w84 3/15 kur. 8-13

Jihadhari na Muziki Unaovunja Heshima!

“Ee [Yehova], unifundishe njia yako, na kuniongoza katika njia iliyonyoka.”—ZABURI 27:11

1. Ni kwa njia gani kipawa kilichotolewa na Yehova cha muziki hakina kifani?

KWA neema Yehova Mungu aliwapa wanadamu kipawa cha muziki. Huo ulikuwa wonyesho usio na kifani wa fadhili zisizostahilika zake, kwa maana ingawa muziki hauhitajiwi ili kuendeleza uhai, unawezesha wanadamu kutoa maoni yao ya moyoni—huzuni zao na furaha zao. (Mwanzo 4:21) Muziki unaweza kuleta faraja kunapokuwa na masikitiko au ulete furaha kubwa zaidi nyakati za shangwe. Basi, ilifaa Yakobo akaandikia Wakristo wenzake hivi: “Mtu wa kwenu . . . ana moyo wa kuchangamka? na aimbe zaburi.”—Yakobo 5:13.

2. Muziki na nyimbo zina uhusiano gani na ibada ya Yehova?

2 Kuimba na kupiga muziki ni mambo ambayo yameshirikishwa na ibada ya Yehova kwa muda mrefu. Watu wake wa kale walimsifu yeye kwa shangwe kwa kuimba nyimbo nyakati za kukombolewa. (Kutoka 15:1-21; Waamuzi 5:1-31) Mungu alielekeza tengenezo la kimuziki lianzishwe kwa ajili ya utumishi hekaluni. (Zaburi 68:24-26) Yesu Kristo na mitume wake waliimba nyimbo za sifa baada ya Chakula cha Jioni cha Bwana. (Marko 14:26) Mtume Paulo alihimiza Wakristo wenzake waonyeshe misisimuko yao ya moyoni katika ‘nyimbo za kiroho, wakijifuatanisha wenyewe na muziki katika mioyo yao kwa Yehova.’(Waefeso 5:19, NW) Na mpaka leo hii, kuimba ni sehemu ya ukawaida ya ibada kati ya Mashahidi wa Yehova.

3. Kuna ushuhuda gani wa kuonyesha kwamba muziki una uwezo?

3 Bila shaka muziki una uwezo. Unaweza kugusa mioyo na kuchochea maoni ya moyoni. Kwa hiyo, nyimbo za kitaifa na muziki wa mwendo wa kiaskari zinatumiwa kuchochea watu wapatwe na shauku nyingi ya kutetea nchi yao. Shule za kilimwengu zina nyimbo zinazochochea wanamichezo watimuke. Watangazaji wa biashara wanatumia sauti zenye kuvutia ili wauze bidhaa zao. Ushuhuda huo unaoonyesha kwamba muziki una uwezo unapasa kufanya Wakristo wajihadhari.

Kwa Sababu Gani Kuna Uhitaji wa Kujihadhari?

4. Kwa habari ya muziki, ni lazima waabudu wa Yehova wajihadhari na nini hasa?

4 Hata Shetani Ibilisi anajua kwamba muziki una uwezo mkubwa, na nyakati nyingine anautumia kugeuza moyo na kuongoza watu waiache ibada safi ya Yehova. Basi, katika jambo hilo Wakristo washikamanifu wanahitaji ‘kulinda moyo wao, maana ndiko zitokako chemchemi za uzima.’ (Mithali 4:23) Hasa ni lazima tuangalie muziki tunaosikiliza usije ukatupotosha tuiache “njia iliyonyoka” na kutuingiza katika mwenendo unaovunja heshima na kumharibia Mungu sifa yake.—Zaburi 27:11.

5. Katika kuchagua muziki, kwa sababu gani inatupasa tuwe wachaguzi sana?

5 Yehova amekuwa mkarimu sana kwa kuwapa wanadamu kipawa cha muziki. Lakini kipawa hicho kimetumiwa vibaya mara nyingi sana! Basi, katika kuchagua muziki, tunahitaji kuwa wachaguzi sana na kuwa wenye ufahamu unaofaa. Hata bila kusikia maneno yenyewe, mara nyingi tunaweza kujua ni roho ya namna gani ambayo nyimbo fulani zimekusudiwa kutokeza. Akiwa mbali, Musa aliweza kufahamu kwamba muziki uliosikika ukitoka kwenye kambi ya Waisraeli ‘haukuwa wimbo wenye kuimbwa kwa sababu ya kutenda tendo hodari wala haukuwa wimbo wa kushindwa vitani.’ Alipokuja mwishowe kwenye kambi na kuona namna watu walivyokuwa wakitenda, alijua kwamba muziki wenyewe ulikuwa umekuwa wa namna iliyowaongoza watu kwenye mwenendo wa kuabudu sanamu bila ya kujizuia. (Kutoka 32:15-19, 25, NW) Kwa hiyo sisi leo tunahitaji kuchunguza namna ya roho ambayo muziki tunaosikiliza unatokeza. Je! roho hiyo inatujenga, au muziki wenyewe ni ule unaovunja heshima?

6. Ibilisi amekuwa akitumiaje muziki fulani-fulani, na kwa hiyo ni maneno gani ya Paulo yanayostahili kuangaliwa sana?

6 Mtume Paulo alitambua kwamba Shetani anataka kuvunja heshima ya watu wa Yehova au kuwachafua. Kwa hiyo, Paulo alihimiza waamini wenzake wajitenge na watu wasio waadilifu, kisha akauliza: “Pana urafiki gani kati ya haki na uasi? Tena pana shirika gani kati ya nuru na giza? Tena pana ulinganifu gani kati ya Kristo na Beliari? ” (2 Wakorintho 6:14-17) Leo, Ibilisi amekuwa akitumia kwa ujanja namna mbalimabli za mambo yasiyo ya uadilifu katika muziki, kwa njia hiyo akijitahidi kushawishi watu waingie katika mwendo wa kuvunja heshima na hivyo awageuze wamwache Mungu. Mashahidi walio wakf wa Yehova wanahitaji kuwa macho wazione hatari hizo.

Usiwe na Ushiriki Wo Wote Pamoja na Mashetani!

7. Mkristo anaweza kujuaje kama muziki fulani una mavutano ya kishetani?

7 Katika ulimwengu wa muziki kuna hatari nyingi za kiroho. Kwa mfano, wanamuziki wengi wanaojulikana sana wanahusika katika mafumbo ya kishetani. Wengine wanakubali waziwazi kwamba wanamwabudu Shetani, na mavutano ya kishetani yanaonekana mara nyingi katika muziki na nyimbo zao. Lakini Mkristo anaweza kujuaje kama muziki fulani una mavutano ya kishetani? Katika visa fulani inatosha tu kuangalia jalada la pakiti yenye sahani ya santuri. Huenda ukaona juu ya jalada hilo picha za watu ambao wamevaa mavazi yanayofanya waonekane kama wachawi wa kike, mashetani au maibilisi. Au huenda jalada likawa na picha zenye kuelekea kidogo upande wa mafumbo ya kishetani. Huenda jina la kikundi cha wana-muziki au la jalada lenye sahani yenyewe likaonyesha uhusiano fulani na mashetani, na ndivyo na vichwa na maneno ya nyimbo zenyewe. Kwa mfano, wewe ungekata shauri gani kutokana na vichwa vya nyimbo zinazosema “Kumhurumia Ibilisi” na “Watoto wa Kaburi”? Gazeti New York Post liliripoti kwamba mmoja wa nyimbo za namna hiyo ulikuwa “njia ya kukubali bila kuona haya hata kidogo” kwamba wanamuziki wenyewe walikuwa “wakishirikiana na Shetani kwa umoja kama pete na kidole.”

8. Kwa kutumia njia ya kuficha maana ya maneno wakati muziki unapochezwa kinyume-nyume, ni ujumbe wa namna gani ambao umetiwa katika redoki au kanda fulani za muziki?

8 Pia kumetokezwa redoki (sahani au kanda) zenye ujumbe mbalimbali usiopatana na Maandiko na hata ujumbe wa kishetani kwa kutumia ufundi wa kuficha maana ya maneno zinapopigwa kinyume-nyume, na ufundi huo unatumiwa na vikundi kadha vya wanamuziki. Wakati redoki ya wimbo mmoja unaopendwa na watu wengi sana inapopigwa kinyume-nyume, inarudia-rudia kusema, “Amua kuvuta bangi.” Na wakati wimbo mwingine uliotiwa katika redoki unapopigwa kinyume-nyume, unakuwa na ujumbe huu: “Nitaimba kwa sababu mimi naishi pamoja na Shetani. . . . Ni jambo la wazi kabisa, Shetani wangu mpendwa sana.”

9. Ni mawazo ya namna gani yanayoweza kuingizwa akilini mwa mtu wakati anaposikiliza namna fulani za muziki, na jambo hilo linaweza kuwa hatari kwa njia gani?

9 Bila shaka, kwa kawaida watu hawapigi redoki zao kinyume-nyume. Hata hivyo, wakati mtu anaposikiliza redoki (sahani) fulani za muziki, mawazo yasiyopatana na Maandiko au ya kishetani yanaweza kuingia sana katika akili hiyo iliyofunguliwa wazi iingiwe na maoni yasiyofaa. Gazeti High Fidelity Magazine lilimtaja mkuu mmoja wa eneo fulani la shirika la redoki akisema hivi: “Watu wanatakwa waitikie muziki wa kisasa wa roki sawasawa na vile wanavyoitikia muziki mtulivu wa kisasa ulio wa kujifurahisha tu. . . . Wewe una wajibu wa kujitolea ili muziki huo ukuongoze na kuelekeza mawazo ya akili zako.” Lakini je! hilo ni jambo la akili? Usipotunza akili zako kwa njia ya kiroho, unaweza kuiacha wazi iingiwe na mashetani!—Linganisha Mathayo 12:43-45.

10. Wakristo waaminifu wanapaswa kuwa na maoni gani juu ya kitu cho chote kilicho cha kishetani?

10 Mtume Paulo aliwaandikia hivi waamini wenzake wapendwa: “Vitu vile [mataifa] wavitoavyo sadaka wavitoa kwa mashetani, wala si kwa Mungu; nami sipendi ninyi kushirikiana na mashetani. Hamwezi kunywea kikombe cha [Yehova] na kikombe cha mashetani. Hamwezi kushirikiana katika meza ya [Yehova] na katika meza ya mashetani.” (1 Wakorintho 10:20,21) Uasherati na kuhusika na mashetani na katika mafumbo yao ni mambo yasiyoruhusiwa katika maisha ya Mkristo mwaminifu.—Kumbukumbu la Torati 18:10-12; Wagalatia 5:19-21.

11. Mkristo afanye nini akigundua kwamba ana rekodi au kanda za muziki wa kishetani?

11 Basi, kulingana na mashauri yaliyoongozwa na Mungu, inampasa Mkristo afanye nini akigundua kwamba ana redoki au kanda zinazoonyesha kuwa zina mavutano ya kishetani? Kwa uhakika, anapaswa kuziharibu, kwa maana ni lazima watu wa Yehova waepuke kuwa ‘wenye kushirikiana na mashetani.’ Walipokuwa chini ya hali zinazofanana na hiyo, Wakristo wa kwanza wa huko Efeso walichukua hatua bila kukawia, kwa maana tunasoma hivi: “Na watu wengi katika wale waliotumia mambo ya uganga wakakusanya vitabu vyao, wakavichoma moto mbele ya watu wote; wakafanya hesabu ya thamani yake, wakaona ya kwamba yapata fedha hamsini elfu.” (Matendo 19:19) Hao ‘wenye kumpenda Yehova’ walichukia lililo ovu wala hawakuzuiwa kuchukua hatua na mawazo ya kwamba watapata hasara ya vitu vya kimwili. Bali, wao waliharibu vitu vyao vyenye hali ya ushetani kisha wakapata faida kubwa ya kiroho.—Zaburi 97:10, NW.

Epuka Roho ya Ulimwengu

12, 13. (a) Ni roho gani ya kilimwengu inayoshirikishwa mara nyingi na muziki na wanamuziki wa kisasa, na roho hiyo imeonyeshwaje? (b) Mashahidi wa Yehova wanapaswa kutumiaje Wagalatia 6:7?

12 Wala hatupaswi kusahau ile roho ya kilimwengu ya ghasia nyingi na makelele mengi ambayo mara nyingi inashirikishwa na muziki na wanamuziki wa leo. (Linganisha Waefeso 2:1-7.) Kwa mfano, wakati uimbaji fulani wa muziki ulipofutwa usifanywe ulivyopangwa, maelfu ya mashabiki walifanya ghasia, hata gazeti Toronto Star likaeleza hivi: “Waliwarushia-rushia polisi 268 chupa nyingi, minyororo na silaha nyingine za kutupa wakati wa fujo za dakika 30 . . . Waling’oa viti 200 vilivyochomelewa kwenye viguzo vya chuma cha pua, vikiwa vimeunganishwa na saruji kwa skrubu. Walinyanyua viti vingi vya chuma na kuvirusha jukwaani. . . . Wakang’oa vilango vya chuma cha pua katika sehemu za kuingilia, wakabomoa madirisha katika vibanda vya tikiti na mkahawa wa Kibanda Kikuu, na kuharibu motokaa kadha nje ya uwanja huo.” Je! Mkristo awe wakati wo wote katika ushirika wa watu wa namna hiyo?

13 Kwenye machezo ya namna hiyo, kwa kawaida watu wanakunywa kupindukia na kutumia dawa za kulevya. Tena, muziki na matendo ya wenye kuupiga unatia ndani ya watu roho ya kujirusha-rusha kwa fujo nyingi. Ni wazi kwamba namna ya muziki unaopigwa nyakati kama hizo, pamoja na mambo yanayotia ndani ushetani, dawa za kulevya na jeuri, unaweza tu kuwa wenye kuvunja heshima. Basi, je! Mkristo angeweza kusikiliza muziki uo huo ndani ya nyumba yake mwenyewe asipatwe na madhara? Ni vigumu! Tena hakuna shahidi wa Yehova aliye mwaminifu atakayeipuza kanuni hii ya Biblia: “Mungu hadhihakiwi; kwa kuwa cho chote apandacho mtu, ndicho atakachovuna.”—Wagalatia 6:7.

14. Kwa sababu gani haifai kusikiliza na kuchezea dansi wimbo unaotoa wazo la kufuata mwenendo wa uasherati?

14 Hata hivyo, wengine wamekuwa na maoni haya: ‘Mimi sisikilizi muziki kwa kupendezwa na maneno yenyewe; ninachopenda ni mdundo wenyewe. Una mwendo mzuri wa kuchezea dansi.’ Lakini hata hapo hatari inaweza kuwapo. Kulingana na gazeti The Times-Herald la Newport News, Virginia, “mcheza-dansi mwenye pupa ya muziki wa disko huenda akacheza usiku kucha dansi ya muziki wa disko ulio mashuhuri bila kusikia jambo lo lote jingine katika muziki huo isipokuwa kile kifungu cha maneno yanayompendeza kinachorudiwa-rudiwa mara nyingi.” Ni kweli kwamba muziki wenyewe huenda ukawa na mdundo wa kupendeza sana katika kucheza dansi, lakini maneno yenyewe yanatutia moyo tufanye nini? Ni nini kinachoingia katika akili ya msikilizaji? Kwa mfano, shahidi mshikamanifu wa Yehova anawezaje kucheza dansi kwa kufuata wimbo unaomhimiza tena na tena aende akafanye uasherati?—1 Wakorintho 6:9, 10.

15. Ni maelekeo gani yenye kuvunja heshima yaliyo katika muziki wa kisasa?

15 Bila shaka, maneno ya muziki yanayovunja heshima kwa kutaja uasherati hayahusu muziki wa roki na disko tu. Katika nchi au sehemu nyingi kuna namna fulani-fulani za muziki ambazo huenda zikapendwa na watu wengi wa huko zijapokuwa zina mdundo au zinatumia maneno yenye kutiliwa mashaka sana na Wakristo wa kweli. Kwa habari ya muziki unaohusu vituko vya mashambani, makala moja katika gazeti The News & Observer la Raleigh, Carolina ya Kaskazini, inasema hivi: “Wale waimbaji wajiitao malaika na wadanganyaji wamekuwa sikuzote wakiimba nyimbo za vituko vya mashambani, lakini siku hizi muziki wao unataja ngono za haramu waziwazi sana kwa namna isiyopata kuonekana katika historia ya muziki.” Likisema juu ya elekeo jingine lililo katika muziki wa uasherati unaopendwa na watu wengi, gazeti The Spokesman-Review linasema: “Wanawake wanaimba juu ya ngono za usiku na ngono zinazofanywa kwenye ukumbi wa dansi na ngono kwenye pembe za barabara.” Je! nyimbo hizo zinatimiza jambo gani jingine isipokuwa kuvunja heshima tu?

16. Kuna msaada gani kwa mtu ambaye moyo wake unamsukuma asikilize na achezee dansi muziki unaovunja heshima wenye kutaja ngono?

16 Usisahau kwamba moyo usio mkamilifu wa kibindamu ni mdanganyifu na unatamani kujiingiza hata katika mambo yaliyo hatari. (Yeremia 17:9) Je! moyo wako wewe unakushawishi usikilize au uchezee dansi unachojua ni kibaya machoni pa Yehova? Ikiwa ndivyo, jihadhari! Tafuta msaada wa Mungu kwa sala ili uweze kuendelea ‘kuhakiki ni nini impendezayo Bwana wala usishirikiane na matendo ya giza.’ (Waefeso 5:10-12; Zaburi 5:1, 2) Ukikataa kwa uthabiti usisikilize wala kuchezea dansi muziki unaovunja heshima kwa kutaja ngono, huenda hatua yako ikasaidia kukaripia wengine ambao huenda moyo wao ukawa unawapoteza.

17. Kwa habari ya muziki, wewe unafikiri tunaweza kutumiaje mashauri yaliyo kwenye (a) Waefeso 5:3? (b) Tito 2:11-14?

17 Huenda wale ambao wamejiingiza sana katika roho ya mfumo huu mbovu wa mambo wakafurahia muziki wenye kuvunja heshima kwa kutaja ngono. Lakini Wakristo waaminifu wangewezaje kufanya hivyo? Wao wanashauriwa hivi: “Uasherati usitajwe kwenu kamwe, wala uchafu wo wote wala kutamani, kama iwastahilivyo watakatifu.” (Waefeso 5:3) Je! sisi ‘tumekataa kabisa hali ya kutomcha Mungu na tamaa za kilimwengu’? Basi na tujihadhari si na mambo tunayosema tu, bali pia na yale tunayoyasikiliza, ili nyimbo zinazohusu uasherati zisiwe kati ya hayo. Acheni ‘tuishi kwa utimamu wa akili na kwa uadilifu na utawa katikati ya huu mfumo wa sasa wa mambo.’—Tito 2:11-14, NW.

18. Kwa habari ya nia yetu kuelekea wanamuziki fulani, ni maulizo gani yanayoweza kuulizwa?

18 Lakini wewe binafsi una maoni gani juu ya wanamuziki wa kilimwengu? Jiulize hivi: Je! mimi ninafuata mfano wao katika kuvaa mavazi, kujipamba na katika usemi? Ni kiasi gani cha maongezi yangu kinachohusu habari zao na muziki wao? Je! mimi ninawaabudu kwa kuvaa T-shati au koti zinazowatangaza waimbaji hao, au hata kwa kuangika picha zao au kubandika karatasi zenye sura zao katika ukuta wa chumba changu? Je! jambo hilo linampendeza Yehova, yeye ambaye ibada yangu inapasa kumwendea? Je! mimi ninafuata shauri lile la Biblia linalosema wazi “ikimbieni ibada ya sanamu”?—1 Wakorintho 10:14; Warumi 1:24, 25.

Tofautisha Kati ya Mema na Mabaya

19. Kwa habari ya muziki, uwezo wa kufikiri uliozoezwa inavyofaa unapasa kutumiwaje?

19 Mtume Paulo aliandika hivi: “Chakula kigumu ni cha watu wazima, ambao akili zao, kwa kutumiwa, zimezoezwa kupambanua mema na mabaya.” (Waebrania 5:14) Wazazi na hata vijana Wakristo wanahitaji kutumia uwezo wao wa kufikiri uliozoezwa inavyofaa kutofautisha kati ya mema na mabaya. Wanahitaji kutambua na kukataa kabisa kabisa vishawishi vyenye udanganyifu vya muziki wenye kuvunja heshima. Wakati ile kawaida ya kusema “lo lote linafaa” inapozidi kutia mizizi imara katika ulimwengu huu unaotawalwa na Ibilisi na katika muziki wake, ni lazima Mashahidi wa Yehova, vijana kwa wazee, wazidi kukata shauri kamili wapatanishe maisha yao na viwango vya hali ya juu ya Baba yao wa kimbingu.—Zaburi 119:9-16; 1 Yohana 5:19.

20. Inapendekezwa kijana anayenaswa katika roho ya nyimbo zinazotilika mashaka afanye nini?

20 Usisahau kamwe kwamba muziki una uwezo. Unaweza kugeuza moyo. Je! wewe unajiona ukivutwa katika roho ya nyimbo za kilimwengu zenye kutilika mashaka? Basi chukua hatua ya haraka ulinde moyo wako. Ikiwa wewe ni kijana, zungumza hali yako pamoja na wazazi wako Wakristo. Pia, mpelekee Yehova sala kwa bidii nyingi kumwomba akusaidie kupitia roho takatifu yake.—Mithali 4:23; Luka 11:13; Wagalatia 5:22-24.

21. Wazazi Wakristo wanaweza kusaidiaje watoto wao waepuke muziki unaovunja heshima?

21 Ninyi wazazi, mnafanya nini kusaidia watoto wenu watofautishe kati ya muziki unaokubalika na ule wa namna ya kuvunja heshima? Kwa kuwa ninyi ni Wakristo, je! mnaweza kuwaruhusu wasikilize nyimbo zinazohusu ushetani, uasherati, matumizi mabaya ya dawa za kulevya na bado hilo liwe ni jambo linalofaa? Haya, basi, kabla hamjanunua redoki (sahani ya muziki) au kabla hamjaruhusu watoto wenu wasikilize muziki fulani, tumieni wakati mchunguze jalada la pakiti ya sahani yenyewe mwone kama inaonyesha alama za mavutano machafu. Angalieni vichwa na maneno ya nyimbo zenyewe. Ikiwa nyimbo hizo zinavunja heshima, zungumzeni jambo hilo na vijana wenu kwa fadhili. Mnaweza kuwaonyesha kwamba Wakristo wote wanapaswa kuwa ‘watoto wachanga katika uovu, bali katika akili zao wawe watu wazima,’ bila kutafuta maarifa ya kujua maovu wala kujaza akili zao maoni yenye kuvunja heshima. (1 Wakorintho 14:20) Baada ya mazungumzo ya namna hiyo, bila shaka wewe na watoto wenu mtaziharibu redoki zo zote mlizo nazo ambazo zinatilika mashaka zikilinganishwa na Maandiko, kisha nyote pamoja mkate shauri kwamba hamtasikiliza tena kamwe muziki unaovunja heshima.

22. (a) Kwa sababu gani sisi hatukosi jambo lo lote lenye mafaa kwa kukataa muziki unaovunja heshima? (b) Inatupasa tuwe na nia na maoni gani katika kuchagua muziki?

22 Kuna namna nyingi sana za muziki unaokubalika na wenye kujenga unapolinganishwa na Maandiko, kutia ndani nyimbo za Ufalme za kupendeza sana zinazofurahiwa na Mashahidi wa Yehova ulimwenguni pote. Kwa hiyo sisi hatukosi jambo lo lote lenye mafaa kwa kukataa muziki unaovunja heshima. Kwa kuwa na funzo la Biblia la ukawaida na kujifunza vichapo vya Kikristo vinavyohusiana na Biblia, acheni tuzoeze uwezo wetu wa kufikiri utofautishe kati ya mema na mabaya. Halafu acheni tuambatane na yaliyo mema. Ikiwa muziki wo wote unapingana na viwango vya Mungu vya uadilifu, ukatae. Kubali kufuata maagizo yake na uwe imara katika kubaki kwenye “kijia cha uadilifu.” (Zaburi 27:11, NW.) Kwa vyo vyote, jihadhari na muziki unaovunja heshima! Wakati ule ule, uchaguzi wako wa kibinafsi wa muziki na umletee Mungu sifa, yeye “atupaye vitu vyote kwa wingi ili tuvitumie kwa furaha.”—1 Timotheo 6:17.

Wewe Ungejibuje?

◻ Tuna ushuhuda gani wa kuonyesha kwamba muziki una uwezo?

◻ Unaweza kujuaje kama muziki fulani una mavutano ya kishetani?

◻ Ufanye nini ikiwa una rekodi au kanda za muziki unaoonyesha alama za mavutano ya kishetani?

◻ Ikiwa moyo wa mtu unamsukuma asikilize au achezee dansi muziki unaovunja heshima, kuna msaada gani?

◻ Wazazi Wakristo wanaweza kusaidiaje watoto wao waepuke muziki unaovunja heshima?

[Picha katika ukurasa wa 10]

Muziki unaovunja heshima hauwafai watu wa Yehova

[Picha katika ukurasa wa 12]

Je! Wakristo wa kweli wafuate mfano wa wanamuziki wa kilimwengu katika kuvaa mavazi, kujipamba na katika mtindo wa maisha?

    Maktaba Kwenye Mtandao (1980-2025)
    Toka
    Ingia
    • Kiswahili
    • Shiriki
    • Mapendezi
    • Copyright © 2025 Watch Tower Bible and Tract Society of Pennsylvania
    • Masharti ya Utumiaji
    • Sera ya Faragha
    • Mpangilio wa Faragha
    • JW.ORG
    • Ingia
    Shiriki