Kupata Shangwe Yamuziki—Ni Nini Ufunguo?
UKOSEFU mbaya sana wa adili na ibada ya sanamu ni mambo yaliyozoewa sana katika ulimwengu wa kale. Kwa sababu hiyo, mtume Paulo aliona kuwa ilihitajiwa kabisa kutoa shauri imara juu ya mwenendo wa Kikristo. Kwa kundi katika Efeso yeye aliandika hivi: “Basi, hili, nasema mimi na kushuhudia katika Bwana, kwamba nyinyi msiendelee kutembea tena kama vile mataifa hutembea pia katika utovu wa faida ya akili zao, huku wao wakiwa katika giza kiakili, na kutengwa na uhai ambao ni wa Mungu, kwa sababu ya ujinga ambao umo ndani yao, kwa sababu ya utovu wa hisi wa mioyo yao.”—Waefeso 4:17, 18, NW.
Je! hilo si elezo zuri pia la jinsi mambo yalivyo leo? Hii inatia na uwanja wa muziki. Mwingi wa muziki wa ki-siku-hizi huonyesha mtindo ambao ‘umetengwa na maisha ya kumcha Mungu.’ Mara nyingi maneno ya muziki huonyesha kwamba yametungwa na ‘moyo usio na hisia,’ usio na fadhili au huruma.
Lakini mtume Paulo alipeleka shauri lake hatua nyingine zaidi kwa kusema: “Hisi zao za mema na mabaya zikiisha kufishwa ganzi, wao wamejiachilia wenyewe kwenye ngono nao hufuatia kwa bidii ya moyo kazi ya maisha ya ukosefu wa ustahifu wa kila aina.”—Waefeso 4:19, The Jerusalem Bible.
Huku ‘kufuatia kwa bidii ya moyo kazi ya maisha ya ukosefu wa ustahifu’ kunaonyeshwa katika muziki mwingi wa leo. Yale maneno na kusudio la muziki hutosheleza tamaa ya kizazi ambacho kimejitia sana katika ngono, jeuri, dawa za kulevya, na anasa. Inawapasa Wakristo waoneje maovu hayo? Angalia maneno ya Paulo: “Sasa hiyo siyo njia ambayo mmejifunza kutoka kwa Kristo hata kidogo, isipokuwa kama nyinyi mlishindwa kumsikia ifaavyo wakati nyinyi mlipofundishwa ni nini ukweli ulio katika Yesu.”—Waefeso 4:20, 21, JB.
“Mgeuzo wa Kiroho” Wahitajiwa Kabisa
Sisi tunaweza kutumiaje shauri hili la upole kwa habari ya muziki unaoonyesha roho ya ulimwengu? Katika habari ya kwamba ikiwa sisi tuna “akili ya Kristo,” yaani, ikiwa sisi tuna mwelekeo wake wa kiakili, sisi hatutataka kusikiliza muziki ambao ni wa “kidunia, wa kinyama, wa kishetani.”—1 Wakorintho 2:16; Yakobo 3:15, NW.
Lakini huenda ukauliza, ‘Naweza kubadilije ladha yangu ya muziki?’ Paulo anasaidia tena, kwa kuwa yeye asema: “Lazima uache njia yako ya zamani ya maisha; lazima uweke kando unafsi wako wa zamani, ambao hufisidiwa kwa kufuata tamaa zenye kudanganya. Lazima akili yako ifanywe upya kwa mgeuzo wa kiroho.”—Waefeso 4:22, 23, JB.
Jibu ndilo hilo, kufanywa upya kwa akili kwa mgeuzo wa kiroho. Hili lahusisha ndani mengi zaidi ya ladha yetu ya muziki. Linataka kuelimishwa upya, kuinuliwa kwa viwango na kanuni. Lamaanisha badiliko katika njia yetu ya kufikiri, seti tofauti ya kima. Nalo lahusisha ndani kuona mambo kwa maoni ya Mungu na Kristo. Kama vile Paulo alivyolieleza wazi sana: “Mlapo au mnywapo, au mtendapo neno lo lote, fanyeni yote kwa utukufu wa Mungu.”—1 Wakorintho 10:31.
Muziki mwingi wa ki-siku-hizi haumletei Mungu utukufu. Tofauti kabisa na hilo, unadharau zile kanuni wanazotetea Wakristo na ambazo wengi wamekuwa na nia ya kufia ndani ya magereza na kambi za mateso. Kwa hiyo, kwa nini itupase kuifikiria kuwa dhabihu ikiwa tunalazimika kufanya badiliko katika ladha yetu ya kimuziki ili tusiwe ‘tukiupenda ulimwengu na vitu vilivyo katika ulimwengu’?—1 Yohana 2:15-17, NW.
Muziki Mzuri—Ni Nini Ufunguo?
Ikiwa, kwa sababu ya kuheshimu kwetu kanuni za Biblia, sisi tunakataa muziki wenye kushusha tabia, tutaubadilisha na nini? Basi, kwa nini usipeleleze njia mpya za muziki? Huenda zikawa zenye kufurahika zaidi na zenye kujenga zaidi ya zile tulizopendelea wakati uliopita. Kutoa kielelezo, aliyekuwa hapo kwanza mwanamuziki wa roki alisema hili juu ya mabadiliko aliyofanya:
“Ilikuwa lazima mimi nifanye jitihada ya kuondoka kwenye sauti rahisi ya roki kwenda kwenye muziki wa aina yenye kukubalika yenye kupendwa na watu wengi na muziki wa kistadi usio na makelele mengi. Lakini nilipong’amua kwamba ulikuwa na maana zaidi na kwamba mimi singeweza kushirikishwa tena na roho ya muziki wa ki-siku-hizi zaidi, ulikuwa rahisi na wenye kuridhisha zaidi. Ghafula ukawa wenye kujenga. Mimi niling’amua nilichokuwa nimekosa kwa sababu ya maoni yangu mabaya ya hapo kwanza yasiyo na sababu nzuri dhidi ya aina tofauti ya muziki.”
Kuna mweneo mpana wa muziki bora wa kikawaida, pamoja na muziki wa kitamaduni na baadhi ya muziki wa ki-siku-hizi, ulio na melodia nzuri, maneno safi, na usioonyesha falsafa zinazopinga kanuni za Biblia. Ufunguo ni kupata na kuwa na shangwe ya muziki ambao hautavuta vibaya kufikiri kwetu, muziki ambao ni ‘wenye uadilifu, safi, wenye kunenwa vizuri, mwema, na wenye kustahiki sifa.’—Wafilipi 4:8, NW.
Fungu la Muziki Katika Maisha ya Mkristo
Kwa wengine, njia moja ya kupata shangwe ya muziki ni kwa kuimba au kujifunza kupiga chombo cha muziki. Furaha kuu inaweza kutokana na muziki unaopigwa na mtu mmoja au kikundi cha wapiga muziki pamoja na jamaa na marafiki. Hata hivyo, kama vile ilivyo kwa mambo yote, usawaziko unahitajiwa. Tafrija au jambo la kupisha wakati halipasi kuruhusiwa liwe la kunasa maisha yote ya Mkristo. Hilo likitukia, hata muziki wenye kujenga, kwa sababu ya kuzidi, ungekuwa na athari isiyo ya kujenga kwa sababu ya kuzidi. Ndipo Mkristo angekuwa katika hatari ya kuwa ‘mpenda anasa kuliko kuwa mpenda Mungu.’—2 Timotheo 3:4, NW.
Pia muziki ni sehemu isiyotenganika ya ibada yetu kwa Yehova. Katika Israeli wa kale, Asafu na ndugu zake waliimba hivi: “Mpeni Yehova shukrani, enyi watu; iteni juu ya jina lake, julisheni vitendo vyake miongoni mwa vikundi vya watu! Mwimbieni, mfanyieni melodia, jishughulisheni wenyewe na matendo yake yote ya ajabu.” Ndiyo, muziki unaweza kusifu Mungu na kumpendeza.—1 Mambo ya Nyakati 16:8, 9, NW.
Zile nyimbo za Ufalme zinazotumiwa na Mashahidi wa Yehova kwenye Majumba ya Ufalme yao zinategemea maandiko ya Biblia, zaburi, sala, na mafundisho. Je! sisi hatuwezi kufurahia sana muziki huu uliowekwa wakfu? Na je! haitupasi sisi kuonyesha shangwe yetu kwa kuimba nyimbo hizi kwa hisia na idili? Hata katika pindi nyingine zisizo za mikutano ya Kikristo, je! hatuwezi kuchangamsha maisha yetu kwa mitungo hii mitamu ya nyimbo iitwayo Kingdom Melodies?
Katika mitungo hii ya kiokestra, wanamuziki wote ni Mashahidi wa Yehova. Baadhi yao ni wanamuziki stadi ambao hupiga muziki katika okestra ya upatanisho wa sauti. Wengine, kutia na yule aliyekuwa hapo kwanza mwanamuziki wa roki aliyenakiliwa hapo juu, ni vijana wenye majaliwa ambao huona shangwe ya namna nyingi za muziki safi. Wao hawahisi kwamba wanakosa chochote kwa kukataa kabisa muziki unaoonyesha mielekeo ya kidunia, ya kiibilisi. Kielelezo chao kizuri huonyesha kwamba sisi pia, tukiruhusu kanuni za Biblia ziongoze uchaguzi wetu, tunaweza kupata shangwe nyingi yenye kujenga katika muziki, wa kilimwengu na ule ulio mtakatifu pia.—Waefeso 5:18-20.
[Sanduku katika ukurasa wa 28]
“Muziki wa roki una uvutio mmoja tu, uvutio wa kishenzi, kuvutia tamaa ya ngono—si mapenzi, si eros, bali tamaa ya ngono isiyostaarabika na isiyoelimishwa. . . . Vijana wanajua kwamba roki ina mdundo wa kufanya ngono.”—The Closing of the American Mind, cha Allan Bloom.