Sura ya 13
Miaka Itakayofuata
1, 2. (a) Ni magumu gani yanayoweza kutokea watoto wakiisha kuondoka nyumbani? (b) Wengine wanajaribuje kushughulika na tatizo la uzee?
MAISHA yetu yasipojaa utendaji fulani wa mwili au wa akili, tunachoshwa nayo. Maisha yanaonekana kuwa bure, nasi tunakuwa na wasiwasi. Mara nyingine tatizo hilo linatokea kwa watu waliooana wakati watoto wao wanapokuwa watu wazima na kuondoka nyumbani. Wakati wa miaka yao mingi iliyopita, maisha yalijaa madaraka ya uzazi. Sasa utendaji wote na daraka la kuzaa watoto linakwisha ghafula (pasipo kutazamiwa).
2 Zaidi ya hayo, mageuzo ya mwili yanaanza kutokea kadiri miaka inavyopita. Makunyanzi yanatokea, nywele zinakuwa mvi, huenda nywele zikapunguka, na kutokea maumivu yasiyokuwapo zamani. Uhakika ni kwamba tunazidi kuzeeka. Bila kukubali mambo hayo ya hakika, watu wengine wanajitahidi sana waonyeshe kwamba wao ni vijana kama walivyokuwa zamani. Mara wanaanza kufanya rafiki wengi—wakifanya haraka kwenda kwenye karamu au wakishiriki sana michezo. Haraka-haraka hiyo ya utendaji inatoa jambo la kufanya, lakini je! inaleta furaha inayoendelea? Je! itamfanya mtu ajione anahitajiwa kweli kweli ili maisha yake yawe na maana ya kweli?
3. Ijapokuwa huenda tafrija ikafurahisha, jambo gani linapaswa liepukwe?
3 Bila shaka, tafrija inaweza kufurahisha. Na huenda katika maisha yako ya baadaye ukaona kwamba unao wakati wa kufanya mambo fulani usiyoweza kufanya wakati watoto wako walipokuwa wadogo. Lakini kuruhusu utafutaji wa anasa uwe jambo kubwa maishani kunaweza kuleta magumu mazito.—2 Timotheo 3:4, 5; Luka 8:4-8, 14.
UZURI WA KUWA MSHIRAMANIFU
4, 5. Jambo gani laweza kutokea mtu mwenye umri wa uzee anapojiona kwamba inampasa aonyeshe kwamba yeye angali ana nguvu za kuvutia wanaume au wanawake?
4 Wakati huu wa maisha, watu wengi wanadhani kwamba inawapasa waonyeshe kwamba wangali wanavutia wanaume au wanawake. Huenda wakaanza kuonyesha hivyo kwa kufanya mapenzi na mtu fulani katika kikusanyiko cha starehe. Sana sana wanaume wanafanya mapenzi na wanawake vijana, na katika wakati huu wa “adili mpya” wako vilevile wanawake wengi wanaotafuta kutuliza wasiwasi wao kwa kufanya mapenzi na watu wasio wenzi wao wa ndoa. Wajapokuwa labda wameoana miaka mingi, wengine huanza kusitawisha mawazo ya kuanza “maisha mapya” na mwenzi mpya wa ndoa. Huenda wakajaribu kutetea wanayofanya kwa kutaja makosa ya mwenzi wao wa ndoa—na huku wakifanya makosa yao yaonekane si mazito, pamoja na kukosa kwao ushikamanifu kwa mwenzi wao wa ndoa na vilevile kwa kanuni za haki.
5 Labda wanajua kwamba Yesu alisema: “Kila mtu atakayemwacha mkewe, isipokuwa ni kwa sababu ya uasherati [porneia: uasherati mbaya sana] , akaoa mwingine, azini.” Ijapokuwa hapa Yesu alikuwa akionyesha kwamba si haki mtu kutaliki (kumwacha) mwenzi wake wa ndoa “kwa kila sababu,” wao wanataka kutumia sababu yo yote ili wapate talaka inayoruhusiwa na sheria ya serikali. (Mathayo 19:3-9) Ndipo wanapoanza kuchukua mwenzi mpya, mara nyingi huyo ni mtu fulani ambaye walipendana naye kabla ya kuanza kuomba talaka. Wajapoyajua mambo ambayo Neno la Mungu linasema juu ya mwenendo huo, huenda wakatoa sababu kwamba kwa rehema yake kuu, Mungu ‘atafahamu.’
6. Yehova Mungu ana maoni gani juu ya kutoheshimu mapatano ya ndoa?
6 Ili tuepuke kushawishwa na fikira hizo za uasherati, inatufaa tuyaangalie mambo ambayo Yehova aliwaambia watu wake wa Israeli kupitia kwa nabii wake Malaki: “ndilo . . . jambo ambalo ninyi watu mnafanya, hili linatokeza kufunikwa kwa madhabahu ya Yehova kwa machozi, kwa kulia na kuugua, hata sasa hakuna kuligeukia toleo la zawadi [kwa kibali] wala kufurahia cho chote kutoka mkononi mwenu. Nanyi mmesema, “Kwa sababu gani?” Kwa sababu hii, kwamba Yehova mwenyewe ameshuhudia kati yako na mke wa ujana wako, ambaye wewe mwenyewe umetendea mambo ya udanganyifu . . . Nanyi watu inawapasa mjilinde wenyewe kwa habari ya roho zenu, na mtu asimtendee mke wa ujana wako mambo ya udanganyifu. Kwa maana yeye amechukia talaka,’ Yehova Mungu wa Israeli amesema.” (Malaki 2:13-16, NW) Ndiyo, kumtendea mwenzi wa ndoa mambo ya udanganyifu, kudharau mapatano ya ndoa—hayo ni mambo yanayolaumiwa na Mungu; yanaharibu uhusiano wa mtu na Mpaji-Uzima.
7. Sababu gani kutoheshimu mapatano ya ndoa hakuongozi kwenye furaha?
7 Je! hiyo ndiyo njia ya kufanya maisha yawe bora? Hata. Ndoa mpya yo yote inayoanzishwa na watu hao iko juu ya msingi usio na nguvu. Kwanza, wameonyesha kwamba hawawezi kutegemewa hata katika uhusiano huo wa maana sana. Ni kweli kwamba huenda wakaona jambo fulani lenye kuvutia katika utu wa mwenzi huyo mpya, jambo ambalo mwenzi wa zamani hakuwa nalo. Lakini ili wapate hilo, wanatafuta furaha yao wenyewe pasipo kujali kwamba kufanya hivyo kunaleta maumizo na masikitiko. Bila shaka hiyo siyo sifa inayoleta furaha ya ndoa.
8. Katika ndoa, kilicho bora kuliko uzuri wa mwili, ni nini?
8 Uzuri wa kuendelea kuwa mwaminifu kwa mwenzi wa ndoa unapita uzuri wo wote wa mwili. Uzuri wa mwili unatoweka kadiri miaka inavyopita, lakini uzuri wa ushikamanifu unaongezeka kadiri kila mwaka unavyopita. Kutafuta kumfurahisha mwenzako, na kutaka kutanguliza faida zake kuliko faida zako, kunaweza kuleta furaha isiyo na mwisho, maana kweli “kuna furaha nyingi katika kutoa kuliko zilivyo katika kupokea.” (Matendo 20:35, NW) Ikiwa watu wawili wameoana muda wa miaka fulani, na ikiwa wamepashana habari na kutumainiana, ikiwa wameshiriki pamoja kufanya kazi na miradi na matumaini, nyakati za taabu pamoja na mema—nao wamefanya hivyo kwa upendo—maisha yao yataungana kweli kweli, yatafungamana. Wana mambo mengi sana wanayoshiriki pamoja—kiakili, kimoyoni na kiroho. Ule upendo wa mahaba ambao labda uliwapumbaza akili kidogo wasione makosa ya mmoja na mwenzake kabla ya kufunga ndoa yataleta hali ya kujitoa kwa moyo wote kunakomfanya kila mmoja aone makosa ya mwenzake kuwa nafasi ya kutoa msaada, kutimiliza uhitaji fulani. Kati yao kuna hali ya kuona kutumainiana, hali ya kujiona salama, kujua kwamba watasaidiana bila kujali magumu yanayoweza kutokea. Linaonekana kwao kuwa jambo la asili kushikamana wao kwa wao. Kama Mika 6:8, NW linavyoeleza: “Amekuambia yaliyo mema, Ewe mwanadamu, wa udongo. Naye Yehova anataka nini kwako ila kutumia haki na kupenda upendo mshikamanifu, na kuwa mnyenyekevu katika kutembea pamoja na Mungu wako”?—Maneno ya pembeni.
WATOTO WAKUBWA—UHUSIANO MPYA
9-11. (a) Je! Mungu alikusudia uhusiano wa wazazi na watoto wao uendelee kuwa ule ule katika maisha yote? (b) jambo hilo linahusuje shauri ambalo huenda wazazi wakawapa watoto wao wakubwa? (c) Watoto wao wanapooa au kuolewa, ni ukichwa wa nani ambao wazazi wamepaswa waheshimu?
9 Ijapokuwa mume na mke wanapaswa waendelee kuwa pamoja maisha yao yote, hivyo sivyo Muumba alivyopangia wazazi na watoto wao. Ni kweli kwamba wakati watoto wenu walipokuwa wakikua waliwahitaji ninyi kila siku. Si kwamba kulikuwako mahitaji ya kimwili tu yaliyopaswa yatimizwe, bali uongozi ulitakiwa vilivile. Wakati walipokuwa hawako tayari kuitikia, labda mlisema kwa nguvu sana juu ya mambo fulani yaliyopaswa yafanywe kwa faida yao wenyewe. Lakini wanapokuwa na nyumba yao wenyewe, uhusiano kati yenu na wao unageuka kidogo. (Mwanzo 2:24) Hiyo haina maana kwamba maoni yenu kuelekea wao yanageuka, lakini daraka linageuka. Kwa hiyo namna mnavyawatumikia inahitaji kugeuka.
10 Huenda nyakati nyingine bado wakahitaji shauri. Nao ni ushuhuda unaoonyesha hekima ikiwa wanasikiliza shauri jema kutoka kwa wale walio na ujuzi zaidi katika maisha. (Mithali 12:15; 23:22) Lakini mnapowapa shauri wana au mabinti wanaojitegemea, ni jambo la hekima kulitoa katika njia inayoonyesha kwamba mnafahamu kwamba sasa ni juu yao kuamua wenyewe.
11 Hilo ni jambo la maana sana ikiwa wameoa au wameolewa. Kuna nchi fulani ambako desturi zilizoimarishwa muda mrefu zinamweka bibi-arusi chini ya usimamizi wa mama-mkwewe. Mahali pengine, wakwe wanajiingiza sana katika mambo ya jamaa. Lakini hilo linaleta furaha? Muumba wa jamaa anajua kilicho bora, naye anasema hivi: “Mwanamume atamwacha baba yake na mama yake naye ataambatana na mkewe.” (Mwanzo 2:24) Sasa daraka la kufanya maamuzi haliko juu ya wazazi wa mume wala juu ya wazazi wa mke, bali juu ya mume. “Mume ni kichwa cha mkewe, kama Kristo naye ni kichwa cha Kanisa,” Neno la Mungu linasema. (Waefeso 5:23) Furaha ya kutumikia watoto wako wakubwa, na baadaye wajukuu wako, yaweza kuongezwa wakati mpango huo unapoheshimiwa.
FURAHIA HUTUMIKIA WENGINE
12. (a) Watoto wao wakiisha kuanza nyumba zao wenyewe, wazazi wanaweza kuongezaje kupendana wao kwa wao? (b) Ni jambo gani jingine wanaloweza kufanya ili maisha yao yawe na manna zaidi?
12 Kuna uhitaji tulio nao sote wa kujiona kwamba maisha yetu ni yenye kufaa, na yana maana. Kutimiza uhitaji huo ni kwa maana sana ili tuwe na hali nzuri. Zaidi ya watoto wako, kuna wengine wengi ambao unaweza kusaidia mahitaji ya maisha yao. Namna gani mwenzi wako mwenyewe wa ndoa? Watoto walipokuwa wakikua, uangalifu mwingi ulielekezwa kwao. Sasa mna nafasi ya kutumikiana zaidi ninyi kwa ninyi. Hilo laweza kusaidia kuongeza sana uhusiano wenu. Lakini kwa nini uwatendee fadhili waliomo nyumbani mwako mwenyewe tu? Unaweza ‘kukunjuliwa moyo’ kwa kusaidia jirani zako wanaokuwa wagonjwa au kwa kutembelea wale wenye umri wa uzee wanaojiona upweke au kwa kusaidia katika njia yo yote uwezayo, kuwapa vitu vya kimwili wale wanaoingia katika hali ya uhitaji bila wao kutaka. (2 Wakorintho 6:11, 12) Biblia, inatuambia habari ya Dorkasi, mwanamke aliyejipatia upendo mkuu kwa sababu ‘alijaa matendo mema na zawadi za rehema alizokuwa akitoa’ akiwapa wajane. (Matendo 9:36, 39, NW) Inasifu wale wanaoonyesha fadhili kwa wale walio na taabu. (Mithali 14: 21) Maandiko yanasema vilevile kwamba, “kuwatazama yatima na wajane katika dhiki yao” ni sehemu ya lazima ya ibada inayompendeza Mungu. (Yakobo 1: 27) Nayo Biblia inatutia sote moyo hivi: “Msisahau kutenda mema na [kushiriki vitu pamoja na wengine]; maana sadaka kama hizi ndizo zimpendezazo Mungu.”—Waebrania 13:16.
13 Ni kusudi gani linalofanya kusaidia wengine kufae?
13 Je! hilo linamaanisha kwamba kujishughulisha kabisa na matendo ya kuonyesha wengine fadhili ndiyo njia inayoleta furaha? Kwa hakika hilo laweza kuongoza kwenye kipingamizi, isipokuwa una kusudi la kiroho, yaani, kutamani kumwiga Mungu katika kuonyesha upendo. (1 Wakorintho 13:3; Waefeso 5:1, 2) Kwa sababu gani? Kwa sababu huenda ukakata tamaa wakati watu hawathamini fadhili zako au wanapojaribu kutumia ukarimu wako katika njia isiyofaa.
14, 15. Ni nini kinachofanya maisha yawe yenye furaha na yenye kuridhisha?
14 Kwa upande mwingine, mtu anapotumia kweli kweli maisha yake katika kumtumikia Mungu, furaha yake kubwa kuliko zote inatokana na kujua kwamba jambo analofanya linampendeza Muumba wake. Naye hatumii uwezo wake awatumikie wengine kwa mali tu za kimwili. Yeye ana “Habari Njema ya utukufu wa Mungu,” Yehova, na pendeleo la kuishiriki pamoja na wengine. (1 Timotheo 1: 11) Kutokana na Biblia, yeye anajua namna ya kushindana na magumu ya maisha sasa, na lo! tumaini la wakati ujao ambalo Mungu anatoa ni la ajabu kama nini. Na ni furaha kama nini kushiriki habari njema hizo pamoja na wengine, kisha kuwaelekeza kwenye chanzo chake, Yehova Mungu! Kama mwandikaji aliyeongozwa na Mungu wa Zaburi 147:1 alivyosema: “Haleluya. Msifuni Bwana ; maana ni vema kumwimbia Mungu wetu, maana kwapendeza, kusifu ni kuzuri.”
15 Maisha yetu wenyewe yanajaa maana tunapoyafahamu mapenzi ya Yehova juu ya uzima na tunapomheshimu yeye. (Ufunuo 4:11) Utapata furaha za kweli ukishiriki sana kuzitoa kweli za Biblia kwa watu wengine, kwa kadiri hali zako zinavyoruhusu. Ijapokuwa huenda watoto wako wenyewe wakawa watu wazima, unaweza kufurahia kusaidia ‘watoto wa kiroho’ wakue. Na unapowaona wakiendelea kukua kuwa Wakristo waliokomaa, utajiona kama mtume Paulo alipoandikia wengine aliokuwa amesaidia katika njia hiyo: “Maana tumaini letu, au furaha yetu, au taji ya kujionea fahari ni nini? Je! si ninyi . . .? Maana ninyi ndinyi utukufu wetu, na furaha yetu.”—1 Wathesalonike 2:19, 20.
UWE MWENYE KUBADILIKANA WAKATI HALI ZINAPOBADILIKA
16, 17. (a) Wakati wa magumu, ni jambo gani linalopaswa kuepukwa? (b) Hata ikiwa mtu anafiwa na mwenzi wake wa ndoa, ni nini kinachoweza kumsaidia asiwe peke yake katika kushindana na magumu mapya?
16 Bila shaka, wakati mwingine watu wengi wanaona kwamba hawawezi tena kufanya kazi nyingi kama walivyokuwa wakifanya. Inawapasa wawe wenye kubadilikana, kuwa tayari kufanya mageuzo. Yakiwapo magumu ya afya, hayo yanataka kuangaliwa. Lakini ni jambo la hekima kusawazika, si kujishughulisha sana na mambo hayo hata mtu ashindwe kuona nafasi zinazotolewa na kila siku. Yatakuwako magumu, na ikiwa kuna jambo lenye kujenga ambalo mtu anaweza kufanya juu ya magumu hayo, inafaa kulifanya. Lakini kuhangaika hakutimizi lo lote, na kuwaza kwamba afadhali mambo yangekuwa vingine, hakuyabadili. Basi, badala ya kutamani sana wakati wa zamani, zitumie nafasi za sasa.
17 Jambo lilo hilo linapasa (linahusu) miaka ya maisha itakayofuata, ikiwa unakuja kuwa katika hali ya kuwa peke yako. Ikiwa ulikuwa na ndoa ya furaha, bila shaka utafurahia kukumbuka mambo ya wakati huo. Lakini wakati unasonga mbele, na huo ni wakati mageuzo yanapohitajiwa. Kuna magumu mapya ya kushindana nayo, nawe ukiishi katika njia ya kumwamini Mungu, hutakuwa peke yako katika kushindana nayo.—Zaburi 37:25 ; Mithali 3:5, 6.
18-20. Ni mambo gani yanayoweza kufanya maisha kuwa ya maana hata wakati wa miaka, itakayofuata?
18 Ijapokuwa maisha yawe na mambo fulani yasiyofurahisha, kuna mengi yanayoweza kutuletea furaha—rafiki wema, nafasi za kutumikia wengine, kufurahia chakula kizuri, hali yenye kupendeza sana ya jua wakati wa machweo (magharibi), kuimba kwa ndege. Zaidi ya hayo, ijapokuwa huenda hali zetu za wakati huu zisiwe bora, Mungu anatuhakikishia kwamba atamaliza uovu na kuwaondolea wanadamu huzuni yote, maumivu makali, magonjwa na hata mauti (kifo) yenyewe.—Ufunuo 21:4.
19 Ni kweli kwamba mtu ambaye maisha yake yamekuwa yenye maoni ya kupenda sana mali, anaweza kuona kwamba miaka yake inayofuata haina jambo lo lote kabisa (ya bure kabisa). Mwandikaji wa kitabu cha Mhubiri alisimulia matokeo ya maisha hayo kwa kusema: “Mambo yote ni ubatili.” (Mhubiri 12:8) Lakini kwa habari ya watu wenye imani, kama Ibrahimu na Isaka, Biblia inasema kwamba walifikia mwisho wa maisha yao wakiwa ‘wazee sana, wameshiba siku.’ (Mwanzo 25:8; 35:29) Ni jambo gani lililofanyiza tofauti hiyo? Watu hao walimwamini Mungu. Walisadiki kwamba katika wakati wake Mungu, wafu wangeishi tena, nao waliutazamia wakati huo, ambapo Mungu mwenyewe angesimamisha serikali ya haki kwa ajili ya wanadamu wote.—Waebrania 11:10, 19.
20 Ikiwa huyaruhusu magumu ya wakati huu yakupumbaze hata ukose kuyaona mambo mengi mazuri yaliyo karibu yako, na wakati ujao wa ajabu ambao Mungu amewekea watumishi wake, maisha yako vilevile yatakuwa na maana. Kila siku itakufurahisha, mpaka katika miaka itakayafuata.
[Picha katika ukurasa wa 176]
Kadiri maisha ya watu wawili yanavyozidi kupatana, ndivyo hao wawili wanavyozidi kuwa mmoja