Roho Zisizoonekana—Je! Zinatusaidia? Au Zinatuumiza?
1, 2. (a) Watu wengine wanaamini nini juu ya misiba inayofanyizwa na vitu kama umeme wa mvua? (b) Watu wengi wanaamini nini juu ya wafu?
WINGU jeusi lafunika. Kunatokea mngurumo mkubwa. Matone mazito ya mvua yanapiga chini. Jamaa yenye watu saba imekusanyika ndani ya nyumba ndogo nao wanatumaini ya kwamba wazazi wao waliokufa (mizimu) watawalinda. Umeme wa mvua unapiga ghafula kwa mshindo wa kuogopesha na nyumba inawaka moto. Katika jamaa hiyo watu wawili tu ndio wanaokoka. Watu hao wawili sasa ‘wanaogopa kukaa katika kijiji kile kile, maana wanadhani ya kuwa kimelogwa na mchawi (mlozi) anayetaka kuimaliza kabisa jamaa yote.’
2 Taarifa hiyo ilitokea katika gazeti linaloitwa The Times of Swaziland, Januari 28, 1977. Labda jamaa hao walijua kwamba umeme (radi) wa mvua unafanyizwa katika mawingu. Lakini taarifa hiyo inaonyesha kwamba waliamini vilevile kwamba adui anaweza kuagiza roho zisizoonekana zielekeze umeme mahali fulani, tena waliamini kwamba wazazi waliokufa (mizimu) wanaweza kutoa ulinzi unaohitajiwa.
3. Watu wengi wanaamini ni vitu gani vinavyofanyiza misiba inayotokana na motokaa, magonjwa na magumu mengine?
3 Ebu sasa tazama katika mji wa Kiafrika na makao ya mwaguzi (mpiga ramli) au mganga wa kienyeji. Kuna mama mwenye mtoto mchanga ambaye ni mgonjwa. Mtoto alipoanza kushikwa na homa na ugonjwa wa kuchafuka tumbo, mama yake alimpeleka haraka kwenye hospitali mjini. Baada ya kwenda huko mara nyingi muda wa juma nyingi na kutumia dawa ambazo madaktari wamependekeza huko hospitali zitumiwe, mtoto anaendelea kuwa mgonjwa sana. Mama amekata tamaa, kisha amemwendea mganga wa kienyeji, akitumaini atamponya mtoto wake. Mama huyo si yeye peke yake aliyemwendea mganga wa kienyeji. Vilevile kijana amekuja kutafuta dawa imsaidie aone kazi. Mzee anayefunga safari ndefu, amepokea hirizi (kamba ya dawa) sasa hivi achukue katika safari yake. Bila shaka, watu hao wote wanajua kwamba ugonjwa unaletwa na viini (vijidudu vidogo sana vya magonjwa), wanajua kwamba hali mbaya ya uchumi ndiyo inayofanya kuwe na ukosefu wa kazi, wanajua kwamba kuendesha motokaa na huku umelewa, na magari yasiyotengenezwa vizuri ndiyo yanayofanyiza misiba ya barabarani. Lakini wanaamini vilevile kwamba misiba ile ile yaweza kuletwa au kuzuiwa na roho zisizoonekana, na ya kwamba mganga wa kienyeji amepewa uwezo na roho hizo zisizoonekana.
4, 5. Kwa sababu gani ibada ya roho zisizoonekana (uchawi) inaongoza sana maisha za watu wengi katika sehemu mbalimbali za ulimwengu? Namna gani?
4 Humu Afrika, na katika visiwa vingi vya Pacific, Asia, sehemu za Amerika ya Kusini na mahali penginepo kuzunguka dunia, mamilioni ya watu wana imani zinazofanana na hizo. Katika maisha yao ya kila siku, wanahangaika sana na mambo ambayo roho hizo zisizoonekana zaweza kuwatendea, yawe mema au mabaya. Wanaamini kwamba mauti sio mwisho wa maisha bali ni njia ya kufungulia roho itoke katika mwili. Wao wanadhani mauti ni muda ambao roho hiyo inakwenda kwenye maisha mengine au kwenye “ulimwengu wa roho” (kuzimu).
5 Si watu wanaoishi mashambani, wala makabila fulani wala watu wasio na elimu tu ndio wanaoamini hivyo. Hata watu walio na elimu wanaoishi katika miji mikubwa wanaamini hivyo. Kama vile wafuasi wa dini za kienyeji na za kikabila wanavyoamini, wafuasi wengi wa makanisa ya Jumuiya ya Wakristo pamoja na madhehebu ya Kiislamu wanaamini kwamba matukio ya maisha yanaongozwa au yanahusiana (yanakamatana) na roho zisizoonekana. Kukitokea misiba, kama vile ugonjwa mkubwa au mauti ya ghafula katika jamaa, wanamwendea mwaguzi au mganga wa kienyeji. Huenda mganga huyo akatumia “mifupa yenye nguvu za uchawi” au njia nyingine ili awaambie wanaouliza kama roho za wazazi wao waliokufa (mizimu) zimekasirishwa au kama wamelogwa na adui fulani. Huenda akawapa hirizi (kamba ya dawa) za kuvaa au wachukue dawa ya kunywa ya kuwalinda. Mara nyingi mbuzi, kondoo au kuku anachinjwa ili roho hizo zisizoonekana zipate kutulizwa.
6. Ni sababu gani chache zinazofanya watu wengi sana wawaendee wachawi?
6 Sababu zinazofanya watu kuzunguka dunia wawaendee wachawi au waganga ni nyingi: ili walinde nyumba na jamaa yao; ili wamlinde mtoto aliyezaliwa sasa hivi; ili waondoe ugumba (hali ya kutozaa) au wazuie mimba zisiharibike; ili wawaone wevi; ili wapate rafiki; ili wapendwe, ili biashara yao ipate kufanikiwa (kusitawi), wapate mawindo, wapite mitihani (majaribu) shuleni, hata washinde katika mashindano ya michezo. Timu (vikundi) za michezo ya mpira zimeajiri (zimewalipa) waganga wawasaidie washinde. Watu wengine wakipoteza kazi wanamwendea mganga na kupewa dawa wapake (wapakae) kope za macho yao, au mzizi waweke chini ya ulimi wao wanapochunguzwa na atakayekuwa mkubwa wao wa kazi ili kuona kama wanafaa kupewa kazi. Katika sehemu za kulima mashamba watu wanatoa maombi ya pekee wanapopanda mazao yao au wanapotaka kufanyiza mvua ije. Kati ya mataifa mengi, kila kabila au sehemu ya nchi inajifanyia sherehe na desturi zao wenyewe wakati mtu anapokufa. Lakini karibu yote hayo yanafanywa kwa kusudi la kutuliza hasira ya roho zisizoonekana au kuziomba msaada. Ijapokuwa huenda uhusiano wa mambo hayo usionekane wazi, sherehe (desturi) nyingi sana za kienyeji na mazoea ya uzazi, kutahiri, majando (sherehe za kutahiri watoto na kupewa mafundisho), ndoa, kuwinda, kufuga ng’ombe, kumiliki (kuwa na uenyeji wa) mashamba na vifo, yanahusiana moja kwa moja au yanahusiana kwa njia nyingine na kuziabudu roho hizo (mizimu).
7. Sasa kunatokea maulizo gani, na ni jambo gani linaloonyesha kwamba majibu ya wanadamu peke yake hayatoshi (hayafai)?
7 Je! kweli kuna roho zisizoonekana, ambazo zina uwezo kuliko wanadamu? Kuna ushuhuda wenye kusadikisha unaoonyesha kwamba ziko. Kwa sababu hiyo, je! tukitaka kuzungumza na roho hizo zisizoonekana au tukiziomba, tutapata faida au tutaumizwa? Je! roho hizo ni roho za wazazi wetu waliokufa (mizimu)? Kwa mfano, je! kweli watu wa ukoo wetu waliokufa wanaweza kuwasaidia walio hai na kuwalinda au kuwapa shauri? Ikiwa kuna faida ya kuziomba msaada roho hizo zisizoonekana, ni kwa sababu gani tunasikia mara nyingi sana habari za pupa (tamaa mbaya) udanganyifu, uasherati na hata uuaji kati ya wale wanaoshiriki sana kuziabudu roho hizo? Sababu gani kuna mawazo, mazoea na maoni mengi sana yaliyo tofauti, na mengi ya hayo ni yenye kupingana? Twende wapi tupate majibu yasiyo na makosa?
TUNAVYOWEZA KUPATA MAJIBU YASIYO NA MAKOSA
8. Ni mkusanyo gani wa “barua” ambao Muumba ametoa? Kwa sababu gani?
8 Hata maoni yao juu ya roho yaweje, watu wengi wanakubali kwamba bila shaka kuna mmoja aliye Chanzo (Chemchemi) cha uzima wote, Muumba wa milele. Akiwa Mpaji-Uzima wa kwanza, anaweza kutajwa kwa kufaa kuwa Baba mkuu wa wanadamu wote. Basi, lifikirie ulizo hili: Ikiwa ungekuwa ndiwe baba ya jamaa, na kama ungekaa mbali sana na watoto wako, je! ungekosa kuwaandikia barua mara kwa mara? Baba wema wanafanya hivyo, wakiwapelekea watoto wao habari za hali yao na kuwapa shauri la upendo. Je! wanadamu wana njia yo yote kama hiyo ya kupashana habari na Muumba na Baba yao? Jibu ni, Ndiyo, kuna mkusanyo wa “barua” 66 au maandishi yaliyoongozwa na kutolewa na Muumba ambayo ndani yake tumewekewa habari na shauri bora. Mkusanyo huo wa maandishi yaliyoongozwa na Mungu ni: Biblia.
9. Ni nini linaloonyesha kwamba Biblia si kitabu cha taifa au jamii moja ya watu?
9 Biblia haikuandikwa na Wazungu wa Ulaya, bali na watu wa Mashariki ya Kati, katika Asia. Hata hivyo iliandikwa kwa faida ya watu wote kila mahali. Haibagui (haipendelei) watu kwa sababu wanakaa mahali fulani, ni wa taifa au rangi nyingine, kwamba ni rangi ya manjano, rangi nyeusi, rangi kahawa wala rangi nyeupe. Ndani yake tunaona maneno haya ya mtume Petro yaliyoongozwa na Mungu: “Hakika natambua ya kuwa Mungu hana upendeleo; bali katika kila taifa mtu amchaye na kutenda haki hukubaliwa na yeye.”—Matendo 10:34, 35.
10. Biblia ni kitabu cha pekee na kilicho tofauti katika njia gani?
10 Kati ya vitabu vingi vyote vilivyoandikwa, Biblia ndicho kitabu cha zamani sana katika historia ya wanadamu kuliko maandishi mengine yo yote ya kale. Iliandikwa na watu kama 40 kuanzia na Musa yapata miaka 3,500 iliyopita (katika mwaka 1513 K.W.K.). Hata hivyo, vitabu vyote vya Biblia 66 vinapatana sana. Maelfu ya mamilioni ya nakala nzima au sehemu zake, yameenezwa katika lugha zaidi ya 1,600. Ni kweli kwamba Biblia ndicho kitabu peke yake kilichoandikwa kinachopatikana katika lugha fulani. Zaidi sana, ndicho kitabu peke yake duniani kinachoeleza waziwazi habari ya mwanzo wa wanadamu, sababu ya kuwako magumu yao na wakati wao ujao utakavyokuwa. Bila shaka Biblia ni kitabu cha pekee.
11. Jina la Muumba ni jina gani, na ana sifa gani?
11 Biblia inatufunulia jina la Muumba wa mbingu na dunia—Yehova—ambalo ni jina la Kiebrania lenye maana ya “Anafanya Kuwe.” Zaburi 83:18 inasema hivi kwa habari zake: “Wajue ya kuwa Wewe, uitwaye jina lako YEHOVA, ndiwe peke yako Uliye juu, juu ya nchi yote.” Yeye ndiye “Mungu asiyeweza kusema uongo,” anayetajwa katika Tito 1:2. Basi unaweza kumtumaini Yehova. Yeye hasemi uongo, hadanganyi, hafanyi hila. Vilevile, Zaburi 86:15 inasema habari zake hivi: “Lakini Wewe [Yehova] , u Mungu wa rehema na wema, mvumilivu, mwingi wa fadhili na kweli.” Tunawezaje kuwa na hakika ya maneno hayo? Twawezaje kuwa na hakika kwamba kitabu chake, yaani, Biblia, ni kitabu cha kweli?
UNABII WA BIBLIA UNATIMIZWA
12. (a) Ni jambo gani linaloonyesha kwamba Biblia ni ya kweli? (b) Ni unabii gani juu ya Yesu Kristo uliotimizwa miaka mingi wakati ulipokwisha kuandikwa?
12 Ushuhuda wenye nguvu unaoonyesha kwamba Biblia ni ya kweli ni kwamba ina mamia ya unabii ambao umetimizwa. Unabii ni kutabiri matukio ya wakati ujao. Kwa mfano, kuna unabii mwingi sana juu ya Mwalimu Mkuu, Yesu Kristo. Unabii wote huo ulitolewa zamani mamia ya miaka kabla (mbele) ya kuzaliwa kwake. Hata hivyo wote ulitimizwa. Nabii Isaya alitoa unabii wa kwamba Yesu angezaliwa na bikira. (Isaya 7:14) Unabii huo ulitimizwa baada ya miaka zaidi ya 700. (Mathayo 1:23) Unabii wa Mika 5:2 ulitangulia kutaja kwamba angezaliwa Bethlehemu. Unabii wa Zekaria 11:12 ulitangulia kuonyesha kwamba angesalitiwa (angetolewa) kwa vipande 30 vya fedha. Zaburi 22:16-18 ilitangulia kutaja kwamba mikono na miguu yake ingetiwa majeraha (ingeumizwa) na ya kwamba mavazi yake yangepigiwa kura. Hata kilio chake kwa sababu ya maumivu makali katika mti wa mateso kilitangulia kutajwa katika Zaburi 22:1. Unabii wote huo, na mwingine mwingi, ulitimizwa, kama habari wale walioona mambo hayo zinavyoonyesha.—Mathayo 2:1-6; 26:14, 15; Yohana 20:25; Mathayo 27:35, 46.
13. Ni unabii gani wa kale unaotimizwa leo?
13 Je! hayo hayatupi ushuhuda wenye nguvu kwamba Biblia ni kitabu cha kweli? Lakini, labda mwingine atasema, ‘Ndiyo, ingawaje yote hayo yalitukia zamani sana.’ Hiyo ni kweli, lakini hata leo tunaona unabii mwingi wa Biblia ukitimizwa. Tumeona vita vikubwa na kuuawa kwa wanadamu kuliko wakati wo wote zamani tangu mwaka 1914, pamoja na upungufu wa chakula na magonjwa ya kuenea mahali pote kama inavyoelezwa kwa mfano katika Ufunuo 6:1-8. Viongozi wengi wa ulimwengu wanakubali kwamba hawajui namna ya kuondoa magumu yasiyohesabika yanayoendelea kuongezeka kati ya wanadamu. Mambo hayo yanaogopesha kama vile Biblia ilivyotangulia kusema: “Dhiki ya mataifa wakishangaa . . . watu wakivunjika mioyo kwa hofu, na kwa kutazamia mambo yatakayoupata ulimwengu.”—Luka 21:25, 26; soma vilevile 2 Timotheo 3:1-5.a
14. Ni maulizo gani ambayo Biblia itatujibia kikweli?
14 Basi, Biblia inatuambia nini juu ya roho zisizoonekana? Ni nani, nao walitoka wapi? Namna gani uwezo wao wa kutusaidia ama kutuumiza? Na yatupasa tufanye nini ili tuweze kufurahia maisha yenye furaha, amani na salama ambayo watu wote wa kawaida wanataka?
NI NANI WALE WANAOKAA KATIKA MAKAO YA KIROHO?
15, 16. (a) Je! wako watu wengine wa kiroho zaidi ya Yehova Mungu? (b) Watu wote wa kiroho au wanadamu wamepata uzima kutoka kwa nani?
15 Biblia inaonyesha kwamba sisi wanadamu tulio hapa duniani sio watu peke yetu tulio hai na tulio na akili katika ulimwengu wote. Inafunua kwamba, kama vile kulivyoko viumbe vyenye mwili, vinavyovuta (vinavyopumua) hewa ya dunia, vinavyokunywa maji yake na kula chakula chake, vivyo hivyo viko viumbe vya kiroho, visivyotegemea kuishi kwa riziki ya dunia. Nayo inaonyesha kwamba Mkubwa wao katika makao hayo ya kiroho ndiye Muumba mwenyewe, Yehova Mungu. Kwa habari zake Yesu alisema hivi: “Mungu ni Roho, nao wamwabuduo yeye imewapasa kumwabudu katika roho na kweli.”—Yohana 4:24.
16 Sasa duniani kuna watu kama milioni elfu nne (4,000,000,000) wanaoishi ndani yake. Zaidi ya Muumba, Biblia inafunua kwamba kuna mamilioni ya watu wengine wa kiroho katika makao ya kiroho, wanaojulikana kama malaika. (Danieli 7:9, 10; Ufunuo 5:11) Wengine hao wote walipata uzima wao kwa Muumba wa mbingu na dunia wakaishi zamani kabla (mbele) ya kuumbwa kwa wanadamu. Kama Ufunuo 4:11 unavyosema: “Umestahili wewe, [Yehova] wetu na Mungu wetu, kuupokea utukufu na heshima na uweza; kwa kuwa wewe ndiwe uliyeviumba vitu vyote, na kwa sababu ya mapenzi yako vilikuwako, navyo vikaumbwa.” Hakuna watu, wanadamu wala roho, wasiopata uzima kutoka kwa Yehova Mungu, Muumba.
17. (a) Ni nani aliyekuwa wa kwanza kumwasi Mungu? (b) Ni waasi gani wengine waliojiunga naye?
17 Habari ya kweli ya Biblia inaonyesha kwamba mwana na binti wa kibinadamu wa kwanza wa Mungu, yaani, Adamu na Hawa, walipokwisha kuumbwa katika Edeni, malaika fulani mwenye nguvu aliongozwa na ubatili na kutaka makuu, akamwasi Mungu. Aliweza kuwashawishi watu wawili wa kwanza washiriki uasi wake kwa kutumia udanganyifu na choyo. Kwa kuwa aligeuka akawa adui wa Yehova, Muumba, yeye anaitwa Shetani, jina ambalo katika Kiebrania maana yake ni “mpinzani” au “adui.” (Mwanzo 3:1-13; Ufunuo 12:9) Baadaye alishawishi wana wengine wa mbinguni wa Mungu au malaika wafuate mwendo wa uasi unaofanana na huo.
18. (a) Viumbe vya kiroho viliasi wakati gani? (b) Ni nini kilichowashawishi waache kumtumikia Yehova?
18 Mtume Petro anasema habari za roho hao “wasiotii hapo zamani, uvumilivu wa Mungu ulipokuwa ukingoja, siku za Nuhu.” (1 Petro 3:19, 20) Historia ya Biblia inaonyesha kwamba uasi huo ulitokea kwa sababu ya kuvutwa na uzuri wa wanawake, ukawafanya wana hao wa kiroho washuke duniani, na kuvaa mwili wa kibinadamu na kwa njia hiyo wakaacha mahali walipogawiwa kufanya utumishi wa Yehova. Tunasoma katika Mwanzo 6:2 juu ya siku za Nuhu zilizotangulia gharika hivi: “Wana wa Mungu waliwaona hao binti za wanadamu ya kuwa ni wazuri; wakajitwalia wake wo wote waliowachagua.”
19. Ni nini lililowapata malaika hao waasi wakati wa Gharika ilipokuja?
19 Yehova Mungu hakuruhusu jambo hilo liendelee kwa wakati usiojulikana. Alileta gharika ya maji duniani, ikaharibu kabisa waovu wote, akalinda watumishi wake waaminifu peke yao. Kwa sababu hiyo, wana wa kiroho wasiotii walilazimika kuvua (kuondosha) miili ya kibinadamu, yaani, wakaacha umbo la kibinadamu wakarudia makao yao ya kiroho. Baada ya hapo wanatajwa kuwa mashetani au roho wabaya. Ili kuonyesha kwamba Mungu hakuwaruhusu tena wavae mwili wa kibinadamu, naye amewaweka katika hali isiyo ya heshima na yenye laana, Yuda 6 anasema hivi: “Malaika wasioilinda enzi yao wenyewe, lakini wakayaacha makao yao yaliyowahusu, [Mungu] amewaweka katika vifungo vya milele chini ya giza [kuu] kwa hukumu ya siku ile kuu.”
20. (a) Ni nani aliye mungu wa ulimwengu huu? (b) Uwezo wake ni mkubwa kadiri gani?
20 Tangu wakati huo, Shetani amekuwa “mungu” wa ulimwengu huu na taratibu yake mbovu kwa kusaidiwa na roho hao au mashetani waovu. Labda jambo hilo litakushangaza. Lakini soma Yohana 14:30 na 2 Wakorintho 4:4, NW nawe utaona kwamba Neno la Mungu linaposema juu ya “mtawala wa ulimwengu” au “mungu wa taratibu hii ya mambo,” halimaanishi Yehova Mungu, bali linamaanisha Shetani Ibilisi. Mtume Yohana anaandika hivi: “Ulimwengu mzima uko katika nguvu za yule mwovu,” vilevile anamtaja Shetani Ibilisi kuwa “audanganyaye ulimwengu wote.”—1 Yohana 5:19, NW; Ufunuo 12:9.
21. Sababu gani maarifa sahihi ya Neno la Mungu ni ya maana?
2121 Basi, Biblia yaonyesha kwamba si roho wazuri tu, kama malaika walioko, bali vilevile wako mashetani au roho wabaya. Ni jambo la maana kujua kweli hizo, maana ndio ufunguo unaofungua mlango wa kufahamu namna roho zisizoonekana zinavyotuhusu sisi na matukio ya maisha yetu ya kila siku. Na tuone namna maarifa sahihi ya Neno la Mungu yanavyotusaidia tupate jibu la maulizo ya maana yafuatayo.
UJUMBE WA ROHO UNATOKA WAPI?
22. Msichana katika Brazil alipatwa na nini juu ya ujumbe (habari) uliotoka katika ulimwengu wa roho?
22 Katika sehemu mbalimbali za dunia watu wengi wanaamini kwamba ujumbe (habari) unaweza kupokewa kutoka ulimwengu wa roho. Yaliyompata msichana fulani mdogo katika Brazil ni mfano mmoja unaoonyesha watu wengi wanaosema kwamba wamepokea ujumbe (habari) wa namna hiyo. Siku moja alianza kusikia “sauti.” Aliomba wachawi wamsaidie. Miaka iliyofuata alikuwa akiona kwa ghafula kitu cheusi mbele yake naye akawa katika hali kama ya usingizi. Akiwa katika hali hiyo alikuwa akipendekeza dawa za magonjwa na kufanya mambo fulani ili aponye watu walioshambuliwa na mashetani.
23. (a) Wagonjwa wengine wanajaribuje kuponya magonjwa yao? (b) Wanaamini ujumbe huo unatoka wapi?
23 Mara nyingi mgonjwa anamwendea mchawi au mganga ili apate dawa ya kuponya ugonjwa wake. Ndipo mganga huyo anapomwambia aende nyumbani arudi kesho yake. Halafu usiku akiwa anaota ndoto, mgonjwa huyo anaambiwa mzizi (dawa) wa kuchimba na mahali pa kuupata ili apone ugonjwa wake. Inaaminiwa kwamba ujumbe huo unatoka kwa mtu wa ukoo (jamaa yake) aliyekufa, labda nyanya ambaye anaelekea kama anamwona katika ndoto.
24. Watu wana maoni gani mbalimbali juu ya wafu?
24 Wengi wa hao wanaoamini ujumbe huo wanaamini vilevile kwamba wazazi wao waliokufa wanaishi katika ulimwengu wa roho (kuzimu) na ya kwamba wazazi hao waliokufa wanaweza kusaidia ama kuumiza wale walio hai duniani. Wafuasi wa makanisa ya Jumuiya ya Wakristo wanaamini kwamba wakati wa kufa, nafsi ambayo wanasema ni roho isiyoweza kufa, inakwenda ama mbinguni ama motoni, au, ikiwa wao ni Wakatoliki, wanaamini kwamba inaweza kwenda mahali wanapoita toharani (purgatori) kabla ya kwenda mbinguni. Watu wachache wanaamini kwamba mauti ndio mwisho, yaani, hakuna kuishi baada ya kufa. Kwa wazi imani za wanadamu juu ya wafu zinapingana. Basi, sababu gani usichunguze uone asemavyo Yehova Mungu, Roho Mwenye Nguvu Zote, aliyeumba uhai wote juu ya jambo hilo?
JE! NAFSI HAIWEZI KUFA?
25. Twawezaje ‘kumwacha Mungu apatikane kuwa wa kweli’? (Soma vilevile 2 Timotheo 3:16.)
25 Kwanza, na tuchunguze imani ya watu wengi ya kwamba nafsi haiwezi kufa hata kidogo. Je! hivyo ndivyo unavyoamini? Tunawezaje kuwa na hakika? Bila shaka Yeye aliyeiumba nafsi anajua, maana anakaa katika makao ya kiroho, akiwa Roho Mwenye Nguvu Zote, Yehova Mungu. Biblia yasema hivi: “Mungu na apatikane kuwa wa kweli, lakini kila mwanadamu apatikane kuwa mwongo.” (Warumi 3:4, NW) Je! wewe una nia ya kukubali Neno la Mungu kuliko neno la wanadamu? Biblia inafunua nini?
26. (a) Usemi huu “nafsi isiyoweza kufa” unapatikana mara ngapi katika Biblia? (b) Ni viumbe gani vingine, zaidi ya wanadamu, vinavyotajwa nafsi katika maandishi ya kwanza ya Biblia kama inavyoonyeshwa katika Biblia ya New World Translation? (Les Saintes Ecritures Traduction du monde nouveau)
26 Ikiwa ungesoma Biblia tangu mwanzo mpaka mwisho, ungeshangaa kuona kwamba mambo ambayo inasema juu ya nafsi ni tofauti sana na yale ambayo watu wengi wanaamini. Kwanza, ungeona kwamba usemi huu “nafsi isiyoweza kufa” hauonekani po pote katika Biblia, hata mara moja. Kwa upande mwingine, ungeona kwamba samaki, ndege na wanyama, wote wanatajwa “nafsi” katika mahali mbalimbali.—Tazama Mwanzo 1:20, 21, 24, 30; Hesabu 31:28, katika New World Translation of the Holy Scriptures, Les Saintes Ecritures Traduction du monde nouveau.
27. Je! nafsi zinaweza kuharibiwa? Ezekieli 18:4, 20, katika Biblia ya Kiswaitili ya Zaire na New World Translation ya Kiingereza, Lea Baintes Ecritures Traduction du monde nouveau ya Kifaransa, linaonyeshaje hivyo?
27 Labda utashangaa hata zaidi kuona kwamba katika Kutoka 12:15, 19; Mathayo 10:39; Matendo 27:22; Isaya 53:12; Zaburi 30:3; 6:4, na katika maandiko mengine mengi, Biblia inasema kwamba “nafsi” yaweza ‘kukatiliwa mbali,’ yaweza ‘kupotezwa’ na kuokolewa katika kaburi, hata ‘kumwagwa katika mauti.’ Katika unabii wa Ezekieli, Yehova Mungu anatuambia waziwazi kwamba “nafsi inayofanya zambi, itakufa.” (Ezekieli 18:4, 20, Biblia ya Kiswahili ya Zaire na New World Translation of the Holy Scriptures ya Kiingereza, Les Saintes Ecritures Traduction du monde nouveau ya Kifaransa) Kwa kuwa nafsi inaweza kukatiliwa mbali na kupotezwa, kwa wazi inaweza kufa.
28. (a) Biblia inasemaje juu ya kutoweza kufa? (b) Ni imani gani ya watu wengi isiyoungwa mkono na Biblia?
28 Biblia inaonyesha waziwazi kwamba sisi hatuzaliwi tukiwa na hali ya kutoweza kufa, kama watu wengi sana wanavyodhani. Yesu Kristo aliyefufuliwa anatajwa kati ya viumbe vyote vya Yehova Mungu kuwa “yeye peke yake [ambaye] hapatikani na mauti.” (1 Timotheo 6:16) Tena 1 Wakorintho 15:50-54 inaeleza kwamba watumishi fulani wa Mungu watapokea hali ya kutoweza kufa kama zawadi ya uaminifu wao kwake. Hilo linamaanisha kwamba ile imani ya watu wengi ya kwamba kila mtu anazaliwa akiwa na nafsi isiyoweza kufa haiungwi mkono hata kidogo na Neno la Mungu. Basi, tutalitumaini neno la nani, lile la Muumba au la wanadamu? Bila shaka Roho Mwenye Nguvu Zote, Yehova Mungu, anastahili tumaini letu. Wanadamu wanaweza kusema uongo, lakini Mungu wa kweli hasemi uongo.
NI JAMBO GANI LINALOTUKIA WAKATI WATU WANAPOKUFA?
29. Ulikuwa uongo gani ambao ndio wa kwanza kuandikwa, nani aliyeusema?
29 Ni jambo gani linalowapata wazazi wetu wanapokufa, na ni nini lingeweza kutupata sisi ikiwa ni lazima tufe? Ebu fikiria lililowapata wazazi wetu wa kwanza, wale watu wawili wa kwanza, Adamu na Hawa. Walikuwa watu wakamilifu nao wangeweza kuishi milele ikiwa wangeendelea kumtii Mungu. Lakini Mungu aliwaonya juu ya matokeo mabaya ambayo wangepata ikiwa wangekosa kutii, akisema, “Utakufa hakika.” (Mwanzo 2:17) Baadaye, adui na mdanganyifu mkuu, Shetani, alimfikia Hawa akamwambia uongo ambao ndio wa kwanza kuandikwa. Kwa kutaka kumdanganya na kumwondoa Hawa na Adamu mumewe upande wa Mungu, Shetani alitumia nyoka kama msemaji wake, akisema hivi, “Hakika hamtakufa.”—Mwanzo 3:4.
30. Ni jambo gani lililowapata watu wa kwanza wawili wakati wa kufa?
30 Ni nani aliyesema kweli, Mungu au Shetani? Je! bado tunaweza kumwona Adamu akiishi mahali fulani duniani? Hapana. Adamu alikufa kama Mungu alivyosema. (Mwanzo 5:5) Watu wale wa kwanza wawili walipokufa, ikawa kama Mungu alivyokuwa amewaambia waziwazi: “[Utairudia] ardhi, ambayo katika hiyo ulitwaliwa; kwa maana u mavumbi wewe, nawe mavumbini utarudi.” (Mwanzo 3:19) Mungu hakuwaambia kwamba watakwenda mbinguni wala motoni wala kwenye ulimwengu wa roho.
31. Biblia inasemaje juu ya hali ya wafu?
31 Kwa habari ya hali ya wafu, Neno la Mungu linasema hivi: “Wafu hawajui neno lo lote.” (Mhubiri 9:5) Je! wanaweza kuwaonyesha walio hai upendo au chuki? Tena Biblia inajibu hivi: “Mapenzi yao na machukio yao, na husuda yao, imepotea yote pamoja . . . kwa kuwa hakuna kazi, wala shauri, wala maarifa, wala hekima, huko [kaburini] uendako wewe.” (Mhubiri 9:6, 10) Ili ionyeshe ukweli wa hayo, Zaburi 146:4 inasema kwamba mwanadamu “huurudia udongo wake, siku hiyo mawazo yake yapotea.” Nayo Zaburi 115:17 inaongeza hivi: “Sio wafu wamsifuo [Yehova], wala wo wote washukao kwenye kimya.”
32. (a) Katika Biblia, mauti inalinganishwa na nini? (b) Je! wafu wanaweza kusaidia au kuumiza walio hai?
32 Kwa sababu ya hayo, mara nyingi hali ya mauti inafananishwa katika Biblia na usingizi. Matendo 13:36 linasema kwamba Mfalme Daudi alipokufa, “alilala.” Wathesalonike wa Kwanza 4:13, 14 inataja Wakristo waliokuwa wamekufa kuwa wale “waliolala” usingizi. Vilevile Yesu alisema habari za Lazaro katika njia iyo hiyo, alipokwenda kumfufua katika mauti. Alisema hivi: “Ninakwenda nipate kumwamsha.” (Yohana 11:11-14; Danieli 12:13) Kwa hiyo, unaweza kufahamu sababu kwa nini haikupasi uwaogope watu waliokufa hata kidogo, wala kujaribu kutuliza (kupoleza) hasira yao wala kujaribu kwa vyo vyote kuomba kibali yao. Neno la Mungu linaonyesha kwamba wamekufa, hawana fahamu, wako kimya wasiweze kupashana habari na walio hai wala kuonyesha upendo, chuki wala tendo lo lote. Wala hawawezi kuwasaidia wala kuwaumiza walio hai.
UFUFUO
33. (a) Lazaro aliona tukio gani la ajabu? (b) Alikuwa yuko wapi muda wa siku nne?
33 Tafadhali fikiria kwa uangalifu tukio lile la ajabu juu ya Lazaro. Yesu alipofika nyumbani kwake, zilikuwa zimepita siku nne tangu Lazaro afe. (Yohana 11:39) Mwili wake ulikuwa umekwisha anza kuoza. Ndipo Yesu alipofanya jambo ambalo mganga wa kienyeji wala mtu anayeponya kwa imani hawezi kufanya hata kidogo. “Akalia kwa sauti kuu, Lazaro, njoo huku nje. Akatoka nje yule aliyekufa.” (Yohana 11:43, 44) Alitoka wapi? Au “kuzimu” (mahali ambapo watu wanadhani zinakaa roho za wafu, mizimu)? Hapana, alitoka ndani ya kaburi alimokuwa amelala bila kufahamu cho chote, akiwa amelala usingizi wa mauti muda wa siku nne.
34. Ni mwujiza gani mwingine ulioandikwa katika Marko 5:42, nao wazazi wa msichana mdogo walionaje?
34 Wakati mwingine Yesu alimfufua msichana mwenye umri wa miaka 12 katika wafu. Ebu wazia namna wazazi wake walivyofurahi ilipokuwa hivyo! Habari katika Marko 5:42 inasema kwamba “wakashangaa mshangao mkuu.” Kuona binti yao mdogo akiwa baridi na bila pumzi muda mchache, kisha kumpokea akiwa hai na mzima, lo! hiyo ilikuwa ajabu. Bila shaka jambo hilo lilikuwa bora kuliko kupokea ujumbe unaodhaniwa kuwa unatoka kwa mpedwa aliyekufa, kupitia kwa mchawi au mganga.
35. (a) Yesu atafanya nini kwa kadiri kubwa wakati wa utawala wake wenye amani wa miaka elfu? (b) Paulo alithibitishaje (alikazaje) jambo hilo?
35 Lakini hapa pana jambo la maana sana tunaloweza kujifunza sote. Ufufuo wa wafu ambao Yesu alifanya alipokuwa duniani ulikuwa wonyesho mdogo tu wa ufufuo ulio mkubwa sana ambao atafanya wakati wa utawala wake wenye amani wa miaka elfu moja, ambao sasa ni karibu. Yesu mwenyewe alisema hivi: “Wote waliomo makaburini wataisikia sauti yake. Nao watatoka.” (Yohana 5:28, 29) Ukieleza juu ya wakati huo ulio mzuri sana, Ufunuo 20:13, ZSB unasema hivi: “Bahari ikatoa wafu waliokuwa ndani yake; Mauti na Hadeze [kaburi] zikatoa wafu waliokuwa ndani yao. Wakahukumiwa kila mutu kwa kadiri ya matendo yake.” Mtume Paulo alisema hivi: “Nina tumaini kwa Mungu . . . ya kwamba kutakuwa na ufufuo wa wafu, wenye haki na wasio haki pia.”—Matendo 24:15.
36. Ahadi ya ajabu juu ya ufufuo inaonyesha nini juu ya hali ya wafu?
36 Basi, tafadhali jibu maulizo haya akilini mwako mwenyewe: Je! ahadi hiyo iliyo wazi juu ya ufufuo haionyeshi kwamba wazo la kwamba wafu wanaishi mahali fulani ni la uongo? Ikiwa wafu wangekuwa hai na kuishi mbinguni au katika ulimwengu fulani wa roho, lingekuwa kusudi gani la ufufuo? Haungehitajiwa. Kama Neno la Mungu linavyosema, ni wazi kwamba wazo hilo la kwamba ‘mauti ni muda tu wa kutoka kwa roho kwenda katika maisha mengine’ ni la uongo kabisa. Biblia inafundisha waziwazi kwamba wafu wamekufa kweli kweli, hawana fahamu, wanalala mpaka watakapoamshwa kwa kufufuliwa katika taratibu mpya ya Mungu.
37. Sasa ni maulizo gani yanayopaswa kujibiwa?
37 Lakini, labda utasema hivi: ‘Ikiwa ni hivyo, ni kwa sababu gani kunatokea vitu vya ajabu kama mizuka na ujumbe ambao umepokewa?’ Wakati wetu huu, watu wengi kuzunguka dunia wamepokea habari kutoka ulimwengu wa roho kupitia kwa wachawi, waganga, ndoto na njia nyingine. Kwa kuwa wafu hawana fahamu na hawawezi kupashana habari na walio hai, ujumbe huo unatoka wapi?
CHANZO CHENYEWE CHA UJUMBE WA ROHO
38. (a) Ni nani wanaokaa katika ulimwengu wa roho? (b) Mungu anapashana habari na sisi leo kwa njia gani?
38 Tumekwisha kujifunza namna walivyo wale wanaokaa katika ulimwengu wa roho. Zaidi ya Roho Mwenye Nguvu Zote, Yehova Mungu, na malaika zake waaminifu, kuna Shetani adui wa Mungu, na jeshi lake la malaika wasioaminika au mashetani. Tumekwisha ona njia ambayo katika hiyo Mungu ametoa ujumbe wake au njia anayotumia ili apashane habari nasi. Ni kupitia kwa Neno lake lililoongozwa, yaani, Biblia, ambalo alipitisha kwa watu waaminifu zamani nalo limetunzwa mpaka leo hii ili tupate kuongozwa.
39. (a) Ujumbe unaoonekana kama unatoka kwa wafu unatokana na nini hasa? (b) Ni nani aliye ‘baba wa uongo’?
39 Basi, namna gani ujumbe mwingine huo? Ingeweza kuwa kwamba unatoka kwa adui wa Mungu na mashetani wake badala ya kutoka kwa wazazi wetu waliokufa? Unadhani lingekuwa jambo lisilowezekana malaika hao wabaya kujigeuza au kujifanya kuwa watu waliokufa na kwa njia hiyo wadanganye watu? Kwa kuwa Shetani alijaribu kudanganya watu wawili wa kwanza juu ya mauti, je! hiyo isingekuwa njia yake ya ujanja (udanganyifu) ya kujaribu kutegemeza fundisho lake la uongo? Ndiyo, sana sana ikiwa tunakumbuka kwamba Biblia inamtaja Shetani kuwa “mwongo, na baba wa huo.”—Yohana 8:44.
40. (a) Tunaweza kukata shauri gani kutokana na 2 Wakorintho 11:14, 15? (b) Kulingana na 1 Timotheo 4:1, ni nani wanaoongoza mpango wa kudanganya?
40 Lakini labda utasema: ‘Basi, ni kwa sababu gani ujumbe mwingine kati ya huo unaonekana kuwa mzuri au wenye kusaidia, kama vile kuponya ugonjwa kupitia kwa mchawi au mganga?’ Mungu alimwongoza mtume Paulo ajibu ulizo hilo kwa vyepesi sana, akisema: “Wala si ajabu. Maana Shetani mwenyewe hujigeuza awe mfano wa malaika wa nuru. Basi si neno kubwa watumishi wake nao wakijigeuza wawe watumishi wa haki.” (2 Wakorintho 11:14, 15) Kwa wazi, mara nyingi mashetani wanajifanya kama wanasaidia ili wadanganye na kupoteza watu kwa vyepesi zaidi. Paulo anaonya zaidi juu ya mpango huo wa kudanganya kwa kusema: “Wengine watajitenga na imani, wakisikiliza roho zidanganyazo, na mafundisho ya mashetani.”—1 Timotheo 4:1.
41. Imetupasa kutazamia nini ikiwa ujumbe wa roho ungetokana na chanzo chema?
41 Ikiwa ujumbe wote huo wa roho ungetokana na chanzo chema, ungekuwa ujumbe mwema, sivyo? Kama Kristo Yesu alivyosema: “Ama ninyi watu mwufanye mti uwe mzuri na matunda yake yawe mazuri ama mwufanye mti kuwa mbaya na matunda yake yawe mabaya; kwa maana mti unajulikana kwa matunda yake.” (Mathayo 12:33, NW) Ni “matunda” ya namna gani tunayoona mara nyingi yakihusiana (yakikamatana) na mazungumzo hayo ya roho?
42. (a) Yaliyompata mjane katika Lisbon yanaonyeshaje lazima ya kujua mahali unakotoka ujumbe wa roho? (b) Je! Roho Mkuu, Yehova Mungu, anaogopesha watu?
42 Ebu mfikirie mjane fulani katika Lisbon, Ureno (Portugal). Mwanamke huyo alisoma vitabu vinavyosema mambo ya kupashana habari na roho zisizoonekana kisha akaanza kusikia sauti ikimwambia namna ya kuandika vitabu katika Kifaransa. Jambo hilo lilimpendeza naye akaendelea kupokea ujumbe huo. Lakini, baadaye alianza kusikia sauti zenye kuogopesha chumbani mwake usiku. Mara nyingine hata alijisikia kana kwamba nguvu isiyoonekana ilikuwa ikijaribu kumwangusha chini kutoka orofani. Lililoonekana kwanza kuwa lenye faida, sasa likawa jambo la kumwogopesha sana. Bila shaka wewe umepata kusikia watu wakisema kwamba wamepata mambo yanayofanana na hayo, labda kupata magumu yaliyo mabaya hata wakaanza kutafuta sana wasipate msaada. Lakini, hivyo ndivyo Roho Mkuu, Yehova Mungu anavyowatendea watu? Biblia inatuambia kwamba Mungu ni upendo na kwamba yeye anataka tumpende. (1 Yohana 4:8) Tena inasema katika 1 Yohana 4:18 kwamba tunaweza kumkaribia Yehova Mungu tukiwa na uhuru wa kusema kwa sababu “katika pendo hamna hofu; lakini pendo lililo kamili huitupa nje hofu . . . mwenye hofu hakukamilishwa katika pendo.”
43. Yehova anatufundisha tuonyeshe wengine nini, na hilo latokeza ulizo gani?
43 Kwa sababu yeye ni upendo, Roho Mkuu, Muumba wetu, anapendezwa sana na hali yetu njema. Anatufundisha tusiwe na choyo, tuwaonyeshe wengine upendo wa namna iyo hiyo ambao anatuonyesha sisi. Lakini mara nyingi tunaona nini kwa wale wanaozoea mambo ya uchawi?
KUPENDA FEDHA
44. Waganga wa kienyeji au wachawi wanapendaje fedha kinyume cha roho ambayo Yesu na wanafunzi wake walionyesha?
44 Ni mara ngapi umesikia waganga au wachawi wakitumikia watu bila malipo? Yesu aliwaambia wanafunzi wake hivi, “mmepata bure, toeni bure.” (Mathayo 10:7, 8) Je! hivyo ndivyo wanavyofanya wale wanaozoea mambo ya uchawi? Katika nchi moja ya upande wa kusini mwa Afrika mganga mmoja au mtu anayeponya kwa imani anafika nyumbani na kuinyunyizia majivu yaliyochangamana na dawa ya majani na maji, labda hata kutia alama za msalaba katika mlango na ‘kuichanja’ jamaa iliyomo kwa dawa hiyo. Je! hayo yanafanywa kwa kuonyesha hisani (wema), bila malipo? Hata kidogo, mahali pake, mganga huyo anamtoza (anamlipisha) mwenye nyumba hiyo fedha nyingi karibu mshahara wake wote kwa ulinzi huo unaodhaniwa kuwa unaweza kumzuia asiumizwe na roho zisizoonekana.
45. Waganga wa kienyeji wanatumia njia gani nyingine mahali fulani, ili wachume fedha?
45 Mahali pengine, waganga wanachukua vyombo fulani na kuvifanyia mambo ya uchawi. Kisha wanaviacha makusudi njiani ili watu wavichukue. Mara nyingi wanaofanya hivyo wanaogopa wakiisha kuvichukua vyombo hivyo kwamba wataumizwa sasa, nao wanawaendea waganga wakapate msaada. Lakini lazima walipe fedha ili wapate msaada huo, kwa hiyo waganga hao wanalipwa fedha. Unadhani inafaa kufanya hivyo?
46. Ni jambo gani lililompata Paulo katika Filipi? Kwa sababu gani?
46 Katika nyakati zinazotajwa na Biblia, pupa (tamaa mbaya) ii hii ilionyeshwa na watu waliokuwa wakifanya mambo ya uchawi. Alipokuwa bado yuko katika mji wa Filipi, mtume Paulo alisumbuliwa nyakati zote na mfanya kazi wa kike aliyekuwa na “pepo wa uaguzi.” Kisha Paulo akaliambia shetani ‘limtoke,’ nayo roho ya kishetani ikamtoka. Paulo alifanya hivyo bila malipo, wala hakuomba alipwe fedha. Lakini badala ya kufurahi, wale mabwana wa kijakazi huyo walikasirika wee, wakaagiza Paulo atupwe gerezani. Kwa sababu gani? Biblia inatuambia kwamba ni kwa sababu walikuwa wakipata “faida nyingi” kwa uaguzi wa kijakazi huyo.—Matendo 16:16-24.
UASHERATI
47, 48. Ni mazoea gani machafu yanayohusiana na roho mbaya?
47 Tumekwisha jifunza kwamba ni uzuri wa wanawake uliofanya wengine kati ya wana wa kiroho wa Mungu waache utumishi wake na matokeo yake wakawa waasi. Je! leo tunaona uasherati ukihusiana (kukamatana) na ibada ambayo watu wanazitolea roho mbaya zisizoonekana? Ni jambo la kawaida mahali pengine kusikia ikisemwa kwamba wanawake wakiwa kitandani wanasikia kuwapo kwa mtu fulani asiyeonekana kwa kiasi cha kwamba nyege zao zinaamka, kana kwamba mtu huyo asiyeonekana anafanya ngono pamoja nao.
48 Katika sehemu nyingine za ulimwengu, wanawake gumba (wasioweza kuzaa au tasa) wanaziomba roho mbaya zisizoonekana kupitia kwa mchawi ili wapate dawa ya kuwafanya waanze kuzaa. Lakini nyakati nyingine wanaambiwa wafanye ngono na “mganga” kama sehemu ya “dawa” yao.
49. Uasherati ulifanyiza nini kabla (mbele) ya Gharika, nao unafanyiza nini leo?
49 Wewe wadhani kwamba mambo hayo yanaleta mema au yanaweza kusaidia kuwe na jamaa zenye furaha na watu wenye furaha? Biblia inaonyesha kwamba wakati wana hao wa kiroho walipoasi kabla ya gharika kisha wakaanza kufanya uasherati, “dunia ikajaa na jeuri.” (Mwanzo 6:1-11, ZSB) Vilevile leo uasherati unaleta ugomvi, mapigano hata umwagaji wa damu.
MAUAJI NA UKATILI (UJEURI)
50. Yehova anaonaje uuaji?
50 Hakuna ye yote kati yetu anayetaka apoteze uhai wake mikononi mwa mwuaji. Biblia inaonyesha kwamba Yehova Mungu anachukia wauaji. Mojawapo ya Amri Kumi zake inasema hivi: “Usiue.” (Kutoka 20:13) Tunaona uhusiano (ukamatano) gani wa jambo hilo na kuzoea uchawi au kuabudu wazazi waliokufa (mizimu)? Yafikirie mambo haya:
51-54. Toa mifano ya uuaji unaohusiana (unaopatana) na uchawi.
51 Inakatazwa katika nchi zote kuua kwa sababu ya desturi ya ibada na kuwatoa wanadamu wawe sadaka. Lakini, wale wanaoabudu mizimu na waganga walio katika nchi fulani wangali wakiendelea na mazoea hayo yenye ukatili (ujeuri). Kwa mfano katika nchi ya Ghana, kulingana na desturi ya huko jumbe (sultani) mkuu anapokufa, anazikwa pamoja na mifupa ya vichwa vya watu wanaouawa na wauaji wakatili wa siri wanaofuata desturi hiyo ya ibada. Mwaka wa 1974 watu wawili walipatikana wakiwa na hatia ya uuaji wa kikatili wa kufuata desturi ya ibada wakati jumbe (sultani) mkuu alipokufa. Ijapokuwa ni marufuku, desturi hiyo inaendelea kwa kufuata imani inayotegemea uongo wa ibada ya mizimu wa kwamba nafsi za makafara hao (watu wanaouawa kama tambiko au sadaka) zinakwenda pamoja na jumbe (sultani) zikatumikie mahitaji yake huko “kuzimu.”
52 Katika Agosti 9, 1977, gazeti la huko Liberia linaloitwa The Liberian Age, lilikuwa na makala (tungo) kuu hii: “Mauaji ya Kikatili Kulingana na Desturi ya Ibada—‘Kikundi cha Waovu 11’ Chashtakiwa Kuwa na Hatia ya Uuaji Wakati Uchunguzi Unapoendelea.” Lilieleza kwamba wanaume 11, pamoja na wakuu fulani wa serikali wenye vyeo vikuu, walikuwa wamepewa mashtaka ya kumwua kikatili mtu mmoja katika mauaji ya desturi ya ibada, mtu huyo aliondolewa macho, akakatwa kabisa masikio, pua, makende na ulimi wake. Ripoti ilisema kwamba sehemu hizo za mwili zingekuwa hirizi (kamba ya dawa) za kusaidia washtakiwa hao wapate vyeo vya juu zaidi.
53 Taarifa ya habari kutoka Botswana Juni 8, 1977, inasema hivi: “Mganga [mchawi] ameonyesha leo kwamba, yule aliyekuwa mwanasiasa wa Botswana zamani alikuwa amempa orodha ya watu 18 aliokuwa akitaka wauawe kwa uchawi.”
54 Jambo ambalo ni baya hata zaidi ni kwamba vijana na watoto wameuawa. Ripoti itokayo Nigeria yasema hivi:
“Kupenda sana fedha sasa kumeongoza watu wa Nigeria wengi kufuata mazoea ya kishenzi ya kuiba vijana wakachinjwe katika pupa ya kutafuta fedha.
“Kwamba waganga fulani wa Nigeria wanaweza kugeuza vichwa vya wanadamu viwe fedha au sivyo, ni jambo lenye kutiliwa mashaka. Lakini jambo lisilo la kutiliwa mashaka ni la kwamba watoto wa Nigeria wanaibwa kwa kusudi hilo.”—Daily Times, Desemba 31, 1976.
55. Ijapokuwa huenda wengine wakadai kwamba uchawi una uzuri fulani, ushuhuda unaanyesha nini?
55 Bila shaka ikiwa wewe ni mtu anayethamini mema basi mazoea hayo yaliyotangulia kutajwa yatakufanya uchukizwe sana na vilevile usikitike kwa sababu ya mateso yanayofanyizwa. Bila shaka, umesikia mara nyingi watu wakitoa sababu ya kwamba uchawi una uzuri fulani. Kwa mfano, waganga wengi wanarudia-rudia kusema kwamba wanatumia hirizi, vitu vingine vya uchawi na ‘kuloga’ kwa makusudi mema tu. Hata hivyo, ye yote anayewatazama atakubali kwamba mara nyingi wanatumia vitu ivyo hivyo wawalaani wengine ili wapate fedha au zawadi fulani.
56, 57. (a) Kwa sababu gani imekupasa ufikirie jambo hilo kwa uangalifu? (b) Tutapata kweli wapi juu ya jambo hilo?
56 Yafaa sana ufikirie jambo hilo kwa uangalifu. Ijapokuwa huenda ukasikia watu wakisema kwamba mizuka (maajabu au pepo) inatokea, ujumbe wa roho zisizoonekana unapokewa na kuna ndoto zinazoelekea kuwa nzuri, Neno la Mungu lililoongozwa linatuonya kwamba Shetani na malaika zake wabaya wanatenda “kwa uwezo wote, na ishara na ajabu za uongo; na katika madanganyo yote ya udhalimu kwa hao wanaopotea.”—2 Wathesalonike 2:9, 10.
57 Kwa kukumbuka mambo hayo, sasa fikiria ambavyo Neno la Mungu linasema juu ya wachawi na waganga.
AMBAVYO BIBLIA INAONYESHA JUU YA WACHAWI NA WAAGUZI (WAPIGA RAMLI)
58. (a) Ni katika mataifa gani ambamo uchawi uliimarishwa sana karne nyingi zilizopita? (b) Hali katika Kanaani ilikuwaje wakati Waisraeli walipoishinda nchi hiyo? (c) Yehova alikuwa amekwisha wapa Waisraeli amri gani juu ya uchawi?
58 Biblia inafunua kwamba ilikuwa kawaida ya nchi kama Misri, Babeli na Kanaani kuabudu roho wabaya na kuzoea uganga au uchawi miaka mingi iliyopita. (Kutoka 7:10-12; Kumbukumbu la Torati 18:14; Isaya 47:1, 12, 13) Basi si jambo la kushangaza kwamba Yehova Mungu alipoliokoa taifa la Israeli katika utumwa wa Misri na kuwaingiza katika nchi ya Kanaani, walikuta wenyeji wa huko wamejitia sana katika mambo ya uchawi. Ni amri gani ambayo Yehova Mungu aliwapa watumishi wake? Aliwaambia waziwazi kwamba walipaswa wamwabudu yeye peke yake. Tunaweza kuona sababu gani jambo hilo lilifaa, kwa maana yeye ndiye Roho Mwenye Nguvu Zote, Mpaji wa uzima na kwa hiyo ni yeye tu anayestahili kuabudiwa kama Mungu wa kweli wa mbingu na dunia. (Kutoka 20:3-6) Kuzipa roho nyingine zisizoonekana ibada yake kungeonyesha kumdharau sana Muumba. Kwa sababu hiyo Mungu aliwaonya Waisraeli hivi: “Msiwaendee wenye pepo, wala wachawi; msiwatafute; ili kutiwa unajisi na wao.”—Mambo ya Walawi 19:31.
59. Sheria ya Yehova ilisema nini juu ya adhabu ya kuwapa wale wenye kuzoea uchawi?
59 Yehova Mungu aliwaonya Waisraeli kwamba wangekosa baraka na maisha zao vilevile, ikiwa hawangefuata katazo lake la kuabudu roho wabaya, akisema: “Na mtu yule atakayewaendea wenye pepo, na wachawi, ili kuzini pamoja nao, nitakaza uso wangu juu ya mtu yule, nitamtenga na watu wake. Tena mtu mume au mtu mke aliye na pepo, au aliye mchawi, hakika atauawa.”—Mambo ya Walawi 20:6, 27.
60, 61. (a) Basi Yehova anaonaje uchawi? (b) Unafanywa katika njia gani mahali penu?
60 Baadaye, Mungu aliongeza mkazo zaidi akionyesha namna anavyochukia mazoea ya uasi yanayohusiana na kuabudu roho mbaya zisizoonekana, kama vile uchawi na kupiga ramli, akisema kupitia kwa nabii Musa hivi: “Utakapokwisha kuingia katika nchi akupayo [Yehova] , Mungu wako, usijifunze kutenda kwa mfano wa machukizo ya mataifa yale. Asionekane kwako mtu ampitishaye mwanawe au binti yake kati ya moto, wala asionekane mtu atazamaye bao, wala mtu atazamaye nyakati mbaya, wala mwenye kubashiri, wala msihiri, wala mtu alogaye kwa kupiga mafundo, wala mtu apandishaye pepo, wala mchawi, wala mtu awaombaye wafu. Kwa maana mtu atendaye hayo ni chukizo kwa [Yehova].”—Kumbukumbu la Torati 18:9-12.
61 Je! hilo si jambo lililo wazi sana, na je! halionyeshi waziwazi namna Mungu Mwenye Nguvu Zote anavyowaona wachawi na wapiga ramli na ibada yao ya roho mbaya zisizoonekana? Kama Neno hilo lililoongozwa linavyosema, Yehova Mungu anachukia mazoea yote hayo hata yakiwa ya namna gani au yakipatikana katika bara (continent) gani. Yeye anatupa maonyo hayo kwa sababu ya upendo wake ili tusiumizwe na mabaya yanayoweza kuletwa na mazoea hayo.
62. Yesu na mitume wake walifanyiwa nini na roho zenye uovu?
62 Alipokuwa hapa duniani, Yesu Kristo alipingwa na adui ya Mungu, Shetani, pamoja na waasi wa kiroho waliojiunga naye. Shetani alipojaribu kumshawishi Yesu amwabudu ili apewe mamlaka na utukufu, Yesu alijibu hivi: “Kwenda zako, Shetani; kwa sababu imeandikwa [katika Biblia katika Kumbukumbu la Torati 5:9; 6:13], Uabudu [Yehova] Mungu wako, umutumikie yeye peke yake.” (Matayo 4:8-10, ZSB) Mara nyingi yeye na mitume wake vilevile walifukuza roho (pepo) wabaya au mashetani katika watu waliosumbuliwa nao.—Marko 1:39; 3:14, 15.
63. Ni jambo gani litakalowapata Wakristo wanaozoea uchawi?
63 Yesu alifundisha wanafunzi wake kumwabudu Roho Mwenye Nguvu Zote, Yehova Mungu peke yake, na kuliamini Neno lake, Biblia. (Yohana 4:23, 24; 17:6, 17) Wanafunzi wake walikuwa na maoni yale yale juu ya mambo ya uchawi na mazoea yake kama Yehova Baba yao wa mbinguni. Alipoongozwa na Mungu, mtume Paulo aliandikia waabudu wenzake habari hizi: “Basi matendo ya mwili ni dhahiri, ndiyo haya, uasherati, uchafu, ufisadi, ibada ya sanamu, uchawi. . . . nawaambia mapema . . . ya kwamba watu watendao mambo ya jinsi hiyo hawataurithi ufalme wa Mungu.” (Wagalatia 5:19-21) Muumba na Chanzo cha uzima wote hawezi naye hatawapa uzima wa milele watu wanaochukua ibada yake na kuzipa roho mbaya zisizoonekana kinyume cha Neno lake. Kama unabii ulio katika kitabu cha Ufunuo unavyosema, watu wanaoendelea kuwa kati ya “wachawi” bila kutubu, wataingia katika “mauti ya pili,” inayomaanisha uharibifu wa milele ambao hakuna kufufuka kutoka huko.—Ufunuo 21:8; 22:15.
64. (a) Biblia inaweka uchawi katika upande gani? (Tazama Wagalatia 5:19, 20.) (b) Ni roho ya namna gani ambayo ingeruhusu watu waiabudu na kuitumikia?
64 Ndiyo, Biblia inapanga uchawi kuwa mmojawapo wa “matendo ya mwili” pamoja na uasherati na uchafu. Tumekwisha ona ushuhuda mwingi unaoonyesha kwamba uchawi ni mchafu na unaumiza. Unaondoa ibada yetu na bidii yetu kwa Yeye aliye na haki ya kuwa nayo, yaani, Yehova Mungu. Kwa hiyo, roho yo yote isiyoonekana ambayo ingeruhusu watu waiabudu na kuitumikia haingeweza kuwa roho nzuri, bali ingekuwa roho mbaya au shetani. Mtume Yohana alisaidiwa na malaika aandike sehemu ya Biblia. Lakini wakati Yohana alipoanguka chini mbele ya malaika huyo ili amsujudie, malaika huyo mwaminifu alimwambia hivi: “Angalia, usifanye hivi; mimi ni mjoli wako na wa ndugu zako walio na ushuhuda wa Yesu. Msujudie Mungu.”—Ufunuo 19:10.
65. Ni roho ya namna gani ambayo ingeshirikiana na mwaguzi, mpiga ramli au mchawi?
65 Kwa kuwa Neno la Mungu linaonyesha kwamba kuwa mchawi au mtu anayepashana habari na wafu au mpiga ramli ni jambo ambalo Mungu anachukia, basi ni wazi kwamba roho yo yote isiyoonekana ambayo ingeshirikiana na watu hao ni roho mbaya au shetani vilevile. Ujumbe wo wote unaopokewa kutokana na chanzo hicho haungekuwa umetokana na Mungu wa kweli, Roho Mwenye Nguvu Zote, wala haukubaliwi naye.
66. Isaya alisema imetupasa tumwendee nani tupate kweli na tumaini hakika la wakati ujao?
66 Ndiyo maana kupitia kwa nabii wake Isaya, Mungu aliwaambia Waisraeli maneno haya ya kuonya: “Na wakati watakapokuambia, Tafuta habari kwa watu wenye pepo na kwa wachawi; waliao kama ndege na kunong’ona; je! haiwapasi watu kutafuta habari kwa Mungu wao? Je! waende kwa watu waliokufa kwa ajili ya watu walio hai?” (Isaya 8:19) Ikiwa tunataka tuijue kweli na kuwa na tumaini hakika juu ya wakati ujao, yatupasa tumwendee Mungu aliye hai, Muumba wa uhai wote, si kuwaendea wafu wala wachawi.
67. (a) Paulo alimwambia nini mchawi fulani? (b)Yehova anashauri nini juu ya kushiriki mazoea hayo machafu?
67 Vilevile, ndiyo maana wale wanaotenda matendo ya uchawi wanaupinga sikuzote ujumbe unaopatikana katika Neno la Mungu. Katika karne ya kwanza, alikuwako mchawi mmoja katika kisiwa cha Kipro (Cyprus) aliyezuia wengine wasiusikilize ujumbe wa habari njema ulioletwa na mtume Paulo. Paulo alimwambia hivi: “Ewe mwenye kujaa hila na uovu wote, mwana wa Ibilisi, adui wa haki yote, huachi kuzipotoa njia za [Yehova] zilizonyoka?” (Matendo 13:9, 10) Badala ya kuwa kati ya wale wanaozipotoa njia za Mungu zilizonyoka, imetupasa tuwe na nia ya kujitenga kabisa na ibada chafu ya roho wabaya, mazoea yaliyo kinyume cha Neno la Mungu. Mwito huu unatoka kwa Roho Mwenye Nguvu Zote: “Tokeni kati yao, mkatengwe nao, asema [Yehova], msiguse kitu kilicho kichafu.”—2 Wakorintho 6:17.
68. Ni ulizo gani linalojitokeza juu ya watu ambao wameshiriki namna fulani ya uchawi?
68 Labda unaona ni vigumu sana kwako kufanya hivyo. Labda uko kama wengine wengi waliokuwa wakiabudu mizimu (wazazi waliokufa) au kufuata mambo ya uchawi maisha yako yote. Labda watu wa ukoo wako na watu wengi mahali unapokaa wangali wakifuata mapokeo yanayokamatana na hayo, labda wangali wakidhani kwamba roho zinakaa katika miti fulani, miamba (mawe makubwa), mito, milima au mahali pengine. Basi, unawezaje kujitenga na ibada hiyo ya roho zisizoonekana upate kibali, ulinzi na baraka ya Roho Mwenye Nguvu Zote, Yehova Mungu?
KUJITENGA NA UWEZO WA ROHO WABAYA
69-71. Yule msichana nidogo katika Brazil alijitengaje na roho wabaya?
69 Mtu akiisha kushikwa au kuongozwa na roho wabaya, haitakuwa vyepesi kujitenga nao. Lakini, kwa msaada wa Yehova Mungu, inawezekana na imewezekana kwa maelfu ya watu. Mfano wenye kutia moyo ni msichana mdogo katika Brazil aliyeshikwa na roho wabaya na aliyeanza kuwaambia watu dawa za kuponya magonjwa yao. (Tazama fungu la 22.) Miaka iliyofuata, alipokuwa amelala usiku mmoja, alisikia nguvu fulani ikimvuta kutoka kitandani pake. Ijapokuwa alikuwa bado ana usingizi, alitoka nje kwenye shimo lililojaa maji. Ndipo alipojikwaa akaamka. Jambo hilo lilimsumbua sana hata akataka ajitenge na uwezo wa roho hizo mbaya zisizoonekana alizokuwa akipashana habari nazo. Alifanya nini?
70 Hatua ya kwanza ilikuwa kumwomba Mungu amwokoe. Kesho yake mtu fulani aligonga mlangoni pake. Akasikia “sauti” zikimwambia asifungue mlango, ya kwamba “Ibilisi alikuwa akimngojea” hapo. Lakini kwa kufanya sana bidii, aliufungua mlango. Mgeni huyo hakuwa Ibilisi bali kijana wa kiume aliyemtolea nakala ya gazeti la kusaidia kujifunza Biblia, yaani, Mnara wa Mlinzi. Ndani ya gazeti hilo mlikuwamo makala iliyokuwa ikisema juu ya kushikwa na roho wabaya. Akawa na hakika kwamba hilo lilikuwa jibu la sala yake ya bidii.
71 Alianza kujifunza Biblia na kuifuata kwa kugeuza maisha yake, si kujifunza tu bali vilevile kufanya mapenzi ya Mungu. Kidogo kidogo akaanza kujitenga na uwezo wa mashetani. Alifurahi kama nini kuona somo kubwa hili la Yesu likitimizwa kwake: “Mtaifahamu kweli, nayo hiyo kweli itawaweka huru.”—Yohana 8:32.
72. Yule mjane katika Lisbon alifanya nini ili ajitenge na roho zenye uovu?
72 Hivyo ndivyo ilivyokuwa na mjane aliyekuwa katika Lisbon, tuliyetangulia kumtaja. (Tazama fungu la 42.) Wakati uhusiano wake na roho mbaya zisizoonekana ulipoanza kumsumbua sana hata kumwogopesha kitambo kidogo tokea hapo alifikiwa na Mashahidi wa Yehova akaanza kujifunza Biblia pamoja nao. Alijifunza mambo ambayo Biblia inasema juu ya hali ya kweli ya wafu, tumaini la kufufuka na habari njema zenye utukufu za ufalme wa Mungu. Alipofahamu kwamba wengine wengi sana kama yeye katika sehemu zote za dunia walikuwa wamedanganywa na mashetani, alimwamini Roho Mwenye Nguvu Zote, Yehova Mungu, akavunja uhusiano wote na roho mbaya hizo zenye kupoteza.
73. Kwa sababu gani mamilioni ya watu wasiohusiana (wasiopatana) moja kwa moja na uchawi wanahitaji (wanataka) kuijua kweli juu yake?
73 Ndiyo, watu wengi sana kuzunguka dunia wamefunguliwa macho waione kweli juu ya ulimwengu wa roho. Lakini si watu wote wanaosumbuliwa kama hao waliotangulia kutajwa. Mamilioni ya watu wasio wachawi na wasiopata kusikia wenyewe “sauti” za roho wabaya wasioonekana, wangali wanahitaji kugeuka “waziache nguvu za Shetani na kumwelekea Mungu.’ (Matendo 26:18) Kwa sababu gani hivyo? Kwa sababu katika maisha yao ya kila siku wanahangaishwa na mambo kama ndege mbaya (mkosi), “jicho baya,” kushika miiko (vitu vinavyokatazwa kutumiwa), na hirizi za kutoa ulinzi na sherehe zinazohusiana na ibada ya roho wabaya kuliko ibada ya Mungu wa kweli, Muumba mwenye nguvu zote wa mbingu na dunia.
74. Watu wengi wanahitaji (wanataka) kuokolewa na mtego gani?
74 Kama utando wa buibui unaotatanisha (unaotega) na kumshika inzi au kiumbe kingine kinachoingia humo, vivyo hivyo kuna mtego wa mapokeo na desturi za kijamaa na kikabila unaowashika watu wengi katika hali ya woga. Wanaogopa kwamba, wasipoyashika mapokeo yote kayo, hawatapokea msaada kutoka kwa mizimu (wazazi waliokufa) au kwamba wataumizwa na roho nyingine mbaya zisizoonekana. Wanaogopa kwamba watakosa kuzaa watoto au kwamba watoto wao watakufa, au kwamba ng’ombe zao zitapata ugonjwa na kufa, kwamba mashamba yao hayatazaa mazao au kwamba biashara zao hazitasitawi.
75. Inawapasa watu wamwendee nani ili wapate msaada?
75 Kweli ya Neno la Mungu peke yake ndiyo inayoweza kuwaweka huru. Kwa kujifunza yanayosemwa na Neno lake, wanaweza kufahamu kwamba ziko roho mbaya zisizoonekana zinazoshirikiana na wachawi na waganga lakini hazina uwezo wa kushinda uwezo wa Mungu wa kweli. Watu wanaoona kwamba msaada wa Mungu ni bora sana kuliko msaada unaotokana na chanzo kingine, wanafahamu kwamba umizo ambalo mchawi, mganga ye yote au roho mbaya yo yote isiyoonekana ingeweza kujaribu kuwaletea, halingekuwa lenye kuharibu sana kama vile kukosa kibali na baraka ya yeye peke yake aliye Chanzo cha uzima.—Mathayo 10:28.
76. (a) Basi ni hatua gani iliyo ya kwanza katika kujitenga na ibada ya roho wabaya? (b) Sasa kunatokea maulizo gani?
76 Kwa hiyo, hatua ya kwanza ya kuelekea kutoka katika utumwa huo ni kupata kumjua Mungu wa kweli. Tunajua habari za hali ya kweli ya wafu kwa kujifunza Neno la Mungu, ya kwamba wamelala usingizi katika mauti, hawana fahamu na kwamba hawawezi kuonyesha upendo wala chuki, wala kutoa msaada wala kuumiza watu. Tunafahamu vilevile namna walivyo wale wanaokaa katika ulimwengu wa roho na ya kwamba wana wengi wa kiroho wa Mungu waliasi. Lakini ni kwa sababu gani Mungu ameruhusu roho hizo zenye uasi ziendelee mpaka sasa?
77. Katika kumwasi Mungu, je! Shetani na malaika zake wabaya walitilia shaka nguvu za Mungu?
77 Ni kwa sababu uasi huo ulileta mashaka juu ya Yehova Mungu. Shetani na malaika zake wabaya hawatilii shaka nguvu za uweza wa Mungu, maana wanajua kwamba yeye ni mwenye nguvu kuwashinda naye ana nguvu za kuwaharibu. Tunasoma hivyo katika Biblia katika Yakobo 2:19: “Wewe waamini ya kuwa Mungu ni mmoja, [sivyo?]; watenda vema. Mashetani nao waamini na kutetemeka.” Wanatetemeka kwa sababu wanajua kwamba Yehova ametangaza kusudi lake la kuwaharibu. Yesu Kristo kama mjumbe wa Mungu alipokuwa karibu kuwaokoa watu fulani katika nguvu za mashetani, mashetani hao walilia kwa sauti kuu wakiuliza wajue ikiwa alikuwa amekuja ‘kuwaangamiza kabla ya wakati wao.’ (Mathayo 8:29; Marko 1:24) Kwa hiyo wana hao wa kiroho walioasi wanajua kwamba hawana uwezo wa kushindana na Mungu Mwenye Nguvu Zote.
78. (a) Ni jambo gani ambalo Shetani alitilia shaka? (b) Ni shaka gani jingine lililotokezwa, na ni mfano gani tunaopata katika Biblia kuonyesha hivyo?
78 Jambo ambalo Shetani alifanya ni kutilia mashaka uhalali (haki) wa utawala wa Mungu juu ya viumbe Vyake vyote. Maneno aliyomwambia Hawa yanaonyesha kwamba yeye anajaribu kusadikisha watu kwamba Mungu si Baba mwenye upendo anayependezwa sana na hali njema ya viumbe vyake. Kujiunga kwa watu wa kwanza wawili katika uasi kulitokeza vilevile shaka jingine. Shaka hilo lilikuwa juu ya kama wengine wote kati ya viumbe vya Mungu wangeweza kushawishwa wamwepuke Mungu na kumtumaini mwingine. Tunaweza kufahamu jambo hilo kwa habari ya Ayubu mtumishi wa Mungu. Shetani alidai kwamba Ayubu angemtumikia Yehova Mungu wakati usio wa taabu tu. Lakini ikiwa Ayubu angelazimika kupata taabu na mateso, hapo angeacha kumwamini Mungu na kumwepuka.—Ayubu 1:7-12; 2:4, 5.
79. (a) Kungetakiwa nini ili mashaka hayo yaondolewe kabisa? (b) Ni rani linalotukia katika wakati ambao Shetani amebaki nao?
79 Ingetaka wakati mwingi ili mashaka yote hayo yaondolewe kabisa. Basi, hata ingawa watu wale wa kwanza wawili walikuwa wameasi, Yehova Mungu aliwaruhusu waishi kwa muda fulani wazae watoto. (Mwanzo 3:14-19) Amemruhusu Shetani na malaika zake wabaya wakati ili wajaribu kuonyesha ukweli wa upande wao wa shindano kuu. Vilevile ameruhusu wanadamu wakati ili wajaribiwe kama watamwamini Mungu Aliye Juu Zaidi ama watamwepuka kwa sababu za kichoyo. Ni kweli kwamba karibu miaka 6,000 imepita tangu shaka hilo lilipoanza kutokezwa katika Edeni. Lakini Biblia inatuambia kwamba, kwa Mungu wa Milele, “miaka elfu ni kama siku moja.” (2 Petro 3:8) Basi Kwake miaka hiyo elfu sita ni kama siku sita tu. Neno la Mungu linaonyesha kwamba wakati huo unamalizika na kwamba sasa Shetani ana “ghadhabu nyingi, akijua ya kuwa ana wakati mchache tu” unaobaki mpaka Mungu achukue hatua ya kumaliza uasi huo.—Zaburi 90:2, 4; Ufunuo 12:12.
CHUKUA HATUA (AMUA) SASA UKIWA NA IMANI YOTE
80. Sababu gani unaweza kuwa na hakika ya kupata msaada unapomwomba Yehova?
80 Kwa sababu ya uvumilivu, subira na rehema ya Mungu, kila mmoja wetu anapewa nafasi ya kuonyesha upande wake na mtu ambaye atatumaini. Ukitaka uokolewe katika utumwa wa roho mbaya zisizoonekana na mtego wa mapokeo na sherehe zinazowatia watu katika utumwa huo, basi usikawie kutafuta msaada kwa Yehova sasa, “Mungu mwingi wa huruma, mwenye fadhili . . . mwingi wa rehema na kweli.” (Kutoka 34:6) Yesu Kristo, mjumbe wa Mungu alifundisha wafuasi wake kusali hivi: “Utuokoe na yule mwovu.” (Mathayo 6:13) Unaweza kuwa na hakika kwamba Yehova anasikia sala zinazotokana na moyo safi. “Macho ya [Yehova] huwaelekea wenye haki, na masikio yake husikiliza maombi yao.”—1 Petro 3:12; Mithali 15:29.
81. Inakupasa uchukue hatua gani ili ujitenge na mambo ya uchawi? Kwa sababu gani?
81 Vilevile ukiwa na moyo mnyofu, utaunga mkono maombi yako unayomtolea Mungu kwa kutenda kupatana na mambo unayoomba. Jambo hilo lina maana gani kwa habari ya mapokeo na sherehe zinazokamatana na uchawi? Mtume Paulo aliyeongozwa na Mungu anaandika hivi: “Sipendi ninyi kushirikiana na mashetani . . . hamwezi kushirikiana katika meza ya [Yehova] na katika meza ya mashetani.” (1 Wakorintho 10:20, 21) Kwa kuwa Yehova Mungu ana uadui na mashetani, yatupasa tuchague kati ya kuabudu Mungu na kuabudu mashetani. Ikiwa tunataka kufanya urafiki na Yehova na ulinzi wake, yatupasa tujitenge kabisa na mambo ya uchawi katika namna take nyingi. Jambo hilo linatia ndani kutupa vyombo vyo vyote vinavyohusiana na uchawi. Vyombo hivyo vingekuwa njia ya kutuweka katika utumwa na katika mtego wa nguvu ya mashetani. Kutupwa au kuharibu vyombo hivyo ni hatua ya maana kuelekea kujitenga na nguvu hiyo.
82. Neno la Mungu linaonyeshaje kwamba haitupasi tuogope kitu cho chote kama sanamu?
82 Neno la Mungu ni msaada mkubwa vilevile katika jambo hilo, maana laweza kutupa uhodari wa kuchukua hatua hiyo. Linatuonyesha sababu gani haitupasi tuviogope vyombo hivyo, hata ingawa watu wengine wanaviona kama hirizi au kama vina nguvu fulani ya ajabu. Yehova Mungu alitoa maneno haya yenye kutia moyo kupitia kwa nabii wake Yeremia: “Msifuate njia za mataifa . . . Kwa maana sanamu za kuchongwa za mataifa ni uongo mtupu, si kitu bali ni mbao inayokatwa kutoka msituni, inayofanywa na fundi kwa patasi yake; anaipamba kwa fedha na dhahabu, akizikaza kwa nyundo na misumari ili zisiachane. Haziwezi kusema kuliko sanamu inayowekwa kutisha ndege katika shamba la matango; ni lazima zichukuliwe, maana haziwezi kutembea. Usiziogope: haziwezi kudhuru, nazo hazina nguvu ya kutenda mema.” (Yeremia 10:2-5, New English Bible) Mtoto mdogo anaweza kuogopa sanamu inayowekwa kutisha au kufukuza ndege shambani, lakini mtu mzima anajua zaidi. Neno la Mungu linaonyesha kwamba, kama vile sanamu ya mtu inayowekwa kufukuza ndege shambani isivyoweza kusema wala kutembea wala kutoa msaada wala kumwumiza mtu, ndivyo zilivyo sanamu ambazo wanadamu wanafanya kisha wakaziita takatifu.
83. Biblia inaonyeshaje upumbavu wa mtu kuabudu cho chote kinachofanywa kwa mikono ya wanadamu?
83 Biblia inaonyesha upumbavu wa watu wanaotegemea vitu vinavyofanywa kwa mikono ya wanadamu kana kwamba vingeweza kuwa na nguvu kushinda wanadamu. Kwa mfano, unabii wa Isaya ulioongozwa na Mungu unatuambia habari za mtu anayekata mti mkubwa kutoka msituni, sehemu yake anaichukua awashe moto na kuoka mkate kisha sehemu inayobaki anaitumia kufanyiza sanamu naye “husujudu mbele yake akaiabudu, akaiomba, akasema, Uniokoe; maana wewe u mungu wangu. Hawajui wala hawafikiri; maana amewafumba macho, wasione, na mioyo yao, wasiweze kufahamu. Wala hapana atiaye moyoni, wala hapana maarifa, wala fahamu kusema, Nimeteketeza sehemu motoni, naam, pia nimeoka mkate juu ya makaa yake; nimeoka nyama nikaila; nami, je! kilichobaki nikifanye kuwa chukizo? Je! nisujudie shina la mti? Hula majivu . . . asiweze kuiokoa nafsi yake, wala kusema, Je! sio uongo mkononi mwangu?”—Isaya 44:14-20.
84. (a) Je! kipande cha mti, nguo au uzi to kinaweza kutusaidia au kutuumiza? (b) Ni nini kinachoweza kutuumiza sana?
84 Mti ni mti hata ikiwa wanadamu wanafanya sana bidii kuutengeneza. Ndiyo sababu sanamu ya mti yaweza kuteketezwa na kuharibiwa sawasawa na kipande kingine cho chote cha mti. Haiwezi kujilinda isiharibiwe. Vivyo hivyo na nguo au uzi au matope au jiwe au mbegu au cho chote kinginecho ambacho wanadamu wanaweza kutumia kuwa chombo cha matumizi ya kuabudu roho wabaya. Vyote hivyo vyaweza kuharibiwa katika njia moja au nyingine. Ikiwa vitu hivyo haviwezi kujilinda vyenyewe, bila shaka haviwezi kulinda wengine. Lakini umizo kubwa linatokana na kuamini vitu hivyo na kwa njia hiyo, kuruhusu roho chafu, mashetani wadanganyifu watutie katika utumwa wa vitu ambavyo ni uongo na bure kabisa. Neno la Mungu linatuonyesha njia ya kujiokoa na uongo huo.
85. Wakristo fulani katika Efeso walifanya nini?
85 Biblia inatuambia habari za watu waliokuwa na imani na uhodari wa kuharibu mali fulani zilizohusiana na uchawi, ijapokuwa walifanya hivyo kwa hasara kubwa. Baada ya kusimulia kazi ya kutoa ushuhuda juu ya Mungu wa kweli iliyofanywa na mtume Paulo katika mji wa Efeso, kitabu cha Biblia cha Matendo kinaeleza hivi: “Na watu wengi katika wale waliotumia mambo ya uganga wakakusanya vitabu vyao, wakavichoma moto mbele ya watu wote; wakafanya hesabu ya thamani yake, wakaona ya kwamba yapata fedha hamsini elfu.” (19:19) Fikiri namna huo ulivyokuwa utajiri! Hata hivyo, kuwa na kibali ya Mungu Mwenye Nguvu Zote na kuokolewa katika nguvu ya mashetani kulikuwa na maana kubwa sana kwao kuliko kitu kilichofananishwa na fedha hizo.
86. (a) Matokeo ya hayo yalikuwa nini? (b) Imekuwaje vivyo hivyo leo kati ya watu wengi?
86 Sababu gani usitazame huku na huku katika nyumba yako ujiulize mwenyewe ikiwa unaonyesha imani ile ile na kufuata mfano huo, kuondoa cho chote kinachohusiana na ibada ya roho wabaya? Matokeo ya kufanya hivyo katika Efeso yalikuwa yenye kutia moyo sana: “Hivyo ndivyo neno la [Yehova] lilivyozidi na kushinda kwa nguvu.” (Matendo 19:20) Ndivyo imekuwa hata leo kati ya maelfu ya watu ambao wameacha mambo ya uchawi wakamwelekea Mungu wa kweli na ibada yake. Nguvu za kweli ya Neno la, Mungu imewaongoza wakusanye vitabu vyote, hirizi zote, talasimu (dawa) zote, vikuku vyote, nyuzi zote za ulinzi, mavazi yote na kila chombo kinachohusiana na uchawi, wakaviharibu.
87. Mwanamke katika sehemu ya kusini ya Afrika alifanya nini, nayo matokeo yalikuwa nini?
87 Kwa mfano, mwanamke mmoja katika sehemu ya kusini ya Afrika aliyekuwa mchawi aliukubali msaada uliotolewa na mmoja wa Mashahidi wa Yehova ajifunze Biblia. Waliposoma pamoja habari ya Biblia iliyotangulia kutajwa, inayosimulia namna watu wenye mioyo minyofu katika karne ya kwanza walivyoviharibu vitabu vyao vyenye mambo ya uchawi, mwanamke huyo ikiwa ingempasa naye afanye vivyo hivyo. Yule Shahidi alionyesha namna jambo hilo lingeweza kuleta kibali ya Mungu, nao walipatana tarehe ya kufanya hivyo. Shahidi alipofika, alikuta mwanamke huyo akiwa tayari na mavazi yake yote ya kidini na vyombo vyote vya uchawi pamoja na mafuta ya taa. Waliwasha moto wakaviteketeza vyombo vyote. Matokeo yalikuwa nini? Mwanamke huyo aliokolewa katika nguvu ya mashetani naye sasa analifurahia pendeleo lenye maana la kusaidia wengine wamtumaini Mungu wa kweli.
88. Mwanamume wa jimbo lile lile alijitengaje na ibada ya roho wabaya?
88 Hali kama hiyo ilitukia, mwanamume mmoja katika jimbo lile lile alikuwa ameanza kupokea mafundisho pamoja na mganga mashuhuri (mwenye kujulikana sana), naye alikuwa amefanya maendeleo ya haraka, akiwa msaidizi mkuu wa mwalimu wake wa mambo ya uchawi. Walakini, mke wa mwalimu huyo alianza kujifunza Biblia pamoja na Mashahidi wa Yehova. Siku moja msaidizi huyo alihudhuria funzo. Maandiko yalizungumzwa yakionyesha kwamba Mungu anakataza kunywa au kula damu. (Mambo ya Walawi 17:10-14; Kumbukumbu la Torati 12:23, 24; Matendo 15:20, 29) Jambo hilo lilimstaajabisha sana mwanamume huyo. Alikuwa karibu ‘kuhitimu’ (kumaliza) mafundisho yake ya “dawa” na uganga, naye alijua kwamba kunywa damu kulikuwa sehemu ya sherehe ya “kuhitimu.” Sasa aliamua kufanya nini? Alitaka kumpendeza Yehova, Chanzo cha uzima wote, badala ya kujaribu kupendeza roho mbaya zisizoonekana na zenye upinzani. Basi aliacha mara hiyo kujizoeza mambo ya uchawi, akazidi kujifunza Biblia pamoja na Mashahidi wa Yehova na sasa anafurahia kuokolewa kwake katika utumwa wa roho zenye choyo zisizoonekana.
89. Ni hatua gani za lazima zinazopaswa zichukuliwe ili upate ushindi juu ya roho mbaya zisizoonekana?
89 Ili ujitenge na roho mbaya hizo zisizoonekana, ni lazima ‘udumu katika kusali’ si kumwomba Yehova Mungu msaada tu. (Warumi 12:12) Neno la Mungu linaonyesha kwamba ni lazima, si kuacha mazoea ya uchawi tu, bali vilevile kuviondoa vyombo vyo vyote vya uchawi ambavyo vingeendeleza uhusiano wako na ibada ya roho mbaya zisizoonekana. Tena, ili upate ushindi na uhuru unaotokana nao, yakupasa uwaombe wengine msaada ili usipate kupigana na maadui wa kiroho ukiwa peke yako.
KUSHIRIKIANA NA WATUMISHI WA MUNGU WA KWELI
90. Sababu gani ni jambo la maana kushirikiana na watu wa Mungu?
90 Biblia inatusihi tukutane pamoja na wengine ili tujengane katika upendo na imani. (Waebrania 10:24, 25) Unaweza kukutana pamoja na nani? Ijapokuwa wafuasi wa makanisa ya Jumuiya ya Wakristo wanajidai kuiamini Biblia wanakuwa mara nyingi kati ya wale wanaokwenda kutafuta msaada kutoka kwa wachawi na waganga katika sehemu mbalimbali za dunia. Walakini, Mashahidi wa Yehova wako tofauti. Wanajiepusha kabisa na cho chote ambacho kingeweza kuwaongoza kwenye kupagawa (kushikwa) na roho mbaya zisizoonekana zinazopingana na mafundisho ya Neno la Mungu. Wanafurahia kusaidia mtu ye yote ajifunze Biblia na kujua kweli yake inayotoa uhuru. Wanafanya hivyo pasipo malipo kwa kufuata mfano wa Yesu na wanafunzi wake. Watafurahi kukusaidia upate majibu ya maulizo yako kwa kujifunza hivyo pasipo malipo.
91, 92. Kuhudhuria mikutano ya Mashahidi wa Yehova kutaleta faida gani?
91 Wanakutana vilevile kwa kawaida ili wajifunze maandishi yaliyoongozwa ya Neno la Mungu wakiwa kikundi. Hata mikutano hiyo ni ya pasipo malipo, hakuna kuombwa kulipwa viingilio. Ni msaada mkubwa kuhudhuria mikutano hiyo ili uendelee kupigana vita ambavyo mtume Paulo anaandika habari zake anaposema hivi: “Sisi tunako kushindana mweleka . . . juu ya majeshi ya roho yenye uovu katika mahali pa kimbinguni.” Ndipo mtume anapoendelea kutusihi sote ‘tuvae silaha kamili kutoka kwa Mungu,’ na ‘kusimama imara, . . . viuno vikiwa vimefungwa kweli, na kuvaa bamba la haki la kukinga kifua, . . . ngao kuu ya imani, . . . kofia ya wokovu, na upanga wa roho, yaani, Neno la Mungu.’—Waefeso 6:12-17, NW.
92 Inaweza kuchukua wakati fulani ili ujue namna ya kutumia vya kufaa silaha hizo zilizo kamili na “upanga wa roho.” Lakini kushirikiana na wengine ambao wamepata, nao wanapata ushindi katika vita yao ya kiroho kutakusaidia ufanye maendeleo mazuri. Imani yako itaongezeka wakati unapozidi kujifunza habari za makusudi ya Muumba wa Ulimwengu Wote na Mtawala, Yehova Mungu, na kufahamu hekima ya sheria na matakwa yake ya haki. Utapata tumaini la ajabu la uzima katika dunia ya paradiso, ambamo wapole wa dunia watafurahia uzima usio na mwisho, bila magonjwa na maumivu, chini ya ufalme wa Mungu kupitia kwa Kristo Yesu. Utajifunza namna unavyoweza kuwa kati ya wale watakaoishi wauone wakati Mungu ‘atakapofuta kila chozi katika macho yao.’—Ufunuo 21:4; Zaburi 37:10, 11; Mathayo 5:5.
93. Ni geuzo gani la utu linalotakiwa?
93 Ili tusiendelee kutawalwa na roho zenye choyo zisizoonekana, yatupasa tulifuate shauri la Biblia “mvue kwa habari ya mwenendo wa kwanza utu wa zamani,” “mkavae utu mpya, ulioumbwa kwa namna ya Mungu katika haki na utakatifu wa kweli.” (Waefeso 4:22-24) Labda mwenendo wetu wa zamani haukuongozwa na mapenzi ya Mungu, bali na mapokeo ya wanadamu na desturi za watu walio katika eneo letu. Yatupasa tuchunguze mwenendo wetu tuone kwamba tunaepuka mambo yote yanayohusiana na ule uongo wa mashetani wa kwamba wafu wanaweza kuwasaidia au kuwaumiza walio hai.—2 Wakorintho 13:5.
ENDELEA KUPIGA VITA VIZURI VYA IMANI
94. Tukiisha kujitenga na imani ya mashetani, tunapaswa tufanye nini ili tuendelee kuwa huru?
94 Ukiisha kujiepusha na imani ya mashetani, inakupasa upige sana vita ili uendelee kuwa huru. Yesu alisema kwamba “mwenye kuvumilia hata mwisho, [huyo peke yake] ndiye atakayeokoka.” (Mathayo 24:13) Yatupasa kila siku tuzidi kupinga jitihada za kutaka kuturudisha katika mtego wa mapokeo na mazoea ya mashetani yatakayotunyang’anya baraka ya Mungu.
95. Ni njia gani ambazo mara nyingi Shetani anatumia ili atufanye tusiwe na nguvu?
95 Shetani na malaika zake wabaya wanaweza kutumia njia mbalimbali za kujaribu kutufanya tuwe dhaifu. Huenda wakatumia watu wa ukoo au rafiki watupinge. Inatokea mara nyingi kama Yesu alivyotangulia kusema: “Adui za mtu ni wale wa nyumbani mwake.” (Mathayo 10:36) Ikiwa unataka kujiepusha na mazoea yote ya mashetani ili uonyeshe kwamba unampenda Mungu na kufuata amri zake hata watu wengine waseme na kufanya nini, fikiria sasa machache kati ya majaribu mengi yanayoelekea kumpata mtu.—1 Yohana 5:3; Wakolosai 2:8.
MTU ANAPOKUFA
96, 97. (a) Ni desturi gani ya mazishi (maziko) inayohusiana sana na ibada ya mashetani? (b) Wakristo wanaonaje mazishi?
96 Ni kawaida katika sehemu za Afrika kufanya mpango wa “makesha” wakati mtu anapokufa. Watu wa ukoo na rafiki wanakusanyika katika nyumba ya marehemu au katika “nyumba ya jamaa” hiyo. Kunatokea maombolezo, kuimba, kupiga ngoma, kunywa na kufanya mazoea mengine kulingana na desturi ya mahali. Mara nyingine marehemu (mtu aliyekufa), akiwa ameoshwa na kuvikwa mavazi yake yaliyo bora anafanyiwa sherehe kuu kanisani au mahali pa hadhara (pa watu wengi) ambapo rafiki na watu wa ukoo wanapoandamana wakilipita jeneza (sanduku la mfu) ili wamtazame mara ya mwisho kabla hajazikwa.
97 Ni kawaida ya watu kuhuzunika akiisha kufa rafiki au mtu wa ukoo. Yesu alihuzunikia kufa kwa Lazaro rafiki yake hata akatoa machozi. (Yohana 11:33, 35) Walakini, machozi ya huzuni ya kweli yako tofauti na kuomboleza na kulia kunakofuatana kwa kawaida na mazishi mengi katika nchi fulani. Ni kawaida kulia, hata kwa kiasi cha kutoa sauti anapokufa mpendwa wetu. (2 Samweli 1:11, 12) Walakini, kulia na kupiga mayowe (makelele) kwa kuogopa kukasirisha roho mbaya zisizoonekana (mizimu), au kwa sababu ya kuogopa washiriki wengine wa jamaa, ni kinyume cha Neno la Mungu. Mara nyingi maneno yanayotamkwa wakati wa kuomboleza na kuimba yanamtaja marehemu au wazazi wengine waliokufa (mizimu) katika sala au kuomba. Kwa kweli makesha mengine yanafanywa kwa kuogopa kabisa watu waliokufa. Basi ijapokuwa si vibaya kwa mtu anayemwogopa Yehova kuhudhuria mazishi, yafaa kulikumbuka shauri la ‘kujitenga wenyewe na kutokugusa kitu kilicho kichafu.’ (2 Wakorintho 6:17) Tunaweza kutafuta njia za kuonyesha kusikitika kwetu na kutoa faraja pasipo kushiriki tendo lo lote linalohusiana na ibada ya roho mbaya. Vilevile, haiwapasi watu wa Yehova wajiruhusu washindwe na huzuni, kwa maana wanalo tumaini la ufufuo. Ndiyo sababu Biblia inasema hivi: “Lakini, ndugu, hatutaki msijue habari zao waliolala mauti, msije mkahuzunika kama na wengine wasio na matumaini.”—1 Wathesalonike 4:13.
98. Ni desturi gani nyingine ambazo vilevile zaweza kuhusiana na imani ya mashetani?
98 Bila shaka, desturi zinazohusiana na mauti, mazishi na vizuizi (miiko) vinavyokuwa juu ya watu wa ukoo wanaobakia zinatofautiana sana kulingana na imani na mapokeo ya mahali. Lakini mara nyingi sana zinategemea imani ya kwamba wafu wanaweza kuwaona walio hai, nazo zina mazoea mengi yaliyo kinyume cha Neno la Mungu. Mtumishi wa kweli wa Mungu hangetaka ajichafue mwenyewe na mazoea hayo. Katika maeneo fulani ya humu Afrika, kila mwaka baada ya mtu kufa, sherehe za pekee zinafanywa ‘ili kumrudisha marehemu (mfu) nyumbani.’ Watu wanaamini kwamba wakati wa kufa nafsi haiendi mara hiyo kwenye ‘ulimwengu wa roho’ bali inakaa bila kufanya lo lote mpaka sherehe ya pili ifanywe kisha yaweza kuingia katika ‘nchi ya roho.’ Mahali pengine mara nyingi mnyama anachinjwa na vinywaji vinatolewa katika mazishi (maziko) ili kutambikia (kutolea sadaka) wazazi waliokufa (mizimu). Wafuasi wa makanisa ya Jumuiya ya Wakristo na vilevile Waislamu wanashiriki sherehe hizo.
99, 100. (a) Sababu gani imewapasa Wakristo wajiepushe na vipindi hivyo? (b) Yehova hawezi kukubalia nini?
99 Walakini, jambo la maana ni lile ambalo Neno la Mungu linasema juu ya mazoea hayo. Kwa mfano, linasema katika Zaburi 106:28, 29 juu ya Walsraeli wasioaminika waliofuata ibada ya uongo kisha wakaanza ‘kuzila dhabihu za wafu.’ Linaonyesha kwamba “wakamkasirisha” Mungu kwa matendo hayo, wakapoteza kibali yake. Tumekwisha jifunza katika Biblia kwamba mtu anapokufa, ni Mungu peke yake anayeweza kumfanya mtu huyo aishi tena kwa kufufuliwa.—Tazama mafungu 33 kufika 36.
100 Ndiyo, vifo, mazishi, ndoa, mimba, uzazi, kutahiriwa, vyote hivyo ni vipindi vya kujihadhari (kuepukana) navyo. Neno la Mungu linaonya hivi: “Amkeni! iweni macho! Adui yenu ibilisi, akiwa kama simba anayenguruma, anazunguka-zunguka akitafuta mtu fulani amtafune.” (1 Petro 5:8, New English Bible) Ni jambo jepesi sana kushindwa na mkazo kisha uvae “dawa” kidogo kama vile hirizi. Lakini mtu anayetaka kibali ya Mungu atakumbuka kwamba Yehova ni “Mungu mwenye kutaka ibada ya pekee.” (Kutoka 20:4-6, NW) Yeye hakubali ibada ya uongo inayotegemea uongo wala hatabariki wo wote wa watumishi wake wakiwa na “uvuguvugu” juu ya amri zake.—Ufunuo 3:16.
NYAKATI ZA UGONJWA
101. Ni hatari gani inayoweza kuwa katika dawa za kienyeji?
101 Katika nyakati za ugonjwa watu wengine wamejaribu madaktari na hospitali nyingi wasipate kupona. Labda wengine wanaweza kudhani kwamba imewapasa sasa watafute dawa za miti-shamba, yaani, watafute msaada wa mganga anayetoa dawa. Wengi kati ya waganga hao wa kienyeji wanatumia dawa za miti-shamba na dawa nyingine za asili ambazo huenda zenyewe zikawa si mbaya. Lakini hatari ni ya kwamba huenda waganga hao wa kienyeji wanaotumia dawa za miti-shamba wakachanganya mambo ya uchawi pamoja na dawa za miti-shamba wanazotumia. Katika Biblia, neno hili “spiritism” (“uchawi”) kama linavyopatikana katika Biblia ya Kiingereza ya New World Translation katika Ufunuo 21:8, linatokana na neno la Kigiriki phar·ma·kiʹa, ambalo maana yake halisi ni “matumizi ya dawa.” Ni kwa sababu katika nyakati za kale wapiga ramli wengi na wengine wenye kuzoea mambo ya uchawi walikuwa wakitumia dawa katika sherehe walizokuwa wakifanya.
102. Uchawi unawezaje kutiwa ndani ya dawa zinazopendekezwa?
102 Huenda waganga wakatia mambo ya uchawi katika dawa zao kwa kutumia (sadaka) tambiko (ndege au mnyama anayetolewa na mgonjwa), kwa kutumia uchawi, au kwa kuloga. Katika nchi ya upande wa magharibi wa Afrika, mwanamume mmoja alielekezwa kwa mwanamke mmoja wa kabila la huko ili apate dawa za miti-shamba aponye maumivu yake ya meno. Alipokuwa akipewa dawa hiyo, mwanamke huyo alimwambia asiitazame. Alipoulizwa sababu, mwanamke alisema kwamba dawa hiyo ‘ingekosa nguvu yake’ ikiwa angeitazama. Lakini dawa yawezaje kujua kama ‘inatazamwa’? Je! vitu hivyo vina macho? Kwa wazi sivyo, kwa hiyo inaonekana kwamba mganga huyo aliamini kwamba majeshi ya roho wabaya yangeipa dawa hiyo nguvu za mwujiza.
103. Waganga wengine wa kienyeji wanatumia njia gani katika mazoea yao?
103 Huenda waganga wengine wa kienyeji hata wakadai kwamba wanaheshimu sheria za Mungu zinazokataza uchawi na kumbe wanatumia uchawi katika mazoea yao. Huenda wakatumia matope yaliyokandwa kuwa dawa ya kubandika (kupaka) au dawa za miti-shamba kwa makusudi ya kuponya. Lakini, wanapoondoa dawa hiyo ya kubandika, wanatokeza kitu fulani, labda jiwe au kitambaa kibovubovu (kichafu-kichafu) kisha wadai kwamba hiki ndicho kinacholeta ugonjwa wanaosema wameondoa katika mwili wa mtu.
104. Tunaweza kusema nini juu ya matambiko (sadaka) yanayohusiana na dawa za kienyeji?
104 Tumekwisha soma juu ya jinsi Mungu anavyowafikiria wale wanaozoea uganga na uchawi na jinsi anavyowaona kuwa “chukizo.” (Kumbukumbu la Torati 18:10-12; tazama mafungu 58 kufika 61.) Mara nyingi dawa za kienyeji zinatumia sherehe, kawaida za ibada na matambiko (sadaka) ya kuituliza ‘miungu.’ Basi, ikiwa mganga wa kienyeji angekuambia ulete kuku au mbuzi wa tambiko, hiyo ingekuwa na maana gani? Mnyama, huyo angetolewa sadaka kwa nani hasa? Mtume Paulo aliyeongozwa na Mungu anasema hivi: “Vitu vile wavitoavyo sadaka wavitoa kwa mashetani, wala si kwa Mungu; nami sipendi ninyi kushirikiana na mashetani.”—1 Wakorintho 10: 20-22.
105. Ikiwa sisi au watoto wetu hatuwezi kupona ugonjwa tukiisha kutumia kila njia inayofaa, imetupasa tufanye nini?
105 Ikiwa tumeokolewa katika utumwa wa nguvu ya mashetani, hatuwezi kujiacha turudishwe katika mtego wa mazoea na mapokeo ya uongo na bado tuendelee kuwa huru. Lakini namna gani ikiwa tumejaribu kila njia inayofaa ya kutaka kuponywa ugonjwa tusipate matokeo mema? Biblia inatuambia hivi: “Umtwike [Yehova] mzigo wako naye atakutegemeza.” (Zaburi 55:22) Mwombe, si ili uponywe kwa mwujiza, bali upate kuwa na hekima ya kuchagua utabibu unaofaa na, zaidi ya yote, upate kuendelea kuwa mwenye afya na mwenye nguvu kiroho, ukishika imani iliyo imara na maoni ya mbele yenye furaha hata ikiwa ugonjwa wako ni mkubwa na unachukua muda mrefu. Vilevile unaweza kumpa Yehova watoto wako. Uzima wao unamtegemea Yeye. Anaweza vilevile kuwalinda si kwa kutumia vitu kama hirizi au nyuzi, sadaka (matambiko), kawaida za ibada au sherehe nyingine.
106. Ni tumaini gani linalowatia nguvu watumishi wa Mungu wanaokuwa wagonjwa na landa hata wakifa?
106 Tunajua kwamba watu wanaozoea uchawi, kutia na waganga wa kienyeji vilevile wanakuwa wagonjwa, kisha wanakufa kwa sababu moja au nyingine. Ijapokuwa watumishi wa kweli wa Mungu pamoja na watoto wao wanaojitenga na mambo ya uchawi wanapata taabu kwa muda au hata kusumbuliwa na ugonjwa fulani usioponyeka, wanalo tumaini la ajabu la kuwategemeza. Wanajua kwamba Yehova Mungu ameweka wakati wa kuondoa magonjwa yote na mauti. Wakati huo wale wanaoendelea kuwa waaminifu kwa Mungu watapokea mipango yenye kutoa uzima, inayofananishwa na “mto wa maji ya uzima” wenye miti kando zake ambayo majani yake “ni ya kuwaponya mataifa.” (Ufunuo 22:1, 2) Kwa hiyo, hata tukiwa tunatazamia kufa, tunaweza kukumbuka maneno haya ya Yesu: “Mtu atakaye kuiokoa nafsi yake, ataipoteza; na mtu atakayepoteza nafsi yake kwa ajili yangu, ataiona.” (Mathayo 16:25) Badala ya kujaribu kuokoa maisha zetu kwa kuwaendea wenye mazoea machafu ya uchawi, tunaweza kutegemea uwezo wa Mungu Mwenye Nguvu Zote na kutumaini kwamba ataturudisha kwenye uzima kutoka mautini kwa kukufuliwa katika taratibu yake mpya yenye afya.
NDOTO
107, 108. (a) Sababu gani Yehova hatumii ndoto atuongoze leo? (b) Kuna matokeo gani mabaya ya kutegemea ndoto?
107 Shetani adui wa kiroho asiyeonekana, anaweza vilevile kutumia ndoto ili aondoe watumishi wa Mungu kwenye ibada safi. Watu wengi wanatia ndoto maanani sana. Mara chache ndoto zinaonekana kuwa zinatabiri matukio yanayokuja kuonekana baadaye. Ni kweli kwamba katika nyakati za kale watumishi wachache wa Mungu, kama Yusufu mwana mpendwa wa Yakobo, walitumiwa watabiri matukio fulani kupitia kwa ndoto. Walakini, yatupasa tukumbuke kwamba siku hizo hawakuwa na maandishi yote ya Biblia ili uwe uongozi wao kamili. Leo tunayo yote. Kwa habari ya maandishi hayo, tunasoma hivi: “Kila andiko limepewa kwa maongozi ya Mungu . . . ili mutu wa Mungu awe mukamilifu, ametengenezwa kabisa kwa kila tendo jema.”—2 Timoteo 3:16, 17, ZSB.
108 Biblia, Neno la Mungu ni uongozi wetu ULIO KAMILI katika kila utendaji mwema. Tangu Mungu alipoliandikisha lote, Neno hilo lililoongozwa na Mungu, wala si ndoto, limekuwa njia ya Mungu ya kuongoza watumishi wake wa kweli mpaka leo hii. Hasa, Neno lake linatuonya juu ya ndoto zinazohusiana na uaguzi (kupiga ramli) na ibada ya uongo, likisema: “Waaguzi wameona uongo; nao wameleta habari za ndoto za uongo.” (Zekaria 10:2; Kumbukumbu la Torati 13:1-3) Neno la Mungu lililoongozwa kwa roho yake litatuongoza katika njia zilizonyoka. Lakini wale wanaozitegemea ndoto wataongozwa bila shaka katika njia za uongo, mbali na ibada safi.—Yeremia 23: 25-27, 32; 27:9, 10.
WAKATI UJAO ULIO MZURI AJABU UKO MBELE YA WAABUDU WA KWELI
109. Neno la Mungu linakuwaje baraka na ulinzi wako?
109 Utegemee unabii wa ajabu unaopatikana katika Neno la Mungu badala ya kuzitumaini ndoto. Neno hilo halikudanganyi bali linakuambia kweli juu ya kuziabudu roho zisizoonekana na juu ya hali ya kweli ya wafu. Linakuokoa katika utumwa wa kuogopa kwa kukuonyesha kwamba wafu hawana fahamu na hawawezi kusaidia wala kuwaumiza walio hai. Linakulinda kwa kuwafunua wazi mashetani kuwa roho zenye kudanganya zinazojifanya kuwa wafu na kwa njia hiyo kudanganya watu wengi. Kwa upande mwingine, unapofuata mafundisho ya Biblia katika maisha yako, utaona kwamba yanaleta faida kubwa, kama vile amani ya akili na furaha ya moyo. Nawe waweza kuona namna unabii wa Biblia unavyotimizwa leo bila kukosea.
110. “BABELI MKUU” ni mfano wa nini?
110 Unabii huo unatuambia nini juu ya wakati ujao? Unatabiri kwamba karibuni ibada yote ya uongo, kutia na ibada ya roho zenye choyo zisizoonekana pamoja na mapokeo na mazoea yanayohusiana (yanayopatana) na uchawi, itaharibiwa kabisa. Dini zote za uongo za ulimwengu mzima pamoja na dini za uongo za Jumuiya ya Wakristo, zinafananishwa katika Biblia na mwanamke mchafu wa mfano anayeitwa “BABELI MKUU.” Anafananishwa kama ufalme wenye mji mkuu ‘uketio juu ya maji mengi’ na maji hayo “ni jamaa na makutano na mataifa na lugha.”—Ufunuo 17:1, 5, 15, 18.
111. Sababu gani Yehova anaonya watu wake watoke katika Babeli Mkuu?
111 Tunaweza kufahamu namna dini ya uongo ya namna mbalimbali imesimamisha milki (utawala) inayofanya watu kuwa watumwa na kuwagandamiza (kuwaonea) katika sehemu zote za dunia mpaka leo hii. Neno la Mungu linauambia mji huo wa mfano hivi: “Mataifa yote walidanganywa kwa uchawi wako.” (Ufunuo 18:23) Mungu anaichukia dini ya uongo kwa sababu inatumiwa na roho zenye choyo zisizoonekana ili ziwadanganye watu na kuwaondoa kwenye ibada safi. Kwa habari ya milki ya dini ya uongo, Babeli Mkuu wa mfano, Biblia inasema hivi: “Atateketezwa kabisa kwa moto. Kwa maana [Yehova] Mungu aliyemhukumu ni mwenye nguvu.” Ijapokuwa mashetani pamoja na Shetani mtawala wao ni wenye nguvu kupita wanadamu, hawawezi kulingana nguvu na Yehova Mungu na majeshi yake ya kimalaika. Roho hizo zenye choyo na zisizoonekana hazitaweza hata kidogo kuwaokoa wale wanaofuata mazoea yaliyo kinyume cha Neno la Mungu, utakapofika wakati wa Mungu wa kuiharibu milki ya ulimwengu ya dini ya uongo, yaani, Babeli Mkuu. Ndiyo sababu Mungu anatuonya hivi: “Tokeni kwake, enyi watu wangu, msishiriki dhambi zake.”—Ufunuo 18:4, 8.
112. Ni vita gani itakayofuata wakati huo? Nani watakaookoka?
112 Kuharibiwa huko kwa dini ya uongo kutafuatana upesi na “vita ya siku ile kuu ya Mungu Mwenyezi.” Ndipo, akiwa mjumbe wa Mungu, Kristo Yesu aliyetukuzwa atayaongoza majeshi yenye utukufu ya malaika wa mbinguni akapigane na adui wote wa Mungu duniani. Katika njia hiyo Mungu ataisafisha dunia kwa kuondoa uovu kwa urahisi kama vile mwanamke anavyoweza kusafisha nyumba yake. (Ufunuo 16:14-16) Je! watu wo wote wataokoka? Biblia inasema kwamba “wanyofu watakaa katika nchi, na wakamilifu watadumu ndani yake. Bali waovu watatengwa na nchi, nao wafanyao hila watang’olewa.” (Mithali 2:21, 22) Ndiyo, “wenye upole watairithi nchi, watajifurahisha kwa wingi wa amani.”—Zaburi 37:10, 11, 29; Mithali 12:7.
113. Mbele yetu kuna wakati gani ulio mzuri ajabu?
113 Je! waweza kuwazia kuishi katika dunia ambayo imerudishwa kuwa paradiso nzuri, yenye watu ambao ni wapole kweli kweli na wenye upendo wakiwa rafiki zako, si chini ya taratibu yo yote ya kisiasa yenye choyo na yenye kuonea, bali chini ya serikali bora sana na yenye haki? (Danieli 2:44; Isaya 65:17, 21, 22, 25) Je! ungependa kuishi katika wakati huo, wakati mapenzi ya Mungu yatakapofanyika hapa duniani kama mbinguni, na mahali ambapo watu hawatajifunza vita tena? (2 Petro 3:13; Mathayo 6:10; Mika 4:3, 4) Magonjwa, maumivu wala kuogopa kufa hayatakuwapo! Na zaidi ya hayo, wale wale waliofanyiza mateso mengi sana duniani kwa kutumia uchawi, yaani, Ibilisi na mashetani wake, wataharibiwa milele! Lo! tumaini zuri ajabu linalotolewa na Neno la Mungu: Uzima wa milele katika dunia ya paradiso katika amani, usalama na afya!—Ufunuo 21:3, 4; 20:10.
114, 115. Basi yakupasa ufanye nini?
114 Ikiwa unapenda uzima, basi endelea kukua (kukomaa) katika kumjua Mungu Mwenye Nguvu Zote na makusudi yake. Katika kumwomba Baba yake wa mbinguni, Yesu Kristo alisema hivi: “Na uzima wa milele ndio huu, Wakujue wewe, Mungu wa pekee wa kweli, na Yesu Kristo uliyemtuma.”—Yohana 17:3.
115 Lakini itakupasa ufanye bidii sana. “Piga vita vile vizuri vya imani,” asema mtume Paulo. Kwa kusudi gani? Ili uushike “uzima ule wa milele.” (1 Timotheo 6:12) Ndiyo, jitenge na mtego wenye kutatiza unaomfanya mtu awe mtumwa wa roho zenye choyo zisizoonekana. Kisha “mpingeni Shetani, naye atawakimbia. Mkaribieni Mungu, naye atawakaribia ninyi.” (Yakobo 4:7, 8) Uwe na imani iliyo imara. Naye “Baba wa rehema, Mungu wa faraja yote” akupe ushindi na furaha ya kumtumikia milele katika taratibu yake mpya yenye haki.—2 Wakorintho 1:3.
[Maelezo ya Chini]
a Ushuhuda zaidi wa ukweli wa Biblia unaweza kupatikana katika vitabu Is the Bible Really the Word of God? na “All Scripture Is Inspired of God and Beneficial”; “Toute Ecriture est inspiree de Dieu et utile.”
[Picha katika ukurasa wa 5]
Kwa sababu ya kuamini kwamba roho zisizoonekana (mizimu) zinaweza kumsaidia mtoto wake apone, mwanamke huyu anamwendea mganga wa kienyeji
[Picha katika ukurasa wa 16]
Sanamu zinazofananisha mizimu (wazazi waliokufa) zina-fanywa kwa kuamini makosa kwamba wazazi hao waliokufa wanaishi katika ulimwengu wa roho
[Picha katika ukurasa wa 17]
Samaki, ndege na wanyama wanaitwa “nafsi” katika Biblia kama mwanadamu anavyoitwa. Lakini hakuna mmojawapo asiyeweza kufa
[Picha katika ukurasa wa 20]
Wakati wa utawala unaokuja wa Yesu Kristo kwa muda wa miaka elfu, watu waliokufa watafufuliwa
[Picha katika ukurasa wa 31]
Katika Israeli wa kale, Mungu aliamuru mtu ye yote aliyezoea uchawi apigwe kwa mawe mpaka afe
[Picha katika ukurasa wa 34]
Miti fulani, miamba mikubwa (mawe makubwa), mito, maporomoko ya maji, milima au mahali pengine panadhaniwa na watu wengine kuwa mahali ambapo roho zisizoonekana (mizimu) zinakaa
[Picha katika ukurasa wa 37]
Imani za uongo zinanasa (zinakamata) watu wengi katika “mtego” wa woga
[Picha katika ukurasa wa 42]
Kama vile sanamu inayowekwa ili kufukuza ndege katika shamba la mazao isivyoweza kutembea, kusema, kusaidia wala kuumiza mtu ye yote, ndivyo na sanamu zo zote za kuabudiwa ambazo watu wanafanya
[Picha katika ukurasa wa 43]
Je! sanamu ya kuabudiwa inayofanywa na wanadamu ina uwezo wo wote wa ajabu? Sanamu inafanywa kutokana na mti ule ule zilikotoka kuni ambazo mtu anawashia moto apike chakula chake. Kwa kuwa sanamu inaweza kuteketezwa na mtu kwa vyepesi kama vile kuni, je! ingekuwa na uwezo wo wote wa kusaidia au kuumiza wanadamu?
[Picha katika ukurasa wa 45]
Maelfu ya watu wameachana na uchawi, wakaviharibu vitu vinavyohusiana (vinavyopatana) nao
[Picha katika ukurasa wa 48]
Kwa kukutana kwa kawaida ili tujifunze Neno la Mungu lililoongozwa na yeye, tunaweza kushinda vita juu ya “majeshi ya roho yenye uovu katika mahali pa kimbinguni”
[Picha katika ukurasa wa 61]
Watu wote na wanyama wote wataishi kwa amani kamili katika dunia ya paradiso, wala njaa, huzuni, magoniwa wala mauti haitakuwapo tena