Sura ya 9
Vijana—Mnawezaje NINYI Kuwa Wenye Furaha?
UJANA unaweza kuwa mmoja wa nyakati zenye kufurahisha sana maishani. Wakati wako ujao uko mbele yako. Basi jipatie faida nyingi kabisa kutokana na wakati huo. Jitahidi sana uipate furaha.
2 Lakini si vyepesi kufanya hivyo. Dakt. Robert S. Brown alifanya uchunguzi wa vijana ambao wamekuwa watu wazima, ambao miaka michache iliyopita walikuwa wamekata kauli waishi kulingana na mawazo waliyoona wanafaa sana kuyafuata katika ujamii na serikalini. Anasema kwamba zaidi ya theluthi moja (1/3) walikuja kujua kwamba ni tatizo kubwa kutimiza walilotaka, wakashuka moyo na kuwa na wasiwasi.
3 Mara nyingi unasikia watu wakisema utatuzi wa matatizo ni kupata elimu nyingi. Lakini leo vijana wengi wanaoipata wangali wakikosa kazi. Wengine wanaopata mshahara mkubwa wanakuja kujua kwamba kazi zao zenye donge nono haziwatimizii kusudi lao maishani. Wala mahaba yanayofanywa na vijana walio wengi hayawaletei furaha. Mahali pengine, asilimia 80 ya ndoa za matineja (vijana wenye umri mdogo kuliko miaka 20) zinavunjika katika muda wa miaka mitano.
4 Wewe unaweza kufanya nini usipatwe na matatizo hayo, ili ujifurahishe sasa na kuridhika wakati ujao? Au, ikiwa wewe ni mzazi, unawezaje kusaidia wazao wako waufikie mradi huo?
KUMFIKIRIA MUUMBA
5 Mara nyingi vijana wanavutwa na vijana wa rika lao, wasiojua mengi maishani. Biblia inatoa maoni haya:
“Mwenye akili ni yule ambaye ameuona msiba na anaendelea kujificha mwenyewe, lakini wale wasio na ujuzi wamesonga mbele na lazima waipate adhabu ya kufanya hivyo.”—Mithali 22:3, NW; 13:20.
Kijana mwenye kutumia akili vizuri atakubali waziwazi kwamba si wanashule au rafiki wengi wanaopendezwa sana kumwona yeye akipata hali njema ya daima. Unaweza kujiuliza, ‘Kama sasa hawanijali, je! wakati ujao wataanza kunijali furaha yangu ikiharibiwa na matendo yangu ya sasa?’
6 Lakini ni nani anayekujali, anayeweza kukupa maoni yenye mafaa makubwa kabisa? Ni Muumba wako. Yeye anawataka vijana wafurahie maisha. Yeye hana maoni mabaya juu ya mambo yote yanayopendeza mioyo na macho ya vijana. Ingawa hawakingi vijana wasipatwe na machungu yanayotokana na mwendo mpotovu, anafanya jambo ambalo ungetazamia lifanywe na mtu anayependezwa nawe kweli kweli: Anakuonya usifanye mambo yatakayokuletea huzuni nyingi na msiba, na anatoa maoni yanayokuonyesha namna ya kuepuka mitego hiyo. (Mithali 27:5; Zaburi 119:9) Katika habari hiyo Biblia inasema:
“Wewe, kijana, uufurahie ujana wako, na moyo wako ukuchangamshe siku za ujana wako, ukaziendee njia za moyo wako, na katika maono ya macho yako; lakini ujue wewe ya kwamba kwa ajili ya hayo yote Mungu atakuleta hukumuni. Kwa hiyo ondoa majonzi moyoni mwako, nawe uuondoe ubaya mwilini mwako.”—Mhubiri 11:9, 10.
7 Hata hivyo, kuna sababu zaidi za kumfikiria Muumba kwa maana haitoshi kumfikiria kwa sababu tu yeye anapendezwa nawe. Vijana wengi wanaendesha maisha yao bila shabaha yo yote maishani, na labda umewaona wakiwa hivyo. Hawana mradi waliojiwekea waziwazi wala viwango imara vya kutegemezea maisha yao. Mara nyingi wanatumia dawa za kulevya, wanavuta sigara na kujifurahisha kwa mambo hatari ili waujaze utupu ulio katika maisha yao, au watafute msisimko fulani waache kuwa na maisha yasiyopendeza. Labda wewe pia umekwisha kufanya mengine ya mambo hayo, kwa kujua au bila kujua hatari zinazohusika. Je! unaridhishwa na maisha yako mpaka sasa na matazamio ya wakati ujao? Je! huu sio wakati wa kutulia kidogo uyafikirie maisha yako?
8 Kama tulivyokwisha kuona, lazima mtu akubali kwamba kuna Muumba wa ulimwengu mzima ndipo aweze kuwa na kusudi la kuishi na kujipatanisha na namna maisha yalivyo hasa. Huyo, ambaye ndiye Mfanyi wetu, ana viwango vinavyopasa kutimizwa. (Zaburi 100:3) Viwango hivyo vinapatana na namna alivyotufanya tuwe tukiishi. Vina mafaa na vinaleta furaha. Tuliona ushuhuda wa jambo hilo katika sura za kwanza-kwanza zilizozungumza juu ya ngono zinazofanywa kabla ya ndoa, kunywa pombe kupindukia na kucheza kamari.a Basi wewe ukitaka maisha ya kupendeza, je! huoni ni hekima kumfikiria Muumba unapowaza namna utakavyoendesha maisha yako, unapowaza ni viwango gani utakavyofuata sana na ni wapi maisha yako yanakoelekea?
MAISHA YENYE KUSUDI NA KUJIHESHIMU
9 Tumeona katika Mhubiri 11:9, 10 maelezo fulani ambayo vijana wanapewa. Kitabu hicho cha Biblia kinamalizia hivi:
“Umalizio wa shauri hilo, kila jambo likiwa limekwisha kusikiwa, ni: Mwogope yule Mungu wa kweli na kushika amri zake. Kwa maana huu ndio wajibu mzima wa mwanadamu.”—Mhubiri 12:13, NW.
10 Duniani kote kuna mamia ya maelfu ya vijana ambao wameyafikiria maisha yao bila mchezo. Wao wamemfikiria Muumba wakajifunza Neno lake. Wameona kwamba moja la matakwa ya kwanza-kwanza yanayowezesha mtu apate furaha ni kuishi kupatana na asemayo Mfanyi wao. Wajibu wako na kusudi la kuishi linapasa liwe ilo hilo. Kuishi kupatana na maagizo ya Maandiko si jambo la kizamani, la kupita kipimo wala la kuchukiza. Bali, kufanya hivyo ni kuwa na njia iliyosawazika ya maisha yenye kusudi. Kunawezesha mtu awe na hekima na matokeo mazuri katika mambo yanayohusu fedha, ukosefu wa kazi, adili, maisha ya jamaa, tafrija na mengine ambayo unakabili sasa au utakayoyakabili baadaye. Mambo ambayo Mashahidi wa Yehova wamejionea wenyewe yanahakikisha kwamba hekima inayotegemea Maandiko
“ni mti wa uzima kwa wale wanaoishika, na wale wanaoishika kwa kuifumbata sana wanapaswa waitwe wenye furaha.”—Mithali 3:18, NW.
Biblia inashauri hivi: “Mwana wangu, usisahau kufundisha kwangu, acha moyo wako ushike kanuni zangu, kwa maana hizi zitakupa wewe siku ndefu zaidi, miaka mirefu zaidi ya maisha, na furaha kubwa zaidi.”—Mithali 3:1, 2, Jerusalem Bible.
11 Unapofuata maoni ya Biblia, huenda ukaonekana kuwa tofauti sana na vijana wengi. Huenda watu wakakutupia maneno makali. (1 Petro 2:20; 4:4) Je! utaacha kufuata mwendo utakaofanya maisha yako yapendeze zaidi?
12 Kuna vijana wengi wanaodai wanajifanyia maamuzi yao wenyewe, na kumbe ni wazi kwamba wanaogopa kuonekana wakiwa tofauti na wengine. Lakini, Biblia ina mifano mizuri ya vijana ambao hawakufuata umati wa watu. Ingawa walikuwa vijana kama wale wengine tu, wakiwa na mapendezi yao wenyewe, mahangaikio na matumaini kama yako, waliacha mawazo na matendo yao yaongozwe na mashauri yenye hekima ya Mungu.
13 Unaweza kusoma mfano mmoja katika Danieli 1:6-20; 3:1-30. Vijana watatu Waebrania waliokuwa wenzi wa Danieli walikuwa na nia ya kujitofautisha na wengi wa jirani zao. Walipoagizwa wainamie sanamu, hilo likiwa ni jambo lililokatazwa na Neno la Mungu, hawakukubali. Je! kama ingalikuwa ni wewe, ungaliweza kukataa? Hata wengine walitaka kuwaua kwa sababu ya msimamo wao. Lakini wao wakazidi kushikilia kanuni zao, nawe utaona katika masimulizi ya kisa hicho kwamba Mungu aliwakubali na kuwalinda. Mwishowe, mfalme wa Babiloni aliwatukuza, na jambo hilo likahakikisha ukweli wa maandishi ya Sulemani: “Mimi pia najua kwamba itakwenda vizuri kwa wale wanaomwogopa yule Mungu wa kweli.”—Mhubiri 8:12, NW; Kutoka 20:4, 5.
14 Vijana hao walianza kuheshimiwa na watu wale wengine, lakini walijiheshimu wenyewe pia. Ndivyo imekuwa kwa vijana wengi walio Mashahidi wa Yehova nyakati za ki-siku-hizi. Wanashule wenzao wamevutwa na masadikisho yao. Wamevutwa pia na jambo la kwamba Wakristo hao wanajua wanakoelekea maishani. Je! wewe hukubali kwamba kuheshimiwa na wengine na kujiheshimu mwenyewe ni mambo yanayofanya maisha yawe yenye kusudi zaidi?
FURAHA YA JAMAA
15 Mashauri ya Biblia yanasaidia pia kufanya maisha za vijana ziwe zenye faida nyingi zaidi kwa kuwaunga-nisha zaidi na watu wa jamaa.
16 Bila shaka unajua jamaa kadha zenye pengo kubwa sana kati ya wazazi na watoto, hata kama watoto wenyewe ni wadogo sana au ni matineja. Mara nyingi mtengano huo mkubwa unatokea wakati wazazi wanapojaribu kuamuru wazao wao juu ya mambo wanayopaswa au wasiyopaswa kufanya, kisha watoto wenyewe wanaudhika sana kwa maana hawataki kuambiwa hayo.
17 Biblia inasaidia kushinda tatizo hilo kwa kutolea vijana na wazazi pia mwongozo wenye usawaziko, kama huu:
“Watoto, ni wajibu wenu wa Kikristo kutii wazazi wenu, kwa maana hili ndilo jambo linalofaa kufanya. ‘Heshimu baba na mama yako’ ndiyo amri ya kwanza ambayo imeongezewa ahadi: ‘ili kwamba yote yaweze kwenda vizuri upande wako, na wewe uweze kuishi muda mrefu katika hiyo nchi.’ Wazazi, msitende watoto wenu katika njia ya kuwafanya wakasirike. Badala ya hivyo, waleeni hao kwa nidhamu ya Kikristo na mafundisho.”—Waefeso 6:1-4, Good News Bible.
18 Bila shaka, hakuna wazazi wakamilifu. Hata hivyo kuheshimu wazazi “ndilo jambo linalofaa” vijana. Kwa nini? Kwa ufupi, ni kwa sababu wazazi wetu wametufanyia mengi sana—walitulisha, wakatutunza tulipokuwa wagonjwa, wakafanya kazi ili tuweze kuwa na makao kisha wakatutimizia mahitaji yetu. Sisi tusingalikuwa na uwezo wa kuajiri mtu atufanyie yote ambayo wametufanyia. Wala mtu huyo asingaliweza kutufanyia hayo akihangaikia hali yetu kwa upendo kama ule tulioonyeshwa na wazazi wetu. Kwa hiyo inatufaa tuwaheshimu, kama vile sisi tungependa tuheshimiwe na watoto ambao huenda tukazaa siku moja.
19 Vijana wanaojaribu kwa unyofu wa moyo kufuata maoni hayo ya Biblia watajisikia salama zaidi. Watakuwa wakisaidia kufanya jamaa iwe na uhusiano wa karibu zaidi, kisha maisha yao yatakuwa ya amani na furaha zaidi. Tena watalindwa wasipatwe na matatizo ambayo wazazi wanatangulia kuyaona kwa sababu ya ujuzi wa kuishi kwingi. (Mithali 30:17) Wala hatutasahau uradhi ambao vijana wanaweza kupata kwa kujua kwamba wanatenda mambo yanayopatana na mapenzi ya Muumba wao.
20 Kukubali mashauri ya Kibiblia kunafaidi vijana kwa njia nyingine nyingi pia. Wanapothamini ubora wa ushirikiano mzuri na kuheshimu mamlaka, wanaweza kuendesha mambo yao vizuri zaidi katika shule, katika uhusiano watakaokuwa nao baadaye pamoja na matajiri wao wa kazi na wakati watakapokuwa wakishughulika na maafisa (wakuu). (Mathayo 5:41) Pia, kuthamini mashauri ya Biblia kutaleta furaha watakapokuwa na wenzi wa ndoa na watoto wao wenyewe.
WAZAZI WANA JUKUMU (DARAKA) LA MAANA SANA
21 Tunapoonyesha namna vijana wanavyoweza kuwa wenye furaha, hatuwezi kulipuza jukumu la maana sana walilo nalo wazazi. Wazazi walio wengi wanatambua wana daraka la kujaribu kuwapa watoto wao chakula kizuri, mavazi na makao yenye kupendeza. Lakini lazima vijana wapate mafundisho, nidhamu (adabu) na mwongozo wa kiadili wa wazazi wao ndipo waweze kuwa watu wema. Biblia imethibitika kuwa ndiyo msingi bora zaidi wa kufanya hivyo. (Mathayo 11:19) Kumbukumbu 1a Torati 6:6, 7 inaeleza kwamba mafundisho hayo yanapasa yafanywe kwa ukawaida katika maisha ya jamaa, wala yasiwe jambo la kutajwa mara kwa mara tu. Pia, mafundisho hayo yanaweza, na yamepasa, kuanzwa wakati watoto wangali na umri mdogo sana.—2 Timotheo 3:15; Marko 10:13-16.
22 Wazazi wengi wenye watoto wadogo hawatashangaa kusoma maneno yafuatayo kwa sababu si mageni kwao: “Upumbavu umefunganishwa pamoja na moyo wa mvulana [au, msichana]; fimbo ya adhabu ndicho kitu kitakachouondolea mbali na yeye.” (Mithali 22:15, NW) Lakini hiyo maana yake nini? Wazazi wengine wanakuwa wakali sana mpaka wanaumiza miili ya watoto wao kwa kuwacharaza-charaza. Wengine wanasema kwamba inapasa watoto waachiliwe wafanye wanavyotaka mpaka watakapokuwa wakubwa. Kila moja ya namna hizo mbili za malezi imepita kiasi kinachofaa.
23 Kitambo kidogo tumesoma kwamba wazazi wanapaswa ‘walee watoto wao kwa nidhamu ya Kikristo na mafundisho.’ (Waefeso 6:4, Good News Bible) Unyama (ukatili) si nidhamu ya Kikristo. (Mithali 16:32; 25:28) Nidhamu yenye upendo inaweza kuonyeshwa kwa neno lisilo na ugeu-geu. Ndivyo inavyokuwa hasa wazazi wakieleza mtoto waziwazi sababu ya sheria waliyotoa na wakishikilia maneno yao pasipo ugeu-geu. Wakati upumbavu ulio katika moyo wa mtoto wa kiume au wa kike unapozidi kumwongoza asitii—na hiyo ni kawaida—akipewa adhabu ya namna fulani, itamwingia ikaze kikiki somo analofunzwa. Huenda dawa ikawa ni kumnyang’anya pendeleo fulani. Ingawa hivyo, Neno la Mungu linasema kwamba huenda katika visa fulani adhabu ya kimwili—kutandika (kupiga), lakini bila hasira nyingi—ikahitajiwa.—Mithali 23:13, 14; 13:24.
24 Watoto wadogo wanapoendelea kuwa wakubwa, njia ya kushughulika nao itabadilika. Ijapokuwa labda kumtandika viboko kivulana mdogo kulisaidia zaidi siku za utoto wake, anapoendelea kuwa mkubwa katika umri huenda njia zilizo tofauti zikafaa zaidi. Vivyo hivyo, inawapasa wazazi nao wamwongezee kidogo kidogo mwana au binti uhuru wa kutenda mambo na kuchukua madaraka.—1 Wakorintho 13:11.
25 Unahitajiwa kabisa upende watoto wako ili uwasaidie na matatizo yao. Hilo ndilo linalopasa kuwa kusudi la nidhamu, na kufanya hivyo kunaifanya ipokewe kwa urahisi zaidi. Kukosa kutolea watoto mwongozo na nidhamu ni kama kuwakana kwa kusema siwe uliyewazaa. Jambo hilo linaelezwa kwenye Waebrania 12:5-11, inayoonyesha kwamba Yehova mwenyewe anatia watu nidhamu kwa upendo.
26 Ni jambo la maana pia kumpenda Mungu. Jambo hilo litaongoza wazazi wachukie mambo anayokataza Mungu, kama kusema uongo, kula pupa, kuiba, kulalana mwanamume na mwanamume au mwanamke na mwanamke, na uasherati. (1 Wakorintho 6:9, 10; Zaburi 97:10) Wazazi wanaoonyesha kwa njia hiyo kwamba wanampenda Mungu watawawekea watoto wao mfano unaofaa, na hilo ni jambo la maana. Pamoja na hilo, inawapasa wazazi wasitawishe katika watoto wao kuchukia mabaya, kumpenda Mungu na kupenda mema ili watoto wafuate mfano wao katika mambo hayo.
27 Kwa kuwa jamaa ni kama ulimwengu ambao ndio wa kwanza kukanyagwa na kijana, imewapasa wazazi wajitahidi kuifanya jamaa iwe mahali penye imara na usalama. Imesemwa kwamba moja la mambo makubwa zaidi ambayo baba anaweza kufanya afaidi watoto ni kumpenda mama yao. Maisha ya kinyumbani yakitegemea upendo na hekima ya Kikristo, vijana watakuwa na msingi imara wa kusimamia. Watakuwa na viwango vinavyofaa, kisha watasaidiwa wamfikirie Muumba wao tangu ujana na kuendelea.—Mhubiri 12:1, 13, 14.
[Maelezo ya Chini]
a Muziki, matembezi ya wavulana na wasichana, mavazi, michezo, shule na mahangaikio mengine ya vijana yamezungumzwa kwa msaada wa Biblia katika kitabu Kupata Faida Zote za Ujana Wako.
[Mambo ya Kuzungumziwa]
Sababu gani vijana wanashindwa sana kupata furaha? (1-4)
Sababu gani inakupasa umfikirie Mungu? (5-8)
Sababu gani unatazamiwa utake kufanya mapenzi ya Mungu? (Zaburi 128:1, 2) (9, 10)
Je! ni vibaya ikiwa maisha ya kumfikiria Mungu yanakufanya uwe tofauti na watu wengine? (11-14)
Wewe una sababu gani za kukufanya ufuate Maandiko katika jamaa yenu? (15-20)
Wazazi wanaweza kuwasaidiaje watoto wao wafuate mwe-ndo wa hekima? (21)
Ni nidhamu (adabu) ya namna gani ambayo wazazi wanapaswa kuwapa watoto wao? (22-24)
Upendo wa jamaa utasaidiaje kutatua matatizo ya watoto? (25-27)
[Sanduku katika ukurasa wa 89]
KUPATA KUSUDI MAISHANI
Idara ya Afisi ya Waziri Mkuu wa Japan ilifanya uchunguzi katika nchi mbalimbali. Ilichunguza maoni ya vijana juu ya kusudi la maisha na wakati ujao. Alipoyafikiria sana maoni waliyotoa, Profesa Sanshiro Shirakashi alikata kauli ya kwamba “vijana wa ulimwengu wanatazamia mabaya tu” wakati ujao, na jambo hilo linaharibu mwenendo wao na maoni yao ya ujumla juu ya maisha. Lakini badiliko linaweza kufanywa.
Mwanafunzi ambaye jina lake ni Linda anasimulia haya: “Nilipokuwa katika masomo ya chuo kikuu, niliweza kuona kwamba mtindo wa maisha niliyolelewa nayo ulikuwa ukitoweka. Hali ziliendelea kuwa mbaya zaidi ulimwenguni pote, nami sikuwa na utatuzi wala wazo lo lote juu ya mahali ambako ningeweza kwenda nipate utatuzi.”
Msichana huyo alipokuwa likizoni nyumbani California, wawili wa Mashahidi wa Yehova walifika mlangoni pake. Yeye anasema: “Waliniambia utatuzi nilioutaka umo katika Biblia. Tukazungumza habari za dunia-paradiso ambayo Mungu ataanzisha chini ya taratibu mpya yake na habari za ahadi aliyotoa kuumaliza uovu. Kabla ya hapo sikuwa nimefundishwa kwamba kweli hizo nzuri ajabu zimo katika Biblia.”
Linda aliporudi Arizona, alitafuta kundi la huko la Mashahidi wa Yehova kisha akakubali kufundishwa Biblia kila juma bila malipo. Alijifunza viwango vya kufuata maishani, navyo vikaimarisha maisha yake. Pia, alipata kusudi la kuishi, na leo hii ni mwenye furaha zaidi maishani, na faida anazopata ni nyingi zaidi.
[Picha katika ukurasa wa 92]
Wewe ulitunzwa na nani ulipokuwa mgonjwa?
[Picha katika ukurasa wa 93]
Kujifunza Neno la Mungu kunasaidia watoto wapate furaha