Watchtower MAKTABA KWENYE MTANDAO
Watchtower
MAKTABA KWENYE MTANDAO
Kiswahili
  • BIBLIA
  • MACHAPISHO
  • MIKUTANO
  • hp sura 10 kur. 96-102
  • Afya Bora na Maisha Marefu Zaidi—Vipi?

Hakuna video yoyote kwa sasa.

Samahani, haikuwezekana kupakia video.

  • Afya Bora na Maisha Marefu Zaidi—Vipi?
  • Furaha​—Namna ya Kuipata
  • Vichwa vidogo
  • Habari Zinazolingana
  • MASHAURI YANAYOENDELEZA AFYA NZURI
  • TUMBAKO, VILEO NA DAWA ZA KULEVYA
  • SABABU NA NAMNA YA KUFUATA MASHAURI YA MUNGU
  • Je! Dawa za Kulevya Zinaleta Maisha Bora?
    Kupata Faida Zote za Ujana Wako
  • Kuiheshimu Zawadi ya Uhai
    Amani na Usalama wa Kweli—Wewe Unaweza Kuupataje?
  • Dawa za Kulevya
    Kutoa Sababu kwa Kutumia Maandiko
  • Je, Kuvuta Sigara Ni Dhambi?
    Maswali ya Biblia Yajibiwa
Pata Habari Zaidi
Furaha​—Namna ya Kuipata
hp sura 10 kur. 96-102

Sura ya 10

Afya Bora na Maisha Marefu Zaidi​—Vipi?

AFYA nzuri inaweza kuongeza sana furaha ya mtu. Lakini sisi sote tunakuwa wagonjwa nyakati nyingine. Na ugonjwa mbaya sana unaweza kuua mtu. Matatizo hayo yamezungumzwa katika Biblia, nayo inatoa maongozi yanayoweza kusaidia mtu afurahie afya bora na maisha marefu zaidi.

2 Maandiko yanatukumbusha kwamba Yehova Mungu ndiye Chemchemi ya uhai. Kwa sababu ya yeye “tunaishi, tunakwenda, na kuwa na uhai wetu.” (Zaburi 36:9; Matendo 17:25, 28) Naye anatueleza mengi juu ya namna tunavyoweza kujitunza wenyewe. Kuna magonjwa yenye kugharimisha sana watu na kuharibu viungo vya miili yao yanayoweza kuepukwa kwa kuyatii mashauri yaliyo katika Neno lake. Wale ambao wameyatii wana sababu ya kukubaliana na mwandikaji wa Biblia aliyesema: “sheria ya kinywa chako [Mungu] ni njema kwangu, kuliko maelfu ya dhahabu na fedha.”—Zaburi 119:72; 73:28; Mithali 4:20-22.

MASHAURI YANAYOENDELEZA AFYA NZURI

3 Biblia si kitabu kilichokusudiwa kiwe na maongozi yanayohusu afya. Lakini ina mashauri yanayoendeleza afya nzuri. Jambo hilo linaweza kuonekana wazi-wazi katika sheria za uongozi ambazo Mungu alilipa taifa la Israeli. Mifano ni hii: Muda mrefu kabla elimu ya tiba ya ki-siku-hizi haijakuwapo, sheria ya Mungu aliyowapa Israeli ilitaka mtu aliyekuwa na ugonjwa wenye kuambukia wengine, au aliyeelekea kuwa nao, afungiwe mahali pa pekee. (Mambo ya Walawi 13:1-5) Kinyesi (mavi) kilipasa kiondolewe mbali katika makao ya kibinadamu, na hivyo magonjwa yalizuiwa yasienee au uchafuzi wa maji ukaepukwa. (Kumbukumbu la Torati 23:12-14) Ikiwa mavazi au vyombo vya kutumia viligusa mnyama aliyekuwa amejifia mwenyewe (labda kwa sababu ya ugonjwa), ilikuwa lazima vitu hivyo visafishwe kabla ya kutumiwa tena au viharibiwe. (Mambo ya Walawi 11:27, 28, 32, 33) Makuhani Waisraeli walipaswa kuoga kabla ya kutumikia madhabahuni, na hivyo wakawekea wale wengine mfano mwema wa usafi.—Kutoka 30:18-21.

4 Tangu wakati huo madaktari wamejifunza mafaa ya kujitunza kwa njia hizo, nazo hata sasa zingali zina mafaa yafuatayo: Kutokukaribiana sana na wengine ikiwa wewe au wao wanaelekea kuwa na ugonjwa unaoweza kuambukia. Kujiangalia usichafue maji ya kunywa au chakula kwa kuingiza katika vitu hivyo takataka za kibinadamu au za namna nyingine. Kuweka vyombo vya kupikia na vya kulia katika hali ya usafi. Kutunza usafi wa mwili wako kwa kuoga kwa ukawaida, na pia kwa kunawa mikono baada ya kwenda chooni.

5 Kama ilivyo kawaida, magonjwa ya kisonono na kaswende yanapatikana kwa kugusana na mtu katika uasherati, na huo unakatazwa na Mungu. (Waebrania 13:4; Waefeso 5:5) Lakini Wakristo wanalindwa wasipatwe na magonjwa hayo ya kuchukiza sana kwa kuwa safi kabla ya ndoa na kufanya ngono na mwenzi wa ndoa peke yake baada ya kuoana.

6 Pia, afya bora inaweza kutokana na kufuata mashauri ya Kimaandiko yanayohusu maisha yote ya mtu. Kwa mfano, Biblia inasifu kufanya kazi kwa bidii. Inasema mtu anayetimiza fungu kubwa la kazi iliyopangiwa siku hiyo, atalala vizuri zaidi. Tena inapendekeza sana kufurahia chakula na kinywaji unachoweza kujipatia kwa kufanya kazi ngumu, lakini uepuke anasa ya ulafi. Je! wewe hukubali kwamba ukifanya kazi kwa bidii, upate usingizi wa kutosha, ufurahie vyakula vyako kisha uwe na “kiasi katika mazoea,” utakuwa mwenye afya bora na furaha nyingi zaidi?—Mhubiri 2: 24; 5:12; 9:7-9; Waefeso 4:28; 1 Timotheo 3:2, 11, NW.

TUMBAKO, VILEO NA DAWA ZA KULEVYA

7 Dakt. Joel Posner anaeleza kwamba katika United States, kwa mfano, asilimia 60 ya fedha zinazotumiwa kulinda afya ya watu ni za magonjwa yanayohusiana na uvutaji wa tumbako na vileo. Biblia inasaidiaje katika jambo hili?

8 Akifuata sana maoni ya Mungu juu ya usafi au utakato, mtume Paulo aliandikia Wakristo hivi: “Rafiki wapendwa, acheni sisi tujitakase wenyewe na kila kitu kinachochafua ama mwili ama roho.” (2 Wakorintho 7:1, Twentieth Century New Testament) Watu wengi wameona kwamba kuvuta tumbako kunapingana na shauri hilo. Ni jambo lisilo asili ya mwanadamu kuvuta moshi uingie mapafuni. Unachafua mwili na kufupisha urefu wa maisha ya mtu. Uchunguzi mwingi umethibitisha kwamba wavutaji wa tumbako (sigara) ndio wanaopatwa zaidi na ugonjwa wa moyo, kansa (donda baya sana) ya mapafuni, mpigo wa juu mno wa damu na mchochota wa mapafuni wenye kuua.

9 Pia, yafikirie matokeo yanayopata watu walio karibu na mvutaji wa tumbako (sigara)—jamaa yake na wenzake. Yesu Kristo alisema kwamba amri iliyo ya pili katika sheria ambayo Waisraeli walipewa na Mungu ni hii: “Inakupasa upende jirani yako kama wewe mwenyewe.” (Marko 12:31, NW) Wewe unataka kufanya hivyo, au hutaki? Lakini matokeo ya kuvuta tumbako ni nini? Tumbako inaumiza mtumiaji na kuharibu afya ya wengine wanaouvuta ndani ya milli yao moshi unaotokea.

10 Namna gani kutumia vileo (pombe)? Watu wengi wanafurahia ladha yavyo na kuburudika. Biblia haikatazi vinywaji vyenye vileo vikali, ambavyo mwili unaweza ‘kuvichoma’ (kuviyeyusha) viwe joto la kuupasha mwili au viwe chakula. (Zaburi 104:15; Mhubiri 9:7) Lakini inaonya hivi: “Divai ni mdhihaki, kileo chenye kulewesha kina makelele mengi, na kila mtu anayepotoshwa nacho si mwenye hekima.” (Mithali 20:1, NW) Tena Biblia inakataza ulevi waziwazi kabisa. (1 Wakorintho 6:9, 10; 1 Petro 4:3) Ni wazi kwamba mtu ye yote anayekunywa mno, mara nyingi mno, “si mwenye hekima,” kama maandiko yanavyosema. Baada ya muda fulani, huenda ini lake likaharibika, kisha aumie sana au hata afe. Huenda tumbo likaharibiwa. Mtu mwenye kulewa anaweza kuwa na maelekeo ya kupatwa na ugonjwa wa moyo na ule unaoingilia ubongo kwa ghafula na kupoozesha mwili. Huenda kumbukumbu lake na usawaziko wa misuli (minofu) ya mwilini vikaharibiwa pia.

11 Mashauri ya Biblia yanayohusu ulevi yanasaidia pia kuhusu matumizi ya dawa za kulevya kama heroin, cocaine, tambuu, bangi au kasumba, LSD, ugoro na miraa. Vitu hivyo vinatumiwa mahali pengi sana, lakini kusudi si kwamba ni “chakula” wala dawa, bali ni ‘kuona raha’ ya kuleweshwa, kuona maajabu kwa sababu ya kizunguzungu au kwa kusudi la kujisahaulisha matatizo ambayo mtu anayo. Ni kweli huenda ikawa dawa hizo hazikutumiwa nyakati ambazo Biblia ilikuwa ikiendelea kuandikwa. Lakini Biblia inakataza ulevi kwa uthabiti na “ufisadi” unaohusiana na ulevi. Je! shauri ilo hilo lisitumike kuhusu kitu kingine cho chote kinachoweza kulewesha mtu na kumfanya awe na tabia za ufisadi? (Waefeso 5:18) Mara nyingi watu wanaolewa dawa hizo wanajiumiza wenyewe au wanaumizwa na wengine. (Linganisha Mithali 23:29, 35.) Dawa hizo zinahusiana pia na hatari nyingine za afya, kama ugonjwa wa mapafu, uharibifu wa ubongo na wa hali za uzazi, ugonjwa unaosababishwa na ukosefu wa chakula cha kujenga mwili, kisha ugonjwa wa kufura ini. Hakika kufuata mashauri yaliyo katika Biblia kunaweza kuleta faida za afya.

SABABU NA NAMNA YA KUFUATA MASHAURI YA MUNGU

12 Watu wote wenye akili timamu wanapendezwa na taraja la kuwa na afya bora na kuishi maisha marefu zaidi. Hiyo ni sababu moja nzuri ya kutufanya tuyakubali na kuyafuata mashauri ya Kimaandiko ambayo tumezungumza. (Zaburi 16:11) Lakini je! sababu hiyo tu inatosha? Labda unawajua watu fulani ambao wanaona ni afadhali kujiingiza hatarini kuliko kuikosa raha au msisimko wanaoutaka kutokana na kitu fulani. Lakini watu wanaomwamini Mungu na kukubali kwamba yeye ametufunulia utu wake kupitia Biblia hawapaswi kuwa hivyo. Kwa kuwa uhai tulio nao ulitoka kwake, inatupasa tuhangaikie kuutumia kupatana na mwongozo anaotutolea katika Biblia. Tungekuwa watu wasio na shukrani tukiukubali uhai kutoka kwa Yehova kisha kwa makusudi tuyapuze mashauri yake yenye hekima na upendo juu ya tunavyopaswa kutumia maisha yetu.

13 Zaidi ya hilo, kwa kuwa Mungu ndiye Mpaji wa uzima, je! yeye hana haki ya kutuelekeza namna tunavyopaswa kuishi? Yeye ndiye Mwamuzi Mkuu Kabisa katika ulimwengu mzima. Yakobo mwandikaji wa Biblia alimwita kuwa ‘Yeye aliye mpaji wa sheria na hakimu.’ (Yakobo 4:12, NW; Linganisha Isaya 45:9.) Kwa hiyo, ni lazima tujisikie tukitaka kufuata maneno ya Mungu katika tabia zetu binafsi kwa sababu Yeye ndiye amesema tufanye hivyo.

14 Maoni hayo yamechochea sana watu wengi wachukue hatua ili waache zoea lenye madhara ambalo lilikuwa limewachukua muda mrefu kulishinda. Waliyaona wazi zaidi matendo yao mabaya walipofahamu walihitaji kufanya badiliko, si kwa ajili ya afya tu, bali pia kwa sababu hatua hiyo ilipatana na mapenzi ya Mungu. Yesu aliwaambia wafuasi wake kwamba amri iliyo kubwa zaidi ni kupenda Yehova ‘kwa moyo wako wote na kwa nafsi yako yote na kwa akili zako zote.’ (Mathayo 22:37, NW) Ili mtu afanye hivyo, lazima aache kutumia vitu vinavyopumbaza akili na kuiharibu au kuchafua mwili.

15 Msaada mwingine ni kushirikiana na watu wanaojitahidi kufuata mashauri ya Mungu katika maisha yao. Mtume Petro aliandika kwamba kabla watu wengine hawajawa Wakristo, ‘walienenda katika ufisadi, na tamaa, na ulevi, na karamu za ulafi, na vileo, na ibada ya sanamu isiyo halali.’ (1 Petro 4:3) Walipokuwa wakiendelea kujitahidi wabadilike, waliweza kupata nguvu kwa kukutana pamoja na Wakristo wenzao. Hivyo walitiwa moyo wajifunze Neno la Mungu na kulifuata. Na ikiwa wakati wa kufanya mabadiliko yaliyohitajiwa wangedhoofika au kujisikia wakitatizwa sana, wangeweza kupata msaada. Namna gani? Kwa kutembelea Wakristo waliokomaa na kuongea nao, kisha hao wangewahurumia, wafahamu shida zao na kuwajenga.—Mhubiri 4:9, 10: Ayubu 16:5.

16 Ikiwa wewe ungependa usaidizi huo, unakaribishwa uhudhurie mikutano ya Mashahidi wa Yehova. Wakristo wenye ujuzi utakaokuta huko watafurahi kukusaidia ujifunze mashauri ya Biblia na kuyatumia. Unapozidi kuwa na maendeleo upande huo, utaridhika kwa kujua kwamba unajitahidi kumpendeza Muumba wako. Nawe utakuwa umeingia katika njia inayoelekea kwenye afya bora na maisha marefu zaidi, pamoja na furaha.

[Mambo ya Kuzungumziwa]

Wewe una sababu gani za kujua kwamba Mungu anataka uwe na afya nzuri? (1-6)

Ni mashauri gani ya Biblia yanayohusu matumizi ya tumbako? (7-9)

Biblia inatusaidiaje katika maoni yetu juu ya vileo (pombe)? Katika maoni yetu juu ya dawa za kulevya? (10, 11)

Wewe una sababu gani za kufuata mashauri ya Mungu katika maisha yako? Kuna msaada gani? (12-16)

[Sanduku katika ukurasa wa 99]

“Sasa ushuhuda umeongezeka kuonyesha kwamba moshi wa sigara hauumizi mvutaji peke yake, bali unaumiza wale walio karibu naye pia. . . . Ikiwa wewe unavuta sigara inakupasa ufikirie tendo hilo litakuwa na matokeo gani katika mwili na maoni ya mtoto wako na pia katika wewe mwenyewe. Uvutaji wako mwenyewe ni hatari kwa afya ya mtoto wako.”—Dakt. Saul Kapel, mwandikaji wa habari za magazeti ya Kitiba.

[Sanduku katika ukurasa wa 101]

“Uchunguzi uliofanywa umeonyesha kwamba bangi inaleta matatizo ya afya yanayoweza kuwa hatari. Hayo ni pamoja na kuharibika kwa mapafu, na labda ugonjwa wa kansa, machafuko ya akili na mishipa ya fahamu, kushindwa kwa mwili kujikinga na magonjwa, kushindwa kufanya ngono vizuri, kuharibu chembeuzi za ukuzi wa mwili na hata kufanya watoto wazaliwe wakiwa na kasoro za mwili.”—Gazeti “Newsweek.”

[Picha katika ukurasa wa 97]

Usafi ni msaada wa kuwa na afya nzuri

    Maktaba Kwenye Mtandao (1980-2025)
    Toka
    Ingia
    • Kiswahili
    • Shiriki
    • Mapendezi
    • Copyright © 2025 Watch Tower Bible and Tract Society of Pennsylvania
    • Masharti ya Utumiaji
    • Sera ya Faragha
    • Mpangilio wa Faragha
    • JW.ORG
    • Ingia
    Shiriki