Watchtower MAKTABA KWENYE MTANDAO
Watchtower
MAKTABA KWENYE MTANDAO
Kiswahili
  • BIBLIA
  • MACHAPISHO
  • MIKUTANO
  • hp sura 17 kur. 161-167
  • Ni Sheria Za Nani Utakazotanguliza?

Hakuna video yoyote kwa sasa.

Samahani, haikuwezekana kupakia video.

  • Ni Sheria Za Nani Utakazotanguliza?
  • Furaha​—Namna ya Kuipata
  • Vichwa vidogo
  • Habari Zinazolingana
  • JE! TUTII SHERIA ZA KISERIKALI?
  • KUTII KWA KADIRI FULANI
  • Maswali Kutoka kwa Wasomaji
    Mnara wa Mlinzi Unaotangaza Ufalme wa Yehova—1991
  • Sheria za Mungu Hutufaidi
    Mnara wa Mlinzi Unaotangaza Ufalme wa Yehova—2002
  • Utii wa Kikristo kwa Sheria
    Kweli Iongozayo Kwenye Uzima wa Milele
  • Kuheshimu Mamlaka Ni kwa Maana Kabisa kwa Maisha Yenye Amani
    Amani na Usalama wa Kweli—Wewe Unaweza Kuupataje?
Pata Habari Zaidi
Furaha​—Namna ya Kuipata
hp sura 17 kur. 161-167

Sura ya 17

Ni Sheria Za Nani Utakazotanguliza?

TUNAISHI pamoja na sheria—sheria ya maumbile, au uumbaji; sheria zinazotoka kwa Mungu juu ya adili na mwenendo; sheria za kiserikali. Sisi tunazikubali nyingi za sheria hizo na kujifaidi nazo. Lakini namna gani ikiwa sheria fulani inaelekea kutuzuia isivyofaa? Au namna gani sheria mbili zinazokuhusu zikipingana?

2 Kwa kuwa sheria za maumbile zinaongoza mtu atake asitake, watu wengi sana wanazifuata bila ubishi wo wote. Ni mtu gani angekataa kutii sheria ya uvutano, ajiangushe kutoka genge (jiwe kubwa) refu? Sheria hiyo inatufaidi; inafanya nyayo zetu zisiinuke tunapotembea na kukifanya chakula chetu kikae katika sahani. Sheria nyingine za maumbile zinahusu hali za kurithi tabia za wazazi, ambazo zinaamua namna watoto wetu watakavyokuwa. Kwa kufuata sheria za kurithi tabia za wazazi na kuepuka kuoana na mtu wa ukoo wa karibu, tunaiepuka hatari ya kupitishia watoto wetu hitilafu (kasoro) fulani za kimwili. (Linganisha Mambo ya Walawi 18:6-17.) Lakini namna gani sheria zinazohusu mwenendo au adili?

3 Watu wengi wanakuza maoni ya kuchukia sheria zilizotungwa. Sababu moja ni kwamba wanadamu wamekuwa na maelekeo ya kufanyiza sheria zisizohitajiwa na kugandamiza wenzao kwa kutumia sheria. (Mathayo 15:2; 23:4) Walakini, ni hatari kuziona sheria zote kuwa mbaya au kuzoea kuzipuza.

4 Hali ya kufa kwa wanadamu inapochunguzwa, inaonekana ilitokea kwa kuasi sheria huko nyuma. Mungu aliwakataza Adamu na Hawa wasile matunda ya ule mti wa ujuzi wa mema na mabaya. Lakini Shetani akadokezea Hawa kwamba sheria ya Mungu ilikuwa ikiwazuia isivyofaa. (Mwanzo 3:1-6) Takwa la Shetani lilikuwa—‘Kusiwe sheria. Jiwekeeni viwango vyenu wenyewe.’ Roho hiyo ya kupinga sheria imefuatwa na watu wengi sana muda wote wa historia, hata leo hii.

5 Yehova hagandamizi watu wake kwa kuwawekea sheria zenye kuwakataza mambo au kuwalemea bure tu, kwa maana “mahali ilipo ile roho ya Yehova, pana uhuru.” (2 Wakorintho 3:17, NW; Yakobo 1:25) Lakini, Yehova ndiye Mtawala Mwenye Enzi Kuu Zaidi katika ulimwengu mzima, ingawa Shetani hataki watu waamini hivyo. Yehova ndiye Muumba wa ulimwengu huo na pia ndiye Mpaji-Uzima na Mpaji-Riziki wetu. (Matendo 4:24; 14:15-17) Basi ana haki ya kutuelekeza na kufanyiza sheria za kuongoza mwenendo wetu.

6 Watu wengi wanakubali kwamba Mungu ndiye mwenye mamlaka ya kukata maneno, na kwa hiyo ana haki ya kuagiza wanadamu juu ya mambo wanayoweza na wasiyoweza kuyafanya. Yaani, wanakubali kwamba ana haki ya kufanya hivyo, lakini wanapotaka sana kufanya jambo fulani analokataza Mungu hawafuati maagizo yake. Hiyo ni hatari sana. Kuna uthibitisho wa kutosha kwamba amri za Mungu zimewekwa kwa faida yetu. Kwa mfano, tukiepuka ulevi, hasira nyingi na kutamani sana vitu, tutasaidika tufurahie afya bora na kupata uradhi mwingi zaidi. (Zaburi 119:1-9, 105) Vilevile, sheria za Mungu zinaweza kutusaidia tupate kibali na wokovu kutoka kwake. (Mithali 21:30, 31) Kwa hiyo hata ikiwa watu hawajafahamu bado sababu iliyomfanya Yehova atoe amri fulani-fulani, ni upumbavu kwa watu hao kukataa kutii, labda kwa sababu ya kujitegemea wenyewe kwa kiburi.

7 Mfano mmoja unaoonyesha amri ambazo Mungu ametolea Wakristo ni agizo lililotolewa na halmashauri ya wale mitume na wanaume wazee katika Yerusalemu, waliokuwa baraza yenye kuongoza kundi la kwanza la Kikristo:

“Roho takatifu na sisi wenyewe tumependelea tusiongeze mzigo zaidi kwenu ninyi, isipokuwa mambo haya ya lazima, kuendelea kushika mwiko wa vitu vinavyotolewa dhabihu kwa sanamu na wa damu na wa vitu vinavyonyongwa na wa uasherati.”—Matendo 15:22-29, NW.

8 Tuna sababu nzuri za kutufanya tutii sheria ya Mungu inayokataza “uasherati”—kulindwa tusiwe na magonjwa, uzazi-haramu, ndoa zilizovunjika. Sheria hiyo ina maana ya kwamba haiwapasi wanaume kulalana na wanaume wenzao, wanawake na wanawake wenzao, wala haiwapasi watu kufanya uchafu mwingineo mzito unaohusiana na viungo vya uzazi. Uchafu wa namna zote hizo ndiyo maana ya neno la Kigiriki porneia (uasherati) lililotumiwa katika Matendo 15:29. (Warumi 1:24-27, 32) Lakini namna gani kama zile hatari za “uasherati” zingeweza kuepukwa? Je! bado tungeitii amri ya Mungu kwa sababu kwetu sisi yeye ndiye Mtawala Mwenye Enzi Kuu? Tukifanya hivyo, tunasaidia kuthibitisha kwamba Shetani ni mwongo, kwamba wanadamu watamtii Yehova kwa sababu wanampenda.—Ayubu 2:3-5; 27:5; Zaburi 26:1, 11.

9 Agizo hilo lililoonyeshwa wazi katika Matendo 15:22-29 linajulisha sehemu nyingine ambayo katika hiyo tunaweza kuonyesha utii wetu. Mungu anatuamuru ‘tuepukane na damu’ na nyama za wanyama walionyongwa ili damu ibaki ndani yao. Mungu alimwambia Noa babu yetu wa kale kwamba wanadamu wana ruhusa ya kula nyama ya wanyama, lakini haiwapasi kamwe kuendeleza uhai wao kwa kutumia damu ya kiumbe kingine. (Mwanzo 9:3-6) Wakati Mungu alipokuwa akirudia sheria yake akiwaambia Waisraeli, alisema kwamba “uhai wa mwili u katika hiyo damu.” Njia ya pekee ambayo walitakwa kutumia damu ni kuiweka juu ya madhabahu ilipie dhambi. Ama sivyo, damu iliyotoka kwa kiumbe fulani ilipasa kumwagwa chini, tendo hilo likiwa mfano wa kwamba ilikuwa ni kama inamrudia Mungu. Kutii sheria hiyo kulimaanisha uzima au kifo.—Mambo ya Walawi 17:10-14.

10 Dhabihu hizo zilifananisha kumwagwa kwa damu ya Yesu kwa ajili yetu. (Waefeso 1:7; Ufunuo 1:5; Waebrania 9:12, 23-28) Hata baada ya Kristo kurudi mbinguni, Mungu aliwaamuru Wakristo ‘washike mwiko wa kutokula damu.’ Lakini ni watu wangapi wanaodai kuwa Wakristo wanaomtii katika shauri hili Mpaji Sheria na Mpaji-Uzima wa Kimungu? Mahali pengine pengine ni kawaida ya watu kuchanganya nyama yenye damu na vyakula vyao, utumbo wenye damu au kula chakula cha namna nyingine kilichotiwa damu kwa makusudi.

11 Vivyo hivyo, watu wengi wamekubali kutiwa damu mishipani wakijaribu kurefusha maisha yao. Mara nyingi wanakosa kujua kwamba kutiwa damu mishipani kunaweza kwenyewe kuwatia katika hatari kubwa za kiafya na kwamba karibu kila namna ya upasuaji inaweza kufanywa bila damu. Inaweza kufanywa kwa kutumia matibabu mengine.a Lakini hata kama ingeonekana kwamba maisha yameingia hatarini, je! lingekuwa kosa kumtii Mungu? Sheria ya kimungu haipasi kamwe kupuzwa hata wakati wa hatari.—1 Samweli 14:31-35.

12 Watu wengi wamekubali kufa kwa sababu ya kutetea imani yao ya uhuru wa kusema au wa kuabudu, au hata wengine kwa sababu ya kushikilia wazo fulani la kisiasa. Wametii mtawala au amiri wa kijeshi bila kujali ni hatari gani iliyokuwa mbele yao. Je! sisi hatuna sababu zenye kutulazimisha zaidi tumtii yule aliye Mwenye Enzi Kuu katika ulimwengu mzima? ‘Kabisa kabisa,’ ndilo jibu la mfano wa ukamilifu uliowekwa na watu wengi wenye imani. (Danieli 3:8-18; Waebrania 11:35-38) Wao walijua, kama inavyotupasa sisi pia kujua, kwamba Yehova ndiye Mpaji-Uzima na atawakumbuka na kuwapa thawabu wale wanaomtii yeye—na iwapo lazima, awarudishie uhai kwa kuwafufua katika wakati wake. (Waebrania 5:9; 6:10; Yohana 11:25) Tunaweza kuwa na uhakika wa kwamba kumtii Yehova ndio mwendo unaofaa na wenye faida za kudumu, hata hali iwe ni ya namna gani.—Marko 8:35.

JE! TUTII SHERIA ZA KISERIKALI?

13 Sheria nyingine nyingi zinazotuhusu zinatokana na serikali za kilimwengu. Mkristo azioneje sheria hizo? Mtume Paulo aliandika hivi: “Kumbusha watu waitii kwa ushikamanifu serikali na maafisa wayo, wazitii sheria.”—Tito 3:1, The New American Bible.

14 Katika karne ya kwanza W.K., serikali ya Kirumi haikutenda haki nyakati zote, na wengine wa watawala walikuwa wenye maisha machafu na ya udanganyifu. Hata hivyo Paulo alisema: “Kila nafsi na itii mamlaka zilizo kuu, kwa maana hakuna mamlaka isipokuwa kwa njia ya Mungu.” Zile “mamlaka zilizo kuu” ndizo serikali za kilimwengu zilizopo.—Warumi 13:1, NW.

15 Yehova anakubali kwamba serikali za watu zitaendelea kutimiza makusudi fulani yenye mafaa mpaka utawala wake utakaporudishwa duniani kwa ukamili. Serikali hizo zinasaidia kudumisha hali ya kiasi fulani cha utengemano katikati ya watu na kuwatolea utumishi mwingi wa namna namna, pamoja na kuandikisha ndoa na uzazi. (Linganisha Luka 2:1-5.) Kwa njia hiyo Wakristo wanaweza kwa ujumla ‘kuendelea kuishi kwa utulivu pamoja na utawa na uzito kamili.’—1 Timotheo 2:2, NW.

16 Wakati Wakristo wanapoungoja wakati ambao ufalme wa Mungu utayatatua matatizo ya vita, udhalimu na uonezi, haiwapasi ‘kupinga ile mamlaka’ ya serikali za watu. Inawapasa walipe bila udanganyifu kodi zinazotakwa, watii sheria na kuwapa watawala heshima. Kwa sababu ya kufuata mwendo huo Wakristo wa kweli wamesifiwa mara nyingi na kusaidiwa na maafisa (wakuu), na si mara nyingi wanapopewa adhabu kwa ule “upanga” unaotumiwa kuadhibu wavunjaji wa sheria.—Warumi 13:2-7, NW.

KUTII KWA KADIRI FULANI

17 Nyakati nyingine sheria zinapingana. Huenda serikali ya watu ikataka mtu afanye jambo fulani linalokatazwa na Mungu. Au huenda sheria ya kiserikali ikakataza jambo ambalo Mungu anaamuru Wakristo wafanye. Hapo iweje?

18 Hali hiyo ya kupingana ilitukia wakati watawala walipokataza mitume wasihubiri habari za Yesu Kristo aliyefufuliwa. Soma masimulizi hayo yanayotia imani nguvu kwenye Matendo 4:1-23; 5:12-42. Ingawa mitume walifungwa gerezani na kupigwa mijeledi, hawakuacha kuhubiri. Petro alisema: “Inatupasa kumtii Mungu kuwa mtawala kuliko wanadamu.”—Matendo 5:29, NW.

19 Kwa hiyo kutii kwa Mkristo mamlaka za kiserikali ni kwa kadiri fulani tu. Wajibu wake wa kwanza ni kutii ile Mamlaka Kubwa Kupita Zote. Akipewa adhabu kwa sababu ya kuitii, anaweza kufarijika kwa kujua kwamba Mungu anakubali jambo analolifanya.—1 Petro 2:20-23.

20 Wakristo wa kwanza walielekeana na maamuzi katika upande mwingine uliohusu maelekezo ya Mungu na matakwa ya serikali ya Kirumi. Maamuzi hayo yalihusu kuliunga mkono jeshi la Kirumi au kuwa katika jeshi lenyewe. Mungu alikuwa amesema hivi juu ya watu wake: “Nao watafua panga zao ziwe majembe, na mikuki yao iwe miundu; taifa halitainua upanga juu ya taifa lingine, wala hawatajifunza vita tena kamwe.” (Isaya 2:4; Mathayo 26:52) Basi, ikiwa serikali ya Kirumi ingedai Mkristo aingie katika jeshi au aziunge mkono jitihada za kivita, hapo mpingano ungetokea kati ya sheria ya Kaisari na ya Mungu.

21 Pia Wakristo wa kwanza waliiweka mbele sheria ya Mungu walipoagizwa na wanadamu wamtolee uvumba (ubani) Kaisari wa Rumi akidhaniwa kuwa mungu. Labda watu wengine walidhani tendo hilo lilikuwa la kizalendo. Lakini historia inatuambia kwamba Wakristo waliliona kuwa namna fulani ya ibada ya sanamu. Walikataa kufanyia mtu au kitu cho chote matendo ya kuabudu sanamu, kwa maana walijua ibada yao ilikuwa ya Yehova pekee. (Mathayo 22:21; 1 Yohana 5:21) Tena wao hawakuhusika katika siasa, wala kupaza sauti za kutolea mtawala sifa ya kumwabudu, bali waliendelea kutokuwamo wasiwe “sehemu ya ulimwengu,” kama Yesu alivyokuwa amewahimiza.—Yohana 15:19, NW; Matendo 12:21-23.

22 Je! wewe utayakubali mawazo na maelekezo ya Mungu yanayohusiana na sheria? Kufanya hivyo kutakulinda na huzuni nyingi zinazopata watu wanaodharau sheria za Mungu juu ya mwenendo na adili. Wala hutapewa adhabu bila sababu na mamlaka za kiserikali zilizopo. Lakini zaidi ya yote, mawazo ya Mungu juu ya shauri hilo yanatia ndani kumkubali yeye kuwa Mtawala Mkuu Kupita Wote. Ukifanya hivyo chini ya hali zote, utastahili kuwapo wakati sheria za ufalme wa Mungu zitakapoenea pote katika dunia nzima karibuni.—Danieli 7:27

[Maelezo ya Chini]

a Maoni ya kidini, ya mwenendo na tiba juu ya jambo hili yameonyeshwa katika kijitabu Jehovah’s Witnesses and the Question of Blood (Les Ternoins de Jehovah et is Question du Sang).

[Mambo ya Kuzungumziwa]

Kwa nini inatupasa tufikirie tutakuwa na maoni gani juu ya sheria? (1-4)

Tunahitaji kukubali nini juu ya sheria za Mungu? (5, 6)

Tuna sababu gani za kutii sheria ya Mungu inayokataza “uasherati”? (7, 8)

Tunawezaje kutii sheria ya Mungu juu ya damu? (9-11)

Sababu gani inatupasa tumtii Mungu hata kama uhai wetu umo hatarini? (12)

Inawapasa Wakristo wawe na maoni gani juu ya serikali za kilimwengu, na kwa sababu gani? (Mathayo 22:19-21) (13-16)

Ni mwendo gani unaofaa kufuatwa sheria ya Mungu na sheria ya kilimwengu zikipingana? Toa mfano. (17-21)

Sasa tunaelekeana na jaribu gani? (22)

[Sanduku katika ukurasa wa 167]

“Uchunguzi wa uangalifu juu ya habari zote zilizopo unaonyesha kwamba, kufikia wakati wa Marko Aurelio [aliyekuwa mtawala mwenye amri tangu mwaka 161 mpaka 180 W.K.], hakuna Mkristo aliyepata kuwa askari; wala hakuna askari aliyeendelea kuwa katika utumishi wa kijeshi baada ya kuwa Mkristo.”—“The Rise of Christianity.”

    Maktaba Kwenye Mtandao (1980-2025)
    Toka
    Ingia
    • Kiswahili
    • Shiriki
    • Mapendezi
    • Copyright © 2025 Watch Tower Bible and Tract Society of Pennsylvania
    • Masharti ya Utumiaji
    • Sera ya Faragha
    • Mpangilio wa Faragha
    • JW.ORG
    • Ingia
    Shiriki