Watchtower MAKTABA KWENYE MTANDAO
Watchtower
MAKTABA KWENYE MTANDAO
Kiswahili
  • BIBLIA
  • MACHAPISHO
  • MIKUTANO
  • tp sura 12 kur. 129-141
  • Kuheshimu Mamlaka Ni kwa Maana Kabisa kwa Maisha Yenye Amani

Hakuna video yoyote kwa sasa.

Samahani, haikuwezekana kupakia video.

  • Kuheshimu Mamlaka Ni kwa Maana Kabisa kwa Maisha Yenye Amani
  • Amani na Usalama wa Kweli—Wewe Unaweza Kuupataje?
  • Vichwa vidogo
  • Habari Zinazolingana
  • Maoni Yafaayo Juu ya Mamlaka ya Kilimwengu
  • Mamlaka Ndani ya Nyumba
  • Katika Kundi la Kikristo
  • Kwa Nini Tuheshimu Mamlaka?
    “Jitunzeni Katika Upendo wa Mungu”
  • Ni Mamlaka ya Nani Unayopaswa Kutambua?
    Ujuzi Uongozao Kwenye Uhai Udumuo Milele
  • Maoni ya Mkristo Kuhusu Mamlaka
    Mnara wa Mlinzi Unaotangaza Ufalme wa Yehova—1994
  • Heshima kwa Mamlaka—Kwa Nini Ni Muhimu?
    Mnara wa Mlinzi Unaotangaza Ufalme wa Yehova—2000
Pata Habari Zaidi
Amani na Usalama wa Kweli—Wewe Unaweza Kuupataje?
tp sura 12 kur. 129-141

Sura 12

Kuheshimu Mamlaka Ni kwa Maana Kabisa kwa Maisha Yenye Amani

1-3. (a) Ni nini ambacho kimeshiriki kuleta kukataliwa kwa mamlaka mahali pote katika siku zetu? (b) Mwelekeo huo unaonyeshwa katika njia gani mbalimbali? (c) Ni wapi ambapo jambo hilo limegeuza sana mambo?

ROHO ya kujitegemea inaenea katika ulimwengu wa leo. Hali ya ujumla ya kutotumaini mamlaka imesitawi, hasa miongoni mwa wale waliozaliwa tangu Vita ya Ulimwengu ya Pili. Kwa sababu gani? Kwanza, wazazi wao walikuwa wameona uonevu kwa kadiri isiyopata kutokea zamani, na vilevile matumizi ya wenye mamlaka ya mbinu za ugandamizaji na ufisadi. Walikuza maoni yasiyo na matumaini mazuri kutoka kwa wenye mamlaka. Kwa sababu hiyo, wengi wao walipokuja kuwa wazazi, hawakukaza kikiki katika watoto wao heshima kwa mamlaka. Wala mambo hayakupata nafuu wakati watoto hao walipoona matendo rasmi ya ukosefu wa haki. Matokeo ni kwamba imekuwa kawaida kutoheshimu mamlaka.

2 Ukosefu huo wa heshima unaonyeshwa kwa njia mbalimbali. Nyakati nyingine unaonyeshwa kwa kuchagua namna fulani ya kuvaa au kujipamba inayoonyesha kukataa viwango vinavyokubaliwa. Huenda ukatia ndani kuwakaidi mapolisi hadharani, au hata jeuri na umwagaji wa damu. Lakini si hayo tu. Hata miongoni mwa watu wasioonyesha maoni yao katika njia hizo za wazi zaidi, wengi wanapuuza sheria au kuziepa iwapo hawakubaliani nazo au iwapo wanaona haziwaruhusu wapate mafaa.

3 Hali hiyo imeyageuza sana mambo nyumbani, shuleni, kwenye mahali pa kazi, na katika kushughulika na maafisa wa serikali. Watu wengi zaidi na zaidi hawataki mtu ye yote akiwaambia la kufanya. Wanajitahidi kufikia wanachokiamini kuwa uhuru mkubwa zaidi. Ukielekewa na hali hiyo, wewe utafanyaje?

4. Kwa yale tunayoyafanya katika jambo hili, tunaonyesha mwelekeo wetu juu ya suala gani?

4 Mwendo wako utaonyesha msimamo wako juu ya suala la enzi kuu ya Yehova ya ulimwengu wote mzima. Je! wewe unamheshimu Yehova kweli kweli kama Chanzo cha amani na usalama wa Kweli? Je! utatafuta kujua na kutumia katika maisha yako mambo yanayoelekezwa na Neno lake? Au je! utaambatana na wanadamu wale ambao kwa kujitegemea wanafanya maamuzi yao wenyewe juu ya yaliyo mema na yaliyo mabaya?—Mwanzo 3:1-5; Ufunuo 12:9.

5. (a) Mara nyingi ni nini kinachotokana na kufuata uongozi wa wanadamu wanaoahidia “uhuru”? (b) Mtu anayefanya mapenzi ya Mungu yuko huru kadiri gani?

5 Maarifa sahihi ya Biblia yanaweza kukulinda dhidi ya kupotezwa na wale ambao, wajapokuwa ‘wanaahidia uhuru, wao wenyewe ni watumwa wa uharibifu.’ Kuufuata uongozi wa watu hao kungekuweka tu katika hali ya utumwa kama yao. (2 Petro 2:18, 19) Uhuru wa kweli unaweza kupatikana kwa kujifunza tu na kufanya mapenzi ya Mungu. Amri yake ya kimungu ndiyo “sheria kamilifu iliyo ya uhuru.” (Yakobo 1:25) Inaweza kusemwa hivyo kwa sababu Yehova hatuwekei sisi vizuizi pasipo uhitaji, akituzuia-zuia kwa amri zisizokuwa na kusudi lenye mafaa. Lakini sheria yake inaandaa aina ya mwongozo unaoleta uhuru, amani, na usalama unaotegemea kuwa na uhusiano mwema na Mungu na mwanadamu mwenzetu.

6, 7. (a) Ni nani aliye katika hali nzuri zaidi ya kuyaondoa matumizi mabaya ya mamlaka? (b) Yesu alionyeshaje yale yanayowapata watu wanaochukua sheria mikononi mwao?

6 Mungu anaijua vizuri zaidi ya mtu mwingineye yote kadiri ya ufisadi wa mwanadamu na matumizi yake mabaya ya mamlaka. Naye ametoa ahadi yake kwamba atawataka wenye kufanya uonevu watoe hesabu, hata kama wana vyeo vya juu namna gani. (Warumi 14:12) Katika wakati uliowekwa rasmi wa Mungu, “waovu watatengwa na nchi, nao wafanyao hila watang’olewa.” (Mithali 2:22) Lakini kama tukikosa subira na kuchukua sheria mikononi mwetu, hii haitatuletea faida yo yote yenye kudumu.—Warumi 12:17-19.

7 Katika usiku wa kusalitiwa na kukamatwa kwake, Yesu alitilia hilo mkazo kwa mitume wake. Kwa sababu ya hali zilizokuwamo nchini, kutia na kuwapo kwa wanyama wa mwitu, mara nyingi watu walitembea wakiwa wamechukua silaha. Kwa hiyo katika pindi hiyo zilikuwapo panga mbili miongoni mwa mitume wa Yesu. (Luka 22:38) Kulitukia nini? Basi, wao waliona haki ikipotoshwa wazi sana wakati Yesu alipokuwa akikamatwa bila sababu. Kwa hiyo haraka haraka mtume Petro akachomoa upanga wake na kulikata sikio la mmojawapo watu wale. Lakini Yesu alilirudisha sikio lililokatwa na kumwonya Petro kwa upole hivi: “Rudisha upanga wako mahali pake; maana wote waushikao upanga, wataangamia kwa upanga.” (Mathayo 26:52) Hata katika siku zetu, watu wengi wangaliweza kuokolewa wasipatwe na kifo cha mapema mno kwa kulifuata shauri hilo.—Mithali 24:21, 22.

Maoni Yafaayo Juu ya Mamlaka ya Kilimwengu

8. (a) Kama inavyoelezwa kwenye Warumi 13:1, 2, inawapasa Wakristo waoneje juu ya watawala wa kilimwengu? (b) Ni nini maana ya taarifa “zimewekwa na Mungu katika vyeo vinavyozihusu”?

8 Alipokuwa akiwaandikia Wakristo katika Roma, mtume Paulo aliongozwa na roho ya Mungu azungumze namna walipaswa wajiongoze kuhusiana na mamlaka za kilimwengu. Yeye aliandika hivi: “Acheni kila nafsi itii mamlaka zilizo kuu, maana hakuna mamlaka isipokuwa kwa njia ya Mungu; mamlaka zilizopo zimesimama zikiwa zimewekwa na Mungu katika vyeo vinavyozihusu. Basi yeye anayepinga mamlaka amechukua msimamo dhidi ya mpango wa Mungu; wale ambao wamechukua msimamo dhidi yao watapokea hukumu kwao wenyewe.” (Warumi 13:1, 2, NW) Je! hiyo maana yake ni kwamba Mungu ndiye amewapa watawala hao wa kilimwengu uwezo? Biblia inajibu hapana waziwazi! (Luka 4:5, 6; Ufunuo 13:1, 2) Lakini wapo kwa ruhusa yake. Na ‘cheo kinachozihusu’ ambacho zimekalia katika historia yote ya kibinadamu kiliamuliwa na Mungu. Cheo hicho kimekuwa nini?

9. Ingawa maafisa wanajitia katika mazoea mabaya, kwa sababu gani tunaweza kuwaheshimu?

9 Andiko lililotajwa sasa hivi linasema ni ‘kikuu.’ Hivyo maafisa wa serikali hawapaswi kutendwa ukosefu wa heshima. Sheria wanazozifikiliza hazipasi kudharauliwa. Hiyo haimaanishi kwa lazima kwamba uvutiwe na watu hao mmoja mmoja, wala kwamba ukubali ufisadi wo wote ambao huenda wanafanya. Lakini heshima inaonyeshwa kwa kufaa kwa sababu ya cheo walicho nacho.—Tito 3:1, 2.

10. Kulipa kodi kumepasa kuonweje, na kwa sababu gani?

10 Kwa kadiri kubwa, sheria za kilimwengu zinafaidi. Zinasaidia kudumisha utengemano na kutoa uhakikisho wa kadiri fulani ya ulinzi kwa watu na mali zao. (Warumi 13:3, 4) Pia, kwa kawaida serikali zinaandaa barabara, utumishi wa kutunza afya, ulinzi dhidi ya moto, elimu, na utumishi mwingine unaowapa watu manufaa. Je! wamepaswa walipwe kwa ajili ya utumishi huo? Je! tulipe kodi mbalimbali? Mara nyingi ulizo hilo linatokeza maoni ya chuki kwa sababu ya kodi za juu na matumizi mabaya ya mara kwa mara ya pesa za serikali. Katika wakati wa Yesu, pia, ulizo hilo lilihusika na mawazo ya kisiasa. Lakini Yesu hakushikilia kwamba hali iliyokuwapo ilitoa ruhusa yo yote ya kukataa kulipa kodi. Akirejeza kwenye pesa iliyokuwa imetengenezwa na Kaisari wa Kiroma, alisema hivi: “Mlipeni Kaisari yaliyo ya Kaisari, na Mungu yaliyo ya Mungu.” (Mathayo 22:17-21; Warumi 13:6, 7) Hapana, Yesu hakuliunga mkono wazo la kila mtu kufanya anavyoona mwenyewe.

11, 12. (a) Maandiko yanaonyeshaje kwamba kuna mamlaka nyingine inayopaswa kufikiriwa? (b) Wewe ungefanyaje kama watawala wa kilimwengu wangetoa maagizo yenye kupingana na matakwa ya Mungu, na kwa sababu gani?

11 Hata hivyo, Yesu alionyesha kwamba “Kaisari,” serikali ya kilimwengu, haikuwa ndiyo mamlaka ya pekee ya kufikiriwa. “Mamlaka zilizo kuu” si kuu kuliko Mungu wala hata hazilingani naye. Tofauti na hivyo, zina cheo kidogo sana kwa kulinganishwa naye. Kwa hiyo uwezo wazo una mipaka, si kamili. Kwa sababu hiyo, mara nyingi Wakristo wamekabiliwa na uamuzi mgumu. Ni uamuzi ambao lazima nawe pia uelekeane nao. Wakati ambao wanadamu wenye uwezo wanapojidaia kilicho cha Mungu, wewe utafanya nini? Wakikataza jambo linaloamriwa na Mungu, wewe utamtii nani?

12 Mitume wa Yesu walieleza msimamo wao kwa heshima lakini kwa uthabiti kwa kuwaambia washiriki wa mahakama kuu katika Yerusalemu: “Sisi hatuwezi kuacha kusema juu ya mambo ambayo tumeona na kusikia. . . . Ni lazima sisi tutii Mungu kuwa mtawala kuliko wanadamu.” (Matendo 4:19, 20; 5:29, NW) Nyakati nyingine serikali zimeweka vizuizi nyakati za dharura, na hiyo inaeleweka. Lakini nyakati nyingine vizuizi vya kiserikali huenda vikafanyizwa ili kuvuruga ibada yetu kwa Mungu na kufanya isiwezekane kutimiza wajibu mbalimbali tuliopewa na Mungu. Iweje basi? Neno la Mungu lililoongozwa na roho linajibu: “Lazima sisi tutii Mungu kuwa mtawala kuliko wanadamu.”

13, 14. (a) Imetupasa tuwe waangalifu kadiri gani tusije tukakosa kutii sheria za kilimwengu kwa sababu za kibinafsi tu? (b) Onyesha sababu za hili kutokana na Maandiko.

13 Ingawa kuheshimu wajibu huo kwa Mungu huenda kukapingana na yale ambayo “Kaisari” anataka, kufanya hivyo ni tofauti na kuvunja kwa njia ya kujitegemea sheria tusizokubaliana nazo. Ni kweli kwamba huenda sheria fulani zikaelekea kuwa zisizohitajiwa au zenye kuzuia mno, kulingana na maoni ya kibinafsi. Lakini hiyo haimpi mtu haki ya kupuuza sheria zisizopingana na sheria za Mungu. Matokeo yangekuwa nini kama watu wote wangetii sheria zile tu walizozifikiria kuwa zenye kuwafaidi wao wenyewe? Jambo hilo lingeweza kuleta machafuko ya utawala.

14 Nyakati nyingine huenda mtu akahisi kwamba anaweza kupuuza mamlaka na kufanya yale tu yanayompendeza yeye ati kwa sababu hataelekea kupatikana na kuadhibiwa. Lakini kuna hatari kubwa katika kufanya hivyo. Ijapokuwa huenda kwanza kudharau sheria kukahusu mambo madogo, kuachwa kwa mtu bila kuadhibiwa huenda kukamjasirisha kwenye tendo kubwa zaidi la kutokutii sheria. Kama inavyosema Mhubiri 8:11: “Kwa sababu hukumu juu ya tendo baya haitekelezwi upesi, mioyo ya wanadamu huthibitishwa ndani yao ili kutenda mabaya.” Lakini je! sababu halisi ya kutii sheria ni kuogopa adhabu tu kwa sababu ya kutokutii? Kwa Mkristo, unapasa uweko mvuto wenye nguvu zaidi. Mtume Paulo aliiita “sababu yenye kulazimisha”—tamaa ya kuwa na dhamiri safi. (Warumi 13:5, NW) Mtu ambaye dhamiri yake imezoezwa na kanuni za Kimaandiko anajua kwamba kufuatia mwendo wa kutokutii sheria kungekuwa kuchukua msimamo “dhidi ya mpango wa Mungu.” Bila kujali kama wanadamu wengine wanajua au hawajui tunayoyafanya, Mungu anajua, na matazamio yetu ya uzima wa wakati ujao yanamtegemea yeye.—1 Petro 2:12-17.

15. (a) Ni nini kinachopaswa kumwongoza mtu katika mwelekeo wake juu ya mwalimu au mwajiri-kazi? (b) Kwa njia hiyo tunaepuka kuongozwa na roho ya nani?

15 Ndivyo ilivyo na mwelekeo wa kijana juu ya mwalimu wake na mwelekeo wa mtu mzima juu ya mwajiri-kazi wake wa kilimwengu. Uhakika wa kwamba watu wengi walio karibu yetu wanafanya mabaya silo jambo linalopasa kuamua. Jambo la maana si kama mwalimu au mwajiri-kazi anajua tunayoyafanya. Ulizo ni, Yaliyo mema ni nini? Ni nini kinachompendeza Mungu? Tena, ikiwa yale ambayo tunaulizwa kufanya hayapingani na sheria ya Mungu au kanuni za uadilifu, tunafanya ushirikiano. Kwa ujumla walimu ni wawakilishi wa serikali ya kilimwengu na kwa sababu hiyo ni mawakili wa “mamlaka zilizo kuu.” Kwa hiyo wanastahili heshima. Na kwa habari ya waajiri-kazi wa kilimwengu, kanuni ya Biblia kwenye Tito 2:9, 10 inaweza kutumiwa, hata ingawa Paulo alikuwa akiandika juu ya uhusiano tofauti, ule wa watumwa kwa wenyeji wao. Paulo alisema: ‘Mwapendeze sana, . . . mkionyesha sana uaminifu mwema, kusudi [ninyi] mpate kukupamba kufundisha kwa Mwokozi wetu, Mungu, katika mambo yote.’ (Tito 2:9, 10, NW) Hivyo, tunaepuka uvutano wa Shetani, ambaye roho yake ‘inatenda kazi sasa katika wana wa kutokutii,’ nasi tunajenga uhusiano wenye amani na wanadamu wenzetu.—Waefeso 2:2, 3, NW.

Mamlaka Ndani ya Nyumba

16. Ni takwa gani la maisha ya kijamaa yenye upatani linaloelezwa katika 1 Wakorintho 11:3?

16 Sehemu nyingine ambamo heshima kwa mamlaka inaweza kufanyiza mahusiano yenye amani ni katika jamaa. Mara nyingi mno heshima hiyo inayofaa inakuwa imekosekana, na matokeo yanakuwa mvunjiko wa mahusiano ya kijamaa na mara nyingi kunatokea kugawanyika-gawanyika kati ya watu wa nyumba hiyo. Ni nini linaloweza kutendwa ili kufanya hali hiyo iwe bora? Kanuni ya ukichwa, kama inavyoonyeshwa kwenye 1 Wakorintho 11:3, ina jibu: “Kichwa cha kila mwanamume ni Kristo, na kichwa cha mwanamke ni mwanamume, na kichwa cha Kristo ni Mungu.”

17. (a) Kwa habari ya ukichwa, ni nini cheo cha mwanamume? (b) Kristo aliweka mfano gani mwema juu ya ukichwa wa mume?

17 Angalia kwamba taarifa hiyo ya mpango wa Yehova haielekezi kwanza kwenye ukichwa wa mwanamume. Badala yake, inavuta fikira kwenye uhakika wa kwamba kuna mtu ambaye mwanamume amepasa awe akimtegemea kwa mwelekezo, mtu ambaye inampasa awe akiufuata mfano wake. Mtu huyo ni Yesu Kristo. Yeye ndiye kichwa cha mwanamume. Na katika kushughulika na kundi lake, ambalo linafananishwa na bibi-arusi, Kristo aliionyesha njia ya kufanikisha ukichwa wa mume. Mfano wake mwema uliamsha itikio la nia ya kupenda katika wafuasi wake. Alipoongoza, badala ya kuwa bwana mkubwa, mkali na mwenye kudai kuwaelekea wafuasi wake, Yesu alikuwa “mpole na mnyenyekevu wa moyo,” hata wakapata burudisho kwa nafsi zao. (Mathayo 11:28-30) Je! yeye aliwadharau kwa sababu ya mapungukio yao? Tofauti na hivyo, yeye aliwashauri kwa upendo na hata akautoa uhai wake ili awasafishe dhambi. (Waefeso 5:25-30) Lo! ni baraka kama nini kwa watu wa nyumba yo yote kuwa na mwanamume anayejaribu kwa moyo mweupe kuufuata mfano huo!

18. (a) Ni kwa njia gani mbalimbali mke anaweza kuonyesha kwamba anaiheshimu mamlaka ya mumeye? (b) Imewapasa watoto waonyesheje heshima kwa wazazi wao, na kwa sababu gani?

18 Kunapokuwa na ukichwa huo nyumbani, si vigumu kwa mwanamke kumheshimu mumewe. Nao utii wa watoto kwa wazazi wao unakuja kwa vyepesi zaidi. Lakini kuna mengi ambayo mke na watoto wanaweza kushiriki kuyafanya walete furaha ya kijamaa. Mke anaonyesha kwamba ana ‘heshima yenye kina kirefu kwa mumeye’ kwa bidii yake katika kutunza watu wa nyumba yake na kwa roho yake ya ushirikiano. Je! ndivyo ilivyo katika nyumba yako? (Waefeso 5:33; Mithali 31:10-15, 27, 28) Kwa habari ya watoto, wakimtii baba na mama kwa nia ya kupenda, hiyo inaonyesha kwamba wanawaheshimu wazazi wao, kama Mungu anavyotaka. (Waefeso 6:1-3) Je! hakungekuwako amani zaidi, na hisia nyingi zaidi ya usalama wa kibinafsi katika nyumba ya namna hiyo kuliko katika moja ambamo heshima kwa mamlaka inakosekana?

19. Ikiwa ni wewe peke yako katika jamaa unayejaribu kuongozwa na Neno la Mungu, inakupasa ufanye nini?

19 Unaweza kusaidia kufanya kao lako liwe mahali pa namna hiyo. Bila ya kujali kama washiriki wengine wa jamaa wanachagua kutegemeza njia za Yehova au sivyo, wewe unaweza kufanya hivyo. Huenda wale wengine wakaufuata mfano wako mwema. (1 Wakorintho 7:16; Tito 2:6-8) Hata wasipofanya hivyo, utakayoyafanya yatasimama yakiwa ushuhuda wa kufaa kwa njia za Mungu, na hilo ni jambo lenye thamani kubwa.—1 Petro 3:16, 17.

20, 21. (a) Biblia inaonyeshaje kwamba mamlaka ya mume na ya wazazi si kamili? (b) Kwa hiyo, huenda mke Mkristo au watoto wanaoamini wakaelekewa na uamuzi gani, na imewapasa wasukumwe na nini?

20 Kumbuka kwamba mpango wote wa mamlaka ya kijamaa umetokana na Mungu. Hivyo wanaume wanapaswa kujiweka chini ya Kristo, wake chini ya waume zao “kama ipendezavyo katika Bwana,” na watoto chini ya wazazi wao “maana jambo hili lapendeza katika Bwana.” (Wakolosai 3:18, 20; 1 Wakorintho 11:3) Kwa hiyo Mungu hawezi kuwekwa nje ya jambo hilo, au anaweza? Hiyo maana yake ni kwamba mamlaka ya mume juu ya mkeye, na ya wazazi juu ya watoto wao, ni ya kadiri tu. Yaani, mwenzi Mkristo na watoto wanapaswa kujiweka chini ya Mungu na Kristo kwanza, wakitii mashauri yao. Kwa wenzi wengine au wazazi wasioamini huenda wazo hilo likawa lisilopendeza kwanza. Lakini kwa kweli linawafaidi, kwa sababu litasaidia kufanya mwenzi anayeamini, na watoto, wawe wenye kutegemeka na wenye kuonyesha heshima zaidi.

21 Hata hivyo, namna gani kama mume angedai mkeye afanye jambo fulani ambalo lisingekuwa ‘lenye kupendeza katika Bwana’? Atakalofanya mke litaonyesha kama kweli ‘anamwogopa Mungu wa kweli’ au sivyo. (Mhubiri 12:13, NW) Ndivyo ilivyo watoto wanapokuwa wenye umri wa kutosha kulifahamu na kulitii Neno la Mungu. Ikiwa wazazi wao hawana tamaa kama yao ya kumtumikia Yehova, ni lazima watoto waamue kama watakuwa washikamanifu kwa Mungu au watawaunga mkono wazazi wao wasio washikamanifu. (Mathayo 10:37-39) Lakini kando ya wajibu wa kwanza walio nao kwa Mungu imewapasa watoto wawe watiifu katika “kila jambo,” hata iwapo hiyo inamaanisha kufanya mambo wasiyoyapenda. (Wakolosai 3:20, NW) Mwenendo huo huenda hata ukavuta wazazi wao kwenye maandalizi ya Yehova ya wokovu. Wakati msukumo wa matendo ya mtu unapokuwa ni ushikamanifu kwa Yehova na njia zake za uadilifu, badala ya kuwa ni ukosefu wa utii unaotokana na roho ya kujitegemea, jambo hilo “lapendeza katika Bwana” kweli kweli.

Katika Kundi la Kikristo

22, 23. (a) Waangalizi Wakristo wanawatumikiaje washiriki wa kundi? (b) Kwa hiyo, Waebrania 13:17 inasema imetupasa tuwe na mwelekeo gani juu yao?

22 Ushikamanifu uo huo kwa Yehova unapasa uonyeshwe katika mwelekeo wetu juu ya kundi lake la Kikristo na wale wanaolitunza. Yehova ameandaa waangalizi walichunge “kundi.” Wao hawapokei mshahara kwa kazi yao bali wanajitoa kwa sababu ya hangaiko la kweli kwa ndugu na dada zao Wakristo. (1 Petro 5:2; 1 Wathesalonike 2:7-9) Wanalisaidia kundi liitimilize kazi ya kuzihubiri habari njema za Ufalme wa Mungu. Pia, kwa kujali kila mshiriki wa kundi, wanasaidia washiriki hao wajifunze namna ya kutumia kanuni za Biblia katika maisha zao. Vilevile, ikiwa mshiriki ye yote wa kundi anachukua hatua fulani isiyo ya kweli bila kujua kwa ukamili, jitihada inafanywa kumrekebisha upya. (Wagalatia 6:1, NW) Mshiriki ye yote kidharau shauri la Kimaandiko na kuzidi tu kukaa katika kosa zito, waangalizi wanahakikisha kwamba ameondoshwa. Hivyo kundi linalindwa na mavutano yake yenye kutia ufisadi.—1 Wakorintho 5:12, 13.

23 Kwa kuthamini uandalizi huo wenye upendo wa Yehova wa kuhakikisha amani imo miongoni mwa watu wake, inatupasa tusikilize onyo la upole linalopatikana kwenye Waebrania 13:17: “Watiini wenye kuwaongoza, na kuwanyenyekea; maana wao wanakesha kwa ajili ya [nafsi] zenu, kama watu watakaotoa hesabu, ili kwamba wafanye hivyo kwa furaha wala si kwa kuugua; maana isingewafaa ninyi.”

24, 25. (a) Mambo ambayo wazee wanafundisha yamepasa yaongozeje namna tunavyowaona? (b) Ni wakati gani na mahali gani imetupasa tuyatumie yale tunayofundishwa kutokana na Biblia? Kwa sababu gani?

24 Biblia inakazia kwamba sababu moja kubwa inayofanya waangalizi hao au wazee wastahili heshima ni kwamba wanafundisha “neno la Mungu.” (Waebrania 13:7; 1 Timotheo 5:17) Na kuhusu uwezo wa “neno” hilo, Waebrania 4:12, 13, (NW) linasema hivi: “Neno la Mungu liko hai na linatokeza uwezo na limenoleka kuliko upanga wo wote wenye makali mawili na linapenya ndani mpaka kwenye ugawanyaji wa nafsi na roho, na wa viungo na mafuta yavyo, na linaweza kutambua fikira na makusudio ya moyo. Na hakuna uumbaji hata mmoja usioonekana wazi kwenye uonaji wake, bali vitu vyote viko uchi na vimefunuliwa waziwazi kwenye macho ya yeye ambaye sisi tuna hesabu ya kufanya pamoja naye.”

25 Hivyo kweli zilizo katika Neno la Yehova zinafunua wazi tofauti iliyopo kati ya vile ambavyo huenda mtu akaonekana kwa nje na vile alivyo kweli kweli. Ikiwa yeye anamwamini Mungu kikweli na anatamani kikweli kumpendeza Muumba wake, msukumo wa matendo yake utaonyesha “utukufu wa Mungu” ifaavyo hata anapokuwa haonwi na wazee wa kundi. (Warumi 3:23) Yeye hangejitia katika mwenendo fulani usio wa Kimaandiko ati kwa sababu haumo kati ya makosa mazito ambayo yangeweza kufanya mtu aondoshwe katika kundi. Kwa sababu hiyo, ikiwa mtu ye yote anaelekea kupuuza shauri lo lote linalopatikana katika Neno la Mungu, inampasa achunguze kwa uangalifu mwelekeo wake kwa Mungu ni nini hasa. Je! yeye anaendelea kuwa kama mtu yule ambaye Zaburi 14:1, inasema hivi juu yake: “Mpumbavu amesema”—la, si peupe—bali “moyoni, Hakuna Mungu [Yehova, NW]”?

26, 27. (a) Kwa sababu gani ni jambo la maana kuchukua kwa uzito “kila tamko” la Yehova? (b) Maisha zetu zinapata matokeo gani wakati sisi tunapoheshimu mamlaka hivyo?

26 Wakati aliposhawishwa na Ibilisi, Yesu alitangaza hivi: “Lazima mwanadamu aishi kwa . . . kila tamko linalotoka kupitia kinywa cha Yehova.” (Mathayo 4:4, NW) Je! wewe unaamini kwamba “kila tamko” la Yehova ni la maana, kwamba hakuna hata moja linalopasa kupuuzwa? Kutii mengine ya matakwa ya Yehova, huku ukiyaona mengine kana kwamba hayana umaana, hakutoshi kabisa. Ama twautegemeza ufaaji wa enzi kuu ya Yehova ama twasimama upande wa Ibilisi wa lile suala kwa kujiwekea kiwango chetu wenyewe cha yaliyo mema na yaliyo mabaya. Wenye furaha ni wale wanaoonyesha kwamba wanaipenda sheria ya Yehova kweli kweli.—Zaburi 119:165.

27 Watu wa namna hiyo hawanaswi na roho ya ulimwengu yenye kuleta migawanyiko. Wala hawajitii katika mwenendo wa aibu wa wale wanaotupilia mbali vizuizi vya kiadili. Heshima yenye kina kirefu kwa Yehova na njia zake za uadilifu inazipa maisha zao uimara. Heshima ya namna hiyo kwa Yehova na njia zake inawawezesha kuwa na heshima inayofaa kwa mamlaka za kidunia, na kufanya hivyo ni jambo la maana kabisa kwa maisha yenye amani.

[Picha katika ukurasa wa 134]

Mitume wa Yesu waliambia mahakama kuu: “Ni lazima sisi tutii Mungu kuwa mtawala kuliko wanadamu”

    Maktaba Kwenye Mtandao (1980-2025)
    Toka
    Ingia
    • Kiswahili
    • Shiriki
    • Mapendezi
    • Copyright © 2025 Watch Tower Bible and Tract Society of Pennsylvania
    • Masharti ya Utumiaji
    • Sera ya Faragha
    • Mpangilio wa Faragha
    • JW.ORG
    • Ingia
    Shiriki