Sura ya 12
Zile “Siku za Mwisho” na Ule Ufalme
1. (a) Sasa kunatokea maulizo gani ya maana? (b) Maandiko yanasema nini juu ya siku za mwisho [i] wa dunia yetu, [ii] wa wale wanaoiharibu?
JE! SASA sisi tunaishi katika “siku za mwisho”? “Siku za mwisho” zina maana gani? Kwa matokeo mazuri, hakutakuwako “siku za mwisho” wa dunia yenyewe. Maana Biblia inatuhakikishia hivi: “Ile dunia . . . haitafanywa itikisike kwa wakati usiojulikana, au milele.” Kupatana na kusudi la kwanza la Yehova, uhai wa wanadamu na wanyama utaendelezwa hapa duniani milele. (Zaburi 104:5-24; 119:89, 90, NW; Mwanzo 1:27, 28; 8:21, 22) Walakini, hakika kuna “siku za mwisho” za mataifa yale yenye uovu na watu mmoja mmoja wanaoiharibu dunia ya Mungu. Ni ‘kuja’ kwa ule Ufalme kutakakoleta uharibifu kwa waharabu hao.—2 Petro 3:3-7; Yakobo 5:1-4; Ufunuo 11:15-18.
2. Ni mambo gani hasa ambayo Paulo alitabiria “nyakati za hatari” zetu?
2 Je! sasa inaweza kuwa kwamba tunaishi katika hizo “siku za mwisho”? Chukua tafsiri yo yote ya Biblia usome yale ambayo mtume Paulo aliongozwa na Mungu atabiri juu ya zile “siku za mwisho,” katika Timotheo wa Pili sura ya 3, mistari ya 1 mpaka 5. Kisha ujiulize, Je! hivi ndivyo ulimwengu wa wanadamu ulivyo leo? Hapa, mtume huyo anatabiri “nyakati za hatari,” na kuongeza hivi:
“Watu watakuwa wenye kujipenda wenyewe, wenye kupenda fedha, wenye kujisifu, wenye kiburi, wenye kutukana, wasiotii wazazi wao, wasio na shukrani, wasio safi, wasiowapenda wa kwao, wasiotaka kufanya suluhu, wasingiziaji, wasiojizuia, wakali, wasiopenda mema, wasaliti, wakaidi, wenye kujivuna, wapendao anasa kuliko kumpenda Mungu; wenye mfano wa utauwa, lakini wakikana nguvu zake; hao nao ujiepushe nao.”
3. Sababu gani bila shaka Paulo alikuwa akitaja “siku za mwisho” zenye hatari kushinda za ule mfumo wa Kiyahudi?
3 Kwa kuandika maneno hayo, mtume hakuwa akimaanisha “siku za mwisho” wa ule mfumo wa mambo wa Kiyahudi. Haingaliweza kuwa hivyo, maana Paulo aliandika maneno hayo yapata mwaka wa 65 W.K., wakati miaka zaidi ya 30 ya hizo “siku za mwisho” ilikuwa imekwisha kumalizika, ikabaki miaka mitano tu ili kufikia uharibifu wa Yerusalemu. Wala hali hiyo ya ukafiri haikuwa imesitawi kati ya wenye kujidai kuwa Wakristo. Hizo “siku za mwisho” wa mfumo wa Kiyahudi zilikuwa zimekuwa mbaya vya kutosha. Lakini matukio ya “siku za mwisho” wa mfumo mzima wa mambo wa ulimwengu wa Shetani yangekuwa mabaya zaidi wakati Yesu angekuja kusimamisha ufalme wake.
UTIMIZO WA MARA MBILI
4. Ni nini kilichoongoza wanafunzi waulize lile ulizo katika Mathayo 24:3?
4 Katika mifano yake, Yesu alikuwa amesema juu ya “umalizio wa mfumo wa mambo.” (Mathayo 13:39, 40, 49, NW) Bila shaka, hilo liliamsha kupendezwa kwa wanafunzi wake, na hasa kwa vile watu wa kawaida walikuwa wakiteseka sana, hata wakati huo, kutokana na ule utawala mkatili wa Roma na wa viongozi wa kidini Wayahudi. Walitumaini kwamba ufalme wa Mungu ungeleta faraja. Kwa sababu hiyo, siku tatu kabla ya Yesu kuuawa, wanne wa wanafunzi wake walimfikia alipokuwa akiketi juu ya Mlima wa Mizeituni kwa kuukabili Yerusalemu, wakamwuliza: “Tuambie, Mambo hayo yatakuwa wakati gani, na ni nini itakayokuwa ishara ya kuwapo kwako na ya umalizio wa mfumo wa mambo?”—Mathayo 24:3; Marko 13:3, 4, NW.
5. Maneno ya Yesu ya kujibu yangetimizwaje?
5 Ingawa wanafunzi wa Yesu walikuwa wakifikiria wakati ujao wa karibu tu, jibu la Yesu pindi hiyo lilipasa kuwa na matumizi ya mara mbili: kwanza, wakati wa zile “siku za mwisho” wa mfumo wa Kiyahudi, na, baadaye sana, wakati wa zile “siku za mwisho” wa mfumo wa ulimwengu wa Shetani unaotia ndani dunia nzima inayokaliwa na watu.
6, 7. (a) Maneno ya Yesu katika Mathayo 24:7-22 yalipataje utimizo mdogo? (b) Ni ukumbusho gani wenye kuogofya uliopo mpaka sasa wa utimizo wa maneno hayo?
6 Yale ambayo Yesu aliwaambia wanafunzi hao, kama yalivyoandikwa katika Mathayo 24, mistari ya 7 mpaka 22 (NW), yalieleza mfuatano wa matukio ambayo baadhi yao wangeona kwa utimizo mdogo wakati wa ile miaka 37 ambayo ingeendelea mpaka mwaka wa 70 W.K. Kwa wale Wayahudi wa kizazi cha Yesu, kilipasa kiwe kipindi chenye msukosuko wa vita, upungufu wa chakula, matetemeko ya ardhi, kuchukiwa kwa Wakristo na kutokea kwa akina Masihi wa uongo. Hata hivyo “habari njema hizi za ufalme” zingehubiriwa katika uumbaji wote kuwa ushuhuda. Mwishowe, lile “chukizo kuu,” yaani lile jeshi la Roma ya kipagani, lilivamia kweli kweli “mahali patakatifu” pa hekalu la Yerusalemu. Baada ya kuacha kwa muda mfupi, ambao katika huo wanafunzi wa Yesu waliweza kutii amri yake ya unabii kwa kukimbilia milima wapate usalama, Waroma walikuja tena wakiongozwa na Jenerali Tito. Waliuangusha kabisa Yerusalemu na watoto wao na kubomoa hekalu lao, wasiache jiwe juu ya jiwe.—Ona pia Luka 19:43, 44; Wakolosai 1:23.
7 Kwa utimizo wa “ishara” ya Yesu, wingi huo wa taabu ukaja kuwasumbua sana Wayahudi, nao ukafikia upeo Yerusalemu ulipoharibiwa kwa moto mwaka wa 70 W.K. Wayahudi zaidi ya milioni moja waliangamia pamoja na mji wao, na wale waliosalimika walichukuliwa mateka. Tao la ushindi la Tito linasimama katika Roma mpaka leo hii likiwa ukumbusho wenye kuogofya wa utimizo wa unabii wa Yesu. Walakini, je, “ishara” ya Yesu iliandikwa na kuhifadhiwa katika maandishi iwe onyo tu kwa watu waliokuwa wakiishi katika karne ya kwanza? Je! ni tukio la kikale tu lisilo na maana leo? Jibu lazima liwe, Sivyo!
MATUMIZI YENYE KUHUSU DUNIA YOTE
8. (a) Ule utimizo mdogo wa maneno ya Yesu umepasa utuhusuje sisi leo? (b) Hiyo inatoa kiolezo gani cha unabii cha mambo makubwa zaidi?
8 Ule utimizo mdogo wa maneno ya Yesu wakati wa zile “siku za mwisho” wa mfumo wa mambo wa Kiyahudi umepasa uwe jambo la kututia nguvu tuamini kwamba unabii wa kimungu una nguvu. Walakini, matukio hayo ya karne ya kwanza yanatoa vilevile kiolezo cha unabii cha yale yatakayoupata kwa kadiri kubwa zaidi mfumo wa mambo wa dunia yote wa Shetani. Lazima iwe hivyo, maana kutekelezwa kwa hukumu ya Mungu juu ya Yerusalemu katika mwaka wa 70 W.K. hakukuwa ndiyo dhiki kubwa kuliko zote kufikia wakati huo, wala haikuwa ndiyo ya mwisho. Maneno ya Yesu katika Mathayo 24:21, 22, NW yanatazamiwa kupata utimizo wa kadiri iliyo kamili:
“Maana ndipo kutakuwako dhiki kubwa ambayo haijapata kutukia tangu mwanzo wa ulimwengu mpaka sasa, la, wala haitatukia tena. Kwa kweli, kama siku hizo hazingekatwa ziwe fupi, hakuna mwili ambao ungeokoka; lakini kwa sababu ya wale waliochaguliwa siku hizo zitakatwa ziwe fupi.”
9. Twajuaje kwamba maneno ya Yesu yanaelekeza kwenye siku ya hukumu ya ulimwenguni pote?
9 Maneno ya unabii wa Yesu yanayoendelea, katika Mathayo 24:23-25:46, NW, yanaonyesha pia kwamba ule “umalizio wa mfumo wa mambo” utahusu dunia yote. Yule “Mwana wa mtu,” akiwa mfalme wa Mungu aliyetawazwa, atakapotekeleza hukumu juu ya ulimwengu wa Shetani wakati wa upeo wa kipindi hicho cha taabu, “makabila yote ya dunia yatajipiga-piga kwa kuomboleza.” Hiyo itahusu wanadamu wote wanaokataa uufalme wa Yesu. Hiyo si hukumu inayohusu taifa moja na mji walo tu, bali ni siku ya hukumu ulimwenguni pote.—Mathayo 24:30, NW.
10. (a) Kama inavyoonyeshwa katika unabii wa Yesu, mwisho wa wale wanaofanya watakayo utakuwaje tofauti na wa wale ‘wanaotafuta kwanza ufalme wa Mungu’? (b) Sababu gani ni lazima hilo lihusu dunia nzima?
10 Tena ukionyesha kwamba hukumu ya Mungu itahusu dunia yote, unabii wa Yesu unaendelea kuulinganisha ule “umalizio wa mfumo wa mambo” na kile kipindi kilichokuwa kabla tu ya ile gharika ya siku za Noa, ukisema:
“Maana kama walivyokuwa katika siku hizo kabla ya gharika, wakila na kunywa, wanaume wakioa na wanawake wakiozwa, mpaka ile siku ambayo Noa aliingia katika safina; nao hawakujali mpaka gharika ikaja na kuwakumba wote, ndivyo kuwapo kwa Mwana wa mtu kutakavyokuwa.”
Kama vile Gharika ya wakati huo ilivyoharibu ulimwengu mzima wa watu wasiomwogopa Mungu, ndivyo ile dhiki yenye moto inayofikisha “kuwapo” kwa Masihi kwenye upeo itakavyoondoa katika dunia yetu wale wanaoupuza ule Ufalme wakipendelea kufanya watakayo. Kwa matokeo mazuri, wale ambao ‘wametafuta kwanza ufalme wa Mungu na uadilifu wake’ wataokoka warithi uzima wa milele katika dunia-paradiso. Je! wewe utakuwa mmojawapo?—Mathayo 6:33; 24:37-39, NW; 25:31-4.
11. Ni unabii gani mwingine unaoonyesha kwamba mataifa yote yanahusika, na kwamba kutakuwako waokokaji?
11. Unabii mwingi sana wa Biblia unaonyesha kwamba “dhiki kubwa” inayokuja itahusu “mataifa yote” duniani. (Zaburi 2:2-9; Isaya 34:1, 2; Yeremia 25:31-33; Ezekieli 38:23; Yoeli 3:12-16; Mika 5:15; Habakuki 3:1, 12, 13) Lakini kutakuwako waokokaji!—Isaya 26:20, 21; Daniel! 12:1; Yoeli 2:31, 32.
KUWAPO KWA MFALME KATIKA UTUKUFU WA KIMBINGU
12. (a) Sababu gani “ishara” ya kuwapo kwa Yesu ni ya lazima? (b) Sababu gani si lazima aonekane tena katika mwili wenye nyama?
12 Unabii mkubwa wa Yesu juu ya ile “ishara” ya kuwapo kwake unatuambia kwamba “yule Mwana wa mtu atakapofika katika utukufu wake, na malaika wote pamoja naye, ndipo atakapoketi katika kiti chake chenye utukufu.” (Mathayo 25:31, NW) Kwa kuwa mng’aro wa utukufu huo ungedhuru macho ya kibinadamu, ni lazima yule Mfalme aendelee bila kuonekana na wanadamu. (Linganisha Kutoka 33:17-20; Waebrania 12:2.) Hiyo ndiyo sababu ‘ishara ya kuwapo kwake’ inahitajiwa. Wakati wa kuja kwa Masihi mara ya pili si lazima aache tena maisha yake ya kimbingu ya roho ili aonekane duniani katika mwili wenye nyama, utumiwe kuwa ‘toleo la dhambi.’ Akiisha kutoa dhabihu yake ya kibinadamu “mara moja tu,” yeye anakuja “mara ya pili, pasipo dhambi” akiwa mfalme wa kimbingu asiyeonekana.—Waebrania 7:26, 27; 9:27, 28; 10:8-10; 1 Petro 3:18.
13. Andiko la Luka 19:11-27 linaonyesha nini kwa habari ya wakati wa kurudi kwa Yesu na kukubaliwa kwake kati ya mataifa?
13 Katika usiku wake wa mwisho akiwa pamoja na wanafunzi wake wenye uhusiano mkubwa naye, Yesu alikuwa amewaambia hivi: “Mimi naenda zangu nikawatayarishie mahali. Pia, nikienda zangu na kuwatayarishia mahali, nitakuja tena na kuwapokea nyumbani kwangu mwenyewe.” (Yohana 14:2, 3, NW) Kupatana na hilo, mfano wa Yesu katika Luka 19:11-27, HNWW unamsimulia akiwa kama “mtu mmoja mashuhuri aliyefanya safari kwenda nchi ya mbali ili apokee madaraka ya ufalme, halafu arudi.” Hiyo ingechukua wakati mwingi. Lakini “wananchi wenzake walimchukia na hivyo wakatuma wajumbe waende wakaseme: ‘Hatumtaki huyu atutawale.’ ” Hali kadhalika, kuna watu leo wanaodai kuwa Wakristo, lakini wanarnkataa “mfalme wa wafalme” wakipendelea kuendeleza daima tawala zao wenyewe za kibinadamu zisizokamilika. (Ufunuo 19:16, HNWW) Hao wataadhibiwa vikali kama wale “wananchi” wa mfano wa Yesu.
“MWANZO WA MAUMIVU MAKALI YA TAABU”
14. Yajapokuwa maneno ya kupinga, ni nini kinachothibitisha kuwa ule mwaka 1914 W.K. kuwa ndiyo tarehe ya kurudi kwa Kristo?
14 Mfalme huyo mwenye nguvu, asiyetakwa na mataifa, alianza kutawala dunia yetu wakati gani? Ushuhuda wote unaelekeza kwenye ule mwaka wa 1914 W.K. Lakini mtu fulani atapinga, aseme, ‘Badala ya kuleta utawala wa Kristo wenye amani, mwaka huo ulionyesha mwanzo wa muhula wenye taabu kwa wanadamu!’ Ndivyo ilivyo hasa! Maana, kulingana na unabii wa Biblia, wakati ‘ufalme wa ulimwengu unapokuwa ufalme wa Bwana wetu Yehova na wa Kristo wake’ ndipo mataifa ya dunia yanapokuwa yenye “hasira kuu.” (Ufunuo 11:15, 18, NW) Pia huo ndio wakati Yehova anapomtuma mfalme-mshiriki wake, akisema, “Nenda hali ukitiisha kati ya adui zako.” (Zaburi 110:1, 2, NW) Lakini adui hao hawaharibiwi mara hiyo.
15. Ufunuo 12 unaelezaje kwa kufaa kule kuzaliwa kwa Ufalme?
15 Ufunuo sera ya 12 unasimulia njozi yenye kustaajabisha ambayo katika hiyo mtume Yohana aliona mfano wa kuzaliwa kwa ufalme wa Mungu wa Kimasihi. Kama mtoto wa kiume, huo unatokezwa katika “mwanamke” wa Mungu, yaani, tengenezo lake la kimbingu la viumbe wa kimalaika. ‘Unanyakuliwa mbali mpaka kwa Mungu na kwenye kiti cha enzi chake,’ maana ni lazima ule Ufalme utegemee Yehova na enzi kuu yake iii upate kutenda.—Ufunuo 12:1-5, NW.
16, 17. (a) Sababu ya ule ole mwingi ulio duniani tangu mwaka wa 1914 ni nini? (b) Maneno ya Yesu katika Mathayo na Luka yanaelezaje mwanzo wa taabu hizo?
16 Halafu, lo! vita yatokea mbinguni! Yule Mfalme aliyetawazwa, akiwa na malaika zake wanapigana na Shetani na makundi yake ya kishetani, na kuwavurumisha hao kutoka nje ya mbingu za Yehova mpaka chini kwenye ujirani wa dunia yetu. Kwa sababu hiyo, “ole wa dunia na wa bahari, kwa sababu yule Ibilisi ameshuka kuja kwenu, akiwa na hasira kubwa, akijua ana kipindi cha wakati kifupi.” (Ufunuo 12:7-12, NW) Wakati wa hicho ‘kipindi kifupi,’ yule Mfalme anakusanya wanadamu wenye maelekeo ya uadilifu waje wapate wokovu na anavumisha lile onyo la kutekelezwa kwa hukumu inayokaribia sana juu ya mfumo wa mambo wa ulimwengu wa Shetani.—Mathayo 24:31-41; 25:31-33, NW.
17 Leo tunafahamu ule utimizo wa “ishara” ya Yesu, kama inavyosimuliwa kirefu katika Mathayo sura za 24 na 25, Marko sura ya 13 na Luka sura ya 21. Angalia kwamba hapa Yesu anasimulia “mwanzo wa maumivu makali ya taabu,” kwa maneno haya:
“Taifa litainuka dhidi ya taifa, na ufalme dhidi ya ufalme; na kutakuwako matetemeko ya ardhi makubwa, na mahali hapa na mahali hapa magonjwa ya kipuku na upungufu wa chakula; na kutakuwako maono yenye kutisha na kutoka mbingu ni ishara kubwa.” (Mathayo 24:3, 7, 8; Luka 21:10, 11, “NW”)
Je! hayo “maumivu makali ya taabu” yalikuja kusumbua wanadamu tangu mwaka wa 1914 W.K.?
18. Tangu mwaka wa 1914, vita ikawaje yenye maafa ya kuogopesha sana?
18 Ni katika ule mwaka wa 1914 ile Vita Kuu (baadaye ikaitwa “Vita ya Ulimwengu ya Kwanza”) ilipotokea, ikafuatana na ugonjwa wa kipuku na njaa kuu. Waandikaji wameona ni vigumu kusimulia maafa ya kuogopesha yaliyoenea katika wanja za mapigano, mamilioni walipoangamia katika vita vya mahandaki wakati wa yale machinjano ya miaka ya 1914 mpaka 1918. Katika kile kitabu kinachoitwa Eye Deep in Hell, Paul Nash amenakiliwa kuwa akisema juu ya uwanja wa mapigano wa huko Ulaya: “Hakuna kalamu wala mchoro unaoweza kueleza habari ya nchi hii—ule mwandamano wa kawaida wa yale mapigano yanayotukia mchana na usiku, mwezi baada ya mwezi. Uovu na shetani-mtu pekee ndiye anayeongoza vita hiyo, na hakuna alama ya mkono wa Mungu inayoonwa po pote. . . . Zile risasi hazikomi kamwe . . . kuangamiza watu, kuwalemaza, kuwatia wazimu, zinawatumbukiza katika kaburi ambalo ni nchi hii; kaburi moja lililo kubwa mno, na kuwatupa juu yake wale wafu maskini. Haisemeki, si ya kimungu, ni kazi bure.”
19. Takwimu zinaonyesha nini kwa habari ya ongezeko la matetemeko ya ardhi tangu mwaka wa 1914?
19 Pia, “matetemeko ya ardhi” yametiwa ndani kuwa sehemu ya ile “ishara.” Je! kuna ongezeko la matetemeko ya ardhi tangu mwaka wa 1914? Huenda hiyo ikaonekana inastaajabisha. Lakini takwimu zinastaajabisha hata zaidi! Kama Geo Malagoli alivyoeleza katika kitabu Il Piccolo: “Wakati wa kipindi cha miaka 1,059 (kutoka mwaka wa 856 mpaka 1914) vyanzo vyenye kutegemeka vinaorodhesha kwamba wakati wa miaka hiyo wastani ya watu 1,800 walikufa kila mwaka katika matetemeko ya ardhi, lakini yamekuwako matetemeko ya ardhi makubwa 43 tangu mwaka wa 1915, na yameua wastani ya watu 25,300 kila mwaka.
“KUTOKA MBINGUNI ISHARA KUBWA”
20, 21. (a) Ni “maono ya kutisha” gani ambayo yamekuwa wazi tangu mwaka wa 1914, na kwa sababu gani? (b) Ni utimizo gani wa Luka 21:25, 26 tunaoona leo? (c) ‘Ishara kuu kutoka mbinguni zimezidi kufikiriwaje?
20 Yesu alitabiri hivi pia: “Na kutakuwako maono ya kutisha na kutoka mbinguni ishara kubwa.” (Luka 21:11, NW) Katika Vita ya Ulimwengu ya Kwanza, ule mfululizo wa risasi za mizinga ulionyesha jambo fulani jipya—vita ya kutumia vifaa vyote. Kwa mara ya kwanza meli ya angani, halafu zaidi ya hivyo, eropleni zilianzisha muhula wa vita vya hewani. Ni kweli kwamba huo ulikuwa mwanzo tu katika miaka ya 1914 mpaka 1918. Lakini ungeongoza kwenye hali ambayo Yesu anasimulia zaidi katika unabii wake, akisema:
“Pia, zitakuwako ishara katika jua na mwezi na nyota, na katika dunia huzuni kuu ya mataifa, yakiwa hayajui njia ya kutokea kwa sababu ya kunguruma kwa bahari na msukosuko wayo, huku watu wakizimia kwa sababu ya hofu na tazamio la mambo yanayokuja juu ya dunia inayokaliwa na watu; kwa maana nguvu za mbingu zitatikiswa.”—Luka 21:25, 26, “NW.”
21 Kutaka kwa mwanadamu kushinda anga la juu kumekaza fikira juu ya “jua na mwezi na nyota,” na kuna ishara zenye kuogopesha za kwamba yale Mataifa Makubwa yanakusudia kutumia masetilaiti ili kuanzisha vituo vya kijeshi. Lakini tayari mataifa hayo yana maarifa ya kumimina makombora ya kutupwa bara kwa bara kutoka anga la juu zaidi yaangukie shabaha yo yote wanayochagua. Silaha za sasa za nyukilia zilizo katika ghala za kivita, kama zilivyolundikwa na mataifa yenye upinzani, zatosha kuangamiza wanadamu mara nyingi, na imekadiriwa kwamba kufikia mwaka wa 2,000 huenda mataifa karibu 35 yakawa tayari na silaha hizo za kuangamiza watu kama mainzi.
22. (a) Ile “bahari” halisi imekuwaje na sura mpya tangu mwaka wa 1914? (b) Watu wenye maarifa wanaonya nini juu ya hatari inayokaribia kupata dunia yetu?
22 Ile “bahari,” iliyopata sura mpya kwa kuanzishwa kwa vita vya kutumia nyambizi (sabmarini) katika Vita ya Ulimwengu ya Kwanza, na iliyoingiza United States (Marekani) katika vita hiyo, inaogopesha hata zaidi leo. Sabmarini za kinyukilia zimewekwa tayari kutumiwa katika zile bahari. Gazeti New York Times la Agosti 30, 1980, lilimnakili Marshall D. Shulman, mtaalamu wa Idara ya Serikali kule United States, kuwa akisema kwamba ule uwezekano wa kutokea vita ya nyukilia “waelekea kuongezeka badala ya kupungua.” Tangazo la ukurasa mzima katika New York Times la Machi 2, 1980, lenye kudhaminiwa na wataalamu zaidi ya 600, wakiwa wanaume na wanawake, lilisema: “Vita ya nyukilia, hata iwe ‘ndogo,’ ingetokeza kifo, madhara na magonjwa kwa kadiri isiyo na kifani katika historia ya kuwapo kwa wanadamu.” Wakaongeza kusema kwamba “vita kamili ya nyukilia ingeweza kumalizika kwa muda wa saa moja, na ingeweza kuharibu viumbe hai vingi katika kile kizio cha kaskazini cha dunia.” Yule balozi wa United States aliyetumwa Mosko, alisema katika mwaka wa 1981: “Mimi nauona ulimwengu kuwa wenye hatari zaidi ya vile umepata kuwa wakati wo wote katika historia yao.” Lakini matumizi ya fedha kwa kusudi la kuunda silaha za kuua watu kama mainzi yanazidi kupanda juu.
23. Kwa utimizo wa unabii wa Yesu, wanadamu wanaonekana kuwa wanafikia half gani katika historia?
23 Wanadamu wanaonekana kuwa wanaifikia ile hali iliyotabiriwa miaka fulani iliyopita na Harold C. Urey, mshindi wa Tuzo la Nobeli, aliyesema: “Tutakula woga, tutalalia woga, tutaishi katika woga na kufa katika woga.” Kweli kweli, kuna “huzuni kuu ya mataifa, yakiwa hayajui njia ya kutokea . . . huku watu wakizimia kwa sababu ya hofu na tazamio la mambo yanayokuja juu ya dunia inayokaliwa na watu.”
24. Ni nani anayejua “njia ya kutokea.” na sababu gani imetupasa kusali kwa bidii sana ule Ufalme “uje”?
24 Kwa matokeo mazuri, Yehova, Bwana Mwenye Enzi Kuu, aliyeiumba dunia hii kwa kusudi lake zuri, ‘anajua njia ya kutokea,’ naye ataiandaa njia hiyo kupitia ufalme wa Mwanaye. Lakini kabla hatujachunguza sana ile “njia ya kutokea,” ebu tuukazie fikira zaidi ule unabii wa Yesu, tuone jinsi maneno yake juu ya vita ya ulimwengu, njaa kuu na magonjwa ya kipuku, ambayo ni sehemu za ile “ishara,” yanavyolingana sana na unabii wenye kuvuta sana katika Ufunuo. Kumbuka, ufalme wa Mungu kupitia Masihi ndiyo dawa—ufalme ule ambao kwa bidii sana tunasali “uje”!
[Sanduku katika ukurasa wa 115]
YALE AMBAYO WAANDIKAJI WAMESEMA JUU YA MWAKA WA 1914
Hata baada ya vita ya ulimwengu ya pili, wengi wanautaja mwaka wa 1914 kuwa ndio muda wa badiliko kuu katika historia ya kisasa.
“Kweli kweli ule mwaka wa 1914 wala si ule wa Hiroshima ndio unaoonyesha muda wa badiliko kuu katika wakati wetu.”—Rene Albrecht-Carrie, “The Scientific Monthly,” Julai 1951
“Wakati wote tangu mwaka wa 1914, kila mtu anayejua maelekeo yaliyo katika ulimwengu amesumbuliwa sana na ule ambao umeonekana kuwa kama mwendo wenye msiba na ulioamuliwa kimbele kuelekea msiba mkubwa zaidi. Watu wengi wenye kufikiri sana wamefikia maoni ya kwamba hakuna linaloweza kufanywa kuzuia hatua ya kutumbukia katika uharibifu. Wanaiona jamii ya kibinadamu ikiongozwa na miungu yenye hasira kama yule shujaa wa msiba wa Wagiriki, na jamii hiyo haiwi tena na uwezo wa kujiamulia litakaloipata.”—Bertrand Russell, New York “Times Magazine,” Septemba 27, 1953
“Ule muhula wa kisasa . . . ulianza mwaka wa 1914, na hakuna anayejua utakapomalizika wala utakavyomalizika. . . . Mwisho wake ungeweza kuwa ni kuangamizwa kwa watu kama mainzi.”—Safu ya Mhariri, “The Seattle Times,” Januari 1, 1959
“Katika mwaka wa 1914, ulimwengu kama ulivyojulikana na kukubaliwa wakati huo, ulikoma.”—James Cameron, “1914,” kilichochapishwa mwaka wa 1959
“Ile Vita ya Ulimwengu ya Kwanza ilikuwa mmojawapo misukosuko ile mikubwa ya historia.”—Barbara Tuchman, “The Guns of August,” 1962
“Mawazo na picha zinakuja kwenye akili zangu, mawazo ya wakati ulioutangulia mwaka wa 1914 kulipokuwa na amani ya kweli, utulivu na usalama katika dunia hii—wakati tulipokuwa hatujui woga.... Usalama na utulivu umetoweka katika maisha za watu tangu mwaka wa 1914.”—Waziri wa serikali Mjeremani Konrad Adenauer, 1965
“Ulimwengu mzima ukaharibika kweli kweli kufikia Vita ya Ulimwengu ya Kwanza na tungali hatujui sababu. . . . Hali bora zilikuwa zikitazamiwa. Kulikuwako amani na ufanisi. Ndipo kila kitu kikaharibika kweli kweli. Tangu wakati huo tumekuwa tukiishi katika hali yenye mashaka-mashaka.”—Dakt. Walker Percy, “American Medical News,” Novemba 21, 1977
“Katika mwaka wa 1914 ulimwengu ulipoteza utegemeano ambao umeshindwa kuupata tena tangu wakati huo. . . Huu umekuwa wakati wenye mchafuko na jeuri isiyo ya kawaida, nje na ndani ya mipaka ya kitaifa.”—“The Economist,” London, Agosti 4, 1979
“Katika mwaka wa 1914 ustaarabu ulianza ugonjwa mkali na labda ule wa vipindi-vipindi.”—Frank Peters, St. Louis “Post-Dispatch,” Januari 27, 1980
“Kila kitu kilikuwa kikiendelea kuwa kizuri zaidi na zaidi. Huo ndio ulimwengu nilimozaliwa. . . . Ghafula, bila kutazamiwa, asubuhi moja katika mwaka wa 1914 mambo yote yakakoma.”—Waziri wa serikali Mwingereza, Harold Macmillan, New York “Times,” Novemba 23, 1980