Watchtower MAKTABA KWENYE MTANDAO
Watchtower
MAKTABA KWENYE MTANDAO
Kiswahili
  • BIBLIA
  • MACHAPISHO
  • MIKUTANO
  • su sura 3 kur. 21-29
  • Mfumo wa Sasa Utaendelea Kuwapo Mpaka Lini?

Hakuna video yoyote kwa sasa.

Samahani, haikuwezekana kupakia video.

  • Mfumo wa Sasa Utaendelea Kuwapo Mpaka Lini?
  • Kuokolewa Kuingia Katika Dunia Mpya
  • Vichwa vidogo
  • Habari Zinazolingana
  • ISHARA YENYE MAMBO MENGI
  • “NYAKATI ZILIZOWEKWA ZA MATAIFA”
  • MATARAJA YAKO NI TIMAMU KADIRI GANI?
  • Uharibifu wa Ulimwengu Uliotabiriwa Utakuja Lini?
    Amani na Usalama wa Kweli—Wewe Unaweza Kuupataje?
  • Siku za Mwisho
    Kutoa Sababu kwa Kutumia Maandiko
  • Ufalme wa Mungu Huanza Kutawala Katikati ya Adui Zake
    Kweli Iongozayo Kwenye Uzima wa Milele
  • Zile “Siku za Mwisho” na Ule Ufalme
    “Ufalme Wako Uje”
Pata Habari Zaidi
Kuokolewa Kuingia Katika Dunia Mpya
su sura 3 kur. 21-29

Sura 3

Mfumo wa Sasa Utaendelea Kuwapo Mpaka Lini?

1. Kwa habari ya ahadi za Biblia, wengi wetu tumeuliza nini?

NI JAMBO la asili kutaka kujua itachukua muda gani mpaka yatakapotukia yale mambo yanayosimuliwa waziwazi sana katika Biblia, yanayofikia upeo mkubwa na kuwa Har–Magedoni. Mfumo mbovu wa sasa utaharibiwa wakati gani? Je! sisi tutaishi tuje tuione dunia ikiwa mahali ambapo wenye kupenda uadilifu wanaweza kufurahia amani na usalama kamili?

2. (a) Ni swali gani kama hilo ambalo mitume wa Yesu waliuliza? (b) Je! tunajua barabara wakati mfumo mbovu wa sasa utakapofikia mwisho? (c) Lakini ni habari gani yenye kusaidia sana ambayo Yesu alitoa?

2 Yesu Kristo alitoa maelezo ya ajabu yanayojibu maulizo hayo. Alifanya hivyo mitume wake walipouliza hivi: “Ni nini itakayokuwa ishara ya kuwapo kwako na ya umalizio wa mfumo wa mambo?” Kwa habari ya uharibifu wenyewe wa mfumo mbovu wa sasa, Yesu alisema waziwazi hivi: “Kwa habari ya siku ile na saa ile hakuna anayejua, wala malaika wa mbingu wala Mwana, bali Baba pekee.” (Mathayo 24:3, 36, New World Translation) Hata hivyo alieleza kirefu sana kile kizazi ambacho kingeuona “umalizio [Kigiriki: syn·te΄lei·a] wa mfumo wa mambo,” kipindi cha wakati kinachotangulia “mwisho [Kigiriki: te΄los].” Jisomee mwenyewe Biblia yako katika Mathayo 24:3–25:46, pia katika masimulizi yanayolingana na hayo katika Marko 13:4-37 na Luka 21:7-36.

3. Twajuaje kwamba jibu la Yesu halikuwa likisimulia tu matukio ya karne ya kwanza?

3 Unaposoma masimulizi hayo, utafahamu kwamba, kwa sehemu tu, Yesu alikuwa akisimulia matukio yenye kutoa utangulizi na yenye kutia ndani uharibifu wa Yerusalemu na hekalu lake mwaka wa 70 W.K. Ni wazi kwamba yeye alikuwa akifikiria pia jambo lenye matokeo makubwa zaidi. Kwa nini? Kwa sababu katika Mathayo 24:21 anasema juu ya “dhiki kubwa, ambayo haijatokea namna yake tangu mwanzo wa ulimwengu hata sasa, wala haitakuwapo tena.” Hiyo inaonyesha si uharibifu wa mji mmoja tu na watu wenye kunaswa humo. Na katika Luka 21:31 matukio yanayosimuliwa yanasemwa kuwa yakielekeza kwenye kuja kwa “ufalme wa Mungu” ambao umengojewa muda mrefu. Ni nini iliyo “ishara” inayofaa kuangaliwa sana ambayo Yesu alisema tuitazame?

ISHARA YENYE MAMBO MENGI

4. Ni “ishara” gani ambayo Yesu alitoa?

4 Alitabiri vita, upungufu wa chakula, magonjwa ya kuambukiza yenye kuenea pote, matetemeko makubwa ya ardhi, na roho isiyo ya upendo wakati wa uvunjaji-sheria wenye kuongezeka, lakini tukio moja tu la hayo si ile “ishara.” Ni lazima sehemu zote zilizotabiriwa zitimizwe katika muda wa maisha ya kizazi kimoja ili picha ipate kuwa kamili. Pia, pamoja na hayo ingekuwapo “huzuni kuu ya mataifa, wasijue njia ya kutokea . . . huku wanadamu wakizimia moyo kwa sababu ya hofu” ya mambo yanayotukia katika mbingu juu na katika bahari zinazowazunguka. (Luka 21:10, 11, 25-32, New World Translation; Mathayo 24:12; linganisha 2 Timotheo 3:1-5.) Tofauti na hayo yote, lakini ikiwa sehemu ya ile ishara, Yesu alitabiri kuhubiriwa duniani pote kwa habari njema za Ufalme wa Mungu ijapokuwa kuteswa kwa wafuasi wake katika mataifa yote. (Marko 13:9-13) Je! simulio hilo lenye mambo mengi linauhusu wakati tunamoishi?

5. Ni jambo gani lingefanya matukio hayo kuwa ni zaidi ya kurudiwa kwa historia?

5 Huenda wadhihaki wakadharau, wakisema kwamba mara nyingi, kumekuwa na vita, njaa kubwa, matetemeko ya ardhi, na kadhalika, katika historia ya kibinadamu. Lakini matukio hayo yanakuwa na maana ya pekee yanapotokea yote pamoja, si katika mahali pachache, hapa na hapa tu, bali duniani pote kwa kipindi cha wakati mrefu kilichoanza na mwaka fulani uliotabiriwa zamani.

6, 7. Ni matukio na hali gani za karne ya 20 zinazolingana hasa na ishara hiyo yenye mambo mengi? (Unapojibu, tumia Biblia yako uonyeshe ni visehemu gani vya unabii wa Yesu unavyozungumza.)

6 Fikiria mambo haya ya hakika: Vita iliyotokea mwaka wa 1914 ilikuwa kubwa sana hata ikaja kujulikana kuwa vita ya ulimwengu ya kwanza, na tangu wakati huo amani haijairudia dunia kamwe kamwe. Baada ya Vita ya Ulimwengu ya Kwanza ikaja moja ya njaa kubwa zaidi ya zote ambazo wanadamu wamepata kuona, na hata leo hii watu kama milioni 40 wanakufa kila mwaka kwa kupungukiwa chakula. Ile homa kali ya mafua ya Hispania ya mwaka wa 1918 iliua watu kwa kadiri isiyo na mfano katika historia ya magonjwa. Na ijapokuwa uchunguzi wa kisayansi, makumi ya mamilioni ya watu wanasumbuliwa na kansa hata sasa, ugonjwa wa moyo, magonjwa ya kuchukiza sana ya ngono za ovyoovyo, maleria, kichocho na upofu unaoletwa na mainzi wa mito ya maji. Mara za kutokea kwa matetemeko makubwa ya ardhi zimeongezeka kufikia karibu 20 ya zilivyokuwa kwa wastani wakati wa miaka elfu mbili kabla ya mwaka wa 1914. Woga na huzuni kuu duniani pote zinasumbua watu wa umri wote. Baadhi ya sababu ni hali mbaya ya kiuchumi, uhalifu wa kijeuri na hatari ya kuangamia katika vita ya silaha za nyukilia yenye kutumia silaha za kutupwa kutoka meli zinazopita chini ya maji au zikiteremka kasi sana kutoka mbingu mpaka chini—jambo ambalo halikuwezekana kabla ya karne hii ya 20.

7 Katikati ya yote hayo kazi ya ajabu ya kutangaza habari njema za Ufalme wa Mungu ulimwenguni pote inafanywa, kama Yesu alivyotabiri. Katika nchi na visiwa vya bahari zaidi ya 200, Mashahidi wa Yehova wanatumia mamia ya mamilioni ya saa kila mwaka, bila malipo, wakisaidia watu wa namna zote za maisha waifahamu maana ya matukio hayo ya ulimwengu kwa msaada wa Neno la Mungu. Mashahidi wanatumia bidii kuwaonyesha watu njia inayoongoza kwenye kuokoka “dhiki kubwa” wakiwa raia za Ufalme wa Mungu. Na Mashahidi hao wanafanya hivyo ijapokuwa ‘labda ndio wanaovumilia mateso mengi kwa kosa dogo kuliko kikundi kinginecho chote cha kidini katika ulimwengu,’ kama ilivyosema ripoti moja ya habari ya Kanada.

8. Ni kipindi cha wakati gani pia kilichotiwa katika unabii huo?

8 Ni lazima pia tufikirie kwamba, kama sehemu ya unabii wake, Yesu alielekeza kwenye kumalizika kwa kipindi cha wakati kilicho halisi, akisema: “Yerusalemu utakanyagwa na mataifa, mpaka nyakati zilizowekwa za mataifa zitakapotimizwa.” (Luka 21:24, New World Translation) Je! hizo “nyakati zilizowekwa” zimemalizika?

“NYAKATI ZILIZOWEKWA ZA MATAIFA”

9. (a) Ni “Yerusalemu” gani ‘uliokanyagwa’ na mataifa? (b) ‘Kukanyagwa’ huko kulianza wakati gani?

9 Ili tufahamu jibu, ni lazima tuielewe maana ya Yerusalemu wenyewe. Mji wenye makao ya kifalme katika Mlima Sayuni ulisemwa kuwa “mji wa Mfaume mkuu . . . mji wa Jehova.” (Zaburi 48:2, 8, The Old Testament in Swahili, Mombasa; Mathayo 5:34, 35) Wafalme wa nyumba ya kifalme ya Daudi walisemwa kuwa wameketi “katika kiti cha enzi cha [Yehova].” Kwa hiyo Yerusalemu ulikuwa mfano wenye kuonekana wa kwamba Yehova alitawala dunia. (1 Mambo ya Nyakati 29:23) Hivyo wakati majeshi ya Kibabuloni yaliporuhusiwa na Mungu yaharibu Yerusalemu, yamchukue mfalme wake katika uhamisho na kuiacha nchi ukiwa, yalikuwa yakiukanyaga Ufalme wa Mungu ukiwa unaongozwa kupitia mzao wa Mfalme Daudi. Jambo hilo lilipotukia, mwaka wa 607 K.W.K., liliweka alama ya mwanzo wa “nyakati zilizowekwa za mataifa.” Tangu wakati huo hapana mzao wa Daudi aliyepata kutawala akiwa mfalme katika Yerusalemu.

10. (a) Mwisho wa ‘kukanyagwa’ huko ungemaanisha nini? (b) Basi, Yesu angetawala akiwa katika “Yerusalemu” gani, na kwa nini?

10 Basi, mwisho wa ‘kukanyagwa kwa Yerusalemu’ ungekuwa na maana gani? Kwamba tena Yehova alikuwa amemtawaza mfalme aliyechaguliwa na yeye mwenyewe, mzao wa Daudi, awe sasa na mamlaka, si kati ya Wayahudi tu, bali katika mambo ya wanadamu kwa ujumla. Huyo ndiye Bwana Yesu Kristo. (Luka 1:30-33) Lakini angetawala akiwa wapi? Je! akiwa katika ule mji wa kidunia wa Yerusalemu? Yesu alisema waziwazi kwamba mapendeleo yanayohusiana na Ufalme wa Mungu yangeondolewa katika Israeli wa mwili. (Mathayo 21:43; ona pia 23:37, 38.) Baada ya hapo, waabudu wa Mungu wa kweli walitazamia “Yerusalemu wa juu,” tengenezo la kimbingu la Mungu la viumbe wa roho wenye ushikamanifu, kuwa mama yao. (Wagalatia 4:26) Yesu angetawazwa katika Yerusalemu huo wa kimbingu, atumie mamlaka ya kutawala kuelekea dunia. (Zaburi 110:1, 2) Hilo lingetukia mwishoni mwa “nyakati zilizowekwa za mataifa.” Hiyo ingekuwa wakati gani?

11, na chati (ukurasa wa 27). (a) Kumalizika kwa “nyakati zilizowekwa” kunahesabiwaje? (b) Basi, ni nini kilichoanza wakati hizo “nyakati zilizowekwa” zilipokwisha? (c) Wanahistoria wana maoni gani juu ya mwaka wa 1914? (Ona ukurasa wa 29.)

11 Makumi ya miaka iliyotangulia ilijulikana kwamba hilo lingetukia mwaka wa 1914 mwishoni mwa utimizo mkubwa wa zile “nyakati saba” za Danieli 4:10-17.a Lakini utimizo kamili wa maana yake ulikuja polepole wakati wa ile miaka iliyofuata. Hatua kwa hatua wanafunzi wa Biblia waliona yakifunuliwa mbele ya macho yao mambo mbalimbali ya ile ishara yenye sehemu nyingi ambayo Yesu alisema ingeonyesha kuwapo kwake kwa kimbingu katika mamlaka ya Ufalme. Ikaonekana wazi kwamba kumbe, walikuwa wameingia katika “umalizio wa mfumo wa mambo,” kwamba Kristo alikuwa ameanza kutawala akiwa Mfalme mwaka wa 1914 na kwamba mwisho wa ulimwengu huu mbovu ungekuja katika kizazi kilichoona mwanzo wa mambo hayo.

MATARAJA YAKO NI TIMAMU KADIRI GANI?

12. Ni mataraja gani yenye makosa yanayofanya uamuzi huo kuwa mgumu kwa wengine kukubali? (Mathayo 24:26, 27; Yohana 14:3, 19)

12 Watu fulani wanaoyajua mambo hayo ya hakika yanayotimiza unabii wa Yesu wanaona ni vigumu kukubali uamuzi unaoelekezwa na mambo hayo. Kwa nini? Kwa sababu wanatarajia kitu kingine. Walifundishwa kwamba kuja kwa Kristo mara ya pili kungeonekana na matokeo yangekuwa ni kugeuzwa kwa umati wa wanadamu wawe waamini. Katika karne ya kwanza Wayahudi pia walikuwa na mataraja ambayo hayakutimizwa. Walitumaini kwamba kuja kwa Masihi kungekuwa pamoja na wonyesho wa nguvu ambazo zingewapa uhuru kutoka Roma. Kwa kung’ang’ania mataraja yao yenye makosa, wakamkataa Mwana wa Mungu mwenyewe. Ungekuwa upumbavu kama nini kurudia kosa hilo wakati Kristo amekuwapo katika mamlaka ya Ufalme! Ni bora kama nini kuona mambo ambayo Maandiko yenyewe yanasema hasa!

13. Ni matukio gani ambayo Biblia yenyewe inahusianisha pamoja na kuwapo kwa Kristo?

13 Biblia inaonyesha kwamba Kristo angeanza kutawala katikati ya adui zake. (Zaburi 110:1, 2) Inasema juu ya kufukuzwa kwa Shetani na mashetani wake kutoka mbinguni mpaka kwenye ujirani wa dunia baada ya Kristo kupewa mamlaka ya Ufalme; hivyo kungekuwako kipindi cha ole wa dunia wenye kuongezeka. (Ufunuo 12:7-12) Wakati huo kuhubiriwa kwa ujumbe wa Ufalme kungeongezeka nguvu, ili kuwapa watu nafasi ya kuchukua hatua ya kuja kuokolewa. (Mathayo 24:14; Ufunuo 12:17) Lakini hilo lingetokeza kugeuzwa kwa ulimwengu uwe wa waamini? Hata kidogo. Biblia inaonyesha kwamba hilo lingefuatwa na uharibifu usio na ulinganifu katika historia ya kibinadamu. Ijapokuwa wanadamu hawatapata kumwona kamwe Yesu Kristo aliyetukuzwa kwa macho yao ya mwili, wote ambao kwa kupenda kwao wamekataa kuyakubali mambo ya hakika juu ya kuwapo kwa kifalme kwa Kristo watalazimika ‘kuona’ kwamba ndiye ambaye, kama ilivyotabiriwa, analeta uharibifu juu yao.—Ufunuo 1:7; Mathayo 24:30; linganisha 1 Timotheo 6:15, 16; Yohana 14:19.

14, 15. Kwa nini kupita kwa miaka tangu 1914 hakutupi sisi sababu ya kutia shaka kwamba kweli tumo katika “siku za mwisho”?

14 Lakini sasa imepita miaka 70 tangu mwaka wa 1914. Je! hiyo haitupi sisi sababu ya kutia shaka kama kweli, tangu mwaka huo, tumekuwa katika “siku za mwisho,” na kama kuja kwa Kristo akiwa mwenye kuleta maangamizi ni karibu? Hasha! Kwa habari ya wale ambao wangeuona utimizo wa ile “ishara” tangu mwanzo wayo, kuanzia mwaka wa 1914, Yesu alisema: “Amin, nawaambieni, Kizazi hiki hakitapita, hata hayo yote yatimie.” (Marko 13:30) Watu wa kizazi hicho wangali wapo, ijapokuwa hesabu yao inapungua haraka sana.

15 Ni kweli kwamba takwimu zinaonyesha wastani wa muda wa kuishi kwa watu duniani pote sasa kuwa miaka 60 tu. Lakini mamilioni ya watu wanaishi zaidi ya umri huo. Kulingana na takwimu tulizo nazo, katika mwaka wa 1980 karibu watu 250,000,000 kati ya wale waliokuwa hai mwaka wa 1914 walikuwa bado wanaishi. Kizazi hicho kingali hakijapita. Lakini, inafaa kuangaliwa kwamba, kati ya wale waliozaliwa mwaka wa 1900 au mapema kuliko hapo, tarakimu zilizochapishwa na Umoja wa Mataifa zinaonyesha kwamba watu wenye kukadiriwa kuwa 35,316,000 tu ndio waliokuwa wangali hai mwaka wa 1980. Hivyo hesabu inapungua upesi sana wakati watu mmoja mmoja wanapofikia umri wao wa 70 au 80 na kitu. Yanapochunguzwa pamoja na mambo yote ya ishara ya unabii ya Yesu, mambo hayo ya hakika yanaonyesha kwa nguvu kwamba mwisho ni karibu.—Luka 21:28.

16. Hivyo, mwelekeo wetu umepasa uweje?

16 Sasa sio wakati wa kuwa na utepetevu. Ni wakati wa kuchukua hatua haraka! Kama Yesu alivyowaonya wanafunzi wake: “Jiwekeni tayari; kwa kuwa katika saa msiyodhani Mwana wa Adamu [Yesu Kristo] yuaja.”—Mathayo 24:44.

[Maelezo ya Chini]

a Kwa maelezo zaidi, ona kitabu “Ufalme Wako Uje,” kurasa 127-39, 186-9.

[Sanduku katika ukurasa wa 29]

Wanahistoria Wanavyoona Mwaka wa 1914

Kwa sababu zilizo nzuri, vita iliyoanza mwaka wa 1914 imeitwa Vita Kuu na Vita ya Ulimwengu ya Kwanza. Hakuna vita yenye kuleta hasara kubwa kama hiyo ilikuwa imepata kupiganwa miaka iliyotangulia. Tangu wakati huo vita ambavyo vimekuwa vikipiganwa vimeendeleza tu vita vilivyoanza mwaka wa 1914. Yaangalie maelezo haya juu ya matokeo ya mwaka huo wenye maana sana:

“Ukosefu wa usalama uliokuwako wakati huo ulionekana hasa katika sehemu ya kiuchumi. Vita hiyo ilikuwa imeharibu bila huruma mfumo wenye mambo mengi, wenye kubadilikana na wenye kusawazika vizuri ulio na sheria halisi na kanuni imara. . . . Wala haikuwezekana tena sehemu hiyo irudie ‘hali ya kawaida.’”—Världshistoria—Folkens liv och Kultur (Stockholm; 1958), Buku la 7, kurasa 421, 422.

● “Nusu karne imepita, hata hivyo alama ambayo msiba wa ile Vita Kuu iliachia mwili na nafsi ya mataifa haijafutika . . . Matokeo ya msiba huo juu ya mwili na adili yalikuwa makubwa mno hata kilichobaki hakikuwa kama kilivyokuwa kabla ya wakati huo. Jamii nzima: mifumo ya serikali, mipaka ya kitaifa, sheria, majeshi yenye silaha, uhusiano wa kati ya nchi na nchi, lakini pia siasa, maisha ya jamaa, ufanisi, vyeo, uhusiano kati ya mtu na mtu—kila jambo lilibadilishwa kutoka juu mpaka chini. . . . Hatimaye binadamu akapoteza usawa, usipate kurudishwa kamwe mpaka leo hii.”—Jenerali Charles de Gaulle, akihutubu mwaka wa 1968 (Le Monde, Novemba 12, 1968).

● “Wakati wote tangu mwaka wa 1914, kila mtu anayejua maelekeo yaliyo katika ulimwengu amesumbuliwa sana na ule ambao umeonekana kuwa kama mwendo wenye msiba na ulioamuliwa kimbele kuelekea msiba mkubwa zaidi. Watu wengi wenye kufikiri sana wamefikia maoni ya kwamba hakuna linaloweza kufanywa kuzuia hatua ya kutumbukia katika uharibifu. Wanaiona jamii ya kibinadamu ikiongozwa na miungu yenye hasira kama yule shujaa wa msiba wa Wagiriki, na jamii hiyo haiwi tena na uwezo wa kujiamulia litakaloipata.”—New York Times Magazine, Septemba 27, 1953.

● “Tukitazama nyuma kwa maoni mazuri tuliyo nayo sasa, tunaona waziwazi leo kwamba kutokea kwa Vita ya Ulimwengu ya Kwanza kuliingiza katika karne ya ishirini ‘Wakati wa Taabu Nyingi,’ ambao tangu hapo ustaarabu wetu haujarudia tena hali nzuri—kulingana na usemi wenye maana wa Arnold Toynbee, mwanahistoria Mwingereza. Vurugu zote za nusu karne iliyokwisha zimeanzia moja kwa moja au kwa njia isiyo ya moja kwa moja mwaka wa 1914.”—The Fall of the Dynasties: The Collapse of the Old Order (New York; 1963), cha Edmond Taylor, ukurasa wa 16.

Lakini ni nini iliyo sababu ya matukio hayo yenye kutikisa ulimwengu?

Ni Biblia pekee inayotoa maelezo yenye kuridhisha.

[Chati katika ukurasa wa 27]

1914—Mwaka Uliotiwa Alama na Tarehe za Biblia na Matukio ya Ulimwengu

Tarehe

→ Biblia ilitabiri kipindi cha “nyakati saba,”

baada ya hicho Mungu angempa utawala wa ulimwengu

yeye ambaye angechagua

(Danieli 4:3-17)

→ “Nyakati saba = miaka 2,520

(Linganisha Ufunuo 11:2, 3; 12:6, 14;

Ezekieli 4:6.)

→ Mwanzo wa “nyakati saba”: 607 K.W.K.

(Ezekieli 21:25-27; Luka 21:24)

→ Mwisho wa “nyakati saba”: 1914 W.K.

Yesu Kristo alitawazwa

mbinguni, akaanza kutawala katikati

ya adui zake (Zaburi 110:1, 2)

Shetani alifukuzwa mbinguni;

ole wa wanadamu (Ufunuo 12:7-12)

Siku za mwisho zilianza (2 Timotheo 3:1-5)

Matukio Yaliyotabiriwa Kuwa Alama ya Siku za Mwisho

→ Vita (Vita ya ulimwengu ya kwanza ilianza mwaka wa 1914;

amani haijapata kurudishwa kamwe)

→ Njaa kubwa (Sasa inaua watu kama milioni 40

kila mwaka)

→ Kuenea kwa magonjwa ya kuambukiza (Ijapokuwa

uchunguzi wenye maendeleo ya kisayansi)

→ Matetemeko ya ardhi (Mara za kutokea kwa matetemeko ya ardhi makubwa

mengi zimeongezeka kufikia karibu 20 ya zilivyokuwa kila mwaka

tangu mwaka wa 1914)

→ Woga (Kuogopa uhalifu, kuanguka kwa uchumi,

maangamizi ya vita ya nyukilia)

Ulimwengu mbovu wa sasa utaharibiwa na Mungu kabla hakijapita kizazi kilichoona mwaka wa 1914 (Mathayo 24:3-34; Luka 21:7-32)

    Maktaba Kwenye Mtandao (1980-2025)
    Toka
    Ingia
    • Kiswahili
    • Shiriki
    • Mapendezi
    • Copyright © 2025 Watch Tower Bible and Tract Society of Pennsylvania
    • Masharti ya Utumiaji
    • Sera ya Faragha
    • Mpangilio wa Faragha
    • JW.ORG
    • Ingia
    Shiriki