Sura ya 16
“Umati Mkubwa” Wamshangilia Mfalme
1, 2. (a) Yehova alichukuaje hatua ya kutimiza unabii wake katika Isaya 60:22? (b) Ni ufunuo gani wa ajabu wa kweli ya kimungu uliofanywa mwaka wa 1935?
KUPITIA nabii wake, Yehova alitangaza: “Mdogo atakuwa elfu, na mnyonge atakuwa taifa hodari; mimi, [Yehova], nitayahimiza hayo wakati wake.” (Isaya 60:22) Na, kwa njia ya ajabu, Yehova ‘aliyahimiza.’ Mwaka wa 1935 Mashahidi wa Yehova walikusanyika katika Washington, D.C., U.S.A. Ikajulishwa huko kwamba Yehova alikuwa akichukua hatua ya kukusanya “umati mkubwa” (“mkutano mkubwa”) wa “kondoo wengine”—watu wenye kumwogopa Mungu ambao watapata uzima wa milele katika dunia ya paradiso kupitia ‘kuja’ kwa ufalme wa Mungu.—Yohana 10:16; Ufunuo 7:9.
2 Ufunuo sura ya 7 unasimulia kwamba baada ya kutiwa muhuri kwa lile “kundi dogo” la warithi wa Ufalme, ambao hesabu yao ni 144,000, “umati mkubwa wa watu wasiohesabika; watu wa kila taifa, ukoo, jamaa na lugha” unaonwa umesimama mbele ya kiti cha enzi cha Mungu. Wanaikubali enzi kuu ya Yehova inayotumiwa kupitia Kristo wake. Kwa shangwe wanasema wokovu unatoka kwa Mungu na kwa Mwana-Kondoo. Wakiwa kikundi, hawatahitaji kamwe kufa, maana “ndio wanatoka katika dhiki ile iliyo kuu” (UV) warithi uzima wa milele katika dunia safi.—Ufunuo 7:4, 9, 10, 14, HNWW; Luka 12:32.
3. (a) Je! yule “mdogo” amekuwa “elfu” kweli kweli? (b) Unawezaje kushiriki utimizo wa Ufunuo 7:15-17?
3 Je! wewe umechukua mahali pako kati ya huo “umati mkubwa” wa waabudu leo? Je! wewe ni mmoja wa wale zaidi ya 2,000,000 ‘wanaomtumikia Mungu’ katika dunia yote? Ni kweli kwamba bado unazungukwa na ulimwengu mbovu, wenye kuonea, na huenda ukalazimika kuvumilia mikazo mingi katika maisha yako ya kila siku. Lakini ukiwa mmoja wa wale “kondoo” wa Bwana, unalindwa na Mungu. Si lazima uone tena njaa wala kiu ya kukosa chakula cha kiroho. Si lazima tena uogope hasira ya Mungu yenye kuchoma, maana yule Mwana-Kondoo anakuchunga wewe na kukuongoza kwenye “chemchemi za maji ya uzima.” Kwa hiyo, kwa njia ya mfano, tayari unaushiriki utimizo wa ahadi hii: “Naye Mungu atayafuta machozi yote machoni mwao.”—Ufunuo 7:15-17, HNWW.
MFALME ABARIKI “KONDOO” ZAKE
4. Yesu ana uhusiano gani na “kundi dogo” lake?
4 Katika nyakati za Biblia, na hata kufikia wakati wetu, mchungaji wa Mashariki alifurahia uhusiano wa karibu sana pamoja na kondoo zake. Alimwita kila kondoo kwa jina, nao walijua sauti yake wakaitikia vyepesi alipowaingiza na kuwatoa nje ya zizi. Katika Yohana sura ya 10 Yesu alizungumza hilo kufananisha, kwanza, ule uhusiano wenye upendo kati yake mwenyewe na “kundi dogo” lake la wafuasi wapakwa-mafuta 144,000, akisema: “Mimi ndimi mchungaji mwema; nao walio wangu nawajua; nao walio wangu wanijua mimi; kama vile Baba anijuavyo, nami nimjuavyo Baba. Nami nautoa uhai wangu kwa ajili ya kondoo.” Hao wanakuwa sehemu ya “uzao [mbegu] wa Ibrahimu,” ambao kupitia huo “jamaa zote” za dunia zitajibariki zenyewe.—Yohana 10:14, 15; Mwanzo 12:3; Wagalatia 3:28, 29.
5. (a) Ni uhusiano gani zaidi wenye furaha unaotajwa katika Yohana 10:16? (b) “Kondoo wengine” wanafurahia mapendeleo gani sasa, na kikundi hicho kina taraja gani la wakati ujao?
5 Basi, ni uhusiano gani wa “mchungaji mwema” na zile jamaa za wanadamu zitakazoishi milele duniani? Ni wenye kubarikiwa sana! Maana Yesu anasema hivi juu yao:
“Na kondoo wengine ninao, ambao si wa zizi hili [la wale “kundi dogo”; na hao nao imenipasa kuwaleta; na sauti yangu wataisikia; kisha kutakuwako kundi moja na mchungaji mmoja.”
Leo, “umati mkubwa” wa hao “kondoo wengine” unaonwa ukilisha pamoja na lile “kundi dogo”—wote wakiitii kwa umoja ile “sauti” ya mchungaji wao kwa kuzihubiri “habari njema hizi za ufalme . . . katika dunia yote inayokaliwa na watu kwa ushuhuda kwa mataifa yote.” Lenye furaha ni fungu lako ikiwa wewe ni mmoja wa hao! (Yohana 10:16; Mathayo 24:14, NW) Chini ya ule utawala wa Ufalme, ile hesabu ya “kondoo wengine” itaongezeka kuwa mabilioni kupitia ufufuo wa wale wafu wa kidunia, wakati kusudi la Mungu la kuijaza dunia wanadamu waadilifu litakaposonga mbele likatimizwe kikamili.—Mwanzo 1:28.
6. Unabii wa Yesu unaonyeshaje wakati “kondoo wengine” wanapotokea?
6 Kwamba wale “kondoo wengine” wanatokea wakati wa “umalizio wa mfumo wa mambo” inaonyeshwa na ule mfano ambao Yesu anatumia kumalizia unabii wake juu ya ile “ishara” ya kuwapo kwake. (Mathayo 24:3, NW) Yeye anasema:
“Wakati Mwana wa Mtu atakapokuja katika utukufu wake na malaika wote wakiwa pamoja naye, hapo ataketi juu ya kiti chake cha enzi kitukufu. Mataifa yote yatakusanywa mbele yake, naye atawatenganisha watu kama vile mchungaji anavyowatenga kondoo mbali na mbuzi. Atawaweka kondoo upande wake wa kulia na mbuzi upande wake wa kushoto.” (Matayo 25:31-33, “HNWW”)
Kwa kuwa Mfalme huyo mtukufu na malaika zake hawaonekani kwa macho ya kibinadamu, anatimizaje kazi ya kutenganisha?
7. (a) Ile kazi ya kutenganisha inaelekezwaje? (b) Ni lazima ufanye nini ili upokee hukumu nzuri, na kwa sababu gani?
7 Malaika wanatoa mwelekezo wa kazi hiyo. (Ufunuo 14:6-12; linganisha Matendo 8:26-29; 10:1-8.) Na hapa duniani wale mabaki wa lile “kundi dogo,” wanaoitwa “ndugu” za Mfalme katika Mathayo 25:40, wanaongoza kazi ya kuzihubiri “habari njema.” Mfalme anahukumu watu kulingana na wanavyoitikia “ndugu” zake na ule ujumbe wa Ufalme ambao wanatangaza. Yale ambayo wanatendea “ndugu” zake anayahesabu kuwa ametendewa yeye mwenyewe. Watu wanaowapokea “ndugu” zake kwa ukarimu wanatazamia kupata baraka. Je! wewe ni mmoja wao? Bila shaka, ni lazima utimize takwa la kuukubali ujumbe wa Ufalme kwa moyo wote na kuwa mtumishi wa Yehova aliye wakf na kubatizwa, kwa msingi wa jina la Yesu—maana “hakuna wokovu katika mwingine awaye yote.”—Matendo 4:12; Mathayo 25:35-40.
8. Huenda ukashiriki wito na ahadi gani?
8 Wewe ukiwa mmoja wa “kondoo wengine” wa Bwana, unaweza kutazamia nini? Matokeo yatakuwa nini ukitii “sauti” ya “mchungaji mwema” aliye ‘mfalme’ wako? Katika kutoa hukumu, Mfalme huyo anawaambia hivi wale “kondoo” wanyenyekevu kwenye mkono wake wa kuume wa kibali: “Njoni, mliobarikiwa na Baba yangu, urithini ufalme mliowekewa tayari tangu kuumbwa ulimwengu.” Huenda ukatazamia kushiriki baraka hizo za Ufalme zinazotoka kwa Baba yetu, wakati ‘wenye haki watakapokwenda katika uzima wa milele.’ (Mathayo 25:34, 46) Ndiyo, huenda ukatazamia kushiriki utimizo wa ahadi nyingi za kiunabii, kama ile iliyo katika Isaya, inayosema hivi juu ya Yehova: “Atameza kufa kusiwe tena milele. Na Bwana [Yehova] atapangusa machozi toka nyuso zote; na haya ya watu wake ataiondosha toka dunia yote: maana [Yehova] amesema maneno haya.” Watu waovu wanaweza kukusuta kwa muda mfupi tu. Maana ahadi ya Mungu ni kwamba wote wanaomtumaini Yehova wataingia upesi katika “karamu” ya kweli kweli ya vitu vizuri katika “[dunia] mpya.” Wewe unataka kushiriki “karamu” hiyo, sivyo?—Isaya 25:6-9; 66:22, ZSB.
“MBUZI” NA MATESO
9, 10. (a) Sababu gani si rahisi kufuatia uadilifu leo? (b) Imekupasa uwe na maoni gani juu ya wapinzani, na unaweza kutazamia msaada gani kutoka kwa Mungu?
9 Huenda isiwe vyepesi kwako kufuatia mwendo wa uadilifu katika hizi “siku za mwisho.” Shetani na vibaraka wake huenda wakakudhihaki, wanapofanya bidii yao yote ya mwisho waharibu dunia hii na wanadamu walio juu yake. (2 Petro 3:3, 4; 2 Timotheo 3:1) Unapotembelea jirani zako ukiwa na ujumbe wa Ufalme, huenda ukakuta wengine wanaoonyesha maelekeo yaliyo mfano wa mbuzi. Wanafanya hivyo kwa kuonyesha ubaridi au ukali, au kwa upinzani wa waziwazi.—Mathayo 25:33, 42-45.
10 Walakini, wewe kama mmoja wa wale “kondoo” za Bwana haikupasi ujaribu kuhukumu ni nani “mbuzi” na ni nani “kondoo.” Mwenye kuhukumu hivyo ni yule Mfalme, si “kondoo” zake walio hapa duniani. (Linganisha Warumi 14:10-12.) Na, ijapo huenda ukapata upinzani kwa sababu ya kuwa mtangazaji wa “habari njema,” Mungu atakutia nguvu ufanye mapenzi yake, kama mtume Petro alivyoonyesha kwa maneno haya: “Mungu wa fadhili zisizostahilika zote . . . mwenyewe atamaliza mazoezi yenu, atawafanya mwe imara, atawafanya mwe na nguvu.” (1 Petro 5:10, NW; linganisha 2 Wakorintho 12:10.) Pia, mtume Paulo anatoa onyo hili zuri la upole: “Msitange-tange katika kazi yenu [ya Ufalme]. Mwake ile roho. Mwe watumwa wa Yehova. Lifurahieni tumaini. Vumilieni chini ya dhiki. Endeleeni katika sala.”—Warumi 12:11, 12, NW.
11. Huenda mwenendo mwema wa Kikristo ukawa na matokeo gani yenye furaha?
11 Huenda utumishi wako wa ushikamanifu na sala zako za bidii kwa Yehova, pamoja na mwenendo wako wa Kikristo wenye mfano mzuri, ukawa na matokeo ya kuona wengine ambao pale kwanza walionekana kuwa “mbuzi” wakiwa “kondoo.” Mara nyingi ule mwenendo wa subira, wenye heshima wa wake Wakristo, umekuwa na matokeo ya kuwavuta waume wasioamini wakawa waamini “pasipo lile Neno.” (1 Petro 3:1, 2) Hakika hatutaki kuona watu ‘wakiondoka wakaingie katika kukatiliwa mbali kwa milele.’ Badala yake, imetupasa tutake kuwasaidia waondoe maelekeo ya kimbuzi, ili waufikie uzima wa milele. —Mathayo 25:41, 46, NW.
“KONDOO” WASHIKAMANIFU WANASHIKA UKAMILIFU
12. Wale “ndugu” za Mfalme na wale “kondoo” wametegemezanaje katika nyakati za kisasa?
12 Inapasa kuangaliwa kwamba wale “kondoo” wa mfano wa Yesu walijitoa wenyewe ili wahudumie wale “ndugu” za Mfalme wakati hao walipokuwa wagonjwa na wakiwa gerezani. Na katika sehemu fulani za dunia leo, taabu na mateso, magonjwa na kufungwa gerezani kumepata si wale tu wa “kundi dogo,” bali pia na wale wa “kondoo wengine” wanaotumikia nao kwa ushikamanifu sana na kwa umoja. Kwa mfano, mwaka wa 1933 kufika 1945, wakati Hitler wa chama cha Nazi alipokuwa akijaribu kutawala ulimwengu, Mashahidi wa Yehova walipatwa na mateso makali—kwanza katika nchi za Kinazi na za Kifashisti na baadaye katika mataifa yote yenye kupigana. Wengi wa lile “kundi dogo” na vilevile wa “kondoo wengine” wa Bwana walivawa. Lakini walishinda kiajabu katika kushikamana na ukamilifu wao kwa Mfalme na ufalme wake!
13, 14. Ni tofauti gani ambayo imeonwa kati ya msimamo wa dini za Jumuiya ya Wakristo na ule wa Mashahidi wa Yehova?
13 Mara nyingi wanahistoria wametoa maelezo wakionyesha jinsi Mashahidi wa Yehova walivyo tofauti na dini za Jumuiya ya Wakristo. Wakati wa mikazo, dini za Jumuiya ya Wakristo zinabadili msimamo wazo, lakini Mashahidi wa Yehova wanasimama imara. Kwa mfano, katika kitabu A History of Christianity, kilichochapwa katika London, Uingereza, mwaka wa 1976, Paul Johnson anasema hivi kwanza juu ya makanisa ya Kikatoliki na ya Kievanjeli katika Ujeremani wa Hitler: “Makanisa yote mawili yaliunga mkono ule utawala kwa nguvu sana. Wale maaskofu wa Kikatoliki walishangilia ‘ule mkazo mpya wa kukazia sana mamlaka katika utawala wa Ujeremani’; Askofu Borne-wasser aliwaambia vijana Wakatoliki katika Kathedro ya Trier hivi: ‘Kwa vichwa vilivyoinuliwa na kwa hatua iliyo imara tumeingia utawala mpya nasi tuko tayari kuutumikia kwa uwezo wote wa mwili na nafsi yetu.’ Katika Januari 1934, Hitler alishauriana na viongozi kumi na wawili wa Kievanjeli, na baada ya mkutano wao . . . wakatoa tangazo rasmi lililofunga kwa kiapo kwamba ‘viongozi wa Kanisa la Kievanjeli Ujeremani wathibitishe kwa nia moja ushikamanifu wao usio na masharti kwa utawala wa Nazi na kiongozi wake.’ ”
14 Kisha, akitaja wale wachache wenye kujidai kuwa Wakristo ambao alisema ‘walishikamana na kanuni zao,’ mwandikaji huyo anaendelea kusema: “Waliokuwa na ushujaa kuliko wote ni Mashahidi wa Yehova, waliotangaza upinzani wao wa kimafundisho waziwazi tangu mwanzo na wakateseka kwa sababu hiyo. Walikataa ushirikiano wo wote pamoja na utawala wa Nazi ambao walilaumu vikali kuwa ni wenye uovu kabisa. . . . Wengi walihukumiwa kifo kwa sababu ya kukataa utumishi wa kijeshi . . . ; au wakaishia Dachau au katika nyumba za kutunzia walio na wazimu. Sehemu moja ya tatu waliuawa hasa; asilimia tisini na saba walipatwa na mateso ya namna fulani. Walikuwa ndio kikundi pekee cha Kikristo kilichostaajabisha Himmler.”
15. (a) Maoni yako ni nini juu ya ile barua ya namna ya pekee iliyo hapa? (b) Shetani alifanya jitihada gani wakati wa Vita ya Ulimwengu ya Pili, na ni ushuhuda gani unaoonyesha kwamba alishindwa?
15 Wakiwa si wasuluhishi wa vita, bali wakiwa Wakristo wasiokuwamo wenye kuunga mkono ufalme wa Mungu unaokuja, vijana Mashahidi walikabili kufungwa gerezani na kunyongwa badala ya kuvunja ukamilifu wao, kama ‘barua ya mwisho’ ya namna ya pekee inavyoshuhudia hapa. Katika dunia yote, iwe ni katika nchi zilizoungana pamoja au za urafiki, wale “ndugu” wa Mfalme na “kondoo” wenzi wao walighasiwa, wakapigwa sana, wakafungwa gerezani na kutendwa vibaya. Lakini walishinda katika vita yao ya kiroho. Yule Ibilisi hakuweza kuvunja ushikamanifu wao kwa Ufalme. Walijithibitisha kuwa “si sehemu” ya ulimwengu wa Shetani, kama Yesu zamani.—Yohana 15:19, NW.
MPANGO WA ELIMU WA UFALME
16, 17. (a) Sasa kulianzishwa mpango wa elimu na kazigani? (b) Ni matunda gani ya kazi hiyo yanayopasa kuonwa?
16 Msimamizi wa Sosaiti, J. F Rutherford, alikufa mwaka wa 1942 na kufuatwa na Nathan H. Knorr. Upesi baada ya hapo, Shule za Huduma ya Kitheokrasi zilianzishwa katika makundi yote ya Mashahidi wa Yehova, nazo zimetumika kwa mafaa kuzoeza Mashahidi wa kiume na wa kike wawaambie wengine ujumbe wa Ufalme kwa njia yenye matokeo na yenye kuvuta. Kwa muda wa miaka mingi, vitabu mbalimbali vya mafundisho vimetolewa vitumiwe na shule hizo. Wala umisionari haukusahauliwa. Katika Februari 1, 1943, ile Shule ya Gileadi ilianzishwa katika Tarafa ya New York. Kutoka nchi nyingi za dunia, maelfu ya wahudumu (“mapainia”) wa wakati wote wenye ujuzi wamepelekwa U.S. Marekani, wakazoezwa na kutumwa “duniani mwote” wakazihubiri “habari njema hizi za ufalme.”—Mathayo 24:14, NW; Warumi 10:18.
17 Lo! hiyo kampeni ya elimu duniani mwote imetokeza matunda ya ajabu kama nini! Tunapoendelea na miaka ya 1980 na kitu, jumla ya watu wanaoshiriki mkate na divai kwenye Ukumbusho wa mwaka wa kifo cha Yesu, kuonyesha tumaini lao ni kuungana pamoja naye katika ufalme wake wa kimbingu, imepungua ikawa chini ya 10,000, kadiri “ndugu” za Mfalme wanavyozidi kumaliza mwendo wao wa kidunia wakiwa wameshika ukamilifu. Lakini jumla ya wahudhuriaji wengine, wanaopendezwa kuishi milele duniani wakiwa raia za Ufalme, imeongezeka ikapita 6,000,000. Leo katika makundi ya Mashahidi wa Yehova zaidi ya 45,000 kuzunguka dunia hii, “umati mkubwa” wa wale “kondoo wengine” ndio unaofanya sehemu kubwa zaidi ya kazi ya kutoa ushuhuda. Lo! wewe una nafasi bora sana ya kuwa mmoja wao!
18. (a) Yule “mtumwa mwaminifu mwenye akili” ameendelezaje utumishi wake? (b) Sasa wewe unaweza kushiriki kazi gani yenye maana sana?
18 Ingawa hesabu yao inapungua, wale mabaki wapakwa-mafuta wa lile “kundi dogo” la Yesu, ile jamii ya “mtumwa mwaminifu mwenye akili,” wanaendelea kusimamia utendaji wa Ufalme. (Mathayo 24:45-47) Ili kutimiza hilo, jamii hiyo inafanya kazi kupitia baraza linaloongoza, huo ukiwa ni mpango unaofanana na ule uliokuwa katika kundi la Kikristo la karne ya kwanza. (Matendo 15:6; Luka 12:42-44) Alipokufa N. H. Knorr mwaka wa 1977, Frederick W. Franz akawa ndiye msimamizi wa nne wa Sosaiti, akiwa mwenye umri wa miaka 83. Na Julai 1, 1979, gazeti la Mnara wa Mlinzi lenyewe lilifikia umri wa miaka 100! Limekuwa na karne moja yenye ushuhuda wa Ufalme. Ndiyo, kwa vitabu na kwa neno la kinywa, “habari njema hizi” za Ufalme uliosimamishwa zimetangazwa katika dunia yote kwa ushuhuda. Je! wewe unaishiriki kazi hii yenye pendeleo kwa kufuata kiolezo ambacho Yesu aliacha? Kama Paulo alivyoshauri kwa upole:
“Kupitia yeye daima na tutoe kwa Mungu dhabihu ya sifa, yaani, tunda la midomo inayofanya tangazo la hadhara kwa jina lake.”—Waebrania 13:15, “NW.”
19. (a) Ni mwendo gani unaohusu “moyo” na “kinywa” ambao Paulo alitia moyo ufuatwe? (b) Ni maulizo gani yenye kupatana na wakati yanayoultzwa hapa, nawe unaitikiaje?
19 Mtume Paulo alitangaza hivi katika barua nyingine: “Kwa moyo mtu hutumia imani kwa ajili ya uadilifu, lakini kwa kinywa mtu hufanya tangazo la hadhara kwa ajili ya wokovu.” (Warumi 10:10, NW) Je! wewe unaziamini “habari njema,” ambazo sasa zinakaza fikira kwenye ufalme wa Mungu, uliosimamishwa katika mbingu tangu mwaka wa 1914? Je! wewe ‘unafanya tangazo la hadhara kwa ajili ya wokovu,’ unaposali ufalme wa Mungu “uje” kwa kani zake zote za uharibifu kuondoa tengenezo la Shetani katika dunia hii? Je! wewe una bidii ya kuwaambia wengine “waziwazi, na nyumba kwa nyumba” habari za baraka za Ufalme zitakazowamiminikia wanadamu wote wakati mapenzi ya Mungu yatakapotimizwa karibuni, “duniani kama huko mbinguni”? Je! wewe unaiunga mkono kishikamanifu ile jamii iliyopakwa mafuta ya “mtumwa mwaminifu mwenye akili” ya Wakristo wa kweli, wanapoendelea kuongoza utolewaji wa ule ujumbe wa Ufalme “katika dunia yote . . . na kwenye zile pembe za dunia inayokaliwa na watu,” na ‘kufanya wanafunzi kutoka kwa watu wa mataifa yote, kuwabatiza na kuwafundisha’?—Mathayo 6:10; 24:14, 45-47, UV; 28:19, 20, NW; Matendo 5:42; 20:20, UV; Warumi 10:18, NW.
20. Ni pendeleo gani bora unaloweza kufurahia sasa?
20 Huenda ukafurahia pendeleo bora leo la ‘kutoa hivyo utumishi mtakatifu mchana na usiku mbele ya kile kiti cha enzi cha Mungu.’ Wakati uo huo unajiweka mwenyewe tayari kuwa mmoja wa “umati mkubwa” utakaorithi uzima wa milele katika dunia itakayofanywa tukufu. (Ufunuo 7:9-17, NW) Lakini kwanza ni lazima ule Ufalme “uje” kupigana vita ya Har-Magedoni! Har-Magedoni itakuwa na matokeo gani kwa wanadamu na dunia yetu?
[Sanduku katika ukurasa wa 159]
WASIOKUWAMO MPAKA KIFO CHENYEWE
Wakati wa vita ya ulimwengu ya pili, vijana wengi walio mashahidi wa Yehova waliuawa kwa sababu ya kutokuwamo. Barua ifuatayo ni aina ya pekee ya zile ‘barua za mwisho’ ambazo Mashahidi hao wenye ushujaa waliandikia jamaa zao. Iliandikwa na Marcel Sutter, kijana mwenye umri wa miaka 23, wa Alsace-Lorraine, saa chache kabla hajakatwa kichwa kwa shoka katika gereza la Torgau, Ujeremani, Agosti 1942.
“Wazazi na dada zangu wapendwa sana,
“Mpokeapo barua hii, sitakuwa hai tena. Ni saa chache tu zinazonitenganisha na kifo changu. Nawaomba mwe na nguvu na ushujaa; msilie, kwa kuwa nimeshinda. Nimeumaliza mwendo na kuidumisha imani. Yehova Mungu anisaidie mpaka mwisho. Ni kipindi kifupi tu kinachotutenganisha na ufalme wa Bwana yetu Yesu Kristo. Karibuni tutaonana tena katika ulimwengu mzuri zaidi wenye amani na uadilifu. Nafurahi ninapowazia siku hiyo, kwa kuwa wakati huo hakutakuwako kupiga kite tena. Litakuwa jambo zuri kama nini! Natamani sana amani. Wakati wa saa hizi chache za mwisho nimekuwa nikiwafikiria, na moyo wangu una uchungu kidogo ninapowaza sitaweza kuwapiga busu la kwa-heri. Walakini lazima tuwe na saburi. Wakati unakaribia Yehova atakapotetea Jina lake na kuthibitishia viumbe vyote kwamba yeye ndiye Mungu wa pekee wa kweli. Sasa nataka kumwekea wakf saa zangu chache za mwisho, kwa hiyo nitamaliza barua yangu na kusema kwa-heri mpaka tutakapoonana tena karibuni. Sifa na iwe kwa Mungu wetu Yehova! Kwa upendo wangu mchangamfu na salamu,
“Mwana wenu na ndugu mpendwa,
Marcel”