Maswali Kutoka kwa Wasomaji
● Kuna ushuhuda gani wa kuonyesha kwamba wale wanaotajwa kuwa “kondoo wengine” katika Yohana 10:16 ni watu ‘watakaoishi duniani katika taratibu mpya ya Mungu?—Italia.
Twaweza kujua “kondoo wengine” ni akina nani kwa kulinganisha habari zinazozunguka mstari huo na maandiko mengine.
Yesu Kristo alisema: “Mimi ndimi mchungaji mwema; nao walio wangu nawajua; nao walio wangu wanijua mimi; kama vile Baba anijuavyo, nami nimjuavyo Baba. Nami nautoa uhai wangu kwa ajili ya kondoo. Na kondoo wengine ninao, ambao si wa zizi hili; na hao nao imenipasa kuwaleta; na sauti yangu wataisikia; kisha kutakuwako kundi moja na mchungaji mmoja.”—Yohana 10:14-16.
Maneno hayo yanafunua kwamba Yesu awaona kuwa “kondoo” zake wale wanaojua sauti yake peke yao, yaani, wale wanaotambua ana mamlaka juu yao akiwa mchungaji wao. Hiyo yaonyesha wazi kwamba kundi la “kondoo” ambalo Yesu alitofautisha na “kondoo wengine” lisingaliweza kuwa taifa la Israeli, kwa sababu ni mabaki madogo tu ya taifa hilo yaliyomtambua Yesu Kristo kama mchungaji wao. Basi, “kondoo” wa kundi ambalo lingekuwa “kundi moja” pamoja na wale “kondoo wengine” walikuwa nani? Je! wangekuwa wanafunzi Wayahudi, nao “kondoo wengine” wawe Mataifa ambao baadaye walikubaliwa kuwa Wakristo waliotiwa mafuta? Ingawa wafafanuzi wa Jumuiya ya Wakristo hutoa maelezo hayo, hayapatani na maandiko mengine.
Huko nyuma wakati wa huduma ya Yesu ya kidunia, wote waliomkubali kuwa mchungaji wao waliingia katika hali ya kukubaliwa wawe washiriki wa ufalme wa mbinguni. Yesu aliwaambia wanafunzi wake hivi: “Msiogope, enyi kundi dogo; kwa kuwa Baba yenu ameona vema kuwapa ule ufalme.” (Luka 12:32) Nyakati nyingine Yesu Kristo alilitaja “kundi dogo” hilo la wanafunzi kama “ndugu” zake. (Mt. 12:49; Marko 3:34; Luka 8:21; Yohana 20:17) Wakati baadaye Mataifa walipokubaliwa na Mungu, wakatiwa mafuta kwa roho takatifu yake na kuitwa kwenye uzima wa mbinguni, wao pia wakawa “warithi washirika pamoja na Kristo,” wakawa “ndugu” zake. (Gal. 3:27-29; Rum. 8:17, NW) Basi ni busara kuwaza kwamba “kondoo wengine” ni watu ambao si “ndugu” zake lakini wanaletwa washirikiane nao.
Maneno ya Yesu Kristo juu ya kuja kwake katika utukufu wa Ufalme yahakikisha hilo. Twasoma hivi:
“Hapo atakapokuja Mwana wa Adamu katika utukufu wake, na malaika watakatifu wote pamoja naye, ndipo atakapoketi katika kiti cha utukufu wake; na mataifa yote watakusanyika mbele zake; naye atawabagua kama vile mchungaji abaguavyo kondoo na mbuzi; atawaweka kondoo mkono wake wa kuume, na mbuzi mkono wake wa kushoto.
“Kisha Mfalme atawaambia wale walioko mkono wake wa kuume, Njoni, mliobarikiwa na Baba yangu, urithini ufalme mliowekewa tayari tangu kuumbwa ulimwengu; kwa maana nalikuwa na njaa, mkanipa chakula; nalikuwa na kiu, mkaninywesha; nalikuwa mgeni, mkanikaribisha; nalikuwa uchi, mkanivika; nalikuwa mgonjwa, mkaja kunitazama; nalikuwa kifungoni, mkanijia. Ndipo wenye haki watakapomjibu, wakisema, Bwana, ni lini tulipokuona una njaa, tukakulisha, au una kiu tukakunywesha? Tena ni lini tulipokuona u mgeni, tukakukaribisha, au u uchi, tukakuvika? ni lini tena tulipokuona u mgonjwa, au kifungoni, tukakujia? Na Mfalme atajibu, akiwaambia, Amin, nawaambia, kadiri mlivyomtendea mmojawapo wa hao ndugu zangu walio wadogo, mlinitendea mimi.”—Mt. 25:31-40.
“Kondoo” wanaotajwa hapa wanafunuliwa kuwa tofauti na ndugu za Kristo. Hata hivyo, kama vile ndugu za Kristo wanavyomtambua yeye kuwa “Bwana” wao au mchungaji wao, ndivyo kondoo hao wanavyomtambua pia. Vikundi vyote viwili vinafanyiza kundi moja kwa kumnyenyekea yeye. Kondoo wanaotajwa hapa wanashirikiana kabisa na ndugu za Kristo, na kuwaunga mkono kwa bidii. Lakini wanatofautianaje na ndugu za Kristo?
Mambo ambayo Mfalme Yesu Kristo aliwaambia yanatusaidia kufahamu kwamba kuna jamii mbili zinazotofautiana. Yeye aliwaambia “kondoo” hivi: “Urithini ufalme mliowekewa tayari tangu, kuumbwa [kuwekwa misingi ya, NW] ulimwengu.” (Mt. 25:34) Yanayosemwa juu ya “ndugu” za Kristo ni tofauti na hayo. Ushirika wa ufalme wa mbinguni ambao ungerithiwa na “ndugu” hawa ulitangulia kujulikana kabla ya “kuwekwa misingi ya ulimwengu,” yaani, kabla ya ulimwengu wa wanadamu kutokea kwa kuzaliwa kwa watoto wa wanadamu wawili wa kwanza, Adamu na Hawa. Mtume Paulo alipowaandikia Wakristo wenzake alisema: “[Mungu] alivyotuchagua katika yeye kabla ya kuwekwa misingi ya ulimwengu.”—Efe. 1:4, 5.
Tofauti kati ya nyakati jamii hizo mbili zilipotangulia kuwekewa thawabu yaonyesha wazi-wazi zina matumaini ya kuishi mahali mbali mbali. Juu ya urithi wa “ndugu” za Yesu, mtume Petro aliandika hivi: “Ahimidiwe Mungu, Baba wa Bwana wetu Yesu Kristo, ambaye kwa rehema zake nyingi alituzaa mara ya pili ili tupate tumaini lenye uzima kwa kufufuka kwake Yesu Kristo katika wafu; tupate na urithi usioharibika, usio na uchafu, usionyauka, uliotunzwa mbinguni kwa ajili yenu.” (1 Pet. 1:3, 4) Urithi huo wa kimbinguni unahusu utawala, kwa maana Ufunuo 5:10 wasema: “[Kristo akawafanya] kuwa ufalme na makuhani kwa Mungu wetu; nao [watamiliki] juu ya nchi.”
Lakini “ndugu” za Kristo watatawala nani? Watatawala wanadamu duniani. Hiyo yapatana na Ufunuo 21:3, 4.
Kwa kuwa “kondoo wengine” si ndugu za Kristo, ni wazi kwamba wanaelekea kupata baraka za dunia isiyo na huzuni wala mauti. Hiyo ndiyo thawabu watakayopewa chini ya utawala wa Yesu Kristo na warithi wenzake. Hiyo ndiyo sababu wanatajwa ‘wakirithi ufalme waliowekewa tayari tangu kuumbwa ulimwengu.’ Neno la asili la Kigiriki la ufalme halimaanishi serikali peke yake. bali laweza pia kumaanisha “utawala” au “kutawalwa na ufalme.” Hivyo, “kondoo wengine” wanarithi hali ya kutawalwa na Mfalme Yesu Kristo na wafalme wenzake, “ndugu” zake. Mara tu Adamu na Hawa walipoanza kuzaa watoto ambao wangekuwa na nafasi ya kuwa chini ya utawala wa Ufalme, ahadi ya Mungu juu ya kuwa na utawala huo ilitimia. Katika maana hii, wanadamu walitayarishiwa “ufalme,” yaani, hali ya kutawalwa na ufalme, “tangu kuumbwa ulimwengu.”
Hivyo ushuhuda wa Biblia kwa ujumla waonyesha “kondoo wengine” ni watu watakaopata uzima duniani chini ya utawala wa ufalme wa Mungu unaosimamiwa na Kristo, hata kama watakuwa kati ya “mkutano mkubwa” watakaookoka “dhiki” au kama watakuwa kati ya wanadamu watakaofufuliwa.—Matendo 24:15.