Raia za Kidunia za Ufalme wa Mungu
Makala hii ni ya kutumia kwa mafunzo ya kitabu ya kundi
1, 2. Wale wanaosali “Sala ya Bwana” wanaomba nini hasa?
WATU walio wengi katika nchi zinazojulikana kama “za Kikristo” wamesali inayoitwa kwa kawaida “Sala ya Bwana” au “Baba Yetu.” Sala hii iliyoandikwa katika Mathayo 6:9-13, yamsihi Mungu hivi: “Ufalme wako uje, mapenzi yako yatimizwe, hapa duniani kama huko mbinguni.”
2 Kama wajuavyo watu wote wanaoifahamu Biblia, mbingu ndiyo makao ya Mungu mwenyewe. Wakati mapenzi yake yatakapofanywa duniani’ kama yanavyofanywa mbinguni, dunia hii itakuwa na amani na utulivu nao wakaaji wake watafurahia afya, uzima na furaha chini ya ufalme wa Mungu.
3. Ufalme ‘utakujaje,’ kama inavyoombwa katika sala hiyo?
3 Lazima Ufalme “uje” kuziharibu falme za ulimwengu huu kama vile jiwe lililoonekana na Mfalme Nebukadreza katika ndoto yake, kama ilivyoandikwa katika Biblia, ‘lilivyokuja’ kuiharibu sanamu aliyoiona, nao lazima uzisage falme hizo ziwe unga, kama vile jiwe lilivyoifanyia sanamu. (Ufu. 11:15; Dan. 2:32-35, 44) Hii itasafisha dunia na mambo yote yanayoipinga enzi kuu ya Yehova Mungu, kutayarisha njia mapenzi ya Mungu yatimizwe duniani kabisa. Je! wo wote wataokoka ‘kusagwa’ huko? Na, ikiwa wako, ni akina nani? Ni nini kinachowastahilisha waokoke?
“KONDOO” NA “MBUZI”
4. Yesu alilijibuje ulizo ambalo huenda tukawa nalo juu ya ni nani watakaouokoka uharibifu wa hii taratibu ya mambo?
4 Mojawapo la majibu yenye kudhihirisha sana kwa maulizo haya linatolewa na mfano wa Yesu wa kondoo na mbuzi. Mfano huo ulikuwa mmojawapo wa kadha iliyotolewa kwa kulijibu ulizo la mitume, “Ni nini itakayokuwa ishara ya kuwapo kwako na ya mwisho wa taratibu ya mambo?” (Mt. 24:3, NW) Utimizo wa mfano ni mojawapo ya sehemu za “ishara” hiyo. Wakati wa utimizo wake unaonyeshwa katika maneno yake ya mwanzo: “Hapo atakapokuja Mwana wa Adamu katika utukufu wake, na malaika watakatifu wote pamoja naye, ndipo atakapoketi katika kiti cha utukufu wake; na mataifa yote watakusanyika mbele zake; naye atawabagua kama vile mchungaji abaguavyo kondoo na mbuzi; atawaweka kondoo mkono wake wa kuume, na mbuzi mkono wake wa kushoto.”—Mt. 25:31-33.
5. (a) Ni nini kinachofananishwa na namna mbili za wanyama wanaotajwa katika mfano, katika utimizo? (b) Mfano waonyeshaje kwamba ‘kufika’ kwa Kristo ni kwa muda fulani kabla ya Ufalme kuja kuiharibu hii taratibu ya mambo?
5 Yesu anaelewesha kwamba kondoo na mbuzi wanafananisha jamii mbili za watu katika utimizo. Wakati mtu anapofikiria hili, inakuwa wazi kwamba ‘kufika’ kwa Kristo katika mamlaka ya Ufalme na utukufu lazima kutukie wakati fulani kabla hajauleta Ufalme kuiharibu hii taratibu ya mambo na kabla hajauanza utawala wake wa amani wa miaka elfu. (Isa. 9:6, 7; Ufu. 20:4-6) Ama sivyo, kazi ya kutenga ingefanywaje, kuamua ni nani wanaostahili kuendelea kuishi duniani na wanaostahili uharibifu?
6. Kutenga kunafanywa juu ya msingi gani, nayo hii yaonyeshaje kwamba kutachukua muda fulani?
6 Kutenga hakufanywi kwa sababu za kikabila au za kitaifa. Sivyo, ni hukumu juu ya nyutu. Utu unachukua muda kukuzwa kabisa, na mwendo wa tendo unasitawishwa na mfululizo wa matendo yanayokuwa jambo la kawaida analofanya mtu. Kwa hiyo inachukua kipindi cha wakati kabla hukumu haijaweza kutolewa juu ya utu kamili na mwenendo wa kawaida usiobadilika wa mtu. Hii inahitaji wakati uruhusiwe kabla hukumu ya haki na isiyobadilika haijatangazwa na kufikilizwa juu ya mtu. ‘Lakini,’ huenda mtu akauliza, ‘je! Yesu Kristo hawezi kuhukumu mioyo bila ya kumwona mtu mwenyewe akitenda tendo hili au lile?’ Ndiyo, aweza, lakini anawaruhusu watu waonyeshe kabisa mbele ya watu hukumu wanayostahili.
‘KUURITHI UFALME’
7-9. Twaonaje kwamba “kondoo” wa mfano si warithi wa kimbinguni washirika na Kristo?
7 “Kondoo” wanawekwa katika mkono wa kulia wa kibali. Mfano unaendelea kusema hivi: “Kisha Mfalme atawaambia wale walioko mkono wake wa kuume, Njoni, mliobarikiwa na Baba yangu, urithini ufalme mliowekewa tayari tangu kuumbwa ulimwengu.”—Mt. 25:34.
8 Hesabu isiyotajwa wazi ya “kondoo” hawaambiwi watakwenda mbinguni, wakawe warithi washirika na Yesu Kristo, wakipata “ufufuo wa kwanza” na kutawala naye. Hawa wa pili ni wachache katika hesabu. (Ufu. 14:1-3; 20:4-6) “Kondoo” wa mfano wanapata kuwa wengi mara nyingi zaidi. Wao ndio “mkutano mkubwa sana ambao hapana mtu awezaye kuuhesabu, watu wa kila taifa, na kabila, na jamaa, na lugha.” (Ufu. 7:9, 10) Wao ni sehemu ya hao “kondoo wengine,” ambao Yesu aliwatofautisha na “kundi dogo” la warithi washirika 144,000 kwa kusema hivi:
9 “Kondoo wengine ninao, ambao si wa zizi hili; na hao nao imenipasa kuwaleta; na sauti yangu wataisikia; kisha kutakuwako kundi moja na mchungaji mmoja.”—Yohana 10:16; Luka 12:32.
10. (a) Ni kwa njia gani “kondoo” ‘wamebarikiwa na Baba ya Kristo’? (b) Ni nini maana ya neno “ufalme” kama linavyotumiwa katika mfano?
10 Hawa wenye mfano wa kondoo wamebarikiwa na Baba yao, hasa kwa sababu yeye aliijua mapema jamii ya kondoo ya wakati huu wa kuwapo kwa Kristo, aliiwekea akibani thawabu. ‘Kuurithi ufalme’ kusingemaanisha kurithi sehemu katika viti vya enzi mbinguni. Chini ya neno la awali la Kigiriki la “ufalme” (Ba·si·leiʹa), Liddell and Scott’s Greek-English Lexicon yasema kwamba neno la Kigiriki lina maana ya kiarifa chenye habari ya kutendwa (si kutenda, au passive kwa Kiingereza), yaani ‘kutawaliwa kwa mtu na mfalme,’ na pia laweza kumaanisha “utawala.” Kwa hiyo “mkutano mkubwa” wa “kondoo wengine” unarithi miaka elfu moja ya amani papa hapa chini duniani, katika makao ya kidunia ya Ufalme.—Zab. 2:8; Dan. 2:35-45.
11. Urithi wa Ufalme umetayarishwaje kwa “kondoo” “tangu kuumbwa ulimwengu”?
11 Kwa hiyo, ni nini “kuumbwa ulimwengu” kunakotajwa katika mfano? Hakumaanishi mwanzo wa sayari hii, wala wakati wa kuumbwa kwa Adamu na Hawa, kwa maana Mungu hakuunda ufalme wakati huo, Adamu akiwa mfalme. Ni baada ya Adamu kutenda dhambi Mungu alipoonyesha kusudi lake la kuwa na Uzao ambao ungepata ushindi juu ya nyoka wa mfano, Shetani Ibilisi. (Mwa. 3:15; Ufu. 12:9) Uzao huu ungekuwa Mfalme juu ya wanadamu wote. Adamu na Hawa walikuwa wamekuwa watenda dhambi wa makusudi juu ya Mungu, wakistahili kifo tu. Lakini walipoanza kuzaa watoto, watoto hawa walirithi dhambi. Kwa hiyo, ilikuwako nafasi kwao kukombolewa na dhambi na kuja chini ya ufalme uliosimamishwa wa Uzao. Kwa hiyo “kuumbwa ulimwengu” kwamaanisha wakati ambao Adamu na Hawa walizaa watoto ambao wangeweza kufaidika na mipango hii.—Luka 11:50, 51.
NAMNA AMBAVYO “KONDOO” WANASTAHILI KUOKOKA
12. Yesu asema ni nini kinachowastahilisha “kondoo” baraka?
12 Ni nini msingi ambao kwao “kondoo” wanapokea baraka ya Baba? Ni nini kinachowastahilisha? Yesu anaeleza: “Nalikuwa na njaa, mkanipa chakula; nalikuwa na kiu, mkaninywesha; nalikuwa mgeni, mkanikaribisha; nalikuwa uchi, mkanivika; nalikuwa mgonjwa, mkaja kunitazama; nilikuwa kifungoni, mkanijia. Ndipo wenye haki watakapomjibu, wakisema, Bwana, ni lini tulipokuona una njaa, tukakulisha, au una kiu tukakunywesha? Tena ni lini tulipokuona u mgeni, tukakukaribisha, au u uchi, tukakuvika? na lini tena tulipokuona u mgonjwa, au kifungoni, tukakujia? Na Mfalme atajibu, akiwaambia, Amin, nawaambia, kadiri mlivyomtendea mmojawapo wa hao ndugu zangu walio wadogo, mlinitendea mimi.”—Mt. 25:35-40.
13. (a) Mfano unaendeleaje kuonyesha kwamba “kondoo” si ndugu za kiroho wa Kristo? (b) Ni nini kinachoonyesha kwamba hawamwoni Kristo wakati wa kuwapo kwake na wa hukumu yake juu yao?
13 Twajifunza kwamba fadhili za upendo ndizo “kondoo” walizomwonyesha Kristo kwa matendo yao kwa “ndugu” zake. Hapa tena twaona kwamba “kondoo” wa mfano si warithi wa kiroho waliotiwa mafuta walio washirika na Kristo, watakaokuwa mbinguni pamoja naye. Hawa wa pili wanaitwa “ndugu,” hii ikiwatofautisha na wenye mfano wa kondoo wanaowasaidia “ndugu” hawa. “Kondoo” wanauliza, “Ni lini tulipokuona?” kuonyesha kwamba Kristo haonekani wakati wa kuwapo kwake, akiwahukumu, si kulingana na wanayomfanyia yeye mwenyewe, kwa maana akiwa Mfalme wa kimbinguni hana haja ya msaada wa kidunia. Lakini wanaweza kuwaona “ndugu” za Kristo, nao ndugu hawa wa Kristo ambao wangali duniani wanapatwa na shida mara nyingi.
14. Kwa sababu gani nia ya huruma na fadhili kabisa haitoshi kustahilisha watu kuwa “kondoo”?
14 Ni kwa sababu gani wenye mfano wa kondoo wanatoa msaada? Je! ni kwa sababu ya nia yenye huruma na fadhili kabisa? Wako watu wengi wenye huruma ulimwenguni, wanaomsaidia ye yote mwenye shida. Hii ni tabia njema, ya kusifika. Lakini linapokuwa shauri la kuwasaidia au kuwatetea “ndugu” za Kristo walio “mabalozi” wa Kristo, inakuwa tofauti. (2 Kor. 5:20, NW) Wakati mabalozi hawa wanapotangaza hukumu zinazokuja za Mungu juu ya ulimwengu, kwa kawaida hawapendwi na watu wengi. Mara nyingi wanateswa. Chini ya hali hizo watu wengi wenye huruma wanakuwa waoga, mara nyingi wanapinga, na kukataa kutoa msaada.
15. Ni nini juu ya nia ya kusaidia ya “kondoo” kinachowapa ustahili machoni pa Kristo?
15 Kwa upande mwingine, wale ambao Yesu anawataja kama “kondoo” wanafurahi kusaidia ye yote wawezaye, lakini, hasa, wao wanatumia nguvu zao kusaidia “ndugu” za Kristo kwa kila njia waliyo nayo. Wanafanya hivyo kwa bidii na kwa makusudi kwa sababu wanawajua na kuwakubali hawa kama watumishi wa Mungu. Hii ndiyo inawapa ustahili wa pekee machoni pa Kristo, kupatana na kanuni aliyoitaja mwenyewe: “Ye yote atakayewanywesha ninyi kikombe cha maji, kwa kuwa ninyi ni watu wa Kristo, amin, nawaambia, hatakosa thawabu yake.” (Marko 9:41) “Mtu awaye yote atakayemnywesha mmojawapo wa wadogo hawa ngaa kikombe cha maji ya baridi, kwa kuwa ni mwanafunzi, amin, nawaambia, haitampotea kamwe thawabu yake.”—Mt. 10:42.
16. “Kondoo” wanasaidia ndugu za kiroho wa Kristo kwa kadiri gani?
16 “Kondoo” hawawapi ndugu za kiroho wa Yesu Kristo msaada wa kimwili tu. Hawa wenye mfano wa kondoo wanaiona kazi ambayo “ndugu” hawa wachache wa Kristo waliobaki duniani wanafanya, nao pia wanaifanya pamoja nao, hata kuyashiriki mateso yanayowapata. Kwa kweli, wao sasa ndio wanaofanya sehemu iliyo kubwa ya kazi ya kuhubiri kwa sababu ya idadi zao kubwa. Yaani, wanashirikiana sana na “mabalozi” wa Kristo katika makundi yao, wengi wakipewa vyeo vya madaraka, kwa sababu uzee au afya mbaya inazuia wengi wa “ndugu” za Kristo.
WAWEZA KUWA MMOJA WA “KONDOO”
17. Je! “kondoo” wanakuja sasa kutoka mataifa mengi na lugha, kama mfano ulivyotabiri, nao wanachukua hatua gani wapate kibali kamili ya Baba na Mwana?
17 Kwa sasa hawa wenye mfano wa kondoo wanakuja kutoka “mataifa mengi,” nchi 208 na vikundi vya visiwa, kwa idadi kubwa zinazozidi 144,000 mara nyingi, ambayo ndiyo jumla ya wale watakaotawala mbinguni na Kristo. Wanajiweka wakf na kubatizwa si katika jina la Mwana tu, bali pia katika jina la Baba, Baba ya Mwana, ambaye ni Yehova.—Mt. 28:18-20.
18. Nabii Zekaria alitabirije kukusanywa kwa hawa wenye mfano wa kondoo?
18 Si katika mfano huu tu tunamoona matendo ya hii jamii yenye watu wa mfano wa kondoo yakisimuliwa. Zamani sana, nabii Zekaria alitabiri hali yao, kwa maneno haya: “Itatokea halafu ya kwamba watakuja mataifa na wenyeji wa miji mingi; wenyeji wa mji huu watauendea mji huu, wakisema, Haya! twendeni zetu kwa haraka tuombe fadhili za [Yehova], na kumtafuta [Yehova] wa majeshi; Mimi nami nitakwenda. . . . Siku hizo watu kumi, wa lugha zote za mataifa, wataushika upindo wa nguo yake yeye aliye Myahudi; naam, wataushika wakisema, Tutakwenda pamoja nanyi, kwa maana tumesikia kwamba Mungu yu pamoja nanyi.”—Zek. 8:20-23.
19. Ni nani “yeye aliye Myahudi” ambaye nguo yake inashikwa?
19 Katika utimizo wa unabii huu, mtu ambaye nguo yake inashikwa ni Myahudi wa kiroho, ndugu za kiroho wa Kristo 144,000. (Rum. 2:28, 29) Watu “wa lugha zote za mataifa” wanaokwenda na huyo wanasimuliwa katika Ufunuo 7:9-17, mara tu baada ya kukusanywa kwa 144,000 kusimuliwa.
20. Isaya alisema nini juu ya kukusanya katika “siku za mwisho”?
20 Tena, nabii Isaya alitabiri hivi: “Itakuwa katika siku za mwisho, mlima wa nyumba ya [Yehova] utawekwa imara juu ya milima, nao utainuliwa juu ya vilima; na mataifa yote watauendea makundi makundi. Na mataifa mengi watakwenda na kusema, Njoni, twende juu mlimani kwa [Yehova], nyumbani kwa Mungu wa Yakobo, naye atatufundisha njia zake, nasi tutakwenda katika mapito yake.”—Isa. 2:2, 3.
21. Maneno ya Isaya yanatimizwaje sasa?
21 Ushuhuda wa Biblia na mambo ya hakika yanaonyesha kwamba tumo katika “siku za mwisho” za hii taratibu ya mambo. Kupitia kwa Mfalme wake aliyetawazwa, Yehova anajulisha jina lake na enzi yake kuu. Sheria yatoka Yerusalemu wa kimbinguni, ambako watu wa mataifa wanamkusanyikia. (Gal. 4:26) Kama vile hekalu la Yehova lilivyokuwa juu ya kilima kirefu katika mji wa Yerusalemu, ndivyo ibada safi inavyoinuliwa sasa na tangazo la ulimwenguni pote la ujumbe wa Ufalme. Watu wengi wanasikia nao wanasema hivi kwa nia, “Mimi nami nitakwenda.”
22. Twaweza kuona tumaini la uzima wa milele likionyeshwa wapi duniani, na je! ni tumaini lenye kufaa?
22 Hivyo ibada ya kweli ya Mungu inapanuka duniani, kati ya wale wanaothamini uzima na watakao kuishi milele. Huwezi kuona tumaini hilo mahali pengine po pote. Hata hivyo, ni tumaini lenye msingi imara, tumaini la kweli, lenye msingi wa Neno la Mungu wa Milele. Watu wenye mfano wa kondoo waliotabiriwa katika mfano, pamoja na mabaki ya “ndugu” za Kristo walio duniani, ndio watu wa pekee duniani walio na tumaini la kuuokoka uharibifu wa hii taratibu ya mambo.
23. Inawapasa watu wanaousikia ujumbe wa Ufalme sasa watambue nini na kufanya nini?
23 Je! wewe umepata kuonana na “ndugu” za Mfalme, au walau washiriki wao, watu wenye mfano wa kondoo wanaoifanya kazi ile ile ya kuutangaza na kuufundisha ujumbe mwema wa Ufalme? Ikiwa unawatambua hawa kama wanafunzi wa Kristo utabarikiwa kwa kushirikiana nao katika Majumba ya Ufalme yao, ujifunze kweli za Biblia wanazofundisha, na kuwasaidia katika kazi yao.
—Kutoka Kitabu God’s Kingdom of a Thousand Years Has Approachied.