Chukua Hatua Mara Moja Juu ya “Ishara”!
“Endeleeni kukesha, kwa sababu hamjui siku wala saa.”—MATHAYO 25:13. Byington
1. Ni kwa sababu gani halingekuwa jambo la hekima kuwa kama wale wanawali wapumbavu wa mfano wa Yesu?
KWA KUWA kipindi bora sana kinakuja kwa ajili ya ulimwengu wa wanadamu waliokombolewa, lingekuwa jambo lisilo la hekima kama nini kuwa kama wale wanawali wapumbavu watano wa mfano wa Yesu! Walichukua hatua wakiwa wamechelewa mno na hawakuingia katika “ufalme wa mbinguni.” Hao wapumbavu hawakutenda kama vimulikaji katika wakati uliohitajiwa. (Mathayo 25:1-12) “Habari njema hizi za ufalme” zitakapokuwa zimekwisha kuhubiriwa “katika dunia yote inayokaliwa na watu kwa ushuhuda” na “mwisho” uwe karibu kutokea, watakuwa wamekwisha kupoteza nafasi yao ya kushiriki pendeleo hilo la utumishi ambalo halitarudiwa tena.—Mathayo 24:14, NW.
2, 3. (a) Yesu alimalizia mfano wa wale wanawali kumi kwa kutoa onyo gani? (b) Ni kwa sababu gani onyo hilo lingali linafaa wakati huu, na kwa hiyo jamii ya ‘wanawali wenye akili’ inahitaji kuendelea kuchukua nini?
2 Ndiyo sababu Yesu Kristo alimalizia mfano wake kwa onyo hili: “Endeleeni kulinda, basi, kwa sababu hamjui wala siku hiyo wala saa hiyo.”—Mathayo 25:1-13, NW.
3 Maneno hayo ya Bwana-arusi Yesu Kristo ni ya wakati wake kabisa, hasa sasa, miaka 71 ikiwa imekwisha ya huu “umalizio wa mfumo wa mambo.” Hata katika wakati huu uliosonga sana mabaki ya jamii ya ‘wanawali wenye akili’ hawajui siku wala saa wakati “mlango” utakapofungwa kusiwe nafasi tena ya kukubaliwa kuingia katika Ufalme wa kimbingu pamoja na Bwana-arusi ambaye wameposwa naye. Daima wale wanaotaka kujithibitisha wenyewe kuwa wanawali wenye akili wana lazima ya kuendelea kuchukua mafuta ya kiroho. Kwa kufanya hivyo wanaruhusu nuru yao ing’ae kwa kueneza “habari njema hizi za ufalme” kwa ushuhuda kwa mataifa yote, kwa dunia yote mpaka “mwisho” uje.—Mathayo 24:14, NW; Marko 13:10; Ufunuo 14:6, 7.
“Kondoo” na “Mbuzi” Sasa Wanatenganishwa
4. Kulingana na masimulizi ya Mathayo, ni mfano gani wa mwisho ambao lazima utimizwe ukiwa sehemu ya “ishara” ya “kuwapo” Kwake?
4 Kabla ya kuja “mwisho” wa “umalizio wa mfumo wa mambo,” kazi nyingine ya kutenganisha watu ni lazima ifanywe na kuwa sehemu ya “ishara” inayoonyesha kwamba tumo katika “wakati wa mwisho.” (Danieli 12:4) Huo ni utimizo wa mfano wa Yesu wa kondoo na mbuzi, ambao kwa huo Mathayo anamalizia masimulizi yake ya unabii mkuu wa Kristo unaohusu “ishara” ya “kuwapo” Kwake kusikoonekana na ya “umalizio wa mfumo wa mambo.”
5. Kutenganishwa kwa watu kama kondoo na mbuzi kungefanywa wakati gani?
5 Angalia aliyotabiri Yesu juu ya hilo, kama ilivyoandikwa katika Mathayo 25:31-46. Alianza mfano huo kwa kusema: “Hapo atakapokuja Mwana wa Adamu katika utukufu wake, na malaika watakatifu wote pamoja naye, ndipo atakapoketi katika kiti cha utukufu wake; na mataifa yote watakusanyika mbele zake; naye atawabagua kama vile mchungaji abaguavyo kondoo na mbuzi; atawaweka kondoo mkono wake wa kuume, na mbuzi mkono wake wa kushoto.” Halafu inakuwaje? Yesu aliendelea hivi:
6. Mfalme-mchungaji anawaambia nini watu walio upande wake wa kulia?
6 “Kisha Mfalme atawaambia wale walioko mkono wake wa kuume, Njoni, mliobarikiwa na Baba yangu, urithini ufalme mliowekewa tayari tangu kuumbwa kwa ulimwengu; kwa maana nalikuwa na njaa, mkanipa chakula; nalikuwa na kiu, mkaninywesha; nalikuwa mgeni, mkanikaribisha; nalikuwa uchi, mkanivika; nalikuwa mgonjwa, mkaja kunitazama; nalikuwa kifungoni, mkanijia.”
7. Watu wenye mfano wa kondoo walio waadilifu watauliza nini, naye Mfalme atajibuje?
7 “Ndipo wenye haki watakapomjibu, wakisema, Bwana, ni lini tulipokuona una njaa, tukakulisha, au una kiu tukakunywesha? Tena ni lini tulipokuona u mgeni, tukakukaribisha, au u uchi, tukakuvika? ni lini tena tulipokuona u mgonjwa, au kifungoni, tukakujia? Na Mfalme atajibu, akiwaambia, Amin, nawaambia, kadiri mlivyomtendea mmojawapo wa hao ndugu zangu walio wadogo, mlinitendea mimi.”
8. (a) Wale watu wenye mfano wa mbuzi hawakuchukua hatua mara moja wafanye nini? (b) Kwa hiyo Mfalme atawapeleka mbuzi wapi tofauti na wenye mfano wa kondoo walio waadilifu?
8 “Mbuzi” hawachukui hatua mara moja juu ya “ishara.” Hawafanyi mambo yanayofanywa na jamii ya “kondoo.” Kwa hiyo tunasoma: “Kisha atawaambia na wale walioko mkono wake wa kushoto, Ondokeni kwangu, mliolaaniwa, mwende katika moto wa milele, aliowekewa tayari Ibilisi na malaika zake; kwa maana nalikuwa na njaa, msinipe chakula; nalikuwa na kiu, msininyweshe; nalikuwa mgeni, msinikaribishe; nalikuwa uchi, msinivike; nalikuwa mgonjwa, na kifungoni, msije kunitazama. Ndipo hao pia watajibu, wakisema, Bwana, ni lini tulipokuona wewe una njaa, au una kiu, au u mgeni, au u uchi, au u mgonjwa, au u kifungoni, tusikuhudumie? Naye atawajibu, akisema, Amin, nawaambia, Kadiri msivyomtendea mmojawapo wa hao walio wadogo, hamkunitendea mimi. Na hao watakwenda zao kuingia katika adhabu ya milele; bali wenye haki watakwenda katika uzima wa milele.”
9. Ni kwa kuwa umefanya nini wakati wa utimizo wa kisasa wa mfano wa Yesu wa “kondoo” na “mbuzi” unaweza kuwa na furaha?
9 Inaelekea wewe unashiriki katika utimizo wa mfano huo wa kiunabii. Je! umeyaona mambo mazuri aliyotaja Yesu? Je! wewe umefanyia “ndugu” zake mambo hayo? Unaweza kuwa mwenye furaha ikiwa umetenda kama “kondoo” kuwaelekea!
10. Yesu alitofautishaje “ndugu” zake na wale wanaofananishwa na “kondoo” na “mbuzi,” na kuna msingi gani wa jambo hilo katika Biblia?
10 Yesu alitaja tofauti kati ya “ndugu” zake wa kiroho na wale wanaojithibitisha kuwa kama kondoo au mbuzi. Katika wakati wa utimizo wa mfano huo, “ndugu” zake ni wale ambao wamemfuata kwa kujitoa kwa Mungu bila matakwa yo yote. Kama Yesu, wametoa ushuhuda wa peupe wa jambo hilo kwa kubatizwa katika maji. Zaidi ya hayo, Yehova, Baba ya Mfalme Yesu Kristo, amekuwa Baba yao wa kimbingu kwa kuwazaa kwa roho takatifu Yake na kwa njia hiyo kuwafanya “ndugu” za kiroho wa Mwanaye. Jambo hilo linawaweka katika hali ya kuwa na mahali katika Ufalme wa kimbingu pamoja na Ndugu Mkubwa wao, Yesu Kristo, ‘Mfalme wa wafalme, na Bwana wa mabwana.’ (Ufunuo 19:16) Kwa kukamatana na hilo iliandikwa hivi kumhusu: “Maana yeye atakasaye na hao wanaotakasa wote pia watoka kwa mmoja. Kwa ajili hii haoni haya kuwaita ndugu zake; akisema, Nitalihubiri jina lako kwa ndugu zangu; katikati ya [kundi] nitakuimbia sifa.” (Waebrania 2:11, 12) Hapa Zaburi 22:22 ni andiko linalotumiwa kumhusu Mwana wa Mungu aliyetukuzwa, Yesu Kristo.
11. Je! kuna wengi wa “ndugu” za kiroho wa Yesu duniani sasa, nao wanafanyiza jamii au “kundi” gani?
11 Kungali duniani mabaki ya “ndugu” hao wa Mfalme Yesu Kristo anayetawala. Wakiwa jamii, au ‘kundi,’ wanafanyiza “mtumwa mwaminifu mwenye akili” ambaye Yesu alitabiri katika unabii wake juu ya “umalizio wa mfumo wa mambo.” Alisema: “Ni nani basi yule mtumwa mwaminifu mwenye akili, ambaye bwana wake alimweka juu ya nyumba yake, awape watu chakula kwa wakati wake? Heri mtumwa yule, ambaye bwana wake ajapo atamkuta akifanya hivyo. Amin, nawaambieni, atamweka juu ya vitu vyake vyote.”—Mathayo 24:45-47.
12. (a) Tangu mwaka wa 1919 jamii ya “mtumwa” imekuwa yenye kutokeza katika kufanya nini? (b) “Mtumwa” huyo ‘amewekwa’ juu ya “vitu” gani? (c) “Mtumwa” ambaye sasa anatenda ni sehemu ya nini?
12 Mambo ya uhakika ya kihistoria yanajibu swali la Yesu juu ya ni nani “mtumwa” huyo. ‘Kundi’ linalotumikia kama “mtumwa” limefanyizwa kwa “ndugu” zake aliopewa na Mungu ambao wangali duniani. Ndilo lile lile linalofananishwa na jamii ya ‘wanawali wenye akili.’ Tangu mwaka wa 1919 “mtumwa” huyo amekuwa mwenye kutokeza katika kupakua chakula kipya-kipya cha kiroho kutoka Biblia kwa “watu” wa nyumba ya Bwana, akifanya hivyo kwa wakati “wake.” Kwa hiyo, Bwana asiyeonekana ameweka jamii hiyo ya “mtumwa” yenye kutegemeka “juu ya vitu vyake vyote” vya jinsi ya kiroho. Hasa ndivyo ilivyo kwa kukamatana na kuhubiri “habari njema hizi za ufalme” katika dunia yote, ambayo anaitawala. Mpaka sasa ushuhuda huo wa Ufalme umeongezeka! “Mtumwa mwaminifu mwenye akili” akiwa anatenda ni sehemu maarufu ya “ishara” inayotuonyesha ni saa ngapi.
13. “Mataifa” yote yamekusanywa mbele ya Mfalme huyo tangu wakati gani, na “mtumwa” alianza kukusanya “kondoo” kwenye mkono Wake wa kulia wakati gani?
13 “Kondoo” waadilifu wamefanya mambo mema kwa jamii ya “mtumwa” huyo. Kondoo na mbuzi wa mfano ni watu wa mataifa yote ambao ushuhuda wa Ufalme unatolewa kwao sasa. Kwa hiyo, wakiwa wanawakilishwa na kondoo na mbuzi, “mataifa yote” yamekusanywa mbele ya Mfalme aliyeketi kwenye kiti cha ufalme chake cha kimbingu tangu mwisho wa Nyakati za Mataifa mwaka wa 1914. Kwa kukamatana na kukusanywa huko kulikotabiriwa, mwaka wa 1935 unastahili kuangaliwa. Sosaiti yetu, inayotumiwa na jamii hiyo ya “mtumwa,” wakati huo ilikuwa na afisi za tawi 49 hivi duniani pote. Katika mwaka uo huo fikira za “mtumwa” huyo zilielekezwa hasa kwa wenye mfano wa kondoo wa kidunia, kukiwa na kusudi la kuwakusanya upande wa kulia wa Mfalme Yesu Kristo mwenye kutawala. Kwa hiyo, hao wanaotoka katika mataifa yote walikuja katika ushirikiano wa karibu zaidi na jamii ya “mtumwa.”
14. Kwa sababu ya Yohana 10:16, wenye mfano wa kondoo walio waadilifu walionwa kwa maoni gani mapya, na sasa wanatumikiwa na afisi za tawi za Sosaiti yetu ngapi?
14 Watu hao waadilifu, wenye mfano wa kondoo waliacha kutajwa kijumla tu kuwa “watu wa nia njema” (Luka 2:14, Douay Version) Hawakupaswa tena kuonwa kuwa jamii isiyo kamili, isiyofanywa tengenezo ya watu wenye kumwogopa Mungu katika mataifa yote—kondoo waliopotea. Yesu alisema angekusanya “kondoo wengine” na kuwafanya wawe “kundi moja” pamoja na mabaki ya jamii ya “mtumwa.” (Yohana 10:1) Kukusanywa kwa “kondoo wengine” hao tangu wakati huo na kuendelea ni sehemu yenye kutokeza ya “ishara” inayotia alama “umalizio wa mfumo wa mambo.” Na ili kuwatumikia Sosaiti yetu sasa ina afisi za tawi 95.
Hatua ya Wakati Unaofaa juu ya “Ishara” Yathawabishwa
15. Ili ‘waurithi ufalme,’ “kondoo” ni lazima watimize matakwa gani?
15 Kulingana na mfano wa Yesu, “kondoo” waadilifu wanapaswa kutimiza matakwa fulani wakati wa “umalizio wa mfumo wa mambo.” Ni lazima watambue na kukubali “ndugu” za kiroho wa Kristo wanaofanyiza jamii ya “mtumwa mwaminifu mwenye akili.” Ni lazima pia “kondoo” wafanyie mema jamii ya “mtumwa,” hata kuwatembelea wanapofungiwa gerezani kwa dhuluma. Ni lazima “kondoo” wafanye hilo ili wafurahie baraka za Baba ya kimbingu na ili waalikwe na Mfalme Yesu Kristo ‘waurithi ufalme waliowekewa tayari tangu kuumbwa [“kuwekwa msingi wa, NW] ulimwengu.’—Mathayo 25:34.
16. Kwa maneno “urithini ufalme,” Mfalme anawaalika “kondoo” waingie katika nini, na kuokoka “vita” gani?
16 Kwa kuwa “kondoo” hao si “ndugu” za kiroho wa Mfalme, yeye hawaaliki waketi juu ya viti vya kifalme vya mbinguni na kutawala pamoja naye kwa ile miaka elfu ya pekee ya utawala wake. Kwa maneno yake “urithini ufalme,” anawaalika waingie katika kipindi cha Ufalme baada ya kuharibu falme zote zisizomwogopa Mungu za ulimwengu huu wakati wa “vita ya siku ile kuu ya Mungu Mwenyezi” katika Har–Magedoni. (Ufunuo 16:13-16) Wengi wa wenye mfano wa kondoo wanaoishi sasa wataokoka vita hiyo ya vita na kuingia katika Utawala wa Miaka Elfu wa Kristo bila kufa.
17. Mfalme anasemaje na “kondoo,” naye alipataje kitu cha kuwapa warithi?
17 Kwa hiyo Mfalme Yesu Kristo anazungumza na “kondoo” hao kama kwamba anazungumza na watoto wake ambao wakati wao umefika wa kupata urithi kutoka kwake. Kwa kifo chake akiwa mwanadamu mkamilifu ili atoe dhabihu ya ukombozi kwa wanadamu wote, aliondoa mataraja yote ya kibinafsi ya yeye kufurahia Paradiso ya kidunia. (Luka 23:39-43) Katika habari hiyo Yesu, “Adamu wa mwisho,” anatofautiana na ‘Adamu wa kwanza’ aliyefanya dhambi na kupotezeshea wazao wake wote Paradiso ya kidunia. Kwa hiyo Yesu Kristo aliyefufuliwa, anayekuwa “Baba wa milele” kwa ulimwengu wote wa wanadamu waliokombolewa, ana jambo la kuwapa kuwa urithi watu hao wenye mfano wa kondoo duniani. (1 Wakorintho 15:45; Isaya 9:6, 7) Jamaa ya kibinadamu ilianzishwa kwa ‘Adamu wa kwanza,’ pamoja na mataraja yake yote na nafasi zote za Paradiso. Lakini Paradiso hiyo iliyopotezwa itarudishwa kupitia Ufalme wa Mungu mikononi mwa “Adamu wa mwisho,” Yesu Kristo.
18. Makao ya Ufalme ‘yalitayarishwa kwa ajili ya kondoo tangu kuwekwa msingi wa ulimwengu’ kwa, maana gani?
18 Adamu na Hawa hawakuanza kuwa na watoto mpaka baada ya kufukuzwa nje ya Paradiso hiyo ya kwanza. Mwana wao wa pili, Habili mwadilifu, aliuawa na mwana wao wa kwanza, Kaini. Kwa hiyo mwana wao Sethi alionwa kuwa mwenye kuchukua mahali pa Habili. Kwa watoto hao kuzaliwa, ulimwengu wa wanadamu ulianzishwa. Lakini kabla ya hilo, wakati wazazi wa ulimwengu wa wanadamu walipofukuzwa nje ya Paradiso, Yehova Mungu alitoa ahadi ya rehema kuhusu “uzao” ambao ungeponda kichwa cha Nyoka wa mfano, Shetani Ibilisi. “Uzao” huo ungekuwa Uzao wa kifalme, na jambo hilo lilihusu Ufalme, kulingana na kusudi la Mungu na maoni yake ya kimbele. (Mwanzo 3:15) Basi, Shetani aliye Nyoka na uzao wake wakiisha kuondolewa, waliokombolewa kati ya wanadamu wataingia katika makao ya kidunia ya Ufalme, chini ya serikali ya kimbingu ya Uzao wenye kushinda unaomponda Shetani na uzao wake. Kwa njia hiyo “ufalme” ambao wenye mfano wa kondoo ‘wanarithi’ kutoka kwa Baba wa Milele wao, Yesu Kristo ni makao ya Kifalme ‘waliyotayarishiwa tangu kuumbwa [“kuwekwa msingi wa,” NW] ulimwengu.’
19. Mfumo wa mambo wa baada ya Har–Magedoni utakuwa na mwanzo wa namna gani duniani?
19 Kwa kuwa mbuzi wa mfano wataangamizwa kwenye Har–Magedoni, “kondoo” watakaookoka watakuwa mwanzo wa uadilifu wa mfumo wa mambo wa baada ya Har–Magedoni kwenye dunia-Paradiso. Kuhusu hilo, Yesu alisema: “Hao [wenye mfano wa mbuzi] watakwenda zao kuingia katika adhabu ya milele; bali wenye haki katika uzima wa milele.”—Mathayo 25:46.
20. Tunaweza kuepukaje kufasiri vibaya sehemu za “ishara” hiyo?
20 Wakati wa huu “umalizio wa mfumo wa mambo” tangu mwisho wa Nyakati za Mataifa mwaka wa 1914 “kondoo” na “mbuzi” wanatofautiana katika njia wanayofasiri “ishara” ya “kuwapo” kwa Yesu. Kwa kuwa bila shaka tumo katika wakati wa hukumu, swali hili ni la kuhangaikiwa sana: “Ishara” hiyo inatuonyesha nini? Tukiachiwa , tunaweza kufasiri vibaya sehemu za “ishara” hiyo. Kwa hiyo tunafanya vema kuuliza hivi: Yesu Kristo anasema “ishara” hiyo inapasa kutuonyesha nini? Kulingana na yeye, inapasa kuonyesha kwamba mfumo wa mambo uliopo utakwisha karibuni katika “dhiki kubwa” yenye uharibifu mkubwa zaidi ya Gharika ya duniani pote ya siku za Noa.—Mathayo 24:21.
21. (a) Ingawa “dhiki kubwa” iko mbele, ni kwa sababu gani tunapaswa kufurahi? (b) Kuna nafasi na uwezekano gani kwa jamii ya “kondoo” ya leo?
21 Hata hivyo, furahi, kwa maana “ishara” hiyo inaonyesha pia kwamba Utawala wa Mileani wa Yesu Kristo umekaribia, uko karibu kuanza baada ya kuharibiwa kwa mfumo wa mambo wa Shetani wa duniani. (Luka 21:28) Kwa hiyo, chini ya ulinzi wa kimungu una nafasi bora ajabu ya kuokoka “dhiki kubwa” hiyo uingie moja kwa moja katika mfumo mpya wa mambo, ambamo uadilifu utakaa milele. Kweli kweli, mbele yako kumewekwa uwezekano wa kutokufa kamwe bali wa kuishi bila kikomo na kwa baraka katika dunia-paradiso chini ya enzi kuu ya ulimwengu wote ya Yehova Mungu!
22. (a) Tukichukua hatua juu ya “ishara” hiyo mara moja na kwa njia iliyo sawasawa, tutafanya nini? (b) Kwa kukamatana na “ishara” hiyo, Yesu Kristo atatetewaje?
22 Tuwe tu “ndugu” za kiroho wa Kristo au “kondoo” waadilifu, basi, na tuchukue hatua juu ya “ishara” hiyo mara moja na kwa njia iliyo sawasawa. Na tushiriki zaidi katika utimizo wa sehemu yayo iliyo maarufu: “Habari njema hizi za ufalme zitahubiriwa katika dunia yote inayokaliwa na watu kwa ushuhuda kwa mataifa yote.” Halafu hatutakuwa na kitu cha kuogopa wakati “mwisho” ujapo. Badala yake, furaha yetu itafurika kwa wingi! Halafu, pia, Yesu Kristo atatetewa kuwa mtabiri mwenye kutegemeka wa ile “ishara” yenye sehemu nyingi “ya umalizio wa mfumo wa mambo.”—Mathayo 24:3–25:46.—Kutoka W2/l/85.
Je! Wewe Unaweza Kujibu?
◻ Watu wangetenganishwa kama kondoo na mbuzi wakati gani?
◻ Unaweza kuwa mwenye furaha kwa ajili ya kufanya nini wakati huu wa utimizo wa mfano wa Yesu wa kondoo na mbuzi?
◻ Ni nani wanaofanyiza “ndugu” za Mfalme na “mtumwa mwaminifu mwenye akili”?
◻ Ili ‘kuurithi ufalme,’ ni matakwa gani ambayo wenye mfano wa kondoo ni lazima watimize?
◻ Tutafanya nini ikiwa tunachukua hatua mara moja na kwa njia iliyo sawasawa juu ya “ishara” ya “kuwapo” kwa Yesu?
[Blabu katika ukurasa wa 23]
Chukua hatua mara moja juu ya “ishara” ya “kuwapo” kwa Yesu. Kufanya hivyo kwaweza kumaanisha uzima wa milele katika Paradiso.
[Picha katika ukurasa wa 20]
Kama mchungaji anavyotenganisha kondoo na mbuzi, ndivyo Yesu Kristo anavyotenganisha watu leo. Je! wewe ni mtu mwenye mfano wa kondoo?