Watchtower MAKTABA KWENYE MTANDAO
Watchtower
MAKTABA KWENYE MTANDAO
Kiswahili
  • BIBLIA
  • MACHAPISHO
  • MIKUTANO
  • kc sura 17 kur. 162-173
  • Mfalme Apigana Penye Har-Magedoni

Hakuna video yoyote kwa sasa.

Samahani, haikuwezekana kupakia video.

  • Mfalme Apigana Penye Har-Magedoni
  • “Ufalme Wako Uje”
  • Vichwa vidogo
  • Habari Zinazolingana
  • HATUA ZA KWANZA KUELEKEA PIGANO LILE
  • KUFANYA ULE UKAHABA
  • “OLE” KWA BABULONI
  • YULE MFALME ATENDA!
  • Amani, Usalama, na Ile ‘Sanamu ya Mnyama’
    Mnara wa Mlinzi Unaotangaza Ufalme wa Yehova—1985
  • Kufisha Babuloni Mkubwa
    Ufunuo—Upeo Wao Mtukufu U Karibu!
  • Kuhukumu Kahaba Mwenye Sifa Mbaya
    Ufunuo—Upeo Wao Mtukufu U Karibu!
  • Umoja wa Mataifa—Rafiki au Adui ya Dini?
    Mnara wa Mlinzi Unaotangaza Ufalme wa Yehova—1975
Pata Habari Zaidi
“Ufalme Wako Uje”
kc sura 17 kur. 162-173

Sura ya 17

Mfalme Apigana Penye Har-Magedoni

1, 2. Watu wa ulimwengu wamekuwa wakisema nini juu ya Har Magedoni?

WAKATI Vita ya Ulimwengu ya Pili ilipokaribia kumalizika, Douglas MacArthur, Jemadari wa U.S. alisema: “Tangu mwanzo wa wakati, wanadamu wametafuta amani. . . . Miungano ya kijeshi, miungano ya kupimia mataifa uwezo unaolingana, mashirika ya mataifa, yote nayo yalishindwa, ikawa suluhisho pekee ni kupigana vita vikali sana. Ule uharibifu mkubwa wa vita sasa unazuia hata njia hiyo ya kusuluhisha mambo kwa kupigana. Tumekwisha kuwa na nafasi yetu ya mwisho. Ikiwa hatutavumbua mfumo fulani ulio mkubwa na wenye kufaa zaidi, Har-Magedoni yetu itakuwa mlangoni petu.”

2 Kama miaka 35 baadaye, mataifa yalitumiaje hiyo ‘nafasi ya mwisho’? Gazeti Times la London, Uingereza, lilisema hivi chini ya kichwa “Wajeremani wa Magharibi Waogopa Har-Magedoni”: “Woga wa vita umerudi kusumbua Ujeremani Magharibi wakati hali ya kimataifa inapoonekana kutozuilika kabisa.” Na katika makala yenye kusema “Ulimwengu Wajikwaa Katika Giza,” mhariri wa gazeti Herald la Miami, U.S.A., aliwauliza wasomaji wake kama walikuwa wamefahamu “kwamba Har-Magedoni si fumbo to la maneno unalosoma katika Biblia, ni jambo la kweli,” kisha akaongeza: “Hata mtu asiyefikiri sana anaweza kujumlisha matukio yote yenye uharibifu mkubwa ya miaka michache iliyopita na kufahamu kwamba ulimwengu unaingia kipindi chenye maana kubwa. . . . Kitabadili milele maisha ya wanadamu.”

3, 4. Maoni ya Biblia juu ya Har-Magedoni ni tofauti namna gani?

3 Kweli, wanadamu wamo katika kipindi cha mabadiliko makubwa. Lakini je, sasa sisi tunaikabili Har-Magedoni? Har-Magedoni maana yake nini?

4 Inapendeza kujua kwamba Har-Magedoni ni tofauti na vile watu wanafikiria. Maana Biblia inasimulia vita katika Har-Magedoni kuwa “vita ya siku ile kuu ya Mungu Mwenyezi,” si vita yenye uharibifu mkubwa kati ya mataifa ya kidunia au miungano ya mataifa. Ni vita ya Mungu dhidi ya “wafalme wa ulimwengu wote”—maana yake watawala wale wanaokataa kunyenyekea wakati ufalme wa Mungu ‘unapokuja’ kutimizisha mapenzi yake duniani. (Zaburi 2:6-12; Danieli 2:44) Ni tendo kubwa la Mungu la kuharibu mataifa yenye uovu na wanadamu waovu, kutayarisha njia ya utawala wenye amani wa Masihi wa miaka 1,000.—Ufunuo 16:14, 16; Zaburi 46:8, 9; 145:20; Yoeli 3:9-17; Nahumu 1:7-9.

HATUA ZA KWANZA KUELEKEA PIGANO LILE

5. Tunaweza kutambuaje yule “mzinzi mkuu” wa Ufunuo 17?

5 Ufunuo, sura za 16 kufika 18, unatuambia mengi juu ya matukio duniani yakitangulia vita ile ya Har-Magedoni. Kulingana na unabii, wito huu unatolewa: “Njoo, nami nitakuonyesha adhabu aliyopewa yule mzinzi mkuu, mji ule mkuu uliojengwa juu ya maji mengi.” “Mzinzi mkuu” (kahaba mkuu) huyo baadaye tunajulishwa kuwa ni “Babuloni mkuu, mama wa wazinzi na wa mambo yote ya kuchukiza sana duniani.” Kama vile Babuloni wa kale uliokaa katikati ya Mto Frati uligeuka ukawa “mama” wa mfumo wa kifumbo wa dini iliyoenea katika dunia yote kutoka Babuloni, ndivyo leo “Babuloni mkuu” ulivyo milki ya ulimwengu ya dini ya uongo inayowatawala kiroho “mataifa, watu wa kila rangi na lugha,” kwa hasara yao. (Ufunuo 17:1, 5, 15, HNWW) Inatia ndani maelfu ya madhehebu ya kidini, makubwa na madogo, “ya Kikristo” na yasiyo ya Kikristo, yasiyomkubali wala kumtumikia Mungu wa kweli, Yehova.

6. Ufunuo 16 unataja tukio gani linalokumbusha juu ya Babuloni wa kale?

6 Tunapewa utangulizi wa vita ile katika Har-Magedoni kwa kuonyeshwa malaika mmoja akimwaga bakuli la “ghadhabu ya Mungu.” Wapi? “Juu ya mto mkubwa uitwao Eufrate. Maji yake yakakauka, na hivyo njia ilitengenezwa kwa ajili ya wafalme wa mashariki.” (Ufunuo 16:1, 12, HNWW) Zaidi ya miaka 600 kabla ya mtume Yohana kuandika unabii huo, Wafalme Dario wa Umedi na Koreshi wa Uajemi walishambulia nchi ya Babuloni kutoka mashariki. Wakati wa giza la usiku, Koreshi aligeuza maji ya Mto Eufrate yapite katika mifereji mingine, na yalipopungua, akatuma jeshi lake liingie katika mji kupitia bonde la mto. Katika usiku mmoja, watawala wa Kibabuloni na wakuu walipokuwa wakimtukana Yehova katika karamu ya ulevi wenye makelele mengi, mji huo mkuu ukaangushwa.—Danieli 5:1-4, 30, 31.

7. Sasa tunaona mlingano gani wa siku hizi?

7 Je! tunaona mlingano wa kisasa wa hilo? Ndiyo! Umewadia wakati wa Mungu kutekeleza hukumu juu ya “Babuloni mkuu,” na hasa matengenezo ya Jumuiya ya Wakristo yaliyo kama “binti” yake. Ukafiri na hatia ya damu ya Jumuiya ya Wakristo sasa umekuwa mwingi mno! (Ufunuo 18:24; Yeremia 51:12, 13) Nyakati za majuzi yale “maji,” au “mataifa,” yaliyosaidia zamani dini yake yamekuwa yakipungua. Msaada ambao dini inapewa umekuwa ukikauka, na watu wengi wamekuwa wakifuata mafundisho ya Darwin, Marksi, Lenin na Mao. Pia, kama ilivyotabiriwa kuhusu zile “siku za mwisho,” watu wamekuwa “wapendao anasa kuliko kumpenda Mungu.”—2 Timotheo 3:1, 4.

8. (a) Ni wito gani ambao watu wenye maelekeo ya uadilifu wametii? (b) Ile hali ya dini ya uongo inatofautianaje sasa na ile ya dini ya kweli?

8 Lenye kusaidia kupungua kwa yale “maji” limekuwa ni tendo la watu wenye maelekeo ya uadilifu ambao wametii wito huu wa mbingu kuhusu “Babuloni mkuu”:

“Watu wangu, ondokeni kwake! ili msishirikiane naye katika dhambi yake, msije mkaipata adhabu yake.” (Ufunuo 18:4, “HNWW”)

Ile milki ya ulimwengu ya dini ya uongo, na hasa Jumuiya ya Wakristo, inaomboleza kwa sababu ya kufungwa kwa makanisa, kwa sababu ya viti vilivyo vitupu kanisani na idadi yenye kupungua ya makasisi na watawa wa kike. Walakini, wale wanaojipanga sasa upande wa yule Dario Mkubwa Zaidi, yaani, Yehova Mungu, na Koreshi Mkubwa Zaidi, Kristo Yesu, wanaingia katika ufanisi mwingi sana wa kiroho. Je! wewe ni mmoja wao?

KUFANYA ULE UKAHABA

9, 10. (a) Ni “mnyama” gani mwenye kuogopesha anayetokea katika hizi “siku za mwisho”? (b) Katika hotuba ya watu wote mwaka wa 1942, alitambulishwaje na mwendo wake ulisimuliwaje?

9 “Babuloni mkuu,” ajapodai kuwa wa Mungu, nyakati zote amekuwa na uhusiano wa kisiasa, na katika maana hiyo “wafalme wa dunia wamefanya uzinzi pamoja naye.” Lakini sasa, katika “siku za mwisho,” anayo nafasi kubwa! Nafasi gani? A, anatokea “mnyama mwekundu.” “Mnyama” huyo anaelekea kuwa nini? Bila shaka anahusiana na mataifa ya kisiasa ya dunia, maana hao wanatajwa mara nyingi sana katika Biblia kwa kufananishwa na ‘wanyama.’ (Ufunuo 13:1-4, 11-15; Danieli 7:3-8, 17-25; 8:5-8, 20-22) Lakini hapa tuna mwungano wa “mnyama,” maana mnyama huyo mwenye kuogopesha ana “vichwa saba na pembe kumi.”—Ufunuo 17:3, HNWW.

10 Ni “mnyama” gani mwenye sehemu nyingi ambaye ametokea katika hizi “siku za mwisho,” na amefanya mambo gani ulimwenguni? Katika kusanyiko la kimataifa la Mashahidi wa Yehova mwaka wa 1942, hotuba ya watu wote yenye kichwa “Amani—Je! Yaweza Kudumu?” ilivuta fikira kwenye unabii ulio katika Ufunuo 17:7, 8. Msemaji, N. H. Knorr msimamizi wa Sosaiti, alitambulisha ‘yule mnyama ambaye alikuwako’ kuwa ni Ushirika wa Mataifa—uliotokezwa mwaka wa 1920. Lakini sasa, katika huo mwaka wa 1942 wa wakati wa vita, alisema hivi: “Kwa kweli Ushirika huo uko katika hali ya kuacha kuishi, na unahitaji kufufuliwa ikiwa utaishi tena wakati wo wote. Umeingia katika shimo refu la kutotenda na la kutofaa kitu. ‘Hauko.’ ” Msimamizi Knorr akaendelea kuonyesha kwamba “yule mnyama [ambaye] alikuwako, naye hayuko, . . . yu tayari kupanda kutoka kuzimu na kwenda kwenye uharibifu.” Kwa kupatana na unabii huo wa Biblia, kweli “mnyama” huyo alifufuliwa mwaka wa 1945 akiwa Umoja wa Mataifa.

11. (a) Sababu gani “mnyama” huyo anasimuliwa kuwa “mwenye kujaa majina ya makufuru”? (b) “Mnyama” huyo anangojea hukumu gani?

11 “Mnyama” huyo wa kimataifa, aliyetokezwa ili kudumisha “amani na usalama” kati ya mataifa, kwa kweli ni “mwenye kujaa majina ya makufuru,” maana anadai ati anaweza kufanya yale ambayo ni ufalme wa Mungu pekee kupitia Kristo Yesu waweza kutimiza. (Ufunuo 17:3) Mtume Paulo alitabiri juu ya pindi wale watawala wenye kujivuna wa ulimwengu wa Shetani wangekuwa wakijisifu kuwa wafanya amani. Alisema hivi:

“Siku ya Yehova inakuja sawasawa kabisa kama vile mwivi usiku. Wakati wo wote wasemapo: ‘Amani na Usalama!’ ndipo uharibifu wa ghafula utakuwa juu yao papo hapo kama yale maumivu makali ya taabu juu ya mwanamke mjamzito; nao hawataponyoka kasha.” (1 Wathesalonike 5:2, 3, “NW”)

Kulingana na Neno la Mungu, yule ‘mnyama wa amani na usalama’ atapatwa na hukumu ya haraka, yenye kukata maneno, itakayotekelezwa na Yehova!

“OLE” KWA BABULONI

12. Ni maelezo gani juu ya “kahaba” yule yaliyomshangaza Yohana?

12 Ijapokuwa Mungu anachukia yule mnyama, yaani, Umoja wa Mataifa wenye kujaa makufuru, “Babuloni mkuu” anatafuta kuwa na uhusiano wa kimahaba pamoja naye. Ndiyo, anafananishwa amekaa kama malkia juu ya yule “mnyama”: “Mwanamke huyo alikuwa amevaa vazi la rangi ya zambarau na nyekundu; alikuwa amejipamba kwa dhahabu, mawe ya thamani na lulu. Mkononi mwake alishika kikombe cha dhahabu ambacho kilikuwa kimejaa machukizo na mambo machafu yanayoonyesha uzinzi wake.” Si ajabu kubwa kwamba Yohana aliandika juu ya hali hiyo hivi: “Nilipomwona nilishangaa mno.”—Ufunuo 17:4, 6, HNWW.

13, 14. (a) Ni mwisho gani wenye ole unaongojea dini ya uongo? (b) Utakujaje? (c) Nani wataomboleza Babuloni Mkuu, lakini kwa nini wakiwa mbali?

13 Uhusiano ulio kati ya milki ya ulimwengu ya Kibabuloni ya dini ya uongo na yule ‘mnyama wa amani na usalama,’ yaani, Umoja wa Mataifa, unageuka kuwa wenye kuleta msiba. Ingawa huenda “Babuloni” aliye mfano wa kahaba akadhani kwamba anakaa salama pamoja na shirika hilo la ulimwengu, Neno la Mungu linamtabiria jambo jinginelo hivi:

“Pembe zile kumi ulizoziona na yule mnyama watamchukia huyo mzinzi. Watachukua kila kitu alicho nacho na kumwacha uchi; watakula nyama yake na kumteketeza kwa moto.” (Ufunuo 17:16, “HNWW”)

Ni mwisho wenye ole kweli kweli kwa ile milki ya ulimwengu ya dini ya uongo!

14 Kuharibiwa kwa “Babuloni mkuu” kutakuwa kwa haraka.

“Katika siku moja mapigo yake yatakuja, kifo na kuomboleza na njaa kuu, nave atachomwa kabisa kabisa kwa moto, kwa sababu Yehova Mungu, aliyemhukumu, ni mwenye nguvu.” (Ufunuo 18:8, “NW”) Lakini watakuwako wale watakaomwomboleza. Hao hawatakuwa zile “pembe kumi” za kivita zitakazomgeuka kwa hila, bali ni wengine kati ya watawala wa kisiasa waliokuwa wakisuhubiana kirafiki na makasisi kwa kusudi la kujionyesha tu, na kwa kusudi la kuficha mazoea yao ya udanganyifu. Wote hao watamwomboleza wakiwa mbali, wasije wakashiriki balaa lake, wakisema:

“Ole! Ole kwako Babuloni, mji maarufu na wenye nguvu! Kwa muda wa saa moja tu adhabu yako imekupata.”—Ufunuo 18:9, 10, “HNWW.”

15. Nani wengineo wanaitikiana. na kwa nini?

15 Pia watakuwako watu wenye faida kubwa ya biashara, wahalifu na wengine wafanya biashara za magendo, ambao wametumia uhusiano wao wa kidini kuficha matendo yao maovu kwa “utakatifu” wa kinje-nje na kutuliza dhamiri zao zenye hatia. Hao pia, wataitikiana, wakisema:

“Ole! Ole . . . Kwa saa moja tu utajiri wako umetoweka!” (Ufunuo 18:11-19, “HNWW”)

Yale makathedro (makanisa makubwa-makubwa), mashamba mengi-mengi na utajiri mwingi-mwingi, yale mapesa mengi mno katika benki na vitegauchumi vya kibiashara vya ile dini ya ulimwengu—vyote hivyo vitakuwa vimeharibiwa.

16. Ni vikundi gani vitatu vinavyoelekea kwenye hukumu ya kuharibiwa?

16 Dini ya ulimwengu yenye unafiki, biashara yenye pupa, siasa zenye ufisadi—matawi yote matatu ya tengenezo la Shetani duniani yanaelekea kwenye hukumu ya kuharibiwa na Yehova. Dini ya uongo itakapoharibiwa, kutafuata nini?

YULE MFALME ATENDA!

17, 18. (a) Ni nini kinachofuata kuharibiwa kwa “Babuloni mkuu,” na kwa nini? (b) Mwishowe, nani anayeshinda? (c) Nani watahifadhiwa hai? (d) Unawezaje kuwa mmoja wa hao?

17 Mamlaka hizo za kisiasa zenye kutaka mapinduzi, zinazoharibu dini ya ulimwengu, hazina macho ya ufahamu wa kiroho. Haziukubali ule ufalme wa Kimasihi, uliosimamishwa mwaka wa 1914. Badala yake, zinapinga kwa nguvu wale wanaotangaza ufalme huo, wanaoonyesha wazi kutokuwamo kwao kwa Kikristo katika siasa na vita vya za kilimwengu.—Ufunuo 12:17; Yohana 17:14, 16.

18 Baada ya kuharibu “Babuloni mkuu,” “pembe” hizo za kinyama zinaweza kutazamiwa kufanya ushambulizi wa mwisho juu ya mashahidi Wakristo wa Yehova, wafuasi wa yule Mwana-Kondoo, wanaoonekana kama hawana kinga hapa duniani. (Ezekieli 38:14-16; Yeremia 1:19) Je! adui hao watafaulu katika vita hiyo? Unabii unajibu hivi:

“Watapigana na Mwana-kondoo, lakini Mwana-kondoo pamoja na wale aliowaita na kuwachagua, ambao ni waaminifu, atawashinda kwa sababu yeye ni Bwana wa mabwana na Mfalme wa wafalme.” (Ufunuo 17:14, “HNWW”)

Ijapokuwa hawashiriki pigano hilo, wale mabaki wafuasi wa Yesu wapakwa-mafuta walio hapa duniani, pamoja na wenzi wao ambao pia wameitikia ule wito wa kufanya “utumishi mtakatifu,” watahifadhiwa hai. Je! wewe ni mmoja wa wale wanaosali hata sasa ufalme wa Mungu “uje” kwenye Har-Magedoni?—Warumi 12:1, 2, NW; linganisha 2 Mambo ya Nyakati 20:5, 6, 12-17.

19. (a) Huenda ukawa shahidi atakayejionea kwa macho yake mwenyewe na kuokoka nini? (b) Ni vitu gani vyenye thamani ambavyo wakati huo havitakuwa vyenye faida?

19 Ndiyo, huenda ukawa shahidi atakayejionea kwa macho yake mwenyewe, na kuwa mwokokaji wa ile vita yenye uharibifu mkubwa katika Har-Magedoni. Huenda ukawa mtazamaji wakati yule “Mfalme wa wafalme,” akifuatwa na yale majeshi ya kimalaika ya mbinguni, atakapopigana kwa kuitetea enzi kuu ya Yehova. Huenda wewe ukaliona wakati huo lile pigano la kukata maneno dhidi ya watu waovu, dhidi ya mataifa yenye kiburi na majeshi yao yenye nguvu na wale “wafanya-biashara” wenye utajiri mwingi wanaowaunga mkono! Silaha zao za kinyukilia zenye kugharimu mapesa mengi mno zitawakatisha tamaa katika vita hiyo! Wenye pupa ya kuchuma fedha kwa faida yao, ambao wamefanya biashara ya kuuza mafuta na vyakula wataona zile faida za magendo kuwa za bure-bure tu, wakati masoko ya bidhaa ulimwenguni yatakapoanguka na ile bei ya dhahabu ambayo ni njia ya kuokokea itakaposhuka kabisa. Kwa maana “hivi ndivyo Bwana Yehova Mwenye Enzi kuu amesema, ‘Msiba, msiba usio na kifani, tazama! unakuja. Katika barabara za mji watatupa fedha yao yenyewe, na kitu cha kuchukiza sana ndivyo dhahabu yao wenyewe itakavyokuwa. Wala fedha yao wala dhahabu yao haitaweza kuwakomboa katika siku ya ukali mwingi wa Yehova. . . . nao watalazimika kujua kwamba mimi ni Yehova.’ ”—Ezekieli 7:5, 19, 27, NW.

20. Unaweza kupata usalama wa kweli wapi?

20 Katika siku hiyo ya Har-Magedoni, huenda wewe ukapata usalama, si katika mali zo zote za kimwili, bali kwa kusimama imara upande wa Yehova na “Mfalme wa wafalme” wake. Itategemea utii wako wa maneno haya ya nabii:

“Tafuteni Yehova, ninyi nyote wapole wa dunia, ambao mmetenda uamuzi wa hukumu Wake mwenyewe. Tafuteni uadilifu, tafuteni upole. Inaelekea mnaweza kufichwa katika ile siku ya hasira ya Yehova.” (Sefania 2:3, “NW”; ona pia Isaya 26:20, 21; Danieli 12:1.)

Maana katika Har-Magedoni, yule Mfalme aketiye juu ya yule farasi mweupe wa mfano “huhukumu na kupigana kwa ajili ya haki.” Ingawa ‘anatawala mataifa kwa fimbo ya chuma,’ na kuwaharibu, atauokoa ule “mkutano mkubwa” wenye kuvalia kanzu nyeupe katika “dhiki ile iliyo kuu,” akiwachunga kwa upendo na ‘kuwaongoza kwenye chemchemi za maji yenye uhai.’ Na uwe mmoja wa hao!—Ufunuo 19:11-16, HNWW; 7:9, 14, 17.

21. Nani watakusanyika katika Har-Magedoni, lakini kwa nini itakuwa kazi bure?

21 Ole wao Umoja wa Mataifa, serikali zenye kuuunga mkono na nguvu za kivita walizokusanya! Acheni wakusanyike katika Har-Magedoni “kusudi wapigane na yule aliyekuwa ameketi juu ya farasi [mweupe], pamoja na jeshi lake [la kimbingu]”! Lakini wapi! Yule “Mfalme wa wafalme” anawavurumisha kana kwamba ni katika “ziwa linalowaka moto,” waangamizwe. Mabaki ya tengenezo la Shetani duniani yanaangamizwa pia, kwa maana ule upanga mrefu wa Mfalme ni wenye nguvu kweli kweli, unaweza kutafuta adui ye yote na kumharibu.—Ufunuo 19:17-21, HNWW.

22. Manabii wa Mungu wanasimuliaje vita hiyo katika Har-Magedoni?

22 Kwa makombora na mapigo yanayotupwa kutoka mbinguni, “Yehova atapiga kwa pigo mataifa yale yote” yanayopigana kwa kuupinga ufalme wake, na, bila shaka, katika fujo yao watatupiana silaha za uharibifu, maana ‘mkono wa kila mmoja utakuja hakika juu ya mkono wa mwenziye.’ Lakini ikiwa wewe ni mmoja wa wale wanaoita juu ya jina la Yehova, ‘utaponyoka salama.’—Yoeli 2:31, 32; Zekaria 14:3, 12, 13, NW; Ezekieli 38:21-23; Yeremia 25:31-33.

23. (a) Huo utakuwa upeo mkuu wa nini? (b) Ni maneno gani ya Yesu yamepasa kutufurahisha?

23 Huo utakuwa ndio upeo wa “ishara” ya unabii wa Yesu—“dhiki kubwa, ambayo haijatokea namna yake tangu mwanzo wa ulimwengu hata sasa, wala haitakuwapo kamwe.” Jinsi tunavyoweza kufurahi kwa vile siku hizo ‘zitafupizwa’ kwa ajili ya wale “wateule”! Huenda wewe, pia, ukaokoka kwa kuwa mmoja wa wale “kondoo” ambao Yesu anakaribisha ‘waurithi ufalme’!—Mathayo 24:21, 22; 25:33, 34.

24. (a) Ni hatua gani atakayochukuliwa Shetani wakati huo, na kwa nini? (b) Ni nini kitakachofuata?

24 Vita ile katika Har-Magedoni itakapomalizika, Shetani mwenyewe, mchochezi mwovu anayefanya wanadamu waitawale dunia vibaya, atakamatwa, afungwe na kuvurumishwa katika lile shimo refu kwa “miaka elfu.” Sababu gani? “Asipate kuwadanganya mataifa tena.” (Ufunuo 20:2, 3) Ndipo utakapoanza ule muhula ambao ndio wenye utukufu zaidi katika historia yote ya kibinadamu. Na ile miaka 1,000 itakuwa na maana gani kwa wale washikamanifu ambao wamejitahidi na kusali ili Ufalme huo “uje”? Bila shaka utapendezwa kujua.

[Sanduku katika ukurasa wa 169]

YULE “KAHABA” NA YULE “MNYAMA”

Kumekuwa uhusiano gani kati ya ile milki ya ulimwengu ya dini ya uongo na yule ‘mnyama wa amani na usalama’? Je! “Babuloni mkuu” ametaka faida ya kutawala katika Ushirika wa Mataifa na, baadaye, katika Umoja wa Mataifa? Acha mambo ya hakika yajibu:

Ushirika wa Mataifa ulipokwisha kupendekezwa uundwe mwaka wa 1918, ile “Taarifa Rasmi” ya Baraza la Shirikisho la Makanisa ya Kristo katika Amerika ilifikia kiasi cha kusema: “Sisi Wakristo tunahimiza kuanzishwa kwa Shirika la Mataifa Huru katika Mkutano wa Amani unaokuja. Ushirika huo si kitu chenye kufaidi siasa tu; badala yake ndio wonyesho wa kisiasa wa ule Ufalme wa Mungu duniani. . . . Dunia mpya ambamo uadilifu unakaa isipotokea kwa ushindi, wale mashujaa waliokufa watakuwa wamekufa bure.”

Katika pindi ya ukumbusho wa 20 wa kuzaliwa kwa Umoja wa Mataifa mwaka wa 1965, shirika la magazeti ya Associated Press lilitaarifu kutoka San Francisco, likisema: “Viongozi saba wa kimataifa wa imani za kidini zilizo na washiriki zaidi ya milioni 2,000 ulimwenguni pote walikubaliana kwa sala katika nyumba moja leo kuunga mkono jitihada ya Umoja wa Mataifa ya kutafuta amani ya ulimwengu. Papa Paulo wa Sita alipeleka risala yake ya baraka kutoka Roma . . . ipelekwe kwenye mkutano wa Wakatoliki, Waprotestanti, Wayahudi, Wahindu, Wabuddha, Waislamu na Wakristo (wa Kigiriki) wa Orthodoksi ya Mashariki. . . . Rabi Louis Jacobs . . . aliusimulia ‘ule Umoja wa Mataifa kuwa ndilo tumaini pekee la kuleta amani idumuyo katika ulimwengu ambao kuokoka kwao kwautegemea.’ ”

Katika Oktoba 1965, Papa Paulo wa Sita aliusimulia Umoja wa Mataifa kuwa “lile tengenezo kubwa kuliko matengenezo yote ya kimataifa,” kisha akaongeza: “Mataifa ya dunia yanatumainia Umoja wa Mataifa kuwa ndilo tumaini pekee la upatano na amani.”

Akihutubia Mkutano Mkubwa wa Umoja wa Mataifa Oktoba 2, 1979, Papa Paulo wa Pili alisema: “Sababu rasmi ya kujiingiza kwangu leo bila shaka ni kile kifungo cha pekee cha ushirikiano kinachounganisha Kanisa Katoliki na lile tengenezo la Umoja wa Mataifa.... Mimi natumaini kwamba Umoja wa Mataifa utaendelea wakati wote kuwa ndio chombo cha amani na haki, makao ya kweli ya uhuru wa mataifa na watu mmoja mmoja wanaotamani sana wakati ujao ulio bora.” Hata hivyo katika hotuba yake yenye dakika 62 papa huyo hakutaja Yesu Kristo wala ule Ufalme.

Kwa kuvikubali kwa moyo vitu vinavyowekwa na wanadamu badala ya ufalme wa Mungu, dini ya uongo inategemea tumaini la bure. Baada ya kuonya juu ya kutumainia watawala wa kibinadamu, Zaburi 146:3.6, “NW” inatuambia: “Mwenye furaha ni yeye ambaye tumaini lake liko katika Yehova Mungu wake, yule Mfanya mbingu na dunia.” Na andiko la Luka 2:10-14 Iinamtambulisha Mwokozi wa wanadamu kuwa “Kristo Bwana.”

[Sanduku katika ukurasa wa 173]

MFUATANO WA MATUKIO YENYE KUONGOZA KWENYE HAR-MAGEDONI

● Suala la utawala wa ulimwengu latokezwa, mataifa yazidisha silaha

● Kukauka kwa msaada ambao watu wanatolea dini ya ulimwengu

● Tangazo maarufu la mataifa kusema “Amani na Usalama!”

● “Pembe kumi” za kivita za Umoja wa Mataifa zaangamiza dini ya ulimwengu

● “Pembe” za kinyama zafanya ushambulizi wa mwisho juu ya wafuasi wa “Mwana-kondoo”

● “Mfalme wa wafalme” ayaangamiza mataifa na majeshi katika Har-Magedoni

SHETANI NA MASHETANI WANAPOVURUMISHWA KATIKA SHIMO REFU UTAWALA WENYE UTUKUFU WA KRISTO WA MIAKA ELFU WAANZA

    Maktaba Kwenye Mtandao (1980-2025)
    Toka
    Ingia
    • Kiswahili
    • Shiriki
    • Mapendezi
    • Copyright © 2025 Watch Tower Bible and Tract Society of Pennsylvania
    • Masharti ya Utumiaji
    • Sera ya Faragha
    • Mpangilio wa Faragha
    • JW.ORG
    • Ingia
    Shiriki