Amani, Usalama, na Ile ‘Sanamu ya Mnyama’
“Akanichukua katika [nguvu ya roho] hata jangwani, nikaona mwanamke, ameketi juu ya mnyama mwekundu sana, mwenye kujaa majina ya makufuru, mwenye vichwa saba na pembe kumi.”—UFUNUO 17:3.
1. Ni kwa sababu gani sisi leo tunapaswa kuifikiria njozi ya Yohana na mnyama mwenye vichwa saba na pembe kumi?
MTUME Yohana alimwona mnyama huyo wa kuogopesha katika njozi yenye kuongozwa na roho ya Mungu. Lakini si Yohana peke yake aliyemwona. Inaelekea kabisa kuwa hata wewe umemwona, au angalau ukasoma juu yake katika magazeti. Je! ulimtambua?
2, 3. Ni mfululizo wa viumbe gani ambao Yohana aliona katika njozi yake?
2 Bila shaka, wakati sisi leo tunapomwona mnyama huyo haonekani na sura ambayo Yohana alisimulia. Yohana aliona kitu kilichokuwa mfano wa kitu ambacho kingekuwapo duniani katika “siku ya Bwana.” (Ufunuo 1:10) Leo tunaona utimizo wake. Lile umbo lenye kuchukiza la mnyama aliyeonwa na Yohana linaonyesha namna maoni ya Yehova yalivyo juu ya kinachofananishwa naye—ni kitu cha kumchukiza kiasi cha kutapisha! Katika njozi yake, Yohana alikuwa amekwisha kushuhudia Shetani Ibilisi akitupwa chini kwenye dunia, akiwa “mwenye ghadhabu nyingi, akijua ya kuwa ana wakati mchache tu.” (Ufunuo 12:12) Pia alikuwa ameiona mifumo ya kisiasa ya ulimwengu wa Shetani ikifananishwa na mnyama wa kutisha mwenye vichwa saba na pembe kumi akipanda kutoka kwenye “bahari” ambayo ni wanadamu. (Ufunuo 13;2:17:15; Isaya 57:20; Luka 4:5, 6) Mnyama huyo alikuwa na mamlaka juu ya wanadamu wote, na watu walilazimishwa kuikubali ‘alama ya mnyama’ kwenye mkono wao wa kuume na vipaji vya nyuso zao, kuonyesha wanamuunga mkono.—Ufunuo 13:7, 16, 17, NW.
3 Yohana alikuwa akitazama wakati wanadamu walipokuwa wakifanya sanamu ya kufanana na mnyama huyo. (Ufunuo 13:14, 15) Sanamu hiyo ndiyo aliyoiona katika njozi iliyo juu inayosimuliwa katika Ufunuo sura ya 17. “Sanamu” hiyo yenye vichwa saba na pembe kumi itashiriki sehemu ya maana katika matukio ya wakati ujao; kwa hiyo ni jambo la maana sana tutambue hiyo ni nini. Tunaweza kufanyaje hivyo?
“Sanamu” ya Mnyama Leo
4, 5. Vile vichwa vya yule mnyama wa njozi vinafananisha nini?
4 Malaika alimpa Yohana habari fulani zinazotusaidia. Alisema hivi: “Vile vichwa saba ni milima saba anayokalia mwanamke huyo. Navyo ni wafalme saba. Watano wamekwisha kuanguka, na mmoja yupo, na mwingine hajaja bado. Naye atakapokuja imempasa kukaa muda mchache.” (Ufunuo 17:9, 10) Mtajo wa “wafalme” na “milima”—ambayo mara nyingi katika Biblia inaweza kufananisha serikali kubwa za kisiasa—unaonyesha kwamba vile vichwa vya mnyama vinafananisha serikali. (Yeremia 51:25) Serikali saba zinazohusika ni zipi?
5 Tano zilikuwa zimekwisha kuanguka siku za Yohana, moja ilikuwa ingali ipo, na moja ingekuja. Katika historia ya Biblia, milki tano kubwa-kubwa zilisitawi, zikagandamiza watu wa Mungu, halafu zikaanguka kabla ya siku za Yohana: Misri, Ashuru, Babuloni, Uajemi, na Ugiriki. Wakati Yohana alipokuwa hai, milki ya Kiroma ndiyo iliyokuwa yenye mamlaka. Karne nyingi baada ya kifo cha Yohana, milki ya Kiroma iliacha kuwa ndiyo serikali kuu ya ulimwengu na mwishowe mahali payo pakachukuliwa na milki ya Uingereza. Baada ya muda mfupi, makoloni ya magharibi ya milki hiyo yalipata uhuru kisha yakahusiana sana na Uingereza na kufanyiza serikali kubwa ya ulimwengu ya muungano wa Waingereza na Waamerika. Huyo ndiye ‘mfalme’ ambaye alikuwa “hajaja” katika siku za Yohana. Uhusiano ulikuwa nini kati ya mnyama aliyeonwa na Yohana na zile milki saba zilizofananishwa na vichwa saba vya mnyama? “Yeye ndiye [mfalme] wa nane, naye ni mmoja wa wale saba.”—Ufunuo 17:11.
6. (a) Pembe za mnyama zilimaanisha nini? (b) Ni kwa njia gani zilikuwa ‘hazijapokea ufalme bado’?
6 Kumbuka, pia, kwamba mnyama alikuwa na pembe kumi. Juu ya hizo malaika alisema: “Zile pembe kumi ulizoziona ni wafalme kumi, ambao hawajapokea ufalme bado, lakini wapokea mamlaka kama wafalme muda wa saa moja pamoja na yule mnyama.” (Ufunuo 17:12) Katika Biblia, hesabu kumi inafananisha ukamilifu wa vitu vya duniani. Kwa hiyo pembe hizo zinafananisha serikali za duniani pote zinazomuunga mkono yule mnyama-mwitu kwa muda mfupi (“saa moja”) wakati wa “siku ya Bwana.” Zinatia ndani mamlaka ya saba ya ulimwengu, na pia serikali za kisasa ambazo zimetokana na vile ‘vichwa sita vya mnyama,’ ingawa hivyo sita vimeacha kuwa serikali kubwa za ulimwengu. “Wafalme” hao hawakuwako siku za Yohana.a Kwa kuwa sasa wamepata mamlaka, wao “wampa yule mnyama nguvu zao na mamlaka yao.”—Ufunuo 17:13.
7, 8. (a) Mnyama ambaye Yohana aliona ni nini, kama inavyosimuliwa katika Ufunuo sura ya 17? (b) Anahusianaje na vichwa vile na pembe?
7 Je! sasa wewe unatambua mnyama huyo ni nani? Ndiyo, yeye ndiye lile lile “chukizo kuu lenye kufanyiza uharibifu” lililoanza likiwa Ushirika wa Mataifa na sasa lipo likiwa Umoja wa Mataifa. (Mathayo 24:15; Danieli 12:11; NW, UV) Tengenezo hilo linatokanaje na zile serikali saba kubwa-kubwa? Ni katika maana ya kwamba tengenezo lote linalofanana na mnyama, likiwa mamlaka ya nane linatokezwa na serikali zilizolitangulia, nayo serikali kubwa ya ulimwengu ya muungano wa Waingereza na Waamerika ndiyo mdhamini mkuu walo na yenye kuliunga mkono.
8 Zaidi ya hilo, kama vile malaika alivyomwambia Yohana, “pembe kumi” zote zinampa ‘yule mnyama nguvu na mamlaka’ yazo. (Ufunuo 17:13) Kwa kweli, kama mnyama hangeungwa mkono na serikali zinazofananishwa na vile vichwa na zile pembe, yeye angekuwa hajiwezi. Kwa sababu gani? Kwa sababu yeye ni sanamu tu. (Ufunuo 13:14) Yeye mwenyewe yuko hoi, sawasawa na sanamu zile nyingine zote. (Isaya 44:14-17) Uhai wo wote alio nao unatokana na wenye kumuunga mkono. (Ufunuo 13:15) Nyakati nyingine wao wamechukua hatua ya kukata maneno kwa kutumia Umoja wa Mataifa. Mfano ni wakati wa ile Vita ya Korea.
9. Utambulishaji wetu wa mnyama huyo unathibitishwaje?
9 Utambulishaji wetu wa mnyama huyo unathibitishwa na maelezo zaidi yaliyotolewa na malaika yule: “Yule mnyama uliyemwona alikuwako, naye hayuko, naye yu tayari kupanda kutoka [shimoni] na kwenda kwenye uharibifu.” (Ufunuo 17:8) Hayo yamekwisha kutimizwa kwa sehemu. Vita ya ulimwengu ya pili ilifaulu kuua Ushirika wa Mataifa. Mwaka 1942, wakati Mashahidi wa Yehova walipopata kuufahamu waziwazi unabii huo, ingeweza kusemwa hivi juu ya yule mnyama-Ushirika: “Naye hayuko.”b Lakini mwaka 1945 ‘alipanda kutoka shimoni’ akiwa tengenezo la Umoja wa Mataifa. Je! atafanikiwa katika utume wake wa kuleta amani na usalama? Unabii unasema hapana. Bali, ‘atakwenda kwenye uharibifu.’
Mwenye Kuketi Juu ya Mnyama
10, 11. (a) Ni nani aliyekuwa amempanda mnyama katika njozi ya Yohana? (b) Sehemu hiyo ya njozi imetimizwaje katika nyakati za kisasa?
10 Je! umeona jambo jingine juu ya yule mnyama? Kulikuwa na “mwanamke” mwenye kumpanda. Yeye anatambulishwa kuwa milki ya ulimwenguni pote ya dini ya uwongo, “Babuloni mkuu, mama wa wazinzi [makahaba] na wa mambo yote ya kuchukiza sana duniani.” (Ufunuo 17:3-5, 15, HNWW) Je! dini za ulimwengu ‘zimeketi juu’ ya matengenezo yote mawili, zikijaribu kuyaelekeza njia ya kufuata? Ndiyo, hasa dini za Jumuiya ya Wakristo.
11 Kwa mfano, Pierre van Paassen ambaye ni Mholanzi anayepelekea magazeti makala fupi-fupi, alieleza juu ya “jambo fulani linalohusiana na shauku ya kidini” ya wajumbe wa makanisa ya Kiprotestanti ya Amerika, Uingereza, na Skandinevia ambao walihudhuria vipindi vya Ushirika wa Mataifa. Mwaka 1945, Muungano wa Baraza la Makanisa ya Kristo ya Amerika ulitangaza hivi: “Sisi tumekaza nia tujitahidi kuendelea kupanua kazi za uponyaji na uvumbuaji za Tengenezo la Umoja wa Mataifa.” Mwaka 1965, Papa Paulo wa Sita alitangaza kwamba aliliona tengenezo hilo kuwa lenye “ufanani wa ubuni wa Mungu wenye upendo na wa ajabu kwa kusudi la kuendeleza jamaa ya kibinadamu duniani—ufanani ambao katika huo Sisi tunaona ujumbe wa kimbingu wa ile Gospeli ukiwa wa kidunia.” Kweli viongozi wa kidini wamefanya tengenezo hilo ‘lijae majina ya makufuru.’—Ufunuo 17:3; linganisha Mathayo 24:15, NW; Marko 13:14.
Hauwezi Kuleta Amani
12. Uhusiano umekuwa nini kati ya wenye kuunga mkono tengenezo la Umoja wa Mataifa na Ufalme wa Mungu?
12 Umoja wa Mataifa haufurahii uhusiano mzuri pamoja na Ufalme wa Mungu. Kwa kweli, wenye kuuunga mkono wanapinga Ufalme huo. Malaika alimwambia Yohana: “[Zile pembe kumi zitapigana] na Mwana-kondoo, lakini Mwana-kondoo pamoja na wale aliowaita na kuwachagua, ambao ni waaminifu, atawashinda kwa sababu yeye ni Bwana wa mabwana na Mfalme wa wafalme.” (Ufunuo 17:14, HNWW) Imekuwa kweli kama unabii unavyosema. Mataifa yameendelea ‘kupigana na Mwana-kondoo’ bila kuacha katika muda wote wa wakati huu wa mwisho, wakipinga na kutesa wale wanaotenda wakiwa mabalozi wa Ufalme wake. Ingawa hivyo, yule Mwana-kondoo hashindiki, na pia watumishi wake duniani wanaoendelea kuzihubiri habari njema za Ufalme wa Mungu wajapopatwa na marufuku, vifungo, na hata kifo hawashindiki.—Mathayo 10:16-18; Yohana 16:33; 1 Yohana 5:4.
13. Kwa sababu gani Umoja wa Mataifa hauwezi kamwe kuleta amani halisi?
13 Kwa kweli, Umoja wa Mataifa haungeweza kamwe kuwa kani ya kuleta amani halisi. Si kwamba tu mwenye kuupanda, yaani “Babuloni Mkuu,” ni mmoja wa wachochezi wa vita walio wabaya zaidi, bali pia “amelewa kwa damu ya watakatifu, na kwa damu ya mashahidi wa Yesu.” (Ufunuo 17:6) Vita vya mataifa yanayounga mkono tengenezo hilo vimeilowesha dunia damu. (Mathayo 24:6, 7) Naye mwenye mamlaka anayewategemeza, Shetani Ibilisi, yule “joka” mkubwa, si mfanya amani. (Ufunuo 12:9, 17; 13:2) Wanadamu hawatafurahia kamwe usalama maadamu kuna vipumuaji hivyo. Itakuwa lazima viondolewe.
Hatua Zinazohitajiwa Kabisa Ili Kuwe na Amani
14. (a) Katika njozi ya Yohana, ni jambo gani lililompata mpandaji-mnyama? (b) Jambo hilo litatimizwaje?
14 Kitakachoondolewa kwanza ni dini ya uwongo, kwa njia isiyotazamiwa hata kidogo. Hivi ndivyo mambo yatakavyokuwa: “Pembe zile kumi ulizoziona na yule mnyama watamchukia huyo mzinzi. Watachukua kila kitu alicho nacho na kumwacha uchi; watakula nyama yake na kumteketeza kwa moto.” He! jinsi wanadamu watagutuka! (Ufunuo 17:16, HNWW; 18:9-19) Ataharibiwa na zile “pembe” zenye kuangamiza zilizo za kizalendo, ambazo ni maarufu katika tengenezo la Umoja wa Mataifa. Jambo hilo linatukumbusha vizuri sana unabii wa Yesu kwamba lile “chukizo kuu” lingeuacha “Yerusalemu” katika hali ya ukiwa! (Marko 13:14-20; Luka 21:20) Lakini, ingawa ni mataifa yanayofanya uuaji huo, kwa kweli yanafikiliza tu hukumu ya Mungu juu ya “yule kahaba mkuu,” kutia na Jumuiya ya Wakristo. Matokeo yatakuwaje? Dini ya uwongo ‘haitaonekana tena kabisa.’—Ufunuo 17:1; 18:21.
15, 16. (a) “Dhiki kubwa” ni nini? (b) Itatokeza nini? (c) Shetani atazuiwaje asiharibu mataraja ya wanadamu ya kupata amani?
15 Yesu alisema kwamba uharibifu wa Jumuiya ya Wakristo ungekuwa ndio mwanzo wa “dhiki kubwa, ambayo haijapata kuwako tangu mwanzo wa ulimwengu mpaka leo, wala haitapata kutokea tena.” (Mathayo 24:15, 21, HNWW) Dhiki hiyo itakapokuwa ikiendelea, Ufalme wa Mungu utafikiliza hukumu juu ya sehemu zote za kisiasa na kibiashara za tengenezo la Shetani. (Danieli 2:44) Sasa Yohana anamwona Mfalme akitenda: “Nikaziona mbingu zimefunuka, na tazama, farasi mweupe, na yeye aliyempanda, aitwaye Mwaminifu na Wa-kweli, naye kwa haki ahukumu na kufanya vita.” Waliojipanga kinyume chake ni mataifa ya kisiasa ya dunia pamoja na ile ‘sanamu ya mnyama.’ Matokeo ya vita hiyo ni nini? Hapa tena, ni uharibifu kwa wenye kuharibu amani!—Ufunuo 19:11, 19-21.
16 Hiyo itaacha kukiwa na kipingamizi kimoja tu cha amani: Shetani Ibilisi mwenyewe. Yohana anaendelea kusimulia namna huyo adui mkubwa wa wanadamu atakavyomalizwa nguvu: “Nikaona malaika akishuka toka mbingu, mwenye ufunguo wa shimo [lisilo na] mwisho, na munyororo mukubwa katika mukono wake. Akashika yule joka mukubwa, yule nyoka wa zamani, anayeitwa Diabolo na Shetani, akamufunga miaka elfu.”—Ufunuo 20:1-3, ZSB.
Wakati wa Kufanya Uchaguzi
17. Ni hatua gani zinazopasa kuchukuliwa sasa na watu mmoja mmoja wanaotamani kuona amani halisi?
17 Lo, huo ni wakati wa mabadiliko kwa wanadamu jinsi gani! Lakini ijapokuwa matengenezo na serikali zitaondolewa, ni juu ya watu mmoja mmoja kufanya uchaguzi wao wenyewe kuhusu wanalotaka liwapate. Kwa kuonyesha upendo, Yehova aliamuru hivi: “Lazima kwanza Habari Njema ihubiriwe kwa mataifa yote,” kabla ya dhiki kubwa. (Marko 13:10, HNWW) Wapenda-amani wanakaribishwa ‘watoke’ katika Babuloni Mkuu. (Ufunuo 18:4) Wale walio katika Jumuiya ya Wakristo wanahimizwa ‘wakimbie milimani.’ (Luka 21:21) Wale wanaonyenyekea Ufalme wa Mungu ni lazima waepuke kuwa na ‘alama ya mnyama.’ (Ufunuo 14:9-12, NW; Yohana 17:15, 16) Mkutano mkubwa wa watu wa namna hiyo walio na mioyo inayofaa ‘watatoka katika ile dhiki kubwa.’ (Ufunuo 7:9-14) Kwa kweli, hakuna mtu ambaye ni lazima aangamie pamoja na mfumo wa Shetani.—Mithali 2:21, 22.
18, 19. (a) Inaweza kusemwa nini juu ya wakati dhiki kubwa itakapotokea? (b) Sasa Wakristo wanajitayarishaje kwa ajili ya wakati huo?
18 Matukio hayo yenye kuitikisa dunia yatatendeka wakati gani? Kama ilivyo, “habari njema” zinaendelea kusikiwa kote kote ulimwenguni leo. Lile “chukizo kuu” limekwisha kusimama. (Mathayo 24:14-16) Kwa kweli, ‘sanamu ya mnyama,’ ambayo imekwisha kuingia katika hatua ya pili ya kuwapo kwayo, sasa inakaribia ‘kuenenda kwenye uharibifu.’ (Ufunuo 17:8) Utimizo wa “ishara” unaonyesha kwamba tumekuwa tukiishi katika wakati wa kuwapo kwa Yesu kwa muda wa miaka 71, tangu mwaka 1914. (Mathayo 24:3, NW) Yesu alisema: “Myaonapo hayo yote, tambueni ya kuwa yu karibu, milangoni. Amin, nawaambia, Kizazi hiki hakitapita, hata hayo yote yatakapotimia.” (Mathayo 24:33, 34) Kwa hiyo, bila shaka “dhiki kubwa” iko karibu sana. Je! tunaweza kuutaja wakati wenyewe barabara? Hapana, kwa sasa hatuwezi.
19 Mtume Paulo alitabiri hivi: “Wakati wo wote wanaposema: ‘Amani na usalama!’ ndipo uharibifu wa ghafula utakapokuwa juu yao papo kwa hapo.” (1 Wathesalonike 5:3, NW) Kwa hiyo ile dhiki kubwa itawagutusha kweli kweli wanadamu kwa ujumla. Lakini, haitawagutusha Wakristo. Wao wanajua kwamba inakuja na kufuata shauri la Yesu: “Basi, kesheni ninyi kila wakati, mkiomba, ili mpate kuokoka katika hayo yote yatakayotokea.”—Luka 21:36.
20. (a) Ni kwa sababu gani kwa sasa Wakristo hawawezi kusema ni wakati gani dhiki kubwa itakapokuja?
20 Hata hivyo, Wakristo, pia, hawawezi kujua mapema ni wakati gani barabara itakapofyatuka dhiki kubwa. Yehova hajafunua “siku ile na saa ile.” (Marko 13:32; Mathayo 24:42) Hivyo, kwa mfano wakati Umoja wa Mataifa utakapoutangaza mwaka 1986 kuwa “Mwaka wa Amani ya Kimataifa,” Wakristo wanachungulia tukio hilo kwa kupendezwa. Lakini hawawezi kusema mapema kama hilo litakuwa au halitakuwa utimizo wa maneno ya Paulo yaliyotangulia kutajwa. Ingawa hivyo, wao wanashukuru kwamba Yehova amewawezesha kufahamu maana ya ‘sanamu ya mnyama’ na “chukizo kuu lenye kufanyiza uharibifu.” Hivyo wao wanaliona tengenezo hilo kama vile Yehova anavyoliona na hawadanganywi na jitihada zalo za kuleta amani.
21. (a) Ni amani gani wanayofurahia Wakristo hata sasa? (b) Wanaweza kutazamia nini wakiwa na uhakika?
21 Wale ‘wanaokesha’ na kujinyenyekeza kwa Ufalme wa Mungu wanafurahia amani hata sasa. Yehova, yule “Mungu wa amani,” yuko pamoja nao naye anawapa “amani ya Mungu, ipitayo akili zote.” (Wafilipi 4:7, 9) Kuongezea hilo, wanatazamia wakati usio mbali mno ambapo dunia yote itafurahia utimizo wa unabii huu wa Isaya unaopendeza sana: “Kazi ya haki itakuwa amani; na mazao ya haki yatakuwa ni utulivu na matumaini daima. Na watu wangu watakaa katika kao la amani; na katika maskani zilizo salama, na katika mahali pa kupumzikia penye utulivu.” (Isaya 32:16-18) Huo utakuwa usalama wa ulimwenguni pote. (Isaya 11:9) Na hiyo itakuwa amani halisi kwa sababu Yehova mwenyewe ndiye atakayeifanyiza.
[Maelezo ya Chini]
a Mambo ya kisiasa leo yako tofauti sana na vile yalivyokuwa siku za Yohana. Ni mataifa machache sana yaliyo washirika wa Umoja wa Mataifa yaliyokuwa yametokea wakati huo. Kwa hiyo, ni jambo la kweli kusema kwamba walikuwa “hawajapokea ufalme bado.” Ni machache tu yaliyokuwako, kama Misri. Lakini hata katika nchi hizo, hali ya mamlaka imebadilika sana muda wa karne zilizopita hivi kwamba maelezo ya malaika yule yangali ya kweli: Serikali zilizo na mamlaka sasa zilikuwa ‘hazijapokea ufalme bado’ katika siku za Yohana.
b Wakati Vita ya Ulimwengu ya Pili ilipokuwa ikiendelea kuwaka kweli kweli, msimamizi wa Sosaiti ya Mnara wa Mlinzi alitoa hotuba yenye kichwa “Amani—Je! Inaweza Kudumu?” akihutubia Ulimwengu Mpya wa Kitheokrasi Mkusanyiko wa Mashahidi wa Yehova siku ya Septemba 20, 1942. Humo, alionyesha kutokana na Ufunuo sura ya 17 kwamba, tofauti na vile wengi walivyotazamia, Vita ya Ulimwengu ya Pili haingekuwa Har–Magedoni mwishowe bali kwamba ni lazima kwanza yule ‘mnyama wa amani’ atokea tena kutoka lile shimo refu sana la kutokutenda ili atawale muda wa “saa moja” ya mfano pamoja na mamlaka za kisiasa.”
Wewe Unakumbuka?
◻ Baadhi ya maumbo ya mnyama wa Ufunuo 17 ni gani?
◻ Mnyama huyo anafananisha nini?
◻Kwa sababu gani mnyama huyo wa mfano hawezi kamwe kuleta amani?
◻Ni kwa njia gani mwishowe Ufalme wa Mungu utaletea wanadamu amani na usalama?
◻Watu mmoja mmoja wanaweza kufaidikaje na maarifa ya kujua hivyo?
[Blabu katika ukurasa wa 15]
Papa Paulo wa Sita aliuona Umoja wa Mataifa kuwa “ufanani wa ubuni wa Mungu wenye upendo na wa ajabu kwa kusudi la kuendeleza jamaa ya kibinadamu”
[Picha katika ukurasa wa 17]
Wapenda-amani wanahimizwa ‘watoke’ katika Babuloni Mkuu