Wale Wanyama wa Kitabu cha Ufunuo—Wana Maana Gani?
SIKU ya Jumamosi, Juni 15, 1985, jua la alasiri liling’aa kwa uangavu juu ya majengo ya Umoja wa Mataifa mjini New York. Kama kawaida, wageni walikuwa wamemiminika kuja kuliona jengo hilo la kuvutia, na nyuso za wengi hazikuweza kuficha jinsi walivyovutiwa na mambo yote waliyoona.
Hata hivyo, kufikia sasa Umoja wa Mataifa unaonekana uko mbali sana na kuyaunganisha mataifa. Ni kama vile mwongozaji rasmi alivyosema alasiri hiyo: “Kumekuwako vita 150 tangu Vita ya Ulimwengu ya Pili, na waliouawa ni watu zaidi ya milioni 20. Mpaka sasa hakujawa na serikali ya ulimwengu. Labda tukio hili ndiyo hatua iliyokaribia zaidi kutokeza serikali ya namna hiyo.” Basi je, kuwapo kwa serikali ya ulimwengu ni ndoto isiyoweza kuwa kweli? Amini usiamini, jibu linaweza kupatikana kwa kuwachunguza wale wanyama wa kitabu cha Ufunuo.
Waelezaji wengine wa habari za Biblia hawaoni maana yo yote ya kiunabii katika wanyama wa kitabu cha Ufunuo. Bali, wanawahusisha na matukio yaliyotendeka wakati mtume Yohana alipokuwa angali hai. Kwa mfano, kinapozungumza habari ya wanyama wa Ufunuo, kitabu The Catholic Encyclopedia kinasema: “Ilikuwa desturi ya waandikaji wa mambo yaliyofunuliwa kuwa yangetokea baadaye . . . kueleza njozi zao kwa namna ya unabii na kuzifanya zionekane kama kwamba ziliandikwa mapema zaidi.”
Lakini mtume Yohana alitangaza hivi: “Kwa uongozi wa roho ya Mungu niliingia katika siku ya Bwana.” (Ufunuo 1:10, NW) Ndiyo, kitabu cha Ufunuo kinakazia fikira, si juu ya historia ya zamani, bali juu ya “siku” ya wakati ujao ambapo Bwana Yesu Kristo angeanza kutawala akiwa mbinguni. Kulingana na Ufunuo sura ya 6, “siku ya Bwana” inatiwa alama na vita vya ulimwengu, upungufu wa chakula ulioenea sana, na magonjwa yenye kuua. Matukio yaliyoshuhudiwa duniani wakati wa karne hii ya 20 ni uthibitisho wenye kusadikisha kwamba tumekuwa tukiishi katika “siku ya Bwana” tangu mwaka 1914.—Ufunuo 6:1-8.a
Katika mwaka huo wa kihistoria, Yesu Kristo alianza utawala wake wa Ufalme. (Ufunuo 11:15, 18) Basi ni lazima wanyama wa kitabu cha Ufunuo waonekane wazi baada ya tarehe hiyo. Kwa kweli, wanyama hao wanafananisha adui za Mungu wanaozuia watu wasitegemee Ufalme wa Mungu kuwa ndio mpango wa pekee utakaotosheleza tamaa ya wanadamu ya kupata amani. Adui hao ni kutia na joka moja na wanyama-mwitu watatu. Acheni tuwachunguze kulingana na vile wanavyofuatana katika kutokea kwao.
Lile Joka Kubwa
“Tazama,” akapaaza sauti Yohana, “joka kubwa jekundu, alikuwa na vichwa saba na pembe kumi.” Joka kubwa hilo linafananisha nini? Yohana mwenyewe anaeleza kwamba halifananishi mwingine ila Shetani Ibilisi. Kulingana na njozi ya Yohana, joka hilo lilipinga vikali kuzaliwa kwa Ufalme wa kimbingu wa Mungu katika mwaka 1914. Matokeo yakawa nini? “Yule joka akatupwa, yule mkubwa, nyoka wa zamani, aitwaye Ibilisi na Shetani, audanganyaye ulimwengu wote; akatupwa hata nchi, na malaika zake wakatupwa pamoja naye.”—Ufunuo 12:3, 7-9.
Yohana anaonyesha kwamba jambo hilo lingeletea wanadamu mabaya. “Ole wa nchi na bahari! kwa maana yule Ibilisi ameshuka kwenu mwenye ghadhabu nyingi, akijua ya kuwa ana wakati mchache tu.” (Ufunuo 12:12) Ingawa Shetani amezuiwa kabisa asiweze kutoka nje ya ujirani wa dunia, bado yeye amejikaza sana avuruge Ufalme wa Mungu uliosimamishwa. Anafanya hivyo kwa kupoteza wanadamu, akitumia wanyama watatu. Fikiria maelezo ya Yohana juu ya wa kwanza wa wanyama hao.
Yule Mnyama wa Bahari
“Nikaona mnyama akitoka katika bahari, mwenye pembe kumi, na vichwa saba . . . Na yule mnyama niliyemwona alikuwa mfano wa chui, na miguu yake ilikuwa kama miguu ya dubu, na kinywa chake kama kinywa cha simba; yule joka akampa nguvu zake na kiti chake cha enzi na uwezo mwingi.”—Ufunuo 13:1, 2.
Dubwana hilo linafananisha nini? Akiwa chini ya uongozi Mungu, Yohana anatoa kidokezi cha maana: “Akapewa uwezo juu ya kila kabila na jamaa na lugha na taifa.” (Ufunuo 13:7) Ni nini kinachotumia mamlaka juu ya kila mtu anayeishi duniani? Ni kitu kimoja tu: mfumo wa ulimwenguni pote wa utawala wa kisiasa. Je, kweli mfumo huo unapokea mamlaka kwa yule joka, Shetani? Biblia inajibu ndivyo. Kwa mfano, mtume Yohana alisema: “Ulimwengu mzima umo katika uwezo wa yule mwovu. ‘ Si ajabu kwamba wakati Shetani alipokuwa akimshawishi Yesu jangwani, alimtolea mamlaka ya kusimamia “falme zote za dunia inayokaliwa na watu” kisha akadai hivi: “[Mamlaka hii] imetolewa nikapewa mimi.”—1 Yohana 5:19; Luka 4:5, 6, NW.
Ingawa hivyo, ni nini kinachofananishwa na vile vichwa saba? Yohana alionyeshwa dubwana jingine ambalo lilikuwa lafanana na huyu mwingine. Hilo pia lilikuwa na vichwa saba. Vichwa vya sanamu hiyo vilielezwa kuwa vinafananisha “wafalme saba,” au serikali kubwa za ulimwengu, ambazo kati yazo ‘tano zimekwisha kuanguka, na moja ipo, na nyingine haijaja bado.’ (Ufunuo 17:9, 10) Serikali tano kubwa za ulimwengu zilitokea katika historia ya Biblia kabla ya siku za Yohana: Misri, Ashuru, Babulonia, Umedi-Uajemi, na Ugiriki. Ile ya sita, Roma, ilikuwa ingali katika mamlaka Yohana alipokuwa hai.
Kile kichwa cha saba kilikuwa nini? Kwa kuwa njozi hiyo ilihusiana na “siku ya Bwana,” ni lazima iwe inamaanisha serikali kubwa ya ulimwengu inayosimama katika cheo chenye mamlaka cha Roma wakati wa hizi siku za mwisho tangu mwaka 1914. Historia inaifunua hiyo kuwa muungano wa serikali mbili za ulimwengu, Uingereza na United States ya Amerika. Kabla ya 1914, Uingereza ilikuwa imejenga milki kubwa zaidi isiyopata kuonekana na ulimwengu. Wakati wa karne ya 19, ilikuwa pia imesitawisha uhusiano imara wa kibalozi na kibiashara pamoja na United States. Nchi hizo mbili zilishirikiana kupigana wakati wa Vita ya Ulimwengu ya Kwanza na ya Pili, na uhusiano wazo wa pekee umeendelea mpaka leo. Mwaka 1982, Rais Reagan wa United States alieleza bunge la Uingereza juu ya “urafiki mkubwa ulio kati ya nchi zetu mbili.” Hivi majuzi zaidi, katika Februari 1985, waziri mkuu wa Uingereza alihutubia yale mabunge mawili ya Baraza Kuu la United States akasema: “Mataifa yetu mawili yenye uhusiano wa damu na yasonge mbele pamoja . . . tukiwa imara katika kusudi, kushirikiana katika imani, . . . tunapoikaribia mileani ya tatu ya kipindi cha Kikristo.”
Kwa sababu ya mavutano makubwa ambayo muungano wa serikali kubwa za Uingereza na Amerika unayo katika mambo ya ulimwengu, unafananishwa ukiwa peke yake katika kitabu cha Ufunuo. Jinsi gani? Na yule wa pili wa wanyama wa kitabu cha Ufunuo.
Yule Mnyama wa Nchi Kavu
“Kisha nikaona mnyama mwingine,” anaandika Yohana, “akipanda juu kutoka katika nchi; naye alikuwa na pembe mbili mfano wa Mwana-Kondoo, akanena kama joka.” Kwa kudai kwamba ni ya Kikristo wala haipendi uchokozi, serikali kubwa ya ulimwengu ya muungano wa Waingereza na Waamerika inajifanya kama kwamba ina tabia za kondoo. Lakini kwa kweli imetenda kama joka. Jinsi gani? Kwa kufanya mataifa mengi yawe makoloni yake na kutumia rasilimali za dunia kwa pupa ili kujifaidi yenyewe. Pia, inaifanya “dunia na wote wakaao ndani yake wamsujudie mnyama wa kwanza, ambaye jeraha lake la mauti lilipona . . . ikiwaambia wakaao juu ya nchi kumfanyia sanamu yule mnyama.” (Ufunuo 13:3, 11-15) Jambo hilo lilitimizwaje?
Mfumo wa kisiasa wa Shetani uliopo ulimwenguni pote ulipatwa na ‘jeraha la mauti’ wakati wa vita ya ulimwengu ya kwanza. Ili kuzuia jambo hilo lisitukie tena, Uingereza na Amerika zilitia watu moyo wafuate “ibada” ya mfumo wa kisiasa. Zilifanya hivyo kwa kuongoza mataifa ‘yamfanyie sanamu yule mnyama.’ Jambo hilo lilitukiaje?
Kuelekea mwishoni mwa vita ya ulimwengu ya kwanza, Rais Wilson wa United States alianzisha shughuli ya Kikristo yenye kupendelea Ushirika wa Mataifa uliokuwa umependekezwa wakati huo. Kwa kusudi hilo, mwaka 1919 aliwaambia hivi wajumbe wenye kuhudhuria Mkutano wa Amani Paris: “Wajumbe wa United States wanaiunga mkono shughuli kubwa hii ya kuanzisha Ushirika wa Mataifa. Tunaiona kuwa ndio msingi wa programu yote iliyoonyesha kusudi letu . . . katika vita hii. . . . Sisi tupo hapa tuhakikishe kwa ufupi kwamba mambo yale hasa yaliyoianzisha vita hii yanafagiliwa mbali.”
Baada ya Rais Wilson kumaliza hotuba yake, aliyehutubu si mwingine ila waziri mkuu wa Uingereza, Lloyd George: “Mimi nasimama ili niwe wa pili kuunga mkono azimio hili. Baada ya hotuba bora sana iliyotolewa na Rais wa United States mimi naona kwamba hakuna uhitaji wa maoni kutolewa kwanza ndipo azimio hili halijapendekezwa mbele ya Mkutano huu, nami . . . nasema kwamba watu wa Milki ya Uingereza wanaliunga mkono sana pendekezo hili.”
Baadaye katika mwaka huo, kwenye mkutano uliofanywa London ili kuunga mkono kwamba Ushirika wa Mataifa uhalalishwe kisheria, barua ilisomwa kutoka kwa Mfalme wa Milki ya Uingereza: “Sisi tumeishinda vita. Hilo ni tendo kuu. Lakini halitoshi. Sisi tumepigana ili tupate amani ya kudumu, na tuna wajibu mkubwa wa kuilinda kwa vyo vyote. Kwa kusudi hilo, hakuna jambo la maana kuliko kuwa na Ushirika wa Mataifa wenye nguvu na wa kudumu. . . . Mimi napendekezea raia wote wa Milki kusudi hili, ili kwamba, kwa msaada wa wanaume wengine wote wenye nia njema, kiegemezo na kilinda-amani kilicho hakika, kwa utukufu wa Mungu . . . kipate kusimamishwa.”
Siku ya Januari 16, 1920, Ushirika wa Mataifa ulisimamishwa ukiwa na nchi 42 zilizo washirika. Kufikia mwaka 1934 nchi 58 zilihusika. Yule mnyama wa nchi kavu mwenye pembe mbili alikuwa amefanikiwa kuuongoza ulimwengu ‘umfanyie sanamu yule mnyama.’ Sanamu hiyo, au wakili wa mfumo wa kisiasa wa Shetani uliopo ulimwenguni pote, inafananishwa na mnyama wa mwisho wa kitabu cha Ufunuo.
Yule Mnyama Mwekundu Sana
Haya ndiyo maelezo ya Yohana juu ya mnyama huyo wa mwisho: “Mnyama mwekundu sana, mwenye kujaa majina ya makufuru, mwenye vichwa saba na pembe kumi.” Kwa habari ya mnyama huyo, Yohana aliambiwa hivi: “Yule mnyama uliyemwona alikuwako, naye hayuko, naye yu tayari kupanda kutoka [kwenye shimo refu] na kwenda kwenye uharibifu. . . . Yeye ndiye [mfalme] wa nane.” (Ufunuo 17:3, 8, 11) Kama ilivyosemwa katika maelezo hayo, Ushirika wa Mataifa ulijaribu kutenda kama serikali kubwa ya ulimwengu. Lakini, ulishindwa kuzuia Vita ya Ulimwengu ya Pili, iliyoanza mwaka 1939. Mnyama huyo alitoweka, ikawa ni kama kwamba ameingia katika shimo refu.
Wakati wa Vita ya Ulimwengu ya Pili, serikali kubwa ya ulimwengu ya muungano wa Waingereza na Waamerika ilifanya bidii kulifufua tengenezo hilo la kimataifa. Mwaka 1941 waziri mkuu wa Milki ya Uingereza, Winston Churchill, alifanya mazungumzo ya siri pamoja na Rais Franklin Roosevelt wa United States wakiwa melini katika bahari kuu ya Atlantiki. Walifanya tangazo la pamoja juu ya “matumaini yao ya kuwako kwa wakati ujao ulio bora kwa ulimwengu” na kusimamishwa kwa mfumo mpana zaidi na wenye kudumu wa kuletea watu wote usalama. Mwaka uliofuata, katika Washington, D.C., mataifa 26 yalijiandikisha kuliunga mkono pendekezo hilo la Waingereza na Waamerika katika kile kilichoitwa “Tangazo Rasmi la Umoja wa Mataifa.” Jambo hilo likatokeza tengenezo la Umoja wa Mataifa siku ya Oktoba 24, 1945. Yule mnyama mwekundu sana akatoka kwenye lile shimo refu akiwa na jina jipya. Kwa sasa, mataifa 159 yamejiunga na tengenezo hilo, ambalo, wanatumaini, litaendeleza daima mfumo uliopo sasa wa utawala wa kisiasa wa wanadamu.
Lakini, yote hayo yanafanywa bila kuujali Ufalme wa Kimasihi wa Mungu, uliosimamishwa mbinguni mwaka 1914. Kila mwanadamu aliyepo duniani lazima achague kati ya utawala unaoendeshwa na Mungu au utawala unaoendeshwa na wanadamu. Hivi karibuni, yule mnyama mwekundu sana, pamoja na serikali zote za kibinadamu, atahusika katika pigano pamoja na Mfalme aliyetawazwa, Yesu Kristo. Matokeo yatakuwa nini? “Mwana-Kondoo [Yesu Kristo] atawashinda, kwa maana Yeye ni Bwana wa Mabwana, na Mfalme wa Wafalme.” Ndiyo, yule mnyama mwekundu sana pamoja na mfumo wote wa serikali ya kibinadamu ‘ataenenda kwenye uharibifu.’—Ufunuo 17:11, 14; ona pia Danieli 2:44.
Wakati huo itakuwa baraka kama nini kwamba mtu hakupotezwa na yule joka na wanyama wake watatu! Wale ambao wamejithibitisha kuwa raia washikamanifu wa Ufalme wa Mungu watakapookoka wawe sehemu ya ‘dunia mpya.’ Mungu “atafuta kila chozi katika macho yao, wala mauti haitakuwapo tena; wala maombolezo, wala kilio, wala maumivu hayatakuwapo tena; kwa kuwa mambo ya kwanza yamekwisha kupita.” (2 Petro 3:13; Ufunuo 21:3, 4) Kwa hiyo, jitiishe mwenyewe kwa Ufalme wa Mungu, kwa maana huo tu ndio serikali ya ulimwengu yenye matokeo mazuri. Ndipo hata wewe utakapokuwa katika mstari wa kuelekea kuzifurahia baraka hizo za milele.
[Maelezo ya Chini]
a Jambo hili lilizungumzwa kwa urefu zaidi katika matoleo ya Januari 1 na Januari 15 ya Mnara wa Mlinzi.