Watchtower MAKTABA KWENYE MTANDAO
Watchtower
MAKTABA KWENYE MTANDAO
Kiswahili
  • BIBLIA
  • MACHAPISHO
  • MIKUTANO
  • sj kur. 22-25
  • Mafundisho ya Darasani

Hakuna video yoyote kwa sasa.

Samahani, haikuwezekana kupakia video.

  • Mafundisho ya Darasani
  • Shule na Mashahidi wa Yehova
  • Habari Zinazolingana
  • Kurudi Shuleni Tena
    Huduma Yetu ya Ufalme—1995
  • Ilinde Familia Yako Dhidi ya Mavutano Yaletayo Uharibifu
    Siri ya Furaha ya Familia
  • Je! Watoto Wako Ni Tayari Kurudi Shuleni?
    Huduma Yetu ya Ufalme—1990
  • Michezo na Tafrija
    Kupata Faida Zote za Ujana Wako
Pata Habari Zaidi
Shule na Mashahidi wa Yehova
sj kur. 22-25

Mafundisho ya Darasani

Sehemu nyingine ambayo katika hiyo huenda maoni ya Mashahidi wa Yehova yakageuza masomo yao ya shuleni inahusu taaluma. Hivyo, kwa kuwa tunaamini kwamba hasa ni wazazi walio na daraka la kuchagua jambo ambalo watoto wao watafundishwa, kusudi la mambo yanayotolewa ni kuendeleza ufahamiano na ushirikiano kati ya walimu na wazazi-Mashahidi.

Dini na Sala: Shule fulani fulani zinatia mafundisho ya kidini katika darasa. Wakati mmoja wazazi katika Marekani walitakwa kusema kama wangetaka au hawangetaka watoto wao wafundishwe katika dini ya Kikatoliki, Kiprotestanti au ya Kiyahudi. Mtoto ambaye hakutakwa afundishwe mambo ya kidini alilazimika kuondoka darasani na kufanya masomo yasiyo ya kidini mahali pengine. Lakini ndipo, mwaka wa 1948, Mahakama Kuu ya nchi hiyo iliposema hivi:

“Sheria ya Kwanza Iliyosahihishwa inategemea sharti la kwamba dini na serikali zinaweza kufanya vizuri zaidi kutimiza shabaha zao bora ikiwa kila moja inaachiliwa isihusike na ile nyingine katika eneo la kila moja. . . . Sheria ya Kwanza Iliyosahihishwa imeinua ukuta kati ya Kanisa na Serikali ambao ni lazima uendelezwe ukiwa juu na usiopenyeka.”—McCollum v. Board of Education (1948).

Baadaye, Juni 17, 1963, Mahakama Kuu ya U.S. iliamua pia kusiwe kusoma Biblia na kutolewa kwa sala katika shule za serikali. Hakimu Brennan alieleza kauli yake hivi: “Roho ya katiba zetu za utawala na serikali tangu mwanzo . . . [imekuwa] kuwaacha wazazi wenyewe waamue juu ya mafundisho ya kidini.”

Mashahidi wa Yehova wanakubali kwamba ni daraka la wazazi kuwapa watoto wao mafundisho ya kidini. Kwa hiyo, ikiwa mafundisho ya kidini yanatolewa darasani, wazazi-Mashahidi wanaomba watoto wao wapewe ruhusa ya kutoshiriki namna fulani ya ibada tunayoona kuwa isiyopatana na Biblia, kama vile kusujudia sanamu, wazazi-Mashahidi hawakubali jambo hilo kwa vyo vyote.

Kwa upande mwingine, Mashahidi wa Yehova hawapingi ikiwa darasani kuna somo fulani juu ya dini mbalimbali au juu ya Biblia kwa kusudi la kutaka kujua tu. Hivyo ikiwa shule inafanya mpango wa kualika wawakilishi wa dini mbalimbali waje watoe hotuba, si kwa kusudi la kugeuza wengine waingie dini nyingine, bali kwa kusudi la kuwapasha habari tu wanafunzi juu ya dini hizo, Mashahidi-wanafunzi wanasikiliza kwa heshima. Hali moja na hiyo, wakialikwa, Mashahidi wa Yehova wanafurahi kuvitolea vikundi vya shule hotuba, wakieleza imani zao za kidini.

Katika shule fulani ile Sala ya Bwana, au Sala ya Baba Yetu, inasemwa kwa ukawaida. Ijapokuwa Mashahidi wa Yehova wanaikubali sala hiyo, hawajiungi katika desturi ya kidini ya kurudia-rudia sala hiyo. Sababu yenyewe ni kwa vile wakati Yesu alipotoa hiyo sala ya kielelezo alishauri juu ya kutokusali kwa kuomba “mambo yale yale kwa kurudia-rudia.” (Mathayo 6:7, 8, New World Translation) Sababu nyingine inayotufanya sisi tusishiriki ni kwamba sisi hatuchanganyi ibada yetu pamoja na ile ya dini nyingine.

Elimu Juu ya Ngono: Afya na usafi wa mwili ni masomo ambayo yamefundishwa katika shule kwa muda mrefu. Sisi tunathamini kwamba mitaala hiyo imesaidia sana kufundisha ubora wa usafi, kuzuia magonjwa, utunzaji wa watoto, daraka la jamaa, na kadhalika. Lakini leo shule nyingi zinatoa pia elimu iliyo wazi juu ya mambo ya ngono, ikiwa ni pamoja na njia za kuzuia kutungwa mimba, kupiga punyeto, ngono za watu wa jinsia moja na kutoa mimba.

Kwa jumla elimu juu ya ngono inatolewa bila mwongozo wa kiadili. Kwa kweli, wafunzi wenyewe wanachambua mara nyingi viwango vya adili vya Biblia. Kwa hiyo wazazi-Mashahidi wanahangaikia sana yanayofundishwa katika masomo ya elimu juu ya ngono.

Kitabu kimoja kinachotumiwa katika shule fulani, chenye jina la Dreng og pige, mand og kvinde (Mvulana na Msichana, Mwanamume na Mwanamke), kinasema, “Kila mtu anapaswa awe na haki ya kutosheleza nyege zake bila kujali ana umri gani, awe ni mwanamume au mwanamke, na njia inayotumiwa, mradi asiingilie haki za wengine.” Hivyo, kwa habari ya kufanya ngono na wanyama, kitabu hicho kinasema hivi: “Katika nchi hii [Denmark], . . . ni halali kutosheleza nyege kwa njia hiyo.” Hata hivyo Sheria ya Mungu aliyowapa Waisraeli ilisema: “Mtu awaye yote alalaye na mnyama sharti atauawa.”—Kutoka 22:19.

Kama ilivyotangulia kukaziwa, Mashahidi wa Yehova wanajaribu kufuata kanuni za adili za Biblia na wanazikaza sana katika akili na mioyo ya watoto wao. Kwa hiyo hawataki watoto wao wapokee elimu juu ya ngono kutoka kwa wale wasioheshimu kanuni hizo. Kwa hiyo ikiwa wazazi Mashahidi wanaona kwamba watoto wao wanafundishwa kwa maneno ya mawazo, na/au kwa vitu vinavyoonekana, vinavyoharibu waziwazi kanuni zinazofundishwa nyumbani, wanaweza kuomba watoto wao wasifundishwe masomo yanayohusu ngono.

Sayansi na Mageuzi: Mashahidi wa Yehova wanapendezwa sana na sayansi. Wanawaheshimu wanasayansi wenye kujitoa sana ambao wameongezea sana ufahamu wetu juu ya ulimwengu unaotuzunguka. Tunatia moyo vijana wetu wajifunze sehemu mbalimbali za sayansi, kwani hizo zitawasaidia waongeze uthamini wao wa hekima na uwezo wa Muumba wetu.

Lakini si yote yanayoitwa sayansi yaliyo mambo ya hakika. Pia kuna nadharia, kama vile nadharia ya mageuzi, inayopokezwa kuwa ni sayansi iliyothibitishwa. Mageuzi yanadai kwamba kitu cha kwanza chenye uhai kiligeuka-geuka kutokana na kitu kisicho na uhai. Kisha, kitu hicho kilicho hai kilipotokeza vingine, uzao wacho ukabadilika-badilika na kuendelea mpaka hatimaye ukazaa vitu vyote vilivyo hai, kutia na watu wote ambao wamepata kuishi hapa duniani.

Mashahidi wa Yehova hawaamini nadharia hiyo kuwa ya kweli. Wala sisi hatuendi upande mwingine wa kupita kiasi kuamini kwamba uumbaji ulichukua siku halisi saba. Sisi tunaamini kwamba mwanamume na mwanamke wa kwanza waliumbwa na Mungu, kama vile aina nyingine za uhai. Hivyo ikiwa nadharia juu ya mianzo ya vitu vilivyo hai zinafundishwa darasani, sisi tunathamini wakati walimu wanapoheshimu imani zenye kutegemea Biblia za vijana-Mashahidi. Hakika, sisi tunaona imani hizo zinapatana na mambo ya hakika ya sayansi, ambayo vijana-Mashahidi watafurahia kushiriki pamoja nawe.

Muziki na Mafundisho ya Sanaa: Mashahidi wa Yehova hawaamini kuna ubaya wo wote na muziki wenyewe au mafundisho ya sanaa yenyewe. Lakini, vijana-Mashahidi hawashiriki aina yo yote ya muziki na mafundisho ya sanaa yanayohusiana na sikukuu za kidini au za kizalendo. Wakati wa kushiriki programu ya elimu ya shule juu ya muziki, kuna mambo ambayo vijana-Mashahidi na wazazi wao watafikiria.

Kwa mfano, watafikiria mahali na hali ambazo katika hizo mafundisho hayo yamepokewa, pia namna ya muziki unaopigwa. Ikiwa mafundisho yanahusu kutumikia katika bendi ambayo huenda ikatarajiwa kucheza kwenye mambo yanayohusiana na siasa au dini, mtu ambaye ni mmoja wa Mashahidi wa Yehova hangeweza kushiriki. Hata wakati wa vipindi vya mazoezi, wanafunzi-Mashahidi hawangeshiriki kuimba nyimbo za kisiasa wala nyimbo zinazohusiana na sikukuu za kidini au za kisiasa. Jambo jingine la kufikiriwa lingekuwa ni wakati unaohusika, na kama mikutano ya Kikristo na shughuli za jamaa zingezuiwa.

Mafundisho ya Kupigana: Katika shule fulani fulani mazoezi ya kivita yanatolewa kwa wanafunzi. Hata hivyo Mashahidi wa Yehova wanataka kuwa kati ya wale ambao Biblia inasema: “Watafua panga zao ziwe majembe, na mikuki yao iwe miundu, taifa halitainua upanga juu ya taifa lingine, wala hawatajifunza vita tena kamwe.” (Isaya 2:4) Kwa hiyo, Mashahidi wa Yehova wanaomba ruhusa wasishiriki masomo ya kujizoeza vita shuleni.

Pia Biblia inasema: “Kama yamkini, kwa upande wenu, mkae katika amani na watu wote.” (Warumi 12:18) Pia kufuatwa kwa kanuni hizo katika maisha zetu kunageuza mielekeo yetu juu ya namna nyingine za kupigana. Namna hizo ni pamoja na ufundi wa kupigana, kama vile judo, karate na kendo, na pia kupigana ngumi na kushindana mweleka. Ijapokuwa huenda shughuli hizo zikatajwa kuwa michezo, sisi tunaona kuzishiriki ni kupata mazoezi yenye kusudi la kupigana vita au kuwaumiza wengine. Kwa hiyo, Mashahidi wa Yehova hawashiriki shughuli hizo za kupigana. Ijapokuwa vijana-Mashahidi wanaomba ruhusa wasishiriki shughuli hizo, wanaunga mkono kwa furaha na kwa kadiri wawezavyo mipango mingine ya mazoezi ya mwili inayofanywa wakati wa saa za shule.

[Blabu katika ukurasa wa 22]

Tunatia moyo vijana wetu wajifunze sehemu mbalimbali za sayansi

    Maktaba Kwenye Mtandao (1980-2025)
    Toka
    Ingia
    • Kiswahili
    • Shiriki
    • Mapendezi
    • Copyright © 2025 Watch Tower Bible and Tract Society of Pennsylvania
    • Masharti ya Utumiaji
    • Sera ya Faragha
    • Mpangilio wa Faragha
    • JW.ORG
    • Ingia
    Shiriki