Watchtower MAKTABA KWENYE MTANDAO
Watchtower
MAKTABA KWENYE MTANDAO
Kiswahili
  • BIBLIA
  • MACHAPISHO
  • MIKUTANO
  • su sura 2 kur. 13-20
  • Masuala Yanayoamua Wakati Ujao Wetu Utakavyokuwa

Hakuna video yoyote kwa sasa.

Samahani, haikuwezekana kupakia video.

  • Masuala Yanayoamua Wakati Ujao Wetu Utakavyokuwa
  • Kuokolewa Kuingia Katika Dunia Mpya
  • Vichwa vidogo
  • Habari Zinazolingana
  • LILE SUALA LA ENZI KUU
  • WEWE UTACHAGUA UPANDE UPI?
  • MATAIFA YOTE YANAELEKEZWA KWENYE HAR–MAGEDONI
  • Suala Linalokuhusu Wewe
    Amani na Usalama wa Kweli—Wewe Unaweza Kuupataje?
  • Mungu Ana Kusudi Gani kwa Dunia
    Biblia Inafundisha Nini Hasa?
  • Watawala Katika Makao ya Roho
    Mnara wa Mlinzi Unaotangaza Ufalme wa Yehova—1995
  • “Tazama! Mimi Ninafanya Vitu Vyote Kuwa Vipya”
    “Tazama! Mimi Ninafanya Vitu Vyote Kuwa Vipya”
Pata Habari Zaidi
Kuokolewa Kuingia Katika Dunia Mpya
su sura 2 kur. 13-20

Sura 2

Masuala Yanayoamua Wakati Ujao Wetu Utakavyokuwa

1. (a) Ni masuala gani yanayoendelea ambayo yanafikiriwa sana na watu wengi, na wanatumainia kupata majibu wapi? (b) Mara nyingi wanashindwa kufikiria nini?

MIAKA ya karibuni masuala yenye kuleta ubishi kuhusu wakati ujao wetu yametupwa-tupwa juu yetu kwa mfululizo wa haraka sana. Hali zimekuwa hivyo hata watu kila mahali wanatafuta sana kitulizo. Labda wanamwamini Mungu, lakini huenda inaonekana kwao kwamba ikiwa hali hiyo hapa duniani itakuwa nafuu, wanadamu ndio watalazimika kuitokeza. Watu fulani wanajaribu kufanya hivyo kupitia serikali zilizopo au kupitia maandamano ya kupinga maamuzi ya serikali hizo. Wengine wanaamini kwamba njia pekee inayofaa ni kufanya mapinduzi ya serikali. Wanahisi kwamba kubadili sheria, kubadilisha watawala au hata serikali nzima-nzima bila shaka kutafanya hali ziwe nafuu. Lakini mambo ya hakika yanaonyesha nini? Baada ya kujaribu kwa maelfu ya miaka, wanadamu wameshindwa kutokeza hata serikali moja ambayo imeleta haki bila upendeleo, usalama wa kweli na furaha yenye kuendelea kwa raia zayo wote. Sababu ya hiyo ni nini?

2. Kwa nini hali ulimwenguni ni mbaya sana?

2 Hata makusudi ya watu wenye mamlaka yawe mazuri namna gani, serikali zote za kibinadamu zinaongozwa kwa werevu na majeshi yasiyoweza kuzuiwa na wanadamu walio katika vyeo. Na nani? Na roho wenye kupita uwezo wa kibinadamu, Shetani Ibilisi na mashetani wake. Ni kweli, watu wengi wanadhihaki imani ya kwamba kuna watu wa kiroho kama hao. Lakini Yesu Kristo hakudhihaki. Yeye binafsi alijua asili ya Shetani na alimtaja kuwa “mtawala wa ulimwengu huu.” (Yohana 12:31, New World Translation) Kwa usemi wa mfano, Biblia inafananisha mfumo wa kisiasa wa duniani pote kuwa mnyama-mwitu na kufunua kwamba “yule joka [Shetani] akampa [mnyama] nguvu zake na kiti chake cha enzi na uwezo mwingi.” (Ufunuo 13:1, 2; linganisha Danieli 7:2-8, 12, 23-26.) Na kwa habari ya wakati wetu, Biblia ilitabiri kuongezeka kwa “ole . . . kwa dunia . . . ! Kwani yule Diabolo ameshuka kwenu.” (Ufunuo 12:12, Zaïre Swahili Bible) Hakuna sababu nyingine kuliko hiyo ya mchafuko ambao katika huo jamii ya kibinadamu imetupwa. Lakini ilitokeaje? Tunaweza kufanya nini ili tupate kitulizo?

LILE SUALA LA ENZI KUU

3. Andiko la Mwanzo 2:16, 17 linaonyesha nini juu ya uhusiano unaofaa wa wanadamu kwa Mungu?

3 Sura ya kwanza ya Biblia inatupasha habari kwamba Yehova Mungu alipoumba watu wawili wa kwanza, Adamu na Hawa, na kuwaweka katika bustani ya Edeni aliwaagiza juu ya uhusiano wao na yeye. Alikuwa Baba yao, Mwandalizi wao mwenye ukarimu, pia Mwenye Enzi Kuu ya Ulimwengu Wote. Kwa faida yao, lilikuwa jambo la lazima kwao kuthamini kwamba uzima wao wenye kuendelea ulitegemea kumtii Mungu.—Mwanzo 2:16, 17; linganisha Matendo 17:24, 25.

4. (a) Shetani alitoka wapi? (b) Ni tamaa mbaya gani ambayo aliruhusu isitawi?

4 Wakati huo uumbaji wote ulikuwa mkamilifu. Tofauti na wanyama, malaika na wanadamu walikuwa na uwezo wa kuchagua. Lakini muda mfupi baada ya kuumbwa kwa mtu, mmoja wa malaika, kwa kutumia vibaya uwezo mzuri ajabu wa kufanya maamuzi ya kibinafsi, aliasi enzi kuu ya Yehova. Kwa njia hiyo alijifanya adui, au mpinzani, ambayo ni maana halisi ya jina Shetani. (Linganisha Yakobo 1:14, 15; Ufunuo 12:9.) Akivutwa na kutaka makuu, Shetani alitafuta kushawishi watu wawili wa kwanza waondoke kwa Yehova Mungu na kuwaleta chini ya uvutano wake mwenyewe. Aliona kwamba kupitia kwao ingewezekana dunia ijazwe wanadamu ambao wangekuwa wakimheshimu yeye kuwa mungu wao. (Linganisha Isaya 14:12-14; Luka 4:5-7.) Masimulizi ya mambo yaliyotukia katika Edeni si hadithi ya uwongo. Yesu Kristo alitaja masimulizi hayo kuwa uhakika wa kihistoria.—Mathayo 19:4, 5.

5. (a) Ni masuala gani yaliyotokezwa katika Edeni? (b) Yanawahusu nani?

5 Yesu alisema hivi kwa habari ya Ibilisi: “Hakusimama katika kweli . . . Yeye ni mwongo, na baba wa huo.” (Yohana 8:44) Uwongo wa Ibilisi wa kwanza kuandikwa ni ule aliomwambia Hawa alipotilia shaka ukweli wa Mungu. Alichochea kukataliwa kwa sheria ya Mungu na kutoa sababu kwamba ingekuwa faida kwa kila mtu kujiwekea viwango vyake mwenyewe katika maisha. (Mwanzo 3:1-5; linganisha Yeremia 10:23.) Enzi kuu ya Yehova ilipingwa kwa njia hiyo kule Edeni. Kama matukio ya baadaye yalivyoonyesha, ukamilifu wa viumbe vyote vyenye akili kuelekea Mungu ulitiliwa shaka pia. Je! walimtumikia Mungu kwa sababu walimpenda kweli kweli, au wangeshawishwa waondoke kwake? (Ayubu 1:7-12; 2:3-5; Luka 22:31) Masuala hayo yangehusu kila aliye mbinguni na duniani. Ni hatua gani ambayo Mwenye Enzi Kuu ya Ulimwengu Mzima alichukua?

6. Kwa nini Yehova hakuwaharibu waasi mara hiyo?

6 Badala ya kuwaharibu waasi hao mara hiyo, kwa hekima Yehova aliruhusu kipindi cha wakati fulani ili masuala hayo yajibiwe mara moja na basi. Mungu alifanya hivyo, si ili ajithibitishie mwenyewe jambo lo lote, bali avipe viumbe vyenye uhuru wa kuchagua nafasi ya kujionea matunda mabaya yenye kuzaliwa na uasi juu ya enzi kuu yake, pia nafasi ya kuonyesha msimamo wao binafsi juu ya mambo hayo yenye maana sana. Masuala yakiisha kujibiwa, hakuna ye yote ambaye angeruhusiwa tena kamwe avuruge amani.

7. (a) Serikali za kibinadamu zilianza namna gani? (b) Zimejifanyia matendo gani?

7 Yehova Mungu, akiwa Muumba wa wanadamu, alikuwa Mtawala wao pia aliye halali. (Ufunuo 4:11) Lakini, baadaye Shetani na mashetani wake walianza kuchochea tamaa katika wanadamu, si ya kujiwekea viwango vyao wenyewe tu juu ya mema na mabaya, bali pia kuwatawala wanadamu wenzao. Nimrodi alikuwa ndiye wa kwanza kujiweka kuwa mfalme, atawale miji katika Mesopotamia. Yeye alikuwa “mwindaji [wa wanyama na wanadamu] mwenye nguvu katika kupingana na Yehova.” (Mwanzo 10:8-12, New World Translation) Tangu siku za Nimrodi mpaka sasa, kila aina inayowezekana ya serikali ya kibinadamu imejaribiwa. Lakini matendo ya ujumla, kama mwanafunzi ye yote wa historia anavyojua, yamekuwa yenye upotovu na umwagaji wa damu.—Mhubiri 8:9.

8. Kwa nini Yesu alikataa kujiingiza katika mfumo wa kisiasa wa ulimwengu?

8 Yesu Kristo alipokuwa hapa duniani, Shetani alijaribu kumleta hata yeye chini ya uvutano wake. Alimtolea Yesu “milki zote za ulimwengu” wabadilishane na tendo moja la ibada. Yesu alikataa. (Luka 4:1-13) Baadaye watu walitaka kumfanya mfalme, lakini Yesu akaondoka. (Yohana 6:15) Aliujua mfumo wa kisiasa wa ulimwengu, akajua kwamba hayakuwa mapenzi ya Mungu kwake ajaribu kuufanya kuwa bora.

9. (a) Ili kuondoa matatizo ya wanadamu, ni jambo gani linalopasa kufanywa ambalo ni Ufalme wa Mungu pekee uwezao kulifanya? (b) Ufalme huo ni nini?

9 Yesu alionyesha ushikamanifu kamili kwa Yehova, Mungu na Baba yake. Alizipenda njia za Baba yake na nyakati zote alifanya mambo yaliyompendeza. (Yohana 8:29) Alijua kwamba njia za kuondolea matatizo ya wanadamu zingeletwa na Ufalme wa Mungu, serikali ya kweli ambayo ingetawala kutoka mbinguni na ingetoa mwelekezo wa uadilifu na wa upendo unaohitajiwa na wanadamu. Ufalme pekee ndio ungeweza kuondoa uvutano wa Shetani na mashetani wake. Huo pekee ndio ungeweza kuunganisha jamii na mataifa yote kuwa jamaa moja ya dunia yote yenye kuishi kwa amani. Huo pekee ndio ungeweza kuwaondoa wanadamu katika utumwa wa dhambi na kifo. Huo pekee ndio ungeweza kuletea wanadamu furaha yenye kuendelea. Ufalme huo si mpango fulani wenye kusimamishwa na wanasiasa na kubarikiwa na viongozi wa kidini. Wakristo wa kweli hawatumii silaha za vita vya kimwili ili waendeleze faida zake. Ni serikali ya Mungu mwenyewe, yenye Mfalme mkamilifu wa kimbingu aliyetawazwa na Mungu mwenyewe. Huo ndio Ufalme ambao Yesu alihubiri juu yake na ambao alifundisha wafuasi wake waombe kwa sala.—Danieli 2:44; Ufunuo 20:1, 2; 21:3, 4.

WEWE UTACHAGUA UPANDE UPI?

10. (a) Ni suala gani kubwa ambalo ni lazima kila mmoja wetu akabili? (b) Imetupasa tuwe tukifanya nini kuhusu suala hilo?

10 Suala ambalo ni lazima ukabili ni hili: Je! wewe unakubali kwamba Yehova Mungu, Muumba wa ulimwengu mzima, pia ni Mwenye Enzi Kuu halali, Mtawala Mkuu wa ulimwengu wote? Je! umechukua wakati ujifunze kusudi lake na matakwa yake yaliyoandikwa katika Biblia? Kwa kuheshimu cheo chake na kwa kuthamini njia zake, je! unajithibitisha mwenyewe kwa upendo kuwa mtiifu kwake?—Zaburi 24:1, 10; Yohana 17:3; 1 Yohana 5:3.

11. Kwa nini kuchagua mwendo tofauti hakuleti furaha?

11 Je! watu wanaochagua mwendo mwingine ni wenye furaha zaidi? Yamekuwa matokeo gani ya sababu aliyotoa Shetani kwamba wanadamu wangepata faida kwa kujidai wanajitegemea badala ya kumsikiliza Mungu? Kukataa kukubali kwamba Mungu ndiye mwenye dunia hii na kwamba wanadamu wote, wakiwa watoto wa watu wawili wa kwanza, wanatakwa wawe ndugu na ndugu kumetokeza kuuawa kwa wanaume, wanawake na watoto wasiopungua milioni 99 katika vita vya karne hii pekee. Kutofuata viwango vya adili vya Biblia kumefanyiza jamaa zenye kuvunjika, kuenea kwa magonjwa ya ngono za ovyoovyo, kuharibiwa kwa afya kwa sababu ya mazoea ya dawa za kulevya, na uhalifu wenye jeuri. Hata watu wanaookoka mwisho wenye jeuri wanakutana na kifo kwa sababu ya dhambi iliyorithiwa kutoka kwa Adamu. Ushahidi wote unaonyesha kwamba watu wanajiumiza wenyewe na wale walio karibu yao wanapopuuza matakwa yenye hekima na ya upendo ya Muumba. (Warumi 5:12; linganisha Isaya 48:17, 18.) Bila shaka hiyo siyo aina ya maisha unayotaka. Unaweza kuchagua kilicho kizuri zaidi.

12. (a) Ni mwaliko gani mchangamfu ambao Biblia inatutolea sisi? (b) Tunapoendelea kulifuata Neno la Mungu katika maisha zetu, tutaona nini?

12 Biblia inatoa mwaliko huu kwa uchangamfu: “Onjeni mwone ya kuwa [Yehova] yu mwema; heri mtu yule anayemtumaini.” (Zaburi 34:8) Ili ufanye hivyo, ni lazima upate kumjua Yehova kisha ufuate shauri lake. Ufanyapo hivyo, maisha yako yatajawa na maana. Badala ya kutumia dakika chache za raha ambayo huenda ikakusaidia kwa muda mfupi usahau matatizo lakini inayoleta sikitiko baadaye, utajifunza jinsi ya kushughulika kwa kufanikiwa na matatizo ya maisha na jinsi ya kuwa na furaha yenye kuendelea. (Mithali 3:5, 6; 4:10-13; 1:30-33) Pia utakuwa na taraja la kushiriki baraka za ajabu zitakazoletwa na Ufalme wa Mungu. Ikiwa hiyo ndiyo aina ya maisha unayotamani sana, ni lazima uchukue hatua sasa. Kwa sababu gani?

MATAIFA YOTE YANAELEKEZWA KWENYE HAR–MAGEDONI

13. Kwa nini ni jambo la maana kuchukua msimamo imara upande wa Yehova sasa?

13 Yehova hatavumilia milele wanadamu na matengenezo ambayo ama kwa makusudi ama kwa ubaridi yanafuata uongozi wa Shetani. Hawataruhusiwa waendelee kupuuza sheria ya Mungu, kuitumia vibaya dunia na kuharibia wengine maisha. Watakiona cha-mtema-kuni katika ile ambayo Biblia inaita “siku ya [Yehova] iliyo kuu.”—Sefania 1:2, 3, 14-18.

14. Mataifa yote yanakusanywa sasa kwenye nini?

14 Kwa ufunuo wa mambo ambayo yangetokea wakati wa siku za kumalizia za mfumo wa mambo wa sasa, Yesu Kristo alifichua kwamba ‘roho za mashetani zingetoka na kuwaendea wafalme wa ulimwengu wote, kuwakusanya kwa vita ya siku ile kuu ya Mungu Mwenyezi.’ Kama ufunuo huo ulivyoonyesha, “wakawakusanya hata mahali paitwapo kwa Kiebrania, Har–Magedoni.” Sasa kukusanywa huko kunaendelea!—Ufunuo 16:14, 16.

15, 16. (a) Har–Magedoni ni nini? (b) Kwa nini ni ya lazima?

15 Har–Magedoni inayosemwa na Biblia si jambo linaloweza kuepukwa kwa ususiaji wa silaha za nyukilia. Mashauriano ya kimataifa hayataizuia. Kwa wazi jina hilo limechukuliwa kutokana na mji wa kale wa Megido, lakini kinachohusika ni zaidi ya mahali katika Mashariki ya Kati. Wakisukumwa na “mtawala wa ulimwengu huu” asiyeonekana, mataifa yote, bila kujali siasa zao tofauti-tofauti, yanakusanywa kwenye hali ya ulimwenguni pote inayoonyesha upinzani wao kwa Yehova Mungu. “Wafalme wa dunia nzima inayokaliwa,” pamoja na wafuasi wao wote, wanaongozwa wachukue msimamo wao. Upesi sana kabla ya Har–Magedoni upinzani wao kwa Ufalme wa Mungu na kwa wote wanaoutangaza utaongezeka sana duniani pote. Wawe wanakubali kuna Shetani au sivyo, “ulimwengu mzima uko katika uwezo wa yule mwovu,” kama Neno la Mungu linavyotangaza. Ulimwengu mzima na wote wanaoutumainia, ndiyo, wote wanaofuata njia zao, ni lazima uende.—1 Yohana 5:19; 2:15-17, New World Translation.

16 Ulimwengu huu umejaa upotovu toka juu mpaka chini. Wahalifu wa kupindukia, hata na raia wa kikawaida wote wanaonyesha kutojali kabisa sheria na ukosefu wa kutofikiria miili na mali ya wanadamu wenzao. Zaidi ya yote, wanakataa kutii anayosema Mungu mwenyewe katika Neno lake, Biblia. Hawaiheshimu enzi kuu yake. Ni lazima Mungu achukue hatua ili aliondolee jina lake suto ambalo limeletwa juu yalo, pia kuweka njia tayari ya kufanya dunia iwe Paradiso ambamo wanaopenda uadilifu wataweza kufurahia amani na usalama wa kweli.

17. (a) Uharibifu huo utakuwa mkubwa kadiri gani? (b) Ni nani atakayekuwa akielekeza yatakayotokea?

17 Uharibifu utakapokuja, hakutakuwa na shaka kwamba umetoka kwa Yehova. Uangamizi utaipata dunia yote. Mataifa yatajua kwamba Yehova anachukua hatua wakati majeshi yake ya kuharibu yatakapoanza kutenda. Mamlaka ya kiserikali itakapoanguka, mkono wa kila mtu utageukia mwenziye. Mwana wa Mungu mwenyewe kutoka mbinguni ataelekeza yatakayotokea.—Ufunuo 6:16, 17; 19:11-13; Zekaria 14:13.

18. Ni nani watakaokuwa waokokaji?

18 Tofauti na matokeo ya vita ya silaha za nyukilia yenye kupiganwa na wanadamu, uharibifu huo hautaangamiza watu wote bila kubagua. Lakini waokokaji watakuwa nani? Je! ni wote wanaojidai kuwa wafuasi wa dini fulani, au labda ni wote wanaojidai ni Wakristo? Yesu anawaita “wengi” hao kuwa ‘watendao maovu.’ (Mathayo 7:21-23) Watakaookoka waingie katika “dunia mpya” ni wale ambao wamesitawisha kikweli uhusiano wa karibu sana pamoja na Yehova na Mwanaye wa kifalme, Kristo Yesu. Kwa namna ya maisha yao na kwa kutoa kwao ushuhuda juu ya Ufalme, watakuwa wameonyesha kwamba ‘wanamjua Mungu’ kweli kweli na kwamba ‘wanaitii Injili ya Bwana wetu Yesu.’ Je! wewe unajithibitisha kuwa mtu wa jinsi hiyo?—2 Wathesalonike 1:8; Yohana 17:3; Sefania 2:2, 3.

    Maktaba Kwenye Mtandao (1980-2025)
    Toka
    Ingia
    • Kiswahili
    • Shiriki
    • Mapendezi
    • Copyright © 2025 Watch Tower Bible and Tract Society of Pennsylvania
    • Masharti ya Utumiaji
    • Sera ya Faragha
    • Mpangilio wa Faragha
    • JW.ORG
    • Ingia
    Shiriki