Makundi kwa Ajili ya Kujenga Katika Upendo na Umoja
Labda umepata kuhudhuria mikutano fulani ya Mashahidi wa Yehova karibu na mahali unapoishi. Watu kutoka tabaka zote za maisha—vikundi vya jamaa, waseja, wazee kwa vijana—walikuwa huko. Wote waliungana katika ibada yao na walipendezwa kusaidia wengine.
Katika mpango wo wote ambapo idadi kubwa ya watu inataka kufanya kazi kwa umoja, kuna uhitaji wa kuwa na usimamizi fulani. Mungu ni Mungu wa utaratibu; hivyo, utaratibu huo umepasa uonekane katika kundi la watu wake. Kama katika karne ya kwanza, ndivyo na leo, wanaume Wakristo wenye kustahili, waliokomaa na wenye ujuzi wanawekwa wawe wazee, au waangalizi. Hao wanasimamia kundi na kuyaangalia mahitaji yalo ya kiroho. Wanasaidiwa na wanaume wengine waaminifu wanaojulikana kuwa watumishi wa huduma. Wanaume hao hawapokei mshahara wala faida nyingine ya kifedha bali wanatumikia kwa kujitolea, wakijilipia gharama zao wenyewe, kwa kufanya kazi yao ya kimwili. —1 Wakorintho 14:33, 40; Wafilipi 1:1; 1 Timotheo 3:8, 9.
Hao wanachaguliwaje? Wanahitaji kuwa watumishi waaminifu wa Mungu wanaoonyesha sifa fulani za Kimaandiko. Baadhi za hizo ni hizi: kuwa ‘mwenye kiasi katika mazoea, timamu katika akili, mwenye utaratibu, mkaribishaji wageni, mwenye kustahili kufundisha, mwenye kusikiliza maoni ya wengine; si mwenye kupenda fedha; mwenye kusimamia nyumba yake kwa jinsi nzuri; si mtu aliyegeuka hivi karibuni; kuwa na ushuhuda mzuri kutoka kwa wale walio nje’; ‘kushikamana kwa imara na neno la uaminifu kwa habari ya ustadi wa kufundisha.’ —1 Timotheo 3:1-15; Tito 1:7-9, NW.
Wanaume hao hawachaguliwi wawe katika cheo kwa kupigiwa kura na kundi, ambamo walio wengi huenda mara nyingi wakawa ni Wakristo wapya. Badala yake, wanapendekezwa na wanaume waliokomaa wenye ujuzi walio wazee na walio na ufahamu juu ya kadiri ambayo wale wanaofikiriwa wanatimiza matakwa ya Kimaandiko. Ndipo kuwekwa rasmi kwa wazee na watumishi wa huduma kunafanywa kwa usimamizi wa Baraza Linaloongoza la Mashahidi wa Yehova, kwa kufuata kiolezo kilichowekwa na kundi la Kikristo katika karne ya kwanza.
Wazee hao, au waangalizi, si jamii ya makasisi; wao si mabwana juu ya wengine. Kama Yesu alivyosema, wo wote wanaoongoza ni lazima wawe watumwa wa wote. Katika kundi la Mashahidi wa Yehova, wazee ni wafanya kazi walio wenzi wa wengine kweli kweli kwa ajili ya Ufalme wa Mungu. —Mathayo 20:26, 27; 23:8-11; Warumi 12:8; 1 Wakorintho 3:5; 4:1, 2; Wakolosai 4:11; 1 Wathesalonike 5:12-14.
Wakiwa waangalizi, wanasimamia agizo linalotolewa kwenye mikutano na kuongoza katika utendaji wa kuhubiri. Kuhubiri habari njema za Ufalme katika eneo lote lililogawiwa ni lengo la kwanza la kundi. Waangalizi pia wanatumikia wakiwa wachungaji, wakitembelea washiriki wa kundi kuwatia moyo kama inavyohitajiwa. —Mathayo 24:14; Matendo 1:8; 1 Wathesalonike 2:11, 12; 5:14, 15; 2 Timotheo 2:24-26; Waebrania 13:17; Yakobo 5:13-16; 1 Petro 5:1-4.
Pia wazee wana daraka la kukaripia na kuwapa nidhamu wo wote ambao huenda wakawa wanafuata mwendo wenye makosa na ambao huenda wakawa hatari kwa usafi wa kiroho na wa adili na kwa umoja wa kundi. —1 Wakorintho 5:4, 5, 7, 11-13; Tito 1:9; 2:15; 3:10, 11.
Kushirikiana kwa ukawaida na kundi kutakupa ushirika mwema na faida nyingi za kiroho. —Zaburi 35:18; 84:10.
• Ni nani wanaosimamia mambo ya makundi moja moja?
• Waangalizi wanachaguliwa juu ya msingi gani?
• Wana madaraka gani?
[Picha katika ukurasa wa 13]
Waangalizi wanaliagiza kundi, wanaongoza katika kazi ya kuhubiri nyumba kwa nyumba, wanatia moyo kwa ziara za uchungaji, wanatoa shauri na karipio inapohitajiwa