Makundi Yametengenezwa kwa Ajili ya Kuhubiri Ufalme wa Mungu
ALipokuwa hapa duniani, Yesu Kristo aliuhubiri Ufalme wa Mungu, akienda kijiji kwa kijiji na mji kwa mji. Pia alizoeza na kutuma wanafunzi wake wafanye kazi iyo hiyo. Kabla ya kupaa kwenda mbinguni, aliamuru wafuasi wake kufanya wanafunzi kutoka watu wa mataifa yote. Tangu mwanzo wenyewe, kundi la Kikristo la kwanza lilitengenezwa kwa kusudi la kuhubiri habari njema. Ko kote walikoenda wanafunzi, wangepatikana wakiuhubiri Ufalme wa Mungu. —Mathayo 4:17, 23; 10:1-16; 28:19, 20; Luka 4:43, 44; 8:1; 10:1-9; Matendo 1:8; 4:31; 5:42; 8:12; 19:8; 28:23, 30, 31; Warumi 10:9, 10, 14.
Katika unabii wa Yesu juu ya umalizio wa mfumo wa mambo, yeye alisema hivi: “Habari njema hizi za ufalme zitahubiriwa katika dunia yote inayokaliwa na watu kwa ushuhuda kwa mataifa yote; na ndipo ule mwisho utakapokuja.” Kuhubiri huko ni wajibu wa kwanza wa kundi la Kikristo leo. —Mathayo 24:14, NW; Marko 13:10.
Ulimwenguni pote, makundi yote ya Mashahidi wa Yehova yametengenezwa ili yaeneze kwa utaratibu eneo lao kwa kuzihubiri habari njema za Ufalme wa Mungu. Ili kufanywe kwa njia ya utaratibu, katika kila nchi afisi ya tawi ya Watch Tower Society inagawia kila kundi eneo la kutolea ushuhuda. Kundi linagawa mgawo huo wa eneo katika visehemu vidogo vidogo, ambavyo navyo vinagawiwa kwa wale watakaokuwa na daraka la kuona kwamba watu wanatembelewa. —1 Wakorintho 14:33, 40.
Kwa kawaida Mashahidi wanafikia watu kwa kwenda nyumba kwa nyumba. Kwenye mikutano yao ya kundi, Mashahidi wa Yehova wamezoezwa kutoa mahubiri mafupi ya ujumbe wa Ufalme kwenye milango, wakitumia Biblia zao. Mashahidi wanachukua vitabu vya Biblia na kwenda kuwaachia wenye nyumba wanaotaka kupata maarifa mengi zaidi ya Neno la Mungu.
Ili kumpa kila mtu katika eneo nafasi ya kuusikia ujumbe wenye maana wa Ufalme, Mashahidi wanatunza maandishi ya habari wanapoenda nyumba kwa nyumba, wakionyesha mahali ambapo watu hawakuwa nyumbani au mahali ambapo kwa sababu nyingine haikuwezekana kutoa ushuhuda ulio kamili. Ziara inafanywa wakati mwingine. Kupendezwa kunapoonyeshwa, kunaandikwa, na Mashahidi wanarudia ili kutoa taarifa zaidi ya Kimaandiko. Inapotakiwa, funzo la Biblia la kawaida linaongozwa. Yote hayo yanafanywa bila malipo.
Mashahidi wa Yehova wanatoa pia magazeti kwa watu wanaopita barabarani. Kwa njia hiyo wanaweza kufikia watu wengi ambao hawangeweza kuwakuta nyumbani. Jitihada nyingi zinafanywa ili kufikia kila mtu atakayesikia. —Matendo 17:17; Ufunuo 14:6, 7; 22:17.
Ni kwa sababu gani Mashahidi wanazidi kutembelea watu wakati walio wengi hawaonyeshi kupendezwa ko kote? Imeonwa kwamba hali za watu mmoja mmoja mara nyingi zinabadilika. Nao wanaitikia vizuri wakati wa ziara nyingine, au huenda mtu mwingine wa nyumba fulani akapatikana atakayeonyesha kupendezwa.
Yesu aliwaambia wanafunzi wake hivi: “Endeleeni, basi, kuutafuta kwanza ufalme na uadilifu wake.” Kuhubiri Ufalme wa Mungu ni sehemu ya maana sana katika kutafuta kwetu kwanza Ufalme, na Mashahidi wa Yehova wanafanya hilo kuwa lengo la maana sana katika maisha yao. —Mathayo 6:33; 2 Timotheo 4:2.
• Ni kazi gani ya Yesu na Wakristo wa kwanza iliyotabiriwa kufanywa pia wakati wetu?
• Utendaji wa kuhubiri wa Mashahidi wa Yehova umetengenezwaje?
• Ni kwa sababu gani Mashahidi wanazidi kuwatembelea watu wakati walio wengi hawaonyeshi kupendezwa?
[Picha katika ukurasa wa 16, 17]
Mashahidi wa Yehova wakihubiri Ufalme wa Mungu katika nchi mbalimbali
Thailand
Meksiko
Uholanzi
Korea
Kurasao
Ghana
Uingereza
Australia